YOUTUBE PLAYLIST
Wednesday, April 28, 2010
DJ wa kwanza
The Dynamites
Midomo ya Bata
Lakini kwa ukweli kabisa vyombo vya upulizaji vina raha yake na utamu wake. Wapigaji wake hutengeneza step zao za kucheza na hupanga sauti za kupishana kati ya trumpet na saxaphone na huongeza raha sana katika muziki. Kwa sasa ni bendi chache kama vile DDC Mlimani Park, OTTU, Vijana Jazz, MAK Band, African Beat ndio wanaendeleza upigaji wa vyombo vya kupuliza.
Sunday, April 25, 2010
Akina mama nao- Asia Darwesh
Asia Darwesh ni miongoni mwa wanamuziki wanaoheshimika sana katika jamii ya wanamuziki na wapenzi wa muziki waliowahi kusikia au kufurahia kazi zake. Katika picha hapo juu Asia ambae alikuwa mpiga Keyboards wa kutumainiwa anaoneka picha ya juu akiwa na King Kiki enzi za Double O, na chini akiwa Mk Sound. Asia aliwahi pia kupigia Bicco Stars ambapo yeye pamoja na Andy Swebe na Mafumu Bilali na wenzao (waliihama MK sound), waliweza kuipandisha sana chati bendi hii. Hatimae Asia aliweza kumiliki bendi yake na alipatwa na umauti akiwa na bendi yake ambayo ilifanya vizuri sana huko Uarabuni.
Mzee Joseph Nyerere
Libeneke 2
Katika blog hii tuliwahi kuzungumzia chanzo halisi cha neno LIBENEKE. Nilieleza kuwa neno hili na hasa linapounganishwa na kusema 'endeleza libeneke', lilitokana na wimbo wa Butiama Jazz Band uliokuwa ukitaja majina ya wanamuziki wa bendi hiyo na kila mmoja akiambiwa aendeleze libeneke. Nimepata bahati ya kuongea na aliyekuwa Kiongozi na mpiga solo wa Butiama Jazz Band. Alikuwa na haya ya kusema. Butiama Jazz Band ilianzishwa mwaka 1971, makao yake makuu yalikuwa mtaa wa Kongo maeneo ya Kariakoo, Dar es Salaam, jirani kabisa na DDC. Ilianzishwa na asilimia kubwa ya wanamuziki kutoka Ifakara na ndio maana waliamua kuchukua jina la ngoma ya kwao na kuuita mtindo wa bendi yao Libeneke. Kiongozi wa bendi alikuwa Mzee Makelo na Katibu wa Bendi Mzee Mustafa Mkwega. Mzee Mkwega aliwahi kufanya kazi kwa Hayati Mwalimu Julius K Nyerere na hivyo alikuwa anawasiliana nae kwa karibu. Alikwenda kwa niaba ya wenzie na kumuomba Mwalimu awasaidie vyombo vya muziki, na aliwatuma wakalete Profoma invoice ya vyombo, walipoleta Mwalimu aliitia saini na ilitosha kwenda kupewa vyombo vipya dukani. Kama shukrani kwa Mwalimu waliita bendi yao Butiama Jazz Band. Na kuanzia hapo kila mwalimu alipoenda likizo ya mwaka Butiama bendi ilikwenda huko kutumbuiza wageni mbalimbali waliokuwa wanamfuata Mwalimu huko.
Saturday, April 24, 2010
Maquis Original
Baziano na Kasheba
Kwa wapenzi wa Fauvette na baadae Kasheba Group na Zaita Muzika, sauti ya Baziano si rahisi kusahaulika. Lakini kwa mapenzi yake Mungu, Baziano(wa kwanza kushoto) na mpiga gitaa wake Ndala Kasheba (wa pili kutoka kulia) hatunao tena duniani Mungu awalaze pema peponi. Pichani pia yupo Kasongo Mpinda (mwimbaji) wa pili kushoto, na Matei Joseph (mpiga drums).
Akina mama nao
Ni jambo lisilopingika kuwa akina mama wamekuwa sambamba na wanaume katika kuendeleza gurudumu la muziki wa nchi hii. Kumekuwa na tatizo la mtizamo na hivyo kufanya akina mama kutokuonekana sana katika fani hii kwa vile siyo siri imekua ikipigwa vita katika miaka yote. Pamoja na kuwa hakuna anaetamka hadharani kuwa wanamuziki ni wahuni, lakini taratibu na sheria zinaongea lugha ya kimya kuwa hivyo ndivyo. Nitoe mifano
1. Pamoja na kuwa kuna syllabus ya muziki kuanzia darasa la kwanza, kumekua hakuna jitihada kubwa ya kuhakikisha waalimu wanapatikana. Chuo cha Butimba ndio kimekua chanzo cha waalimu wa muziki lakini akishafika mashuleni hupangiwa vipindi vingine, na muziki huacha kama ulivyo.
2. Leo hii akiingia mwanamuziki kutoka nje ya nchi huhitajika kuwa na work permit, lakini kwa wanamuziki wa nyumbani hakuna taratibu zozote za ajira inayotambulika, hata wahudumu wa ndani wanatetewa bungeni lakini si wanamuziki. Angalia hata Waziri anaeshughulika na Vijana wa Tanzania na Kazi haoni soni kutoa ajira kwa vijana kutoka nje ya nchi yake katika fani ya muziki. Idadi ya wanawake katika muziki imekua kubwa sana kwa sasa ikilinganishwa na zamani lakini bado kuna wanawake wengi waliotikisa anga hizi zamani. Pichani ni muimbaji wa kike wa Afro 70 kutoka South Africa ambaye alisaidia sana kufanya muziki wa Afro kuwa na vionjo tofauti na bendi nyingine. Muimbaji huyu aliitwa Nini, na alirekodi nyimbo moja na Afro70, Mayele. Nini alikua na kaka yake aliyeitwa Vuli ambaye alipiga pia muziki hapa Tanzania na kutunga nyimbo ambayo bado inapiga na bendi kadhaa Tanzania'Lonely Child'. Vuli aliendelea na hatimaye kuwa manamuziki wa Lucky Dube.
Friday, April 23, 2010
Kilimanjaro Band 1
Bendi za Mkoa wa Morogoro
Kati ya mikoa iliyokuwa na Bendi nyingi, sijui kama ulikuweko ulioushinda mkoa wa Morogoro. Ilikuwa kila wilaya ina bendi. Baadhi ya bendi ninazozikumbuka ni Morogoro Jazz, Super Volcano, Cuban Marimba Band, Les Cuban, TK Limpopo, Kilosa Jazz (alikotokea Abel Balthazar), Ifakara Jazz, Sukari Jazz, Imalinyi Jazz, Mahenge Jazz, Kwiro Jazz., Mzinga Troupe. Na hata wale wakali wa wakati huo na ule wimbo wao enye maneno,
Waache waseme watachoka wao,
Mzee Makelo endeleza libeneke,
Waache waseme watachoka wao,
mtindo libeneke unatia fora
Hapa naongelea Butiama Jazz Band, iliyokuwa inapiga muziki kwa mtindo wao uliotokana na ngoma ya kwao Libeneke,wao ni wa Ifakara hivyo nao ni bendi ya mkoa wa Morogoro japo jina lilitokana na mahala alipozaliwa Baba wa Taifa.(Mzee Mkwega aliyekuwa mwenye bendi alikuwa kada mzuri sana wa CCM, hata kifo chake kilimkuta akiwa mtumishi wa CCM ofisi ndogo Dar es Salaam).
Mpaka leo ukienda Ifakara wakati wa msimu wa mavuno ikiwa kuna sherehe za jumla kama vile kipaimara, ndo utajua wanavyopenda ngoma. Kuna vikundi vingi vya ngoma ya Sangula na kila kikundi kimejipa jina la Bendi, hivyo utakuta mabango yakitangaza Tancut Almasi, Msondo, Super Volcano, na kila nyumba yenye sherehe huandaa kundi lake ni raha tupu hapo
Tuesday, April 20, 2010
Those were the days
The Rifters 2
Shaaban Yohana Wanted
Nilikutana na Shaaban Yohana kwa mara ya kwanza katika bendi ya Tancut, ambapo gitaa lake la solo husikika katika nyimbo zote zilizokuwemo katika album za kwanza za bendi ile. Alipiga gitaa katika nyimbo zifuatazo:-
Nimemkaribisha nyoka
Kashasha
Tutasele
Mtaulage
Masafa Marefu
Butinini. Lakini aliniacha Tancut na kwenda Vijana Jazz huko tukakutana tena ambako solo lake linakumbukwa katika nyimbo nyingi kama vile Aza, Ogopa Tapeli,Thereza, Shoga, Malaine nk. Aliacha bendi ya Vijana na kujiunga na Ngorongoro Heroes akatesa sana huko, kisha akatimkia Botswana ambako yuko mpaka leo, muda mwingi akiutumia kama mwanamuziki wa studio.
The Jets
Monday, April 19, 2010
Flaming Stars
Afro70 1974
Dar Es Salaam Jazz-majini wa bahari
Tanzania All Stars
Ukitaka kujua umahiri wa wanamuziki enzi hizo ni vizuri ukazisikiliza nyimbo za Tanzania All Stars. Karibuni nitazitundika wote tuzisikilize, katika wimbo wa Samora, Zahir Ally Zoro aliimba Kireno, Jabali aliimba Kiarabu, Aziz Varda Kihindi we bwana wee. Haya tujikumbushe kwa kuwataja majina wote unaowaona hapo juu.
Usimkwae mtu likwae chua
Chakachua ndio ulikuwa mtindo wao, walikuwa na mpiga solo ambae wapiga magitaa wote waliomjua wanamheshimu kwa upigaji wake. Kuna mwanamuziki Mtanzania aliyeko Japan aliwahi kunambia kuna siku aliwahi kumsikilizisha muziki wa Chakachua mpiga gitaa mahiri George Benson, George Benson alisikitika sana kusikia aliepiga gitaa vile ameshafariki kwani alitaka wakutane watengeneza kitu cha pamoja, huyu si mwingine bali ni Michael Vicent. Na bendi ilikuwa Urafiki Jazz iliyokuwa chini ya Kiwanda cha nguo cha Urafiki Dar Es Salaam
Sunday, April 18, 2010
TP OK Jazz Dar es Salaam 1974
Hunaaaaaaa mwana hunaaaaaa
.
Enzi za Buggy
Leo ni Jumapili ngoja nilete picha ambayo kwa vyovyote ilipigwa Jumapili , maana ndio ilikuwa siku ya Buggy, lile dansi la mchana lililokuwa linaanza saa 7 au nane na kuisha saa kumi na mbili jioni. Unaona mavazi ya siku hizo?, si muda mrefu baada yalipigwa marufuku , na kukaweko na posters kila mahala zikionyesha nguo gani za kuvaa. Vijana wa TANU Youth League walikuwa wakitembea na mikasi na kuchana nguo zilizoonekana hazifai. Loh, Hawa Rifters walikuwa kati ya makundi mengi ya wanamuziki vijana waliokuwa wakipiga muziki wa soul, hapa bwana nyimbo za Otis Redding, Kipofu Clarence Carter, Wilson Pickett , James Brown,Sam and Dave, Isaac Hayes ilikuwa mwendo mdundo
Saturday, April 17, 2010
Msondo Ngoma
Msondo ngoma wana kila haki ya kujiiita Baba ya muziki. Bendi hii ilianza mwaka 1964,kama NUTA Jazz na imekuwa na mtindo wa Msondo miaka yote na imekuwa juu miaka yote. Nani anaweza kujipima na Msondo. Pichani Mzee Abel Balthazal akiwa anapiga gitaa, Mzee Mnenge kwenye saxaphone, jamani majina ya wengine tafadhali.
Orchestra Fuka Fuka
Thursday, April 15, 2010
Tancut almasi Orchestra enzi hizo
Tancut Almasi Orchestra, hapa wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma. Bahati mbaya Ray, Hashim, Kalala, Zacharia wameshatangulia mbele ya haki. Kuna utata kuhusu alipo Mohamed Shaweji. Uniform zinapendeza
(Kutoka kushoto.. Ray Mlangwa, Bakari Buhero, Hashim Kasanga, Mohamed Shaweji, John Kitime, Kalala Mbwebwe, Kawelee mutimwana,Abdul Mngatwa, Kibambe Ramadhan, Zacharia daniel, Akuliake 'King Maluu' Salehe)
Wanamuziki kutoka Kongo II
Katika makala za mwanzo mwazo za blog hii, kuna wadau walitaja nyimbo za bendi ya Nova Success ambazo walizipenda. Nimeona kuwakumbusha zaidi niiweke picha hapa ya Bendi hiyo iliyokuwa ikipiga Top Life Bar Kinondoni. Baadhi ya nyimbo zake ni Maeliza ,Sizeline na Cherie Jamila. Kiongozi wao aliitwa Papa Micky. Mara ya mwisho kusikia kuhusu bendi hii ni pale walipoamua kuelekea Msumbiji
Vijana Jazz ilikotokea
Mwaka 1971 Umoja wa Vijana wa TANU uliamua kuanzisha Bendi na kumpa jukumu hilo mwanamuziki John Ondolo Chacha. Ili kutaengeneza bendi, Marehemu Mzee Ondolo aliweza kuwashawishi vijana wa bendi ya Zezemba wakajiunga nae lakini hawakukaa nae muda mrefu kwani walikuwa ni waajiriwa wa kiwanda cha nguo cha Urafiki, hivyo akalazimika kujenga tena Bendi na kwenda hadi Bagamoyo alipoikuta bendi ya Kizibo na akapata wapigaji kumi. 1972 wapigaji wengine tena wakaacha bendi, hivyo akalazimika kutafuta wengine na kikubwa ni kuwa alimpata mpiga solo Hassani Dalali ambaye aliweza kuwatafuta wenzie. Bendi ilipelekwa JKT mwaka 1973, wakati huu tayari ilishampata mtunzi na mwimbaji kutoka TK Limpopo ya Juma Kilaza, kwa jina Hemed Maneti, na baada ya muda kidogo iliweza kumpata Hamis Fadhili kutoka Jamhuri Jazz.
1974 walienda Nairobi na kurekodi nyimbo ambazo ziliaweka msingi wa bendi hiyo. Baadhi ya nyimbo hizo ni Magdalena, Niliruka Ukuta. Mtindo wa bendi wakati huo ulikuwa Kokakoka Balaa
Belesa Kakere
Wednesday, April 14, 2010
Vyombo vya habari
Katika kusoma magazeti ya zamani,(nitazitoa baadhi ya makala hapa), imeniijia kuwa tunatatizo kubwa la uandishi na utoaji wa habari za shughuli za muziki. Makala za muziki za siku hizi, nyingi ni kuhusu nani kapagawisha wapi au mcheza show gani alikaa vibaya au ana uhusiano na nani. Kimsingi ni kama vile taarifa kuhusu muziki ni gossips zinazoendelea katika uwanda wa wanamuziki. Hakuna taarifa ya taaluma katika muziki huo. Unaweza kupata taarifa nzuri kuhusu Beyonce lakini ukakosa taarifa kuhusu Anna Mwaole ambaye yuko jijini Dar es Salaam. hili liko hata kwenye vituo vya redio vya wilayani, ambako huko nako watangazaji wengi wanaiga kuanzia uongeaji, mpangilio wa vipindi, maadili na kadhalika kutoka redio maarufu za Dar es Salaam.
Huko wilayani nako wanadai hawana taarifa za wasanii wa hapo wilayani kwa kuwa wasanii hawaleti taarifa zao, lakini mtu huyohuyo atakaa masaa kadhaa kwenye internet akitafuta taarifa zote kuhusu msanii wa nje. Napata taabu kujua aina ya mafunzo wanayopata waandishi katika vyuo vya uandishi siku hizi. Na tena nakumbuka kuwa wandishi wengi wa zamani hawakupitia vyuo kama vilivyo siku hizi kwanini hakuna ubora wa uandishi sasa? Kwanini tunakosa ufanisi zaidi siku hizi ? au ni mimi ndio mwenye kuona kuna tatizo ambalo halipo? katika makala nitakazoziposti hapa ambazo ni za miaka ya sabini naona kuna maelezo ambayo nayakosa katika uandishi wa siku hizi.
Orchestra Santa Fe
Kati ya maswali amabayo yamewahi kuulizwa humu ni kuhusu bendi hii Orchestra Santa Fe. Hii ilikuwa mwanzo ni bendi yenye asilimia kubwa ya wanamuziki Wakongo. Mkuu wa 'Libeneke' aliwahi kuuliza kama ndio ilikuwa Bendi ya kwanza ya Kikongo, ninauhakika haikuwa bendi ya kwanza ya Kikongo. Wenye taarifa zaidi kuhusu Bendi hii karibuni. Bendi hii ilikuwa ikipiga pale Gateways Mnazi Mmoja maeneo ambayo kuna wakati yalikuwa maeneo muhimu katika shughuli za starehe jijini Dar es Salaam.
Tuesday, April 13, 2010
Sokomokoooooooooo
Thursday, April 8, 2010
Muziki wa staili moja
Miaka michache iliyopita kulianza hadithi moja ambayo vyombo vya habari vikaishikia bango, na baadae wanamuziki kadhaa nao wakashika bango nakutoa ushauri nasaha wa tatizo hilo. Tatizo hilo lililkuwa kwanini muziki wa bendi Tanzania hauwi maarufu. Kwa utafiti ambao washika bango waliufanya wakatangaza kuwa Tanzania tuna tatizo la kuwa tunapiga aina nyingi mno za muziki ndio maana haujulikani. Kwa hiyo wataalamu hawa wakiwa wanalinganisha na muziki wa Kikongo wakasema Mkongo mmoja akianzisha Kwasakwasa wote wanapiga Kwasakwasa , ikija Kibinda Nkoy wote wanapiga hivyo hivyo , kwa hiyo nasi tuwe na staili moja, tena ikapewa jina Achimenengule. Utafiti huu ni wa ajabu sana, tuanze na nchi yetu ina makabila zaidi ya 110,yenye mila mbalimbali na muziki mbalimbali, inashangaza kujaribu kufikiri wote hawa wapende aina moja tu ya muziki. Huko Kongo ambako kulitolewa mfano hata wakati wa kile kipindi kinachoitwa the Golden Age of Congolese Music, ndipo haswa upigaji wa aina mbalimbali ulipokuwepo. Huku kulikuwa na Dr Nico, Franco, John Bokello,African Fiesta, bendi za vijana kama Lipualipua , Belabela, Orchestra Kiam, Empire Bakuba, Veve, kila moja ilikuwa na aina yake ya muziki,wapi ilikuja kupatikana hiyo theory ya kupiga staili moja ni kitendawili. Tatizo la kudumaa kwa muziki wa Tanzania si kutokupiga staili moja.
Wednesday, April 7, 2010
Kwaya
Taarab inakwenda wapi?
Muziki wa Taarab umekuwa na historia ya kukua na kubadilika kama muziki wa aina nyingine. Lakini nimejitahidi kusikiliza muziki huu wa sasa ambao bado unatangazwa kama muziki wa Taarabu naanza kupata taabu kukubali kama kweli kinachoendelea sasa ni Taarab. Upigaji wake sasa unaanza kusisitiza sana uchezaji, ni ukweli usiopingika kuwa sasa sebene ya Kikongo imeanza kutawala katika tungo mpya za taarabu. Uchezaji wake ambao unaleta utata katika maadili ya Watanzania wengi. Naomba wapenzi wa Taarab na wanaoona wanaifahamu Taarab hii ya sasa ya Alamba alamba watumegee nini hasa kinachoendelea? Juzi nimepata barua pepe kutoka Mtanzania mwenzangu mmoja alioko USA, akilalamika kuwa walitangaziwa kuwa kuna onyesho la Taarab na alipofika huko akakuta mwimbaji mmoja maarufu wa Taarab akiwa na CD yake na kufanya play back ta Taarab, kwa kifupi hakustahimili maana aliona kapunjwa mno. Haya ndugu zangu ukumbi ni wenu
Sunday, April 4, 2010
Hayawi hayawi.........
Hatimae inataka kuwa. Kama ambavyo wapenzi wengi wa Blog hii wamekuwa wanaomba,mwanga umeanza kuonekana kuwa itawezekana. Wenye afro zao wazitimue au wakachome tena nywele hahahaha, wenye raizon zao, wenye slimfit zao,(kama zitawatosha na hivyo vitambi), wenye superfly, pekos, maxi, midi, mini wazitoe vumbi maana wanamuziki wa zamani wameamua kuwa watafanya show moja kubwa ambapo wanamuziki wa toka enzi za buggy watapanda tena stejeni na kujikumbusha yalivyokuwa. Onyesho hilo ambalo pia litahusisha Madjs wa enzi hizo linategemea kufanyika mwezi July. Tayari Kilimanjaro bendi wametoa vyombo na eneo la mazoezi na wanamuziki kadhaa wamekwisha jitokeza kukubali kushiriki. Fuatilia katika blog hii upate kujua nani na nani watakuwepo. Mapato ya onyesho hilo yataenda kwenye huduma ambayo itatajwa baada ya siku chache.
Saturday, April 3, 2010
Teknolojia na ubora wa muziki
SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.
TANCUT ALMASI ORCHESTRA wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...
-
Hawa ndio The Jets (1972), ambao baadae walikuja kuwa STC Jazz, ambayo ndio chanzo cha Biashara Jazz. Waliopo hapa wa kwanza Belino, Raphael...
-
Mara baada ya kutoa ule wimbo maarufu wa Kisambaa Shakaza, Eddy Sheggy mwenyewe na Wasambaa wengine wakaanza kuitwa Shakaza. Eddy Sheggy ali...
-
Suleiman Mbwembwe, aliyekuwa anajulikana pia kwa jina la Electronic Voice, alikuwa mwimbaji na mtunzi aliyeng'ara katika enzi zake. Aki...