YOUTUBE PLAYLIST

Showing posts with label Maquis. Show all posts
Showing posts with label Maquis. Show all posts

Monday, August 22, 2022

KUWA MWANAMUZIKI ZAMANI HAIKUWA LELEMAMA

 

Vijana Jazz Band tukielekea Ifakara

Kuwa mwanamuziki katika miaka ya tisini na kurudi nyuma haikuwa lelemama, ilikuwa kazi ngumu, iliyokuwa yakujitolea haswa. Kati mambo magumu miaka hiyo ilikuwa kusafiri kwenda kufanya maonyesho. Katika zama hizi mwanamuziki anapata mualiko, anatajiwa na fungu atakalolipwa, anachagua aina ya hoteli ya kulala na hata usafiri kama ni wa ndege au gari la abiria  au hata gari binafsi, fursa hizo hazikuweko miaka hiyo.
Kwanza kabisa kulikuwa na taratibu za kiserikali, ili bendi au kikundi cha muziki kitoke katika mkoa ambako ni masikani taratibu zilikuwa ngumu. Kikundi kilianza kwa kuandika barua kwa Afisa Utamaduni wa mkoa kuomba ruksa ya kutoka nje ya mkoa. Afisa Utamaduni akisha kutoa kibali kile, muwakilishi wa bendi hutangulia kwenda kuwakilisha kibali kwa Afisa Utamaduni wa mkoa ambao kundi linaenda ili kupata kibali cha kufanya kazi katika mkoa husika, Afisa Utamaduni Mkoa akisha toa kibali kuingia mkoa wake, ndipo nakala ya kibali hupelekwa kwa Afisa Utamaduni wa Wilaya ili nae atoe kibali cha kuruhusu kundi kufanya maonyesho katika wilaya yake. Kutokana na uchache wa magazeti, vikundi vingi vilianza safari bila matangazo yoyote, kwani kuna wilaya nyingine, magazeti hayakuwa yanafika kabisa au magazeti yalifika machache na hata hayo yaliweza kuchelewa hata siku nne.  Mwakilishi wa kikundi akishafika kwenye mji ambao bendi au kundi lingefanya maonyesho, alishirikiana na Afisa Utamaduni kupata kumbi na kufanya booking ya mahala pa kulala. Matangazo ilikuwa ni karatasi za kuandika kwa mkono na kisha kubandika katika kuta na nguzo mbalimbali. Baada ya hapo alitafutwa mwenyeji ambaye ni mtangazaji naye alipita katika mitaa mbalimbali akitangaza kupitia kipaza sauti cha mkononi. Nakumbuka mwaka mmoja mapema miaka ya 80, nikiwa na Orchestra Mambo Bado, tulifika Mpanda na kuelekezwa kuwa mtu maalumu ambaye hutangaza mambo yote pale, alikuwa bwana mmoja aliyepewa jina la utani la Mshindo Mkeyenge. Huyu alikuwa akipita mitaa mbalimbali na ngoma yake na hiyo hugonga  ili watu wamsikilize na ndipo hapo hutangaza kuwa kuna dansi linakuja na litakuwa wapi na kiingilio chake.

Usafiri wa bendi ulikuwa wa basi za abiria na mara nyingi malori ambamo wanamuziki walijazana humo wakiwa na vyombo vyao. Kati ya safari za aina hii nilizowahi kusafiri kwa roli ni toka Mbeya hadi Chunya na kurudi, kutoka Mtwara na kuzunguka miji ya kusini mingi kama Masasi , Nachingwea, Lindi kutumia lori la aina ya Isuzu Long base. Na nikiwa na bendi ya Tancut kwa ujumla usafiri wetu ulikuwa ni loti aina ya ‘canter’, humo tulizunguka miji kuanzia Makambako, Njombe, Songea, Mbeya, Tunduma na miji mingine mingi, tuliwahi pia kuzunguka miji mingi kanda ya ziwa kutumia  lori aina ya Leylan Albion. Huo ndio ulikuwa usafiri wa masupastaa wa mika hiyo.

 Malazi kwa kawaida hayakuwa ya kifahari, kwa kawaida vyumba vilivyokodishwa vilikuwa ni dabo ili kupunguza gharama, na gesti zenyewe zilikuwa ni zile ambazo gharama zake zikuwa chini. Kulala njaa halikuwa jambo la ajabu, hasa mkipiga dansi na kukosa wateja, hapo ndipo mnaweza kujikuta mmelala ukumbini ili pesa itoshe gharama za kuwasafirisha kwenda mji unaofuata. Miji mingi haikuwa na umeme hivyo bendi nyingine zilikuwa zikizunguka na jenereta, au kukodi kwa ajili ya kila onyesho.

Kama ilivyo katika biashara nyingine uongo nao ulikuwa mwingi sana, utasikia , ‘Bwana bendi ikienda Nyarugusu kule fedha nje nje, wachimba migodi wana pesa sana lazima mtarudi na pesa za kutosha kununua vyombo vipya’ . Hapo harakati za kwenda Nyarugusu zitaanza. Miaka hiyo Nyarugusu ilikuwa mji mmoja maarufu kwa wachimba dhahabu wadogowadogo, lakini sijawahi kuona bendi ikipata fedha za ajabu baada ya kwenda Nyarugusu. Kuna wakati  Bendi tatu tulikutana Mwanza kila moja ikiwa ina mpango wa kwenda Nyarugusu. Vijana Jazz Band,  Maquis  na Ngorongoro Heroes wote tukawa Mwanza. Hali ilikuwa mbaya sana kwa Maquis ambayo ilikuwa safarini huku  kwa zaidi ya miezi mitatu, ilifikia kiasi cha wanamuziki kuanza kurudi Dar es Salam mmoja mmoja.
Lakini ilikuwa ni baada ya safari hii walipojipanga upya na kurekodi vile vibao vyao vikali, Makumbele, Tipwa tipwa na Ngalula na kurudisha heshima yao mjini.

Kifupi hayo ndiyo yalikuwa maisha ya mwanamuziki wakati huo, ujana ulisababisha watu wafurahie kuzunguka huko na huku nchi nzima, wakipata mikasa na kuitungia nyimbo ambazo nyingine bado zinapendwa mpaka leo. Hakika sitaweza kukumbuka sehemu zote ambazo binafsi nimewahi kupiga muziki, kwani pamoja na miji mikubwa tulikuwa pia tunapiga katika vijiji ili mradi tupate pesa za kuendelea na safari.  Najaribu kupata picha vijana wa zama hizi kukubali kusafiri kwa lori kwenye barabara zilizokuwa duni na za vumbi. Nina uhakika madansi mengi yasingelia kwa supastaa kugom kupiga.

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...