YOUTUBE PLAYLIST

Thursday, March 9, 2023

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

 

TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma


 Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika maisha yangu ya muziki,  hakukuwa na wilaya hata moja, kati ya wilaya  zilizokuweko Tanzania Bara kati ya mwaka 1982 na 1992 ambayo sikufika na kufanya onyesho la muziki.
Leo nimekumbuka safari ya kuzunguka Kanda ya Ziwa  nikiwa mmoja wa wanamuziki wa Tancut Almasi Orchestra iliyokuwa na masikani yake Iringa, ikimilikiwa na wafanyakazi wa kampuni ya Tanzania Diamond Cutting Company (kiwanda cha kuchonga almasi).
 Wakala wa mfanya biashara maarufu wa Mwanza alikuja Iringa kufanya mpango ili bendi ikafanye ziara Kanda ya Ziwa. Bendi ilikuwa tayari kwa ziara hiyo lakini ilikuwa na mkataba wa kwenda kufanya onyesho moja kwenye mahafali ya Chuo cha IDM Morogoro, baada ya hapo bendi ingeweza kuelekea Mwanza kuanza ziara ya Kanda ya Ziwa. 
Baada ya onyesho la IDM, usiku uleule tulienda kituo cha treni Morogoro kujaribu kupata nafasi katika treni iliyokuwa iktoka Dar es Salaam na kuelekea Mwanza, bahati mbaya tulichelewa treni. Wakala akisaidiana na viongozi wa bendi waliweza kutafuta ‘Fuso’ usiku uleule, wanamuziki na vyombo tukajazana kwenye ‘Fuso’. Nia ilikuwa tusafiri usiku ule mpaka Dodoma na kuiwahi treni iliyotupita Morogoro. Hilo lilishindikana kwani uzito wa vyombo na watu ulisababisha ‘Fuso’ yetu ipate pancha mara nne, hivyo badala ya kuingia Dodoma alfajiri, tuliingia Dodoma saa nane mchana. Mara baada ya kufika Dodoma, wanamuziki walitafutiwa sehemu ya kula na kulala kwa siku hiyo na pia  kutafutiwa tiketi za kwenda Mwanza na treni kesho yake. Mimi na Katibu Msaidizi wa bendi tukapewa jukumu la kuhakikisha kuwa tunafanya mipango ya kusafirisha vyombo vya muziki. Tulienda kituo cha treni na kuweza kukamilisha taratibu zote za kusafirisha vyombo kutumia mabehewa ya mizigo, vyombo viliingizwa katika behewa moja tayari kwa safari. Uongozi wa Shirika la reli ukatuhakikishia kuwa vyombo vitasafirishwa na treni ya mizigo siku ileile.  Kwa vile treni za mizigo hazikuwa na ratiba maalumu tulilazimika kuweko palepale ili tuhakikishe vyombo vyetu kweli vimeanza safari. Treni za mizigo  kadhaa zilifika na kuondoka na mabehewa kadhaa ya mizigo yaliyokuwepo pale yaliunganishwa na kuondoka, lakini behewa letu likawa haliunganishwi, tulipouliza sababu tukaambiwa kuwa kulikuwa na tatizo la mipira ya breki. Tulishinda pale mchana ule na usiku ukaingia tukiwa pale pale na tukakesha pale tukiumwa na mbu na kuteswa na baridi kali. Kesho yake wanamuziki wenzetu walipata nafasi katika treni la abiria na kuanza safari ya kuelekea Mwanza, sisi wawili na behewa letu la vyombo tukaingia siku ya pili pale kituoni. Hatimae mtu mmoja akatushtua kuwa tusipoangalia tutafikisha hata wiki moja pale, tumtafute muhusika na kumpa fedha kidogo mipira breki itapatikana, tukafanya hivyo na mipira kweli ikapatikana kimiujiza. Behewa letu liliunganishwa kwenye treni ya mizigo na safari ikaanza. Kwa vile ilikuwa ni treni ya mizigo, mimi na mwenzangu tukaingia kwenye kichwa cha treni, nauli tukamlipa dreva wa treni, kwa mara ya kwanza nikaweza kuona jinsi dreva wa treni anavyoendesha treni. Safari ilikuwa nzuri, ila kila tulipokaribia katika kituo, tulilazimika kuingia sehemu ya injini kujificha, kwani dreva hakuwa anaruhusiwa kubeba abiria. Kwa kweli kule ndani kwenye sehemu ya injini kunatisha mno. Tuliingia Mwanza kama saa tano mchana na siku hiyo ilikuwa siku ya sikukuu ya Iddi.  Bendi ilikuwa imeshatangaza kuwa ingefanya onyesho la mchana katika Uwanja wa Kirumba na usiku bendi ingepiga ukumbi wa Shinyanga Hotel. Onyesho la Kirumba lilifanyika vizuri likaisha saa 12 jioni, vyombo vikahamishwa na kupelekwa  kwenye ukumbi wa Shinyanga Hotel ambako onyesho jingine lilianza saa tatu usiku mpaka usiku wa manane. Tulipoanza tu onyesho, akaonekana mtu mmoja anapiga picha za video, onyesho likasimama na kukaweko ugomvi mkubwa kumzuia mpiga video kwani alikuwa hajatuomba ruksa,  hatimae aliruhusiwa kutupiga video baada ya kutulipa shilingi alfu kumi na tatu. Wanamuziki tukagawana shilingi mia tano kila mmoja na .

Baada ya kufanya maonyesho kadhaa  katika kumbi tofauti pale Mwanza ukiwemo ukumbi wa Polisi na ukumbi maarufu  wa Pamba House, bendi ikaendea kufanya onyesho Tarime. Bendi ilisafirishwa na basi la tajiri aliyekodi bendi. Onyesho la Tarime halikuwa na mafanikio sana,  mara baada ya kumaliza onyesho Tarime ilianza safari ya kurudi Mwanza. Baadhi ya wanamuziki walikuwa wamejenga urafiki na wasaidizi wa tajiri aliyekodi bendi, wasaidizi hao wakawaeleza rafiki zao kuwa mpango umesukwa  wa kuitelekeza bendi stendi kuu ya Mwanza, mara baada ya kufika Mwanza wakala angetangaza kuwa basi linaenda ‘service’ hivyo watu na mizigo yote ishushwe. Baada ya hapo basi lingeondoka na lisingerudi tena. Baada ya taarifa hii kufahamika, uongozi wa bendi ukapanga mkakati, kwanza  wanamuziki wangegoma kushuka kwenye basi, na kwa kuwa mkataba ulimtaka wakala kuirudisha bendi Iringa baada ya ziara, bendi ilikuwa tayari kuachana na mkataba kama  wanamuziki wangepelekwa kwenye mgodi wa almasi wa Mwadui. Mgodi wa Mwadui ulikuwa chini ya shirika la STAMICO kama ilivyokuwa kampuni ya Diamond Cutting Company, tulijua kuwa kama tungefika kule ingekuwa kama kufika nyumbani.

Mimi nikaambiwa nishuke pale Mwanza kutafuta mfadhili ambaye angeweza kutukopesha shilingi alfu arobaini, fedha hizi ingekuwa ni mtaji tosha wa bendi kuweza kurudi Iringa kama mambo yasingefana Mwadui. Kweli tulipofika stendi Mwanza,  wakala akatangaza kuwa watu wote na vifaa vyote vishushwe ili basi liende service tayari kwa safari ya kurudi Iringa. Akajibiwa kuwa hakuna haja ya kushusha vyombo kwani havitaingilia service, ugomvi mkubwa ukazuka, hatimae ndipo wakala akaambiwa akitaka aachane nasi basi basi lituache Mwadui, alikubali na basi likaelekea Mwadui……Itaendelea,

No comments:

Post a Comment

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...