YOUTUBE PLAYLIST

Wednesday, April 28, 2010

DJ wa kwanza

Katika kuzungumza na watu kupata mambo kwa ajili ya blog hii, nimepata hili ambalo naomba maoni. Kijana wa zamani mmoja kaniambia DJ wa kwanza anaemkumbuka alikuwa akikaa maeneo ya Keko Cocacola, alikuwa Mkongo fulani ambae jina kamsahau. Je, kuna mwenye kumbukumbu kuhusu hilo?

The Dynamites

Kikundi kingine toka enzi za miaka ya 69/70 hawa waliitwa The Dynamites. Hapa kwa kweli namtambua Salim Willis tu ambaye baadae alikuja kuwa mpiga second solo wa Afro70.

Midomo ya Bata

Upigaji wa vyombo vya kupuliza umepungua sana katika bendi zetu hapa Tanzania. Kumekuwa na maelezo kuwa tatizo hili limetokana na kuanza kutumika kwa Keyboards au vinanda aina ya synthesizer. Vinanda hivi vina uwezo wa kutoa milio mbalimbali ikiwemo ya vyombo vya kupuliza kama trumpet na saxophone. Lakini mi nadhani ni maendeleo ya mtiririko wa uigaji wa nini kinachotokea Kongo. Ni jambo lisilopingika kuwa kwa miaka mingi sana bendi nyingi zimekuwa zikiiga kile kinachotokea Kongo. Mara nyingine hata kufikia kuiga nyimbo nzima kutoka kwa bendi za Kongo. Na mara nyingine kuiga mfumo wa muziki kutoka huko. Kwa misingi hiyo, bendi zetu nyingi ziliamua kuacha kupiga vyombo vya kupuliza mara baada ya kuona bendi nyingi za Kongo zikiacha kutumia vyombo hivyo.
Lakini kwa ukweli kabisa vyombo vya upulizaji vina raha yake na utamu wake. Wapigaji wake hutengeneza step zao za kucheza na hupanga sauti za kupishana kati ya trumpet na saxaphone na huongeza raha sana katika muziki. Kwa sasa ni bendi chache kama vile DDC Mlimani Park, OTTU, Vijana Jazz, MAK Band, African Beat ndio wanaendeleza upigaji wa vyombo vya kupuliza.

Sunday, April 25, 2010

Akina mama nao- Asia Darwesh


Asia Darwesh ni miongoni mwa wanamuziki wanaoheshimika sana katika jamii ya wanamuziki na wapenzi wa muziki waliowahi kusikia au kufurahia kazi zake. Katika picha hapo juu Asia ambae alikuwa mpiga Keyboards wa kutumainiwa anaoneka picha ya juu akiwa na King Kiki enzi za Double O, na chini akiwa Mk Sound. Asia aliwahi pia kupigia Bicco Stars ambapo yeye pamoja na Andy Swebe na Mafumu Bilali na wenzao (waliihama MK sound), waliweza kuipandisha sana chati bendi hii. Hatimae Asia aliweza kumiliki bendi yake na alipatwa na umauti akiwa na bendi yake ambayo ilifanya vizuri sana huko Uarabuni.

Mzee Joseph Nyerere


Mzee Joseph Nyerere alikuwa mpenzi sana wa Vijana Jazz Band. Nakumbuka siku za Jumapili ambapo Bendi ilikuwa na onyesho lake lililoitwa Vijana Day mara nyingi ungemkuta pembeni akisikiliza muziki na pengine akiomba special request. Ilikuwa ni burudani pale ambapo aliamua siku hiyo kucheza maana alikuwa na staili ya peke yake iliyofanya mtu apende kumuangalia. Historia inasema alisoma Tabora Boys na alikuwa Band Master wa bendi ya shule na alipendwa sana kutokana na mbwembwe zake alipokuwa akiongoza na kifimbo cha Band Leader. Mzee Joseph aliwahi kuwa Katibu Mkuu wa TANU Youth League. Pichani akiwa jukwaani na Marehemu Hemedi Maneti katika Ukumbi wa Vijana Kinondoni, kwa mbali nyuma anaonekana Aggrey Ndumbalo akiwa ameshika gitaa na Said Hamisi muimbaji wa Vijana akiwa napiga makofi, wote wamekwisha tangulia mbele ya haki.

Libeneke 2

Katika blog hii tuliwahi kuzungumzia chanzo halisi cha neno LIBENEKE. Nilieleza kuwa neno hili na hasa linapounganishwa na kusema 'endeleza libeneke', lilitokana na wimbo wa Butiama Jazz Band uliokuwa ukitaja majina ya wanamuziki wa bendi hiyo na kila mmoja akiambiwa aendeleze libeneke. Nimepata bahati ya kuongea na aliyekuwa Kiongozi na mpiga solo wa Butiama Jazz Band. Alikuwa na haya ya kusema. Butiama Jazz Band ilianzishwa mwaka 1971, makao yake makuu yalikuwa mtaa wa Kongo maeneo ya Kariakoo, Dar es Salaam, jirani kabisa na DDC. Ilianzishwa na asilimia kubwa ya wanamuziki kutoka Ifakara na ndio maana waliamua kuchukua jina la ngoma ya kwao na kuuita mtindo wa bendi yao Libeneke. Kiongozi wa bendi alikuwa Mzee Makelo na Katibu wa Bendi Mzee Mustafa Mkwega. Mzee Mkwega aliwahi kufanya kazi kwa Hayati Mwalimu Julius K Nyerere na hivyo alikuwa anawasiliana nae kwa karibu. Alikwenda kwa niaba ya wenzie na kumuomba Mwalimu awasaidie vyombo vya muziki, na aliwatuma wakalete Profoma invoice ya vyombo, walipoleta Mwalimu aliitia saini na ilitosha kwenda kupewa vyombo vipya dukani. Kama shukrani kwa Mwalimu waliita bendi yao Butiama Jazz Band. Na kuanzia hapo kila mwalimu alipoenda likizo ya mwaka Butiama bendi ilikwenda huko kutumbuiza wageni mbalimbali waliokuwa wanamfuata Mwalimu huko.

Saturday, April 24, 2010

Maquis Original


Maquis Original wakiwa katika uwanja wa Jamhuri Dodoma. Mwenye nyeusi tupu akiwa na gitaa ni Dekula Kahanga Vumbi, wa pili toka kushoto na suruali nyeusi ni Issa Nundu haya tuwataje wengine hapa.

Baziano na Kasheba


Kwa wapenzi wa Fauvette na baadae Kasheba Group na Zaita Muzika, sauti ya Baziano si rahisi kusahaulika. Lakini kwa mapenzi yake Mungu, Baziano(wa kwanza kushoto) na mpiga gitaa wake Ndala Kasheba (wa pili kutoka kulia) hatunao tena duniani Mungu awalaze pema peponi. Pichani pia yupo Kasongo Mpinda (mwimbaji) wa pili kushoto, na Matei Joseph (mpiga drums).

Akina mama nao


Ni jambo lisilopingika kuwa akina mama wamekuwa sambamba na wanaume katika kuendeleza gurudumu la muziki wa nchi hii. Kumekuwa na tatizo la mtizamo na hivyo kufanya akina mama kutokuonekana sana katika fani hii kwa vile siyo siri imekua ikipigwa vita katika miaka yote. Pamoja na kuwa hakuna anaetamka hadharani kuwa wanamuziki ni wahuni, lakini taratibu na sheria zinaongea lugha ya kimya kuwa hivyo ndivyo. Nitoe mifano
1. Pamoja na kuwa kuna syllabus ya muziki kuanzia darasa la kwanza, kumekua hakuna jitihada kubwa ya kuhakikisha waalimu wanapatikana. Chuo cha Butimba ndio kimekua chanzo cha waalimu wa muziki lakini akishafika mashuleni hupangiwa vipindi vingine, na muziki huacha kama ulivyo.
2. Leo hii akiingia mwanamuziki kutoka nje ya nchi huhitajika kuwa na work permit, lakini kwa wanamuziki wa nyumbani hakuna taratibu zozote za ajira inayotambulika, hata wahudumu wa ndani wanatetewa bungeni lakini si wanamuziki. Angalia hata Waziri anaeshughulika na Vijana wa Tanzania na Kazi haoni soni kutoa ajira kwa vijana kutoka nje ya nchi yake katika fani ya muziki. Idadi ya wanawake katika muziki imekua kubwa sana kwa sasa ikilinganishwa na zamani lakini bado kuna wanawake wengi waliotikisa anga hizi zamani. Pichani ni muimbaji wa kike wa Afro 70 kutoka South Africa ambaye alisaidia sana kufanya muziki wa Afro kuwa na vionjo tofauti na bendi nyingine. Muimbaji huyu aliitwa Nini, na alirekodi nyimbo moja na Afro70, Mayele. Nini alikua na kaka yake aliyeitwa Vuli ambaye alipiga pia muziki hapa Tanzania na kutunga nyimbo ambayo bado inapiga na bendi kadhaa Tanzania'Lonely Child'. Vuli aliendelea na hatimaye kuwa manamuziki wa Lucky Dube.

Friday, April 23, 2010

Kilimanjaro Band 1




Kilimanjaro Band ni kati ya bendi kongwe hapa Tanzania. Ilianza mwanzoni mwa miaka ya sabini. Imewahi kutokea bendi ikapiga katika harusi ya mzazi na pia mtoto. Generation nzima ya familia. Maelfu ya watu wamekwisha hudhuria maonyesho ya Kilimanjaro Band hebu hapa tuone kati ya picha zao za zamani.

Bendi za Mkoa wa Morogoro

Kati ya mikoa iliyokuwa na Bendi nyingi, sijui kama ulikuweko ulioushinda mkoa wa Morogoro. Ilikuwa kila wilaya ina bendi. Baadhi ya bendi ninazozikumbuka ni Morogoro Jazz, Super Volcano, Cuban Marimba Band, Les Cuban, TK Limpopo, Kilosa Jazz (alikotokea Abel Balthazar), Ifakara Jazz, Sukari Jazz, Imalinyi Jazz, Mahenge Jazz, Kwiro Jazz., Mzinga Troupe. Na hata wale wakali wa wakati huo na ule wimbo wao enye maneno,

Waache waseme watachoka wao,

Mzee Makelo endeleza libeneke,

Waache waseme watachoka wao,

mtindo libeneke unatia fora

Hapa naongelea Butiama Jazz Band, iliyokuwa inapiga muziki kwa mtindo wao uliotokana na ngoma ya kwao Libeneke,wao ni wa Ifakara hivyo nao ni bendi ya mkoa wa Morogoro japo jina lilitokana na mahala alipozaliwa Baba wa Taifa.(Mzee Mkwega aliyekuwa mwenye bendi alikuwa kada mzuri sana wa CCM, hata kifo chake kilimkuta akiwa mtumishi wa CCM ofisi ndogo Dar es Salaam).

Mpaka leo ukienda Ifakara wakati wa msimu wa mavuno ikiwa kuna sherehe za jumla kama vile kipaimara, ndo utajua wanavyopenda ngoma. Kuna vikundi vingi vya ngoma ya Sangula na kila kikundi kimejipa jina la Bendi, hivyo utakuta mabango yakitangaza Tancut Almasi, Msondo, Super Volcano, na kila nyumba yenye sherehe huandaa kundi lake ni raha tupu hapo

Tuesday, April 20, 2010

Those were the days


Those were the days my friend,
We thought they would never end,
We would sing and dance for ever and a day.
We'd live the life we chose,
We'd fight and never loose ,
Cause we were young O yes we were young. Katika picha.. Patrick Balisidya na Salim Willis enzi za Afro 70

The Rifters 2


Kuna mara nyingine nakosa la kusema nikifikiria hali iliyopo katika ulimwengu wa muziki leo hapa Tanzania. Akina Raphael walikuwa wanawaza nini wakati wanapiga hapa? na ilikuwa nyimbo gani? wanaonekana wana mawazo hawa ni The Rifters

Shaaban Yohana Wanted


Nilikutana na Shaaban Yohana kwa mara ya kwanza katika bendi ya Tancut, ambapo gitaa lake la solo husikika katika nyimbo zote zilizokuwemo katika album za kwanza za bendi ile. Alipiga gitaa katika nyimbo zifuatazo:-
Nimemkaribisha nyoka
Kashasha
Tutasele
Mtaulage
Masafa Marefu
Butinini. Lakini aliniacha Tancut na kwenda Vijana Jazz huko tukakutana tena ambako solo lake linakumbukwa katika nyimbo nyingi kama vile Aza, Ogopa Tapeli,Thereza, Shoga, Malaine nk. Aliacha bendi ya Vijana na kujiunga na Ngorongoro Heroes akatesa sana huko, kisha akatimkia Botswana ambako yuko mpaka leo, muda mwingi akiutumia kama mwanamuziki wa studio.

The Jets


Hawa ndio The Jets (1972), ambao baadae walikuja kuwa STC Jazz, ambayo ndio chanzo cha Biashara Jazz. Waliopo hapa wa kwanza Belino, Raphael Sabuni, Mgoro katika moja ya maonyesho yao. Marijanio Rajab alijiunga na kundi hili, na kuimba wimbo kama.... Ilikuwa usiku wa manane.

Monday, April 19, 2010

Flaming Stars


Familia ya akina Sabuni ilikuwa maarufu sana katika makundi ya vijana wapenzi wa muziki wa Buggy , John , Cuthbert, Raphael wote walikuwa wanamuziki, na kundi la Flaming Stars lilikuwa ni la akina Sabuni. Katika picha hii ya Flaming Stars unawatambua wangapi.?

Afro70 1974

Afro 70 wakiwa Namanga baada ya kutoka Nairobi kupata vyombo vipya. Walilazimika kupiga Namanga ili wapite na vyombo bila bughudha. Unawakumbuka majina?

Dar Es Salaam Jazz-majini wa bahari

Dar Jazz ndiyo kati ya bendi za kwanza nchini. Bado kuna utata wa kumbukumbu kwani katika kipindi cha mwanzo kulikuwekona Coast Social Orchestra inayosemekana ilikuja kuwa Dar Jazz. Wakati huohuo kulikuweko na YMCA Social Orchestra, hivyo ipi ya mwanzo ni kitendawili bado. Pichani ni Dar Jazz 1968. King Michael Enoch akiwa na kofia na nadhani hatupati taabu kumtambua Patrick Balisidya.Kama unavyoona amlifier ya magitaa ilikuwa moja tu, na chini kwenye kiti, kuna amlifier ambayo iliunganishwa kwenye cone spikas, zile spika za chuma tunazoziona kwenye sehemu za ibada na hizo ndizo zilikuwa kwa ajili ya waimbaji.

Tanzania All Stars


Ukitaka kujua umahiri wa wanamuziki enzi hizo ni vizuri ukazisikiliza nyimbo za Tanzania All Stars. Karibuni nitazitundika wote tuzisikilize, katika wimbo wa Samora, Zahir Ally Zoro aliimba Kireno, Jabali aliimba Kiarabu, Aziz Varda Kihindi we bwana wee. Haya tujikumbushe kwa kuwataja majina wote unaowaona hapo juu.

Usimkwae mtu likwae chua


Chakachua ndio ulikuwa mtindo wao, walikuwa na mpiga solo ambae wapiga magitaa wote waliomjua wanamheshimu kwa upigaji wake. Kuna mwanamuziki Mtanzania aliyeko Japan aliwahi kunambia kuna siku aliwahi kumsikilizisha muziki wa Chakachua mpiga gitaa mahiri George Benson, George Benson alisikitika sana kusikia aliepiga gitaa vile ameshafariki kwani alitaka wakutane watengeneza kitu cha pamoja, huyu si mwingine bali ni Michael Vicent. Na bendi ilikuwa Urafiki Jazz iliyokuwa chini ya Kiwanda cha nguo cha Urafiki Dar Es Salaam

Sunday, April 18, 2010

TP OK Jazz Dar es Salaam 1974

Mwaka 1974, TP OK Jazz chini ya Lwambo Lwanzo Makiadi walitembelea Tanzania, na kupiga show tatu. Moja National Stadium, Diamond na Bahari Beach. Onyesho la Bahari Beach walishirikiana na Afro 70. Matokeo ya ushirikiano huo yalijitokeza kwa nyimbo kadhaa zilizopigwa na Afro 70 kuwa na solo lilifuata mipigo ya Franco. Nyimbo kama Dada Rida, Umoja wa wakina Mama, ni baadhi ya nyimbo hizo,tena hii nyimbo ya pili ilikuwa kama kopi ya wimbo Georgette wa Franco. Ujio huo ulianzisha utamaduni uliodumu kwa muda mrefu wa bendi kupenda kutumia vifaa vya aina ya Ranger FBT.
















Hunaaaaaaa mwana hunaaaaaa

Baada ya Marijan na Safari Trippers kuimba kibao Hanifa, na katika chorus kuimba neno 'huna'. Liligeuka kuwa neno ambalo lilitumika kama vile leo neno 'kufulia' linavyotumika. Ungemsikia binti akimwambia mwanaume 'Hunaaa" na liliweza kuleta ngumi neno hilo. Haya picha ya hali wakati huo kwa wasomaji wa Kiingereza
.

Enzi za Buggy


Leo ni Jumapili ngoja nilete picha ambayo kwa vyovyote ilipigwa Jumapili , maana ndio ilikuwa siku ya Buggy, lile dansi la mchana lililokuwa linaanza saa 7 au nane na kuisha saa kumi na mbili jioni. Unaona mavazi ya siku hizo?, si muda mrefu baada yalipigwa marufuku , na kukaweko na posters kila mahala zikionyesha nguo gani za kuvaa. Vijana wa TANU Youth League walikuwa wakitembea na mikasi na kuchana nguo zilizoonekana hazifai. Loh, Hawa Rifters walikuwa kati ya makundi mengi ya wanamuziki vijana waliokuwa wakipiga muziki wa soul, hapa bwana nyimbo za Otis Redding, Kipofu Clarence Carter, Wilson Pickett , James Brown,Sam and Dave, Isaac Hayes ilikuwa mwendo mdundo

Saturday, April 17, 2010

Msondo Ngoma


Msondo ngoma wana kila haki ya kujiiita Baba ya muziki. Bendi hii ilianza mwaka 1964,kama NUTA Jazz na imekuwa na mtindo wa Msondo miaka yote na imekuwa juu miaka yote. Nani anaweza kujipima na Msondo. Pichani Mzee Abel Balthazal akiwa anapiga gitaa, Mzee Mnenge kwenye saxaphone, jamani majina ya wengine tafadhali.

Orchestra Fuka Fuka

Kuna mdau aliomba azione picha za bendi ya Fuka fuka,hapa ni picha zilizotangaza ujio wa Bendi hii ambayo ilitokana na Orchestra Kamale ya Kongo. Haikukaa Tanzania muda mrefu lakini ndio iliyomleta mwanamuziki Tchimanga Assossa ambaye ameamua kuishi Tanzania toka wakati huo

Thursday, April 15, 2010

Swali la Leo

Mwanamuziki gani huyu aliyeshika gitaa?

Tancut almasi Orchestra enzi hizo


Tancut Almasi Orchestra, hapa wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma. Bahati mbaya Ray, Hashim, Kalala, Zacharia wameshatangulia mbele ya haki. Kuna utata kuhusu alipo Mohamed Shaweji. Uniform zinapendeza
(Kutoka kushoto.. Ray Mlangwa, Bakari Buhero, Hashim Kasanga, Mohamed Shaweji, John Kitime, Kalala Mbwebwe, Kawelee mutimwana,Abdul Mngatwa, Kibambe Ramadhan, Zacharia daniel, Akuliake 'King Maluu' Salehe)

Wanamuziki kutoka Kongo II


Katika makala za mwanzo mwazo za blog hii, kuna wadau walitaja nyimbo za bendi ya Nova Success ambazo walizipenda. Nimeona kuwakumbusha zaidi niiweke picha hapa ya Bendi hiyo iliyokuwa ikipiga Top Life Bar Kinondoni. Baadhi ya nyimbo zake ni Maeliza ,Sizeline na Cherie Jamila. Kiongozi wao aliitwa Papa Micky. Mara ya mwisho kusikia kuhusu bendi hii ni pale walipoamua kuelekea Msumbiji

Vijana Jazz ilikotokea





Mwaka 1971 Umoja wa Vijana wa TANU uliamua kuanzisha Bendi na kumpa jukumu hilo mwanamuziki John Ondolo Chacha. Ili kutaengeneza bendi, Marehemu Mzee Ondolo aliweza kuwashawishi vijana wa bendi ya Zezemba wakajiunga nae lakini hawakukaa nae muda mrefu kwani walikuwa ni waajiriwa wa kiwanda cha nguo cha Urafiki, hivyo akalazimika kujenga tena Bendi na kwenda hadi Bagamoyo alipoikuta bendi ya Kizibo na akapata wapigaji kumi. 1972 wapigaji wengine tena wakaacha bendi, hivyo akalazimika kutafuta wengine na kikubwa ni kuwa alimpata mpiga solo Hassani Dalali ambaye aliweza kuwatafuta wenzie. Bendi ilipelekwa JKT mwaka 1973, wakati huu tayari ilishampata mtunzi na mwimbaji kutoka TK Limpopo ya Juma Kilaza, kwa jina Hemed Maneti, na baada ya muda kidogo iliweza kumpata Hamis Fadhili kutoka Jamhuri Jazz.
1974 walienda Nairobi na kurekodi nyimbo ambazo ziliaweka msingi wa bendi hiyo. Baadhi ya nyimbo hizo ni Magdalena, Niliruka Ukuta. Mtindo wa bendi wakati huo ulikuwa Kokakoka Balaa

Belesa Kakere

Salehe Kakere, maarufu kama Belesa Kakere, hapa akitangaza kuhamia Orchestra Bima Lee. Hebu soma maelezo katika habari yake unapata picha kamili ya mwanamuziki huyu na kazi zake na historia yake kwa ufupi

Wednesday, April 14, 2010

Vyombo vya habari

Katika kusoma magazeti ya zamani,(nitazitoa baadhi ya makala hapa), imeniijia kuwa tunatatizo kubwa la uandishi na utoaji wa habari za shughuli za muziki. Makala za muziki za siku hizi, nyingi ni kuhusu nani kapagawisha wapi au mcheza show gani alikaa vibaya au ana uhusiano na nani. Kimsingi ni kama vile taarifa kuhusu muziki ni gossips zinazoendelea katika uwanda wa wanamuziki. Hakuna taarifa ya taaluma katika muziki huo. Unaweza kupata taarifa nzuri kuhusu Beyonce lakini ukakosa taarifa kuhusu Anna Mwaole ambaye yuko jijini Dar es Salaam. hili liko hata kwenye vituo vya redio vya wilayani, ambako huko nako watangazaji wengi wanaiga kuanzia uongeaji, mpangilio wa vipindi, maadili na kadhalika kutoka redio maarufu za Dar es Salaam.
Huko wilayani nako wanadai hawana taarifa za wasanii wa hapo wilayani kwa kuwa wasanii hawaleti taarifa zao, lakini mtu huyohuyo atakaa masaa kadhaa kwenye internet akitafuta taarifa zote kuhusu msanii wa nje. Napata taabu kujua aina ya mafunzo wanayopata waandishi katika vyuo vya uandishi siku hizi. Na tena nakumbuka kuwa wandishi wengi wa zamani hawakupitia vyuo kama vilivyo siku hizi kwanini hakuna ubora wa uandishi sasa? Kwanini tunakosa ufanisi zaidi siku hizi ? au ni mimi ndio mwenye kuona kuna tatizo ambalo halipo? katika makala nitakazoziposti hapa ambazo ni za miaka ya sabini naona kuna maelezo ambayo nayakosa katika uandishi wa siku hizi.

Orchestra Santa Fe

Kati ya maswali amabayo yamewahi kuulizwa humu ni kuhusu bendi hii Orchestra Santa Fe. Hii ilikuwa mwanzo ni bendi yenye asilimia kubwa ya wanamuziki Wakongo. Mkuu wa 'Libeneke' aliwahi kuuliza kama ndio ilikuwa Bendi ya kwanza ya Kikongo, ninauhakika haikuwa bendi ya kwanza ya Kikongo. Wenye taarifa zaidi kuhusu Bendi hii karibuni. Bendi hii ilikuwa ikipiga pale Gateways Mnazi Mmoja maeneo ambayo kuna wakati yalikuwa maeneo muhimu katika shughuli za starehe jijini Dar es Salaam.

Tuesday, April 13, 2010

Sokomokoooooooooo


Leo nimeona nianze kuanika picha nilizonazo hadharani , tukumbuke yalivyokuwa. Pichani ni Safari Trippers. Wapenzi wa Sokomoko mnakumbuka kipindi hiki. Hebu tupeane kumbukumbu

Thursday, April 8, 2010

Muziki wa staili moja

Miaka michache iliyopita kulianza hadithi moja ambayo vyombo vya habari vikaishikia bango, na baadae wanamuziki kadhaa nao wakashika bango nakutoa ushauri nasaha wa tatizo hilo. Tatizo hilo lililkuwa kwanini muziki wa bendi Tanzania hauwi maarufu. Kwa utafiti ambao washika bango waliufanya wakatangaza kuwa Tanzania tuna tatizo la kuwa tunapiga aina nyingi mno za muziki ndio maana haujulikani. Kwa hiyo wataalamu hawa wakiwa wanalinganisha na muziki wa Kikongo wakasema Mkongo mmoja akianzisha Kwasakwasa wote wanapiga Kwasakwasa , ikija Kibinda Nkoy wote wanapiga hivyo hivyo , kwa hiyo nasi tuwe na staili moja, tena ikapewa jina Achimenengule. Utafiti huu ni wa ajabu sana, tuanze na nchi yetu ina makabila zaidi ya 110,yenye mila mbalimbali na muziki mbalimbali, inashangaza kujaribu kufikiri wote hawa wapende aina moja tu ya muziki. Huko Kongo ambako kulitolewa mfano hata wakati wa kile kipindi kinachoitwa the Golden Age of Congolese Music, ndipo haswa upigaji wa aina mbalimbali ulipokuwepo. Huku kulikuwa na Dr Nico, Franco, John Bokello,African Fiesta, bendi za vijana kama Lipualipua , Belabela, Orchestra Kiam, Empire Bakuba, Veve, kila moja ilikuwa na aina yake ya muziki,wapi ilikuja kupatikana hiyo theory ya kupiga staili moja ni kitendawili. Tatizo la kudumaa kwa muziki wa Tanzania si kutokupiga staili moja.

Wednesday, April 7, 2010

Kwaya

Kwaya, kama neno lenyewe linavyoonekana ni neno la mapokeo likimaananisha aina ya utamaduni wa mapokeo. Ni neno lililotokana na neno 'choir'. Uimbaji wa kikundi cha watu. Muziki huu umepitia mabadiliko mengi yakitokana na sababu mbalimbali. Kwaya ilikuweko mwanzoni katika mashule na katika makanisa, baadae ikawa sehemu ya burudani hasa ikipata msukumo kutoka kwaya za Kusini mwa Afrika. Kwa wale waliokuwa maskauti wanakumbuka kuwa kwaya kilikuwa kipengele muhimu katika route march. Katika harakati za kutafuta uhuru kwaya zilichukua umuhimu sana katika kuhamasisha jamii. Lakini kama ilivyo kwenye muziki wa aina nyingine, muziki huu ulitokea kuwa na mabingwa wake. Si rahisi kumsahau Mzee Makongoro kama uliwahi kumsikia. Alikuwa na nini cha ziada? Mzee huyu alianzisha staili yake mwenyewe ya kwaya. Wakati kwaya nyingi zikiiga muziki wa Jiving wa South Africa yeye alikuja na kitu kipya ambacho bahati mbaya kimekosa mrithi. Karibuni tuliangalie hili swala la kwaya. Je tunaelekea wapi?

Taarab inakwenda wapi?



Muziki wa Taarab umekuwa na historia ya kukua na kubadilika kama muziki wa aina nyingine. Lakini nimejitahidi kusikiliza muziki huu wa sasa ambao bado unatangazwa kama muziki wa Taarabu naanza kupata taabu kukubali kama kweli kinachoendelea sasa ni Taarab. Upigaji wake sasa unaanza kusisitiza sana uchezaji, ni ukweli usiopingika kuwa sasa sebene ya Kikongo imeanza kutawala katika tungo mpya za taarabu. Uchezaji wake ambao unaleta utata katika maadili ya Watanzania wengi. Naomba wapenzi wa Taarab na wanaoona wanaifahamu Taarab hii ya sasa ya Alamba alamba watumegee nini hasa kinachoendelea? Juzi nimepata barua pepe kutoka Mtanzania mwenzangu mmoja alioko USA, akilalamika kuwa walitangaziwa kuwa kuna onyesho la Taarab na alipofika huko akakuta mwimbaji mmoja maarufu wa Taarab akiwa na CD yake na kufanya play back ta Taarab, kwa kifupi hakustahimili maana aliona kapunjwa mno. Haya ndugu zangu ukumbi ni wenu

Sunday, April 4, 2010

Hayawi hayawi.........





Hatimae inataka kuwa. Kama ambavyo wapenzi wengi wa Blog hii wamekuwa wanaomba,mwanga umeanza kuonekana kuwa itawezekana. Wenye afro zao wazitimue au wakachome tena nywele hahahaha, wenye raizon zao, wenye slimfit zao,(kama zitawatosha na hivyo vitambi), wenye superfly, pekos, maxi, midi, mini wazitoe vumbi maana wanamuziki wa zamani wameamua kuwa watafanya show moja kubwa ambapo wanamuziki wa toka enzi za buggy watapanda tena stejeni na kujikumbusha yalivyokuwa. Onyesho hilo ambalo pia litahusisha Madjs wa enzi hizo linategemea kufanyika mwezi July. Tayari Kilimanjaro bendi wametoa vyombo na eneo la mazoezi na wanamuziki kadhaa wamekwisha jitokeza kukubali kushiriki. Fuatilia katika blog hii upate kujua nani na nani watakuwepo. Mapato ya onyesho hilo yataenda kwenye huduma ambayo itatajwa baada ya siku chache.

Saturday, April 3, 2010

Teknolojia na ubora wa muziki

Nadhani kuna haja ya kuongelea swala la teknolojia katika muziki na hapa nitazungumzia teknoljia ya kurekodi. Nyimbo karibu zote ambazo husifika kama zilipendwa zilirekodiwa wakati wa kutumia kanda(tape), kwa teknolojia iliyoitwa 'two track recording' (pichani juu). Kwa teknolojia hii ilihitaji wanamuziki kuwa wazuri sana na fundi nae kuwa mzuri, kwani kama unarekodi wimbo bendi nzima lazima ipige kwa pamoja na akikosea mtu lazima kurudia wimbo wote tena kwa pamoja. Kwa bendi zilizorekodi RTD miaka hiyo zilipewa siku mbili za kurekodi kinachoitwa album siku hizi, yaani nyimbo sita au zaidi kwa kipindi cha siku mbili. Siku ya kwanza Bendi ilitakiwa kufika asubuhi kwenye studio za RTD, ambapo ilifanyika kazi ya kufunga vyombo vyote na kuvijaribu hapo fundi mitambo ndipo alipokuwa na kazi kubalance vyombo vyote viwe vinasikika inavyostahili. Mchana wa siku hiyo ililazimika bendi kurekodi nyimbo zote bila kukosea hata kama ni kumi. Siku ya pili ilitumika kurekodi kipindi cha klab raha leo show. Mwanamuziki yoyote wa siku hizi atakwambia haiwezekani kurekodi nyimbo sita kwa siku moja. Teknolojia ya sasa hutumia njia inayoitwa 'multi track recording', ilianza kwa kurekodi kwenye kanda maalumu tack 4,kisha zikawezekana 8,16,32 na kuendelea. Siku hizi kwa kutumia program za kompyuta ktu una uwezo wa kuwa na mamia ya tracks, hivyo basi hata bendi ya watu mia kila mtu akaweza kuja siku yake na kurekodi kipande chake , akakakirudia mpaka kikawa sawa, na ndio maana siku hizi kurekodi wimbo mmoja inaweza ikachukua hata mwezi na zaidi , kwa kurudia sehemu zenye makosa, kuzibadili kabisa na kadhalika, na siku hizi kuna hata teknolojia inayoweza kurekobisha sauti iliyoimbwa vibaya kwa maana hata kama hujui kuimba unaweza ukatengezwa mpaka uonekane unajua kuimba. Kama kawaida teknolojia mpya ina faida nyingi sana lakini mwisho wa yote faida hizi huonekana pale akiwepo fundi mitambo mzuri na msanii mzuri. Waliorekodi enzi za two track duniani kote husifia ule utamu ambao hupatikana wakipiga pamoja, ambao hupotea kama kazi itarekodiwa kila msanii akija kwa wakati wake.

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...