YOUTUBE PLAYLIST

Thursday, March 9, 2023

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

 

TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma


 Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika maisha yangu ya muziki,  hakukuwa na wilaya hata moja, kati ya wilaya  zilizokuweko Tanzania Bara kati ya mwaka 1982 na 1992 ambayo sikufika na kufanya onyesho la muziki.
Leo nimekumbuka safari ya kuzunguka Kanda ya Ziwa  nikiwa mmoja wa wanamuziki wa Tancut Almasi Orchestra iliyokuwa na masikani yake Iringa, ikimilikiwa na wafanyakazi wa kampuni ya Tanzania Diamond Cutting Company (kiwanda cha kuchonga almasi).
 Wakala wa mfanya biashara maarufu wa Mwanza alikuja Iringa kufanya mpango ili bendi ikafanye ziara Kanda ya Ziwa. Bendi ilikuwa tayari kwa ziara hiyo lakini ilikuwa na mkataba wa kwenda kufanya onyesho moja kwenye mahafali ya Chuo cha IDM Morogoro, baada ya hapo bendi ingeweza kuelekea Mwanza kuanza ziara ya Kanda ya Ziwa. 
Baada ya onyesho la IDM, usiku uleule tulienda kituo cha treni Morogoro kujaribu kupata nafasi katika treni iliyokuwa iktoka Dar es Salaam na kuelekea Mwanza, bahati mbaya tulichelewa treni. Wakala akisaidiana na viongozi wa bendi waliweza kutafuta ‘Fuso’ usiku uleule, wanamuziki na vyombo tukajazana kwenye ‘Fuso’. Nia ilikuwa tusafiri usiku ule mpaka Dodoma na kuiwahi treni iliyotupita Morogoro. Hilo lilishindikana kwani uzito wa vyombo na watu ulisababisha ‘Fuso’ yetu ipate pancha mara nne, hivyo badala ya kuingia Dodoma alfajiri, tuliingia Dodoma saa nane mchana. Mara baada ya kufika Dodoma, wanamuziki walitafutiwa sehemu ya kula na kulala kwa siku hiyo na pia  kutafutiwa tiketi za kwenda Mwanza na treni kesho yake. Mimi na Katibu Msaidizi wa bendi tukapewa jukumu la kuhakikisha kuwa tunafanya mipango ya kusafirisha vyombo vya muziki. Tulienda kituo cha treni na kuweza kukamilisha taratibu zote za kusafirisha vyombo kutumia mabehewa ya mizigo, vyombo viliingizwa katika behewa moja tayari kwa safari. Uongozi wa Shirika la reli ukatuhakikishia kuwa vyombo vitasafirishwa na treni ya mizigo siku ileile.  Kwa vile treni za mizigo hazikuwa na ratiba maalumu tulilazimika kuweko palepale ili tuhakikishe vyombo vyetu kweli vimeanza safari. Treni za mizigo  kadhaa zilifika na kuondoka na mabehewa kadhaa ya mizigo yaliyokuwepo pale yaliunganishwa na kuondoka, lakini behewa letu likawa haliunganishwi, tulipouliza sababu tukaambiwa kuwa kulikuwa na tatizo la mipira ya breki. Tulishinda pale mchana ule na usiku ukaingia tukiwa pale pale na tukakesha pale tukiumwa na mbu na kuteswa na baridi kali. Kesho yake wanamuziki wenzetu walipata nafasi katika treni la abiria na kuanza safari ya kuelekea Mwanza, sisi wawili na behewa letu la vyombo tukaingia siku ya pili pale kituoni. Hatimae mtu mmoja akatushtua kuwa tusipoangalia tutafikisha hata wiki moja pale, tumtafute muhusika na kumpa fedha kidogo mipira breki itapatikana, tukafanya hivyo na mipira kweli ikapatikana kimiujiza. Behewa letu liliunganishwa kwenye treni ya mizigo na safari ikaanza. Kwa vile ilikuwa ni treni ya mizigo, mimi na mwenzangu tukaingia kwenye kichwa cha treni, nauli tukamlipa dreva wa treni, kwa mara ya kwanza nikaweza kuona jinsi dreva wa treni anavyoendesha treni. Safari ilikuwa nzuri, ila kila tulipokaribia katika kituo, tulilazimika kuingia sehemu ya injini kujificha, kwani dreva hakuwa anaruhusiwa kubeba abiria. Kwa kweli kule ndani kwenye sehemu ya injini kunatisha mno. Tuliingia Mwanza kama saa tano mchana na siku hiyo ilikuwa siku ya sikukuu ya Iddi.  Bendi ilikuwa imeshatangaza kuwa ingefanya onyesho la mchana katika Uwanja wa Kirumba na usiku bendi ingepiga ukumbi wa Shinyanga Hotel. Onyesho la Kirumba lilifanyika vizuri likaisha saa 12 jioni, vyombo vikahamishwa na kupelekwa  kwenye ukumbi wa Shinyanga Hotel ambako onyesho jingine lilianza saa tatu usiku mpaka usiku wa manane. Tulipoanza tu onyesho, akaonekana mtu mmoja anapiga picha za video, onyesho likasimama na kukaweko ugomvi mkubwa kumzuia mpiga video kwani alikuwa hajatuomba ruksa,  hatimae aliruhusiwa kutupiga video baada ya kutulipa shilingi alfu kumi na tatu. Wanamuziki tukagawana shilingi mia tano kila mmoja na .

Baada ya kufanya maonyesho kadhaa  katika kumbi tofauti pale Mwanza ukiwemo ukumbi wa Polisi na ukumbi maarufu  wa Pamba House, bendi ikaendea kufanya onyesho Tarime. Bendi ilisafirishwa na basi la tajiri aliyekodi bendi. Onyesho la Tarime halikuwa na mafanikio sana,  mara baada ya kumaliza onyesho Tarime ilianza safari ya kurudi Mwanza. Baadhi ya wanamuziki walikuwa wamejenga urafiki na wasaidizi wa tajiri aliyekodi bendi, wasaidizi hao wakawaeleza rafiki zao kuwa mpango umesukwa  wa kuitelekeza bendi stendi kuu ya Mwanza, mara baada ya kufika Mwanza wakala angetangaza kuwa basi linaenda ‘service’ hivyo watu na mizigo yote ishushwe. Baada ya hapo basi lingeondoka na lisingerudi tena. Baada ya taarifa hii kufahamika, uongozi wa bendi ukapanga mkakati, kwanza  wanamuziki wangegoma kushuka kwenye basi, na kwa kuwa mkataba ulimtaka wakala kuirudisha bendi Iringa baada ya ziara, bendi ilikuwa tayari kuachana na mkataba kama  wanamuziki wangepelekwa kwenye mgodi wa almasi wa Mwadui. Mgodi wa Mwadui ulikuwa chini ya shirika la STAMICO kama ilivyokuwa kampuni ya Diamond Cutting Company, tulijua kuwa kama tungefika kule ingekuwa kama kufika nyumbani.

Mimi nikaambiwa nishuke pale Mwanza kutafuta mfadhili ambaye angeweza kutukopesha shilingi alfu arobaini, fedha hizi ingekuwa ni mtaji tosha wa bendi kuweza kurudi Iringa kama mambo yasingefana Mwadui. Kweli tulipofika stendi Mwanza,  wakala akatangaza kuwa watu wote na vifaa vyote vishushwe ili basi liende service tayari kwa safari ya kurudi Iringa. Akajibiwa kuwa hakuna haja ya kushusha vyombo kwani havitaingilia service, ugomvi mkubwa ukazuka, hatimae ndipo wakala akaambiwa akitaka aachane nasi basi basi lituache Mwadui, alikubali na basi likaelekea Mwadui……Itaendelea,

Friday, January 13, 2023

MAMBO MOTOOO...MAQUIS ORIGINAL WARUDI JUKWAANI

MAMBO MATAMU YAJA
BENDI kongwe iliyokuwa maarufu sana, Maquis Original itauanza mwaka huu kwa kufanya maonyesho mawili makubwa ya kumbukizi ya enzi zake. Maquis Original awali ilikuwa ikiitwa Maquis du Zaire wakati ikiingia nchini Tanzania kwa mara ya kwanza, ilikuwa ikitokea  mashariki ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, wakati huo nchi hiyo ikiitwa Zaire.
 Baada ya kuwasili Tanzania, haikupita muda mrefu bendi ikawa moja ya bendi tishio nchini. Nyimbo za bendi hii hata zile ilizo rekodi mwanzoni baada ya kuingia nchini bado ni nyimbo pendwa kwa waliokuweko enzi hizo na hata ambao wamezaliwa miaka mingi baada ya bendi kuwa imepotea katika ulimwengu wa muziki. Uamuzi wa wanamuziki wa bendi hii kujikusanya na kufanya maonyesho yao hakika ni faraja kubwa kwa wapenzi wa bendi hii. Bendi itafanya maonyesho mawili. Onyesho la kwanza litakuwa tarehe 21 Januari 2023 katika ukumbi wa Break Point Makumbusho na tarehe 27 January katika ukumbi wa Royal Village Dodoma

Hebu tukumbuke enzi hizo kwa kuangalia tangazo la dansi la Orchestra Maquis miaka hiyo ambalo nina uhakika litaleta kumbukumbu kwa wapenzi wa Maquis wa enzi hizo za Mtindo wa Telemka Chekecha Scania LBT III, wakati huo gari za Scania ndizo zilikuwa maarufu nchini na Scania LBT III ilikuwa gari yenye saiz kubwa kuliko zote, na ndio yenye kusifika zaidi. Maquis walikuwa na ufadhili wa kampuni hiyo ya magari, ukumbi wa nyumbani wa bendi hii wakati huo ulikuwa ukumbi wa White House uliokuwa Ubungo. Karibuni tena wapenzi wa White House mchangie, mambo yalikuwa mazito chini ya uongozi wa Chinyama Chiyaza ambae alikuwa mpiga Saxophone katika bendi. Wakati huu Maquis ilikuwa na maendeleo makubwa sana ya kuwa na mashamba, magari, matrekta na hata kuwa na Kota zake pale Sinza Palestina. Hebu angalia majina ya wanamuziki waliokuwa kwenye bendi hiyo, wote walikuwa miamba ya muziki.

Saturday, November 5, 2022

HISTORIA FUPI YA TAARAB YA TANGA

Marehemu Waziri Ally akiwa mdogo akiwa anapiga kinanda katika bendi ya Lucky star

Katika miaka ya 50 wanawake tisa wa Tanga walijikusanya na kuanzisha  kikundi cha kuimba walichokiita Raha til Fuad maana yake Raha ya Moyo. Akina mama hawa chini ya bibie aliyeitwa Mama Akida au aka Mama Lodi, waliendesha kikundi chao wakiwa wanaimba nyimbo za Siti Binti Sadi na tungo zao ambazo waliimba katika melody ya nyimbo za kihindi zilizotamba wakati huo. Kundi hili liliendelea na kuanza kuruhusu wanaume kujiunga hasa wakiwa wapiga vyombo. Hata mtoto wa Mama Akida, Akida Jumbe hatimaye alijiunga na kundi hili kama mpiga accordion kwenye mwaka 1962. Kundi hili ambalo baadae lilikuja kuitwa Young Noverty, liliendelea mpaka kukaweko na mgawanyiko uliozaa kundi la Shaabab Al Waatan ambalo lilitawaliwa zaidi na wanaume.
 Hapo ndipo kukaanza mtindo wa kuweko kundi pinzani katika muziki wa taarab wa Tanga. Jambo ambalo kwa njia ya ajabu sana kwa kipindi kirefu likawa  linadumu kiasi cha miaka kumi kumi. Miaka ya 60, Young Noverty na Shabaab al Waatan, Miaka ya 70 Lucky Star Musical Club na Black Star Musical Club, miaka ya 80 Golden Star Taarab na White Star Taarab, miaka ya 90, Babloom Modern Taarab na Freedom Modern Taarab. Taarab ya Tanga kwa kweli ndio  haswa inastahili kuitwa Modern Taarab, kwani wao hawakufuata Taarab ile iliyoletwa Zanzibar enzi ya Sultan Seyyid Barghash.
Taarab ya Tanga ilikuwa ni ya makundi  yenye wanamuziki wachache kuliko makundi ya Taarab ile ya Zanzibar.
Vyombo vya vikundi vya Taarab ya Tanga
vilikuwa ni pamoja na Gitaa la besi, gitaa la solo, drums bongos ,akodion au kinanda. Nyimbo zao zilikuwa fupi na si ndefu kama zaTaarab ya Zanzibar au ambayo huitwa Taarab asili. Nyimbo za Taarab ya Tanga zilitegemea mipigo ya ngoma za asili za kumbwaya na chakacha na hata baadaye mitindo kama rumba,bossa nova. Na Taarab ya Tanga ndio iliyoanzisha moto wa vikundi vya taarab Tanzania Bara. Moshi kulikuwa na New Alwatan, AzimioTaarab, na Blue Star Taarab , Arusha kulikuweko na Blue Star Taarab, Dodoma ilikuwepo Dodoma Stars, Kondoa  kulikuwa na Blue Stars, Mbeya kulikuweko na Magereza Kiwira, Mwanza kulikuwa na Ujamaa Taarab, Bukoba  walikuwa na Bukoba Stars, na muendelezo huu uliingia mpaka Burundi kutokana na mwana muziki mmoja alie julikana kama Athmani Mkongo, alitoka Burundi na bendi yake kufika Tanga akahama kutoka muziki wa dansi na kuwa mwanamuziki mahiri wa Taarab na baadae kuipeleka kwao Burundi kukazaliwa kundi maarufu la Jasmine Taarab.


Thursday, November 3, 2022

MKOANI PIA KUNA WANAMUZIKI WAKALI, KWANINI WANATENGWA?

 

Kila jamii ina muziki, kuna aina mbalimbali za muziki na zenye matumizi mbalimbali, kadri ya utamaduni wa jamii husika.
Katika zama hizi hasa mijini, muziki huonekana hasa kazi yake ni kwa kuleta burudani. Lakini kwa asili katika jamii zetu mbalimbali muziki ulikuwa na matumizi ya aina nyingi na hata kupewa majina kutokana na shughuli husika.
Kati ya shughuli ambazo muziki ulitumika na sehemu  nyingine bado unatumika ni kwenye  matambiko, tiba,  misiba, sherehe mbalimbali kama mavuno, harusi na kadhalika.
Leo niongelee muziki na siasa za nchi yetu.
Kabla ya Uhuru, katika maeneo mbalimbali nchini, wanamuziki kama marehemu Mzee Moses Nnauye walianzisha vikundi vya muziki kuhamasisha kudai Uhuru, vikundi vya kwaya, ngoma za asili, na muziki wa taarab na muziki wa dansi, vilitunga nyimbo zenye ujumbe  ambao uliwafikia vizuri wananchi wengi na hivyo  kuwahamasisha kuwa wana haki ya kujitawala na kuanza kudai Uhuru.
Mara baada ya kupata Uhuru,Disemba 9 1961, vikundi vya muziki  vilitunga nyimbo zilizoongelea furaha ya kupata Uhuru na pia kuanza kuelezea ndoto za  wananchi baada ya uhuru. Mahusiano ya muziki na siasa yaliongezeka sana, na baada ya Tanzania kuamua kuwa nchi ya Kijamaa, serikali iliwekeza sana katika sanaa, kwani ilitambua kuwa hiyo ilikuwa njia muhimu ya kufikisha taarifa ya malengo ya serikali. Pamoja na kuweko majengo yalikuwa maalumu kwa ajili ya maonyesho ya muziki, pia yalihamasishwa mashindano, matamasha na maonyesho ya aina mbalimbali ya muziki kila kona ya nchi.

Watu waliokuwa vijana na watoto katika miaka ya 60, 70, na 80 wanaweza kukueleza hadithi ndefu jinsi walivyokuwa wakishiriki kwa namna moja au nyingine katika nyimbo mbalimbali zilizohusu mambo ya nchi yao. Kulikuwa na shughuli za muziki kuanzia ngazi ya vijiji, mada mbalimbali zilitungiwa muziki kwa kutumia muziki wa asili, kwaya na muziki wa kisasa. Kwa njia hiyo taarifa za mambo mbalimbali zilieneka kila kona ya nchi japokuwa mawasiliano ya umma  yalikuwa hafifu mno kulinganisha na zama hizi.
 Kulikuweko na Maafisa Utamaduni wa Wilaya na Mkoa nchi nzima, na maafisa hawa wakahamasisha kuanzishwa vikundi vya muziki wa aina mbalimbali kwenye sehemu za kazi, shuleni, vijijini na kadhalika.  Taasisi za serikali na mashirika ya umma vilihamasishwa kuanzisha vikundi vya sanaa, na ndipo kukawepo kundi la sanaa la Taifa, vikundi vya sanaa majeshini ambapo huko pia kukawa na vikundi vya taarab na dansi, mashirika kama Bima, DDC, URAFIKI, TANCUT na mengine mengi yakawa na vikundi vya sanaa vizuri sana, Kurugenzi za mikoa Dodoma na Arusha nazo zikaanzisha vikundi, Umoja wa Vijana wa TANU nao ukawa na vikundi ikiwemo bendi yake maarufu Vijana Jazz band. Vikundi vyote hivyo vilishiriki sana katika kuimba nyimbo mbalimbali za maisha katika jamii na pia siasa, na maendeleo na nchi. Katika mfumo huo walikuja kupatikana akina Mzee makongoro , Mzee Mwinamila, John Komba na kadhalika.  
Viongozi wa ngazi mbalimbali walivitembelea vikundi vilivyo chini ya himaya yao kuvikagua navyo viljitayarisha kuonyesha umahiri wao, hivyo nchi nzima ilichangamka kwa ubunifu katika muziki wake.

Katika ziara ambazo zilichukuliwa kwa uzito mkubwa na  vikundi vyote, zilikuwa ziara za viongozi wakuu wa  nchi. Mazoezi yalikuwa makubwa, kwaya zilitunga nyimbo mpya, ngoma zilitunga nyimbo mpya, bendi na vikundi vya taarab vilitunga nyimbo mpya, kila moja ilijitahidi kwa umahiri ili tu kupata nafasi kuonyesha kazi mbele ya umma na viongozi hao wakuu. Na hakika kabla ya kiongozi kuanza shughuli au  hotuba, wanamuziki waliburudisha umma kwa kazi zao. Ni katika mfumo huo ambapo wanamuziki kama Bi Shakila walipogunduliwa. Ilikuwa ni siku Mwalimu Nyerere alipotembelea Pangani na Shakila akawa mmoja wa wanamuziki wa pale Pangani walioweza kutumbuiza mbele ya Mwalimu Nyerere, na umahiri wake kugunduliwa. Na hali kadhalika wasanii wengi waliokuja kuwa maarufu walionekana kwanza katika maonyesho mbele ya viongozi wakuu.
Machifu wengi wa zamani walitumia wasanii kupata taarifa za hali ya utawala wao. Wasanii wachekeshaji na wanamuziki waliweza kutunga vichekesho au nyimbo zilizokuwa zikielezea ukweli wa jinsi wananchi walivyokuwa wakijihisi wakiwa chini ya Chifu wao, nae alichukua ujumbe huo uliokuwa ukionekana kama utani au wimbo mzuri na kuufanyia kazi.
Zama hizi za dot com mambo ni tofauti sana, ni jambo la kawaida kabisa viongozi wa juu wakiwa katika ziara zao nchini,  kusindikizana na wanamuziki ‘maarufu’ Kitaifa.  Hali hii ya kuletewa msanii ‘maarufu’ kutumbuiza ‘nyumbani kwao’  na kuwadharau wasanii wenyeji ina waacha wasanii wenyeji wakijiuliza maswali kuhusu thamani yao mbele ya kiongozi huyo mkuu. Taratibu hii mpya pia inamyima kiongozi mkuu fursa ya kuona sura nyingine ya sanaa za wananchi anaowaongoza,  na muhimu zaidi anakosa kusikia ujumbe mpya kutoka kwa wananchi wa sehemu anayozuru.
Nina imani kabisa kabisa kuwa wasanii wote wana haki sawa mbele ya viongozi wakuu, hivyo si haki kudharauliwa kwa kipimo cha umaarufu wa kibiashara.

 

 

 

 

 

Monday, October 3, 2022

USHIRIKINA KATIKA MUZIKI HISTORIA NI NDEFUUUU


Imani ya uchawi ni utamaduni ambao umekuweko katika historia ya jamii zote za binadamu. Maandiko ya dini mbalimbali yanatuhakikishia kuwa jambo hilo lipo na hulilaani. Mara nyingi hudhaniwa kuwa kadri maendeleo na elimu yanavyoongezeka ndio imani ya ushirikina inavyopungua na kupotea, lakini ni wazi dhana hiyo si ya kweli, safari ya kuachana na uchawi bado ni ndefu sana, kwani ukipita katika mitaa mingi utaona vibao vikiashiria waganga wanaoweza kutibu matatizo  mbalimbali kama ‘kusafisha nyota’, ‘kuondoa majini’, ‘kurudisha mpenzi aliyekimbia’ na kadhalika, wasomi wenye milolongo ya shahada na stashahada si ajabu kabisa nao kuwakuta kwenye vibanda vya waganga wakitafuta kusaidiwa kwenye mambo ambayo  mtu mwingine ungetegemea yanawezekana kwa juhudi tu za kibinadamu.

Muziki haujakwepa kuguswa na dhana ya ushirikina. Muziki unatumika unatumika katika kufanikisha dhana ya uchawi na wanamuziki wengi wanaamini na kushiriki katika shughuli mbalimbali za uchawi.

Tuanze na dhana ya muziki iliyopewa jina la Kiingereza ‘ healing music’. Duniani kote waganga na wachawi hutumia muziki wa aina yake kupandisha mashetani au kuita mizimu na kadhalika, muziki huu ndio huitwa healing music, huku kwetu mara nyingine huitwa muziki wa kupandisha mashetani. 

Katika maisha yangu ya muziki niliona na kusikia vituko vingi vilivyohusishwa na imani ya uchawi. Mara ya kwanza kuanza kuona vitimbi hivi ‘live’ ni nilipojiunga bado mdogo na kuwa mwanamuziki katika bendi yetu ndogo huko Iringa. Tualianza kupiga muziki wenyewe wachache bila kuwa na wazo lolote la kuhusisha muziki wetu na imani yoyote ya kishirikina. Siku moja akaja mzee mmoja akatukaribisha kufanya mazoezi kwenye sehemu yake ya biashara, na kwa vile tulikuwa hatuna sehemu maalumu tuliona huu ni ufadhili mkubwa.  Tulihamishia vyombo vyetu vichache kwake, na haikuchukua muda mrefu tukagundua kuwa biashara yake ni uganga wa kienyeji. 
Siku moja akatueleza kuwa hatutaweza weza kuwa bendui kubwa bila ‘kusafishwa nyota’. Tulipewa dawa za kuoga na tukaendelea na mazoezi makali tukijua muda wetu wa kuwa bendi kubwa umewadia. Tulikubaliana kuwa tungepunguza deni la kazi yake ya kutusafisha nyota kwa kumlipa kidogo kidogo kila tulipofanya onyesho, kweli tukaanza kumlipa kila tulipopiga. Sikumbuki ni muda gani tuliendelea kumlipa yule mganga, japo kuwa hakuna chochote kilichobadilika katika hadhi ya bendi yetu.
Siku moja mganga yule alienda disco na akamtishia msichana mmoja kwa nyoka aliyekuwa nae mfukoni, hapo ndipo alipokamatwa na polisi na hatukumuona tena deni likayeyuka.
 Miaka mingi baadae nilikuja kujiunga na bendi moja kubwa jijini Dar es Salaam, hapo ndipo nilipoona tena shughuli za ushirikina. Ilikuwa ni siku chache baada ya kurekodi nyimbo mpya za bendi yetu katika studio za Radio Tanzania. Kulikuwa na kipindi kilichoitwa Misakato , kipindi ambacho kilitambulisha nyimbo mpya zilizorekodiwa na studio za redio hiyo, tulikuwa tumekubaliana kuwa wanamuziki wote tukusanyike nyumbani kwa kiongozi wetu ili wote tuzisikilize nyimbo zetu zikirushwa kwa mara ya kwanza hewani.  Zilipoanza kupigwa nyimbo zetu nikashuhudia mmoja wa viongozi wetu akiwa anaifukiza redio kwa moshi kutoka dawa zilizokuwa zimechomwa kwenye kifuu cha nazi,  hii ilikuwa kwa imani kuwa kwa kufanya hivyo, vibaovyetu vipya vikisikika vitatikisa roho za wasikilizaji wake. Katika kundi hili vituko vingi viliendelea hatimae tulizoea kuwa uongozi wa bendi yetu unaamini sana uchawi. Kuna wakati aliletwa mganga ambaye alidaiwa aliwahi kuifanya timu moja maarufu ya soka, ishinde kombe  na kuwa bingwa wa Taifa, hata jina lake aliitwa Bingwa, kutokana na sifa hizo bendi ilimchukua kwa mkataba na kazi yake ikawa ni kukaa mlangoni akijifanya ni muuza machungwa, hapo alitakiwa afanye vimbwanga vyake ili wateja wengi waingie kwenye muziki. Yeye alidai kila anapomenya chungwa kwa kuunganisha maganda kama mkanda, basi na wateja nao wataingia katika ukumbi kwa kuunganika kwa foleni ndefu, huyu alikaa nasi kiasi cha kuweza kuwa  katika misafara mbalimbali ya bendi tulipoenda ziara za mikoani. Harakati za bendi kutafuta umaarufu kwa uchawi ilifikia mpaka bendi ikasafiri hadi kwenda Mpanda, ambako viongozi wa bendi walikwenda kwa mganga na kufanya mambo yao ambayo yalihusisha na hata kumchinja mbuzi. Baadae walirudi na nyama ya mbuzi huyu mpaka tulipokuwa tumefikia, nadhani masharti yalikuwa ni sisi wanamuziki wote tule kipande cha mbuzi yule wa kafala. Sijajua mpaka leo viongozi walifanya nini na nyama ya mbuzi yule maana wanamuziki walifanya mgomo wa kumla yule mbuzi.
 Ushirikina una matatizo ya kufanya watu wasiaminiane hata kwenye bendi yenyewe, haikuchukua muda mrefu bendi ilipoanza kupoteza umaarufu, Kiongozi wa bendi akaaitisha mkutano na kutuambia kuwa kuanguka kwa bendi kunatokana na mmoja wetu kuiloga bendi, hapo ikatolewa tishio kuwa mtuhumiwa asipojitaja mwenyewe na kuomba msamaha mganga aliyeagua hilo aliahidi atamfanya awe kichaa. Jambo ambalo liliungwa mkono na wote kuwa kama ni kweli kuna mtu namna hiyo basi apate uchizi. Hakuna aliyekumbwa na tatizo hilo mpaka leo.
Miezi michache baadae, wanamuziki wawili walioamua kuacha bendi walirudisha sare za bendi kama ilivyokuwa kawaida zama zile. Shati zilikuwa zimechanywa kwenye kwapa na suruali kuchanywa kwenye maungio ya miguu kwa imani kuwa hizo ndizo sehemu zenye jasho kwa hiyo kama wangerudisha sare zao bila kuondoa sehemu hizo wangeweza kurogwa kirahisi na kuharibiwa maisha.

Mpiga tumba mmoja tuliyekuwa nae bendi moja alinichekesha aliponihadithia kuwa kiongozi wa bendi yao moja aliyopitia, aliwahi kuwapeleka kwa mganga aliyewataka waende na vyombo vyao vya muziki. Kisha akawa ana chanja chombo na kukipaka dawa,na baada ya hapo kumchanja mwenye chombo matakoni na kumpaka dawa!!!!
Katika mizunguko kwenye bendi mbalimbali, siku moja bendi yetu ilikuwa na mpambano wa kupiga bendi zaidi ya moja katika ukumbi mmoja. Hili lilichukuliwa kuwa ni jambo kubwa na la hatari linalohitaji matayarisho,  mganga maalumu lazima atafutwe ili kuilinda bendi isimalizwe na wapinzani. Ilikuwa inaaminika kuwa katika mpambano wa bendi, uchawi hutumika kuimaliza bendi ambayo itakuwa haina kinga, siku moja kabla ya pambano, maboksi ya spika yalifunguliwa na ndani yake  kuliwekwa tunguli na hirizi mbalimbali tayari kwa mpambano. Nakumbuka siku hiyo bendi pinzani nayo iligoma kupanga vyombo kwenye jukwaa kuu kwa madai kuwa kuna mbuzi alifukiwa katika jukwaa lile.

Kwa ukweli kabisa hata wanamuziki kutembeleana mara nyingine ilikuwa ni vigumu, kwani ukionekana mwanamuziki wa bendi nyingine katika ukumbi, basi bendi iliyo jukwaani haina raha, anaweza hata akatumwa mtu kufuatilia kila utakachofanya. Na ilikuwa vigumu kuruhusiwa kugusa vyombo vya bendi nyingine kwa wasiwasi wa kuwa unaweza ukaloga kile chombo. Niliwahi kuona bendi ikisimamisha muziki katikati ya onyesho na kudai shabiki mmoja wa bendi pinzani, tena alikuwa mwanamke, atolewe ukumbini kwani alikuwa ametumwa kufanya ushirikina, na hakika alitolewa nje.

Kulikuwa na hadithi nyingi zilizoonyesha ni kiasi gani cha ushirikina bendi ziliweza kufanya ili kupata wateja. Kuna bendi ambayo ilisifika kuwa kila wakimaliza kupiga muziki walipita katika kumbi mzima  na kuokota vizibo vya chupa za bia na soda, mifupa na mabaki ya nyama zilizotupwa na wateja, na hata kupata maji toka vyoo vya ukumbi na kwenda kuloga ili wale walioingia wasiingie bendi nyingine yoyote kasoro yao. Bendi nyingine zilidaiwa kuwa ziliweka mkataba ambapo zililazimika kutoa kafala ya mtu mmoja kila mwaka, hivyo viongozi wa bendi kufiwa na watoto, ndugu na hata wanamuziki wageni waliojiunga katika bendi hizo kukutwa na mauti ambayo habari za chini chini zilidai ni katika kutoa kafala.

 

Bendi mbili ambazo zilikuwa na upinzani mkubwa katika jiji la Dar es Salaam zilidaiwa hata kutaka kuweka uchawi katika chanzo cha maji Dar es Salaam , na kujikuta wakitaka kuumbuana hadharani kuhusu hilo.
Kuna wanamuziki wapiga magitaa wa zamani waliowahi kupatwa na matatizo ya akili na wazee wengi mpaka leo hudai matatizo yao yalitokana na ushindani wa uchawi katika bendi zao. Kama nilivyosema imani ya uchawi huleta kutokuaminiana na hata madhara makubwa ya kutuhumiana mambo ambayo mara nyingi hayana ukweli wowote. Kuna mwanamuziki niliyejaribu kumshawishi aingie katika bendi niliyokuwa nikipigia , alikataa katakata kwa kuwa alidai mmoja wa wanamuziki katika bendi hiyo ni mchawi.
Mwanamuziki mmoja mpiga gitaa mahiri aliwahi kunihadithia jinsi alivyopita uchochoro wa nyumba ya mwanamuziki mwenzake akashangaa kusikia jina lake likitajwa na mwenzie aliyekuwa chumbani kwake na kusema,’ Nyota ya …….(jina la mwanamuziki huyo) izimike kama kaa hili’, akadai alichungulia katika ufa na akakuta mwenzie anatumbukiza kaa la moto kwenye maji.
Ugonjwa wa ukimwi ulipoanza kuuwa wanamuziki kwa mara ya kwanza mara nyingi ulihusishwa na uchawi. Rafiki yangu mmoja nilipomtembelea wakati akiwa hoi kitandani akanambia,’Nikupe siri? Mi ntakufa lakini nauawa na wanamuziki wenzangu kwenye bendi. Nimepata mganga kanitajia na majina kabisa’. Miezi michache baadae mwanamuziki huyu kabla hajafariki alinambia,’Mjomba sijalogwa wala nini, udude huu, unaniua udude’. Alifariki siku chache baada ya kunambia haya.
Kama nilivyosema awali, elimu na teknolojia hazijaondoa kabisa dhana ya uchawi. Siku moja nilimsikia producer maarufu akiwakanya wasanii wa muziki wa Bongofleva wanaoingia studioni mwake, wasifanye mambo ya ushirikina kwenye studio yake.

Na siku chache baada ya hapo tena mwanamuziki mwingine wa muziki huo kawataja ambao aliwaita wabaya wake wanaomloga.!!!!!!! Nikaona loh kumbe shughuli bado inaendelea, wanamuziki hawa wenye umri mdogo tayari wamekwisha jenga imani ya kulogana katika enzi hizi za dijitali, safari bado ndefu sana, USHIRIKAINA BADO UKO HAI KATIKA SANAA YA MUZIKI

Monday, September 12, 2022

MITINDO ILITAMBULISHA BENDI NA MUZIKI WAKE

 



Katika miaka ya karibuni, utamaduni wa kila bendi kuwa na mtindo wake umefifia sana. Lakini ulikuwa utamaduni uliokuwa maarufu sana kuanzia miaka ya sitini. Kila bendi ilipoanza, ilijinasibu kwa kuja na mtindo wake, ingekuwa siku hizi ingetambulika kama kuji ‘brand’.
Ni vigumu kutaja mitindo yote iliyowahi kugunduliwa kwani kuna mingi ambayo haikuwahi kupata nafasi kutambuliwa katika vyombo vya utangazaji au kuwekwa  katika kumbukumbu za aina yoyote. Majina ya mitindo mingine ilikuwa na sababu au historia na maana maalumu, lakini majina mengine yalikuwa ya kutunga tu na kwa kweli hata waliokuwa waliokuwa wakiyatumia hawakuwa na maelezo ya maana ya maneno hayo. Nakumbuka nikiwa bado mwanamuziki mdogo huko Iringa tulikuwa na bendi ambayo mtindo wake ulikuwa ni Chikwala chikwala, namkumbuka aliyetunga jina hili, alikuwa mpiga gitaa la rhythm ambaye pia alikuwa fundi saa. Hata yeye hakuwa na maelezo ya maana kuhusu jina lile, ila kwa wakati ule, ilikuwa ni staili kwa majina ya mitindo  ya bendi kuwa na jina linalojirudia rudia, hii ilitokana na bendi kadhaa Kongo kuwa na majina yaliyojirudia rudia mfano Orchestra Lipua Lipua, Orchestra Bella Bella na Orchestra Shama Shama.
Baadhi ya majina ya mitindo ya bendi yalikuwa Mundo, Saboso,  Msondo, Sokomoko, Dondola, Toyota, Kiweke, Segere matata, Super mnyanyuo, Vangavanga, Libeneke, Chakachua, Sululu, Ambianse, Takatuka, Afrosa na majina mengineyo mengi. Bendi nyingi zilibuni hata aina ya uchezaji wa mitindo yao, na uchezaji mwingine ulibuniwa hata na wapenzi wa bendi hizi. Kila bendi ilikuwa ikijitahidi kuwa tofauti na bendi nyingine. Kwa mfano katika mji wa Tanga ulikuwa na bendi kubwa mbili, Jamhuri Jazz Band na Atomic Jazz Band, kuna wakati bendi ya Jamhuri ilikuwa na mtindo wa Toyota, na baadae Dondola, wakati  Atomic walikuwa na mtindo wa Kiweke, muziki wao ulikuwa tofauti, hivyo Jamhuri ikawa na wapenzi wake na Atomic ikawa na wapenzi wake, na mpaka leo, wazee waliokuwa wapenzi wa bendi hizi mbili hubaki kusifia ubora wa bendi zao, wazee wa Jamhuri husifu mtindo wa upigaji wa gitaa la rythm la Harrison Siwale(Satchmo), huku wapenzi wa Atomic watakwambia hakuna kama Kiweke, kwani upigaji wa gitaa la solo wa John Kijiko, au bass la Mwanyiro haukuwa na mpinzani. Kule Morogoro kulikuwa na Morogoro Jazz Band na Cuban Marimba, bendi hizi zilikuwa na mitindo mbalimbali kwa nyakati mbalimbali, na wapenzi wao walikuwa tayari kutetea ubora wa mitindo ya bendi zao. Cuban Marimba wakisifia mtindo wa Ambianse, Morogoro wakisifia Likembe, au sululu. Na hakika kulikuwa na tofauti kubwa ya mitindo hii miwili japo ilipigwa na bendi zilizotoka mji mmoja.
Nimeanza kwanza kwa kutaja bendi zilizokuwa katika mji mmoja, tena huko mikoani ambako kwanza miji ilikuwa bado na watu wachache kulinganisha na sasa, wanamuziki walikuwa wanajuana na kuishi jirani, hali hiyo ndio iliyokuwa Tabora, ambako pamoja na Tabora Jazz, kulikuweko na Nyanyembe Jazz, Kiko Kids, lakini muziki wa kila bendi ulikuwa tofauti na mwingine. Dar es salaam kulikuwa na bendi nyingi na hivyo mitindo mingi, na pia kulikuwa na bendi za watu wa mataifa kutoka nje ya Tanzania. Kulikuwa na bendi za Magoa, kulikuwa na bendi za Wakongo, nao pia wakawa na mitindo yao.  Hakuna aliyeweza kuchanganya mtindo wa Ogelea piga mbizi ya  Maquis na mtindo wa Chunusi wa  Orchestra Safari Sound, hata pale ambapo wanamuziki wa kutoka bendi moja walipohamia bendi pinzani kila bendi ilibaki na staili yake na kuilinda kwa kuongeza ubora kila mara. Hivyo haikuwezekana ukasema  Sikinde na Msondo zilipiga muziki uliofanana au mitindo ya Sokomoko na Afrosa ilikuwa na ukaribu. Kikubwa ninachotaka kueleza ni kuwa bendi kuwa na mtindo ilikuwa si jina tu bali kulikuweko na kazi ilifanyika ili kupata, kulinda na kuendeleza mtindo ambao bendi iliamua kuwa nao. Nakumbuka wakati wa mazoezi enzi hizo unaweza ukatunga wimbo ukianza kuimba wenzio watakwambia mbona unafanana na bendi fulani na hapo utakarabatiwa mpaka uwe katika mtindo wa bendi husika.

Wiki chache zilizopita nilipata bahati ya kuhudhuria onyesho moja la bendi iliyoko Mbeya, baridi ndio ilinilazimisha kukumbuka kuwa niko Mbeya, upigaji, uchezaji, uimbaji wa bendi hii ulikuwa kama bendi nyingi zilizopo Dar es Salaam. Bendi zimekuwa kama vile zimepewa amri kuwa lazima zipige muziki unaofanana. Toka umeingia mtindo wa ‘sebene’ mwanzoni mwaka 2000, basi ni kama kila ubunifu umesimamishwa. Hata zile bendi ambazo hupiga nyimbo za bendi ya zamani, hulazimisha kuingiza sebene, kwenye nyimbo hizo. Juzijuzi kwenye onyesho moja kubwa la muziki, bendi moja ilikuwa ikipiga wimbo wa Super Volcano unaoitwa Shida, ghafla ukabadilika kwa kuongezewa sebene.  Kipindi aina ya muziki wa sebene ulipokuwa ukiingia nchini, kulikuwa na aina ya muziki wa hapa nyumbani uliokuwa unaitwa Mchiriku. Sasa toka wakati huo,Mchiriku umeweza kujiongeza na kubadilika mpaka sasa unaitwa singeli, tena hata hiyo singeli imeanza kuota matawi, lakini wanamuziki wa dansi wamekwama palepale kwenye sebene. Hili linanikumbusha enzi za teknolojia ya santuri, santuri zilikuwa zinaweza kupata mchubuko na hivyo sindano ikakwama sehemu moja, ikawa inarudia kupiga muziki sehemu ileile haiendi mbele wala hairudi nyuma mpaka betri itakapoisha.

Wednesday, August 31, 2022

USUPA STAA NI DHANA YA ZAMANI INAYOBORESHWA NA TEKNOLOJIA

 




Ma ‘superstar’ ni watu ambao wametokea kujizolea umaarufu mkubwa katika jamii. Superstar anaweza kuwa ametokea katika nafasi mbalimbali katika jamii, anaweza akawa mwanasiasa, mwalimu, mkulima au mtu yeyote katika jamii, hapa kwetu sifa hii zaidi huhusiana na wasanii. Sifa ya ‘usupastaa’ imejitokeza zaidi baada ya tasnia ya filamu kukua, jambo ambalo limeenda sambamba na kuongezeka kwa vyombo vya utangazaji.  Na kwa kweli katika zama hizi tunao watu wengi ambao wanapewa sifa  ya ‘u superstar’ katika jamii. Hakuna chuo maalumu cha kufundisha usupastaa kwani umaarufu wa mtu huweza kutokana na sababu mbalimbali. 

Wasanii huingia katika sanaa kwa njia na sababu mbalimbali, wengine huzaliwa na kipaji, wengine huingia katika fani hiyo kama njia ya kutafuta maisha, wengine huingia kwa kuiga wenzao waliomo katika sanaa, kuna hata waliolazimishwa na ndugu na jamaa kuingia katika fani ya sanaa, na kadhalika. Kutokana na sababu hizi mbalimbali za kujiingiza kwenye sanaa, waliomo humu nao wanakuwa na mategemeo mbalimbali yatakayopatikana katika fani hiyo. Wengine nia yao ni kutengeneza sanaa nzuri, bila kujali sifa wala malipo, wengine wanafanya sanaa ili wapate kipato kizuri na wengine wakitegemea sifa tu kutokana na ubora wa kazi yao. Na wengine kutumia sanaa kama jukwaa la kufanyia shughuli nyingine kabisa ambazo hazihusiani na sanaa. Wasanii waliomo katika sanaa kutafuta kipato, hulazimika kutafuta mbinu mbalimbali ili sanaa yao iuzike, na moja ya njia kubwa ya kuhakikisha sanaa inauzika ni kwa wao kuwa maarufu. Watu wengi wanatabia ya kufuatilia maisha na kununua kazi za sanaa za watu maarufu. Kutokana na sababu hii, msanii huanza mbinu mbalimbali za kupata umaarufu. Msanii atajitokeza kwenye vyombo vya habari kutangaza kazi zake na hata kuelezea maisha yake, picha zake nzuri kusambazwa,na hata kazi hizo kusambazwa ili watu wengi wazifahamu.

Katika nchi ambazo tasnia imejengeneka vizuri, kuna makampuni maalumu ambayo hutumia mamilioni ya fedha kujenga sifa za msanii husika na kazi zake, kwa kutegemea faida kubwa baadae. Msanii huingia katika mikataba ya muda mrefu na kampuni huwekeza katika kujenga sifa ya msanii ili kupata wateja wengi wa kazi za msanii huyo.

Je unapataje ‘u super star’ hapa Tanzania? Kama ilivyo duniani kote kuna wasanii ambao kazi zao zimepokelewa vizuri na jamii na kuwafanya wasanii mbalimbali kuwa maarufu kwa urahisi sana. Lakini kuna mambo mengi ambayo yanapita nyuma ya pazia katika kupata ‘u superstar’ hapa kwetu. Rushwa ni moja ya jambo kubwa katika kujenga ‘ma superstar’ wa hapa kwetu. Na hili halikuanza karibuni, kwa wanamuziki wa zamani wanaelewa hali ilivyokuwa enzi kulipokuwa na redio moja tu, ilivyolazimika kutoa rushwa ili mashahiri ya nyimbo walizotaka kurekodi yakubalike na nyimbo zirekodiwe, kisha kutoa rushwa ili nyimbo zilizorekodiwa zipigwe kwenye vipindi mbalimbali huku sifa za kujenga usupastar wa wasanii hao zikimiminika, hali hii haiko tofauti sana na sasa japo kwa sasa kuna utititiri wa redio na luninga. Watangazaji wengi wamefaidika na rushwa kutoka kwa wasanii waliokuwa na hamu ya ‘kutoka’. Kuna wakati watangazi wa redio mbalimbali walitengeneza umoja, ambapo mwanamuziki alikuwa akilipia ili kazi zake zirushwe hewani. Watangazaji wa vipindi vya redio wengi waligeuka kuwa mameneja wa wasanii na hivyo kuhakikisha wanawatangaza wasanii wao ili wawezekuwa ‘ma supersta’. Rushwa ya ngono sio siri katika tasnia ya sanaa katika kutafuta ‘u superstar’ . Wasanii wa kike wengi wana hadithi ya kupitia katika mtihani huu katika kutafuta ‘kutoka’. Kuna wakati wasanii  wawili wakubwa wa kike, walitangaza mpango wa kuanza kuwajenga wenzao ili wasipitie adha ya kudaiwa rushwa hii. Jambo ambalo linaonyesha wazi kuwa rushwa hii bado iko hai.

Katika kutafuta ‘U superstar’, kuna wasanii ambao wamefanya mambo mengi ya ajabu ikiwemo kutunga visa ambavyo vingewaweka katika vichwa vya habari. Habari za msanii kufumaniwa, kupigwa, kulewa, kulazwa hospitali, kupendana, kuachana na kadhalika vimekuwa vikitungwa na wasanii mbalimbali ili kujiweka katika nafasi ya kutengeneza hadithi kwenye vyombo vya habari kujiongezea umaarufu. Ujio wa mitandao ya kijamii umekuwa tena nafasi nzuri za kutengeneza ‘U superstar’ wasichana ambao wamekuwa wanatumia sanaa kama daraja la kupata ‘U superstar’, wamekuwa wakitumia kurasa zao kwa kutundika picha wakiwa nusu utupu ili mradi kutafuta kujulikana na kupata wateja wa shughuli isiyohusiana na sanaa.

Matokeo ya vurugu hizo zote ni kuwa msanii kuwa ‘superstar’ si lazima awe msanii bora. Wako wasanii wa aina hiyo wengi na ukiulizia kazi zao za sanaa, hazionekani au hazijulikani. Na kwa kazi zao za kisanii ambazo hutolewa hadharani, huishia kupotea baada ya muda mfupi, lakini sifa za ‘u supersta’ zinaendelea kujengwa kwa namna moja au nyingine. Jambo ambalo ni bahati mbaya kwa tasnia nzima ya sanaa, nikuwa masupastaa hawa wajanja wajanja huaminiwa sana hata na viongozi wa ngazi za juu nchini,  na hutumika kama vigezo vya kukua kwa tasnia. Na mara nyingine huombwa hata kutoa ushauri wa namna ya kuboresha tasnia ya sanaa. Mungu isaidie tasnia ya sanaa Tanzania.

Monday, August 29, 2022

UZURI NA UBAYA WA TEKNOLOJIA ZA KISASA ZA KUREKODI MUZIKI

 

Tape recorder ya studio miaka ya 90 kurudi nyuma


Kwa manamuziki ambaye uliewahi kurekodi miaka ya 90 na kurudi nyuma, hakika studio za siku hizi ni tofauti sana. Teknolojia inayotumika kurekodi siku hizi  inarahisisha sana kurekodi. Mwanamuziki mmoja mmoja anarekodi kipande chake, akikosea kuna uwezekano wa kurudia peke yake na wala si kazi ngumu. Waimbaji pia wanaimba mmoja mmoja na kuna uwezekanao hata muimbaji mmoja akaimba mara nyingi kipande kimoja na hatimae ikasikika kama ni kwaya nzima ilikuwa inaimba. Teknolojia inawezesha hata mtu asiyejua kuimba vizuri akarekebishwa na kusikika akiimba kwa sauti tamu ya kuvutia, pia kwa utaratibu huu wimbo mmoja unaweza hata ukachukua mwezi mzima kukamilisha kuurekodi. Kwa kweli kuna tofauti kubwa sana.
Teknolojia imebadili taratibu zote za utengenezaji wa muziki.  Ngoja nirudi nyuma miaka ya 80, nielezea taratibu za kurekodi nyimbo ambazo siku hizi zinaitwa zilipendwa. Kurekodi haikuwa kazi rahisi, hakukuwa na kompyuta ya kutengeneza mapigo na kutoa sauti mbalimbali za muziki na hata kuelekeza mwendo wa wimbo, ililazimika waweko watu halisi wapige muziki na kurekodiwa kwenye kanda zilizoitwa tape. Mashine za kurekodia zilizoitwa ‘tape recorders’ zilikuwa na uwezo wa kurekodi njia mbili  (two track), hebu linganisha hilo na zama hizi ambazo  hata kompyuta ya kawaida ikiwa na program sahihi inaweza kurekodi mamia ya ‘tracks’ bila tatizo lolote.  Hivyo basi teknolojia hii ya two track ililazimisha kundi linalotaka kurekodi liupige wimbo wao wote bila kukosea ‘live’ na akikosea mtu mmoja tu, lazima kufuta wimbo wote na kuanza upya. Hii ilikuwa na maana kuwa kila kundi lililotaka kwenda kurekodi, ilikuwa lazima kufanya mazoezi magumu ya muda mrefu ili kila mwanamuziki awe anauhakika na vipande vyake atakavyovipiga.

Studio kubwa za kurekodi muziki zilikuwa mbili, studio ya Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) na studio za Tanzania Film Company (TFC). Zote zilikuwa na masharti yaliyofanya kazi ya kurekodi kuwa ngumu zaidi. Studio ya RTD ilikuwa inaipa kila bendi siku mbili za kurekodi. Siku ya kwanza kurekodi nyimbo mpya za bendi na siku ya pili kurekodi kipindi cha Club Raha Leo. Kila bendi ilikuwa inahitajika kuja na vyombo vyake. Mapema siku ya kwanza ya ratiba, bendi iliingiza vyombo studio na kazi ya kuvifunga na kuvitayarisha kwa kurekodi ilichukua muda wote wa asubuhi ya siku ya kwanza. Mchana baada ya kula ndipo wanamuziki walipoingia kurekodi nyimbo zao. Kulikuwa na sheria kuwa watu wote ambao si wafanyakazi wa RTD walitakiwa kuwa wameondoka eneo la RTD kabla ya kushushwa bendera saa 12 jioni. Hivyo basi bendi kama ilikuwa na nyimbo 4 au 10 ililazimika kukamilisha kazi ya kuzirekodi zote hizo kati ya saa 8 mchana mpaka saa kumi na mbili jioni. Kama nilivyosema awali, nyimbo zilitakiwa kupigwa na kuimbwa  bila kukosea, kwa kweli kazi iliyokuwa ikifanywa na wanamuziki wa enzi ile ni ya kusifika. Ukisikiliza kwa makini kuna nyimbo nyingi maarufu zilizopendwa huwa zinakuwa na makosa madogo madogo, lakini mara nyingi ilikuwa ni  kutokana na hali niliyoitaja hapo juu. Kuna wimbo mmoja wa African Fiesta ambao alikuwa anaimba Tabu Ley unaitwa Ndaya, wakati wa chorus unamsikia Tabu Ley akijichanganya maneno , lakini nadhani ilionekana upite, hii ilikuwa ikitokea pale wimbo umesharudiwa mara nyingi na wanamuziki wamekwisha choka.
Fundi mitambo alikuwa akitupigia wimbo tusikie baada ya kurekodi na alikuwa akiuliza' Vipi huu?' wenyewe tukiwa tumeridhika tulijibu 'Upite'.

TFC hawakuwa na masharti ya muda wa kuondoka studio, TFC ilikuwa shirika la umma na hivyo  lilikuwa likiendeshwa kibiashara na malipo ya studio yalikuwa kwa  siku. Kwa kuwa bendi hazikuwa na fedha, mara nyingi zililipa malipo ya kutumia studio siku mbili zikizidi sana tatu. Hapo ilikuwa wanamuziki wenyewe wanakuwa makini ili kutumia vizuri muda wao, ili usije ukaisha na fedha za kuongeza muda zisiweko. Nikiwa Vijana Jazz tulitumia studio za TFC kurekodi album iliyokuwa na nyimbo maarufu kama Thereza, VIP na Mfitini. Tulikesha siku mbili kukamilisha album ile.

Teknolojia ya sasa inaruhusu mtu mmoja kama unauwezo wa kupiga vyombo mbalimbali na kuimba,ukaweza hata kutengeneza nyimbo ambazo zitasikika kama vile ni bendi nzima ilikuwa kazini. Kwa mfano kati ya album za kwanza za wanamuziki wa Tanzania ambazo zilitoka kwa kutumia teknolojia hii ya sasa  ya ‘multi track’ ni album ya Dhiki ya Patrick Balisidya. Katika album hii Patrick alipiga vyombo karibu vyote na pia kuimba sauti zote, ukisikia nyimbo hizo utadhani zilipigwa na bendi nzima.

Pamoja na ubora wote wa teknolojia hii, kurekodi kwa mtu mmoja mmoja kunaondoa sehemu kubwa ya utamu katika nyimbo zilizorekodiwa. Hebu fikiria ngoma yoyote ya kiasili, irekodiwe kwa mpigaji ngoma moja moja kuingia studio na kurekodi mapigo yake, utamu ule wa wapigaji kupeana hamasa wakati wa kupiga wote utaondoka. Pengine ndio sababu nyimbo za sasa zinarekodiwa na kusikika vizuri lakini zinakosa uhai fulani wa wapigaji kupiga kwa pamoja, na kuhamasishana, kupata ile 'feeling ya live'. Nyimbo za bendi zamani zilikuwa kwanza tayari zimeshapigwa mara nyingi katika kumbi mbalimbali hivyo kuwa na aina ya uhai ambao huwezi kuupata katika wimbo ambao ni mpya kabisa. Utaratibu huu uliwezesha bendi kuboresha wimbo hatimae siku ya kurekodi wimbo unakuwa umeiva.

Wednesday, August 24, 2022

NIMEPITWA NA WAKATI NGOJA NIKAPUMZIKE

 


Nilipokuwa mdogo nilikuwa naona vibabu vya mtaani kwetu viko vya aina mbili, aina ya kwanza ilikuwa vibabu ambavyo vilikuwa havicheki kila saa vimenuna na kwa ujumla, watoto wote tuliviogopa, na tulianza hata kutunga hadithi kuwa vitakuwa vichawi, au vilipata matatizo makubwa wakati wa ujana na kadhalika. Kundi la pili la vibabu ilikuwa vile vibabu ambavyo huvikuti vimenuna, ukiviamkia vinakujibu kwa furaha na kuanza kuulizia wazazi wako, mambo yako ya shule na kadhalika. Vibabu hivi hata kama una shida ilikuwa rahisi kukusikiliza na kukupa ushauri hata msaada. Na pia kulikuwa na vibibi vya aina hiyohiyo pia, tulikuwa na rafiki yetu bibi yake alikuwa anauza maji, kila baada ya siku chache tulikuwa tukimtembelea bibi kwa kuwa lazima atatugawia senti  kumi kumi kutokana na biashara yake ndogo ya maji, kwa hesabu za harakaharaka alikuwa akitugawia pato lake la siku nzima bila hata kusita, na wala hatukuwa wajukuu zake wa moja kwa moja. Sasa yamenikuta siku hizi mimi ndie sasa nimekuwa babu, na polepole naanza kupata picha kwanini wale babu na bibi zangu walikuwa vile.
Wahenga walikuwa na msemo, nyani mkongwe kakwepa mishale mingi, na ndio ilivyo katika maisha, wakongwe wamekwepa mengi, wameona mengi, kwa asili ya mila na tamaduni zetu, wazee walikuwa na nafasi muhimu katika kutoa ushauri wa mambo kadhaa, lakini hili linapotea taratibu, na hasa ukichukua dhana ya siku hizi isemayo ‘wazee wamepitwa na wakati’.
Wasanii ni sehemu ya jamii, hivyo hata kwenye tasnia hii dhana ya ‘wazee wamepitwa na wakati’ inatumika sana.
Ukongwe katika fani unakupa elimu ya mambo mengi, mengine unafundishwa na wakongwe uliowakuta, mengine unajifunza kazini, hatimae kichwa kinakuwa na majibu ya mambo mengi ambayo kwa utamaduni wa zamani unatakiwa kuyarithisha kwa wanaochipukia katika fani. Lakini hili linakuwa gumu pale inapokuja dhana kuwa ‘wazee wamepitwa na wakati’. Ukisha kutana na hali ya kuonekana umepitwa na wakati kuna mambo mawili unaweza ukaamua, moja unaweza ukawa mtu wa kukasirika kila wakati, kiasi cha kwamba mtaani ukaonekana ni babu moja mwenye hasira zisizo na sababu, watoto wakaanza kuhadithiana kuwa utakuwa mchawi au ulipata matatizo ya akili ulipokuwa kijana. Jambo la pili linaloweza kutokea ni kuamua kuwa mchangamfu na kubaki unacheka na kila mtu, ili usisumbue kichwa chako, na hatimae kuondoka duniani na elimu yako kwa furaha.
Kwa kicheko na furaha sana nakumbuka enzi kabla hakujawa na Baraza la Sanaa la Taifa. Enzi hizo  kulikuwa na taasisi inaitwa Baraza la Muziki la Taifa (BAMUTA), chombo kilichoanzishwa mwaka 1974. Kazi ya BAMUTA ilikuwa kuratibu shughuli za muziki na muziki wa aina zote. BAMUTA iliuangalia muziki kwa mapana yake yote, elimu, vifaa, masoko, maadili, BAMUTA pia ilikuwa na kazi ya kuandaa sera za Taifa za muziki. Katika kipindi cha BAMUTA bendi zilisaidiwa vyombo vya muziki na serikali, BAMUTA ilitungwa vitabu kadhaa vilivyohusu muziki, ukiwemo muziki wa asili. Mitaala ya muziki ilitayarishwa na muziki ukawa somo mojawapo linalofundishika mashuleni, waalimu wake walitayarishwa katika vyuo vya waalimu wa sanaa kama vile Chuo cha Butimba, na wakaenezwa katika vyuo na mashule nchini kote, wengine wakawa maafisa utamaduni na wengine kuwa katika ngazi mbalimbali za wizara ya Utamaduni na sanaa. Kila mkoa ulikuwa na japo bendi moja iliyokuwa na umaarufu, kulikuwa na kwaya nyingi, madisco mengi,  japo wakati huo uwekezaji katika muziki haukuwa mkubwa kama ulivyo sasa. Mazingira yakawekwa yaliyoruhusu wapenzi wa muziki waweze kusikiliza aina mbalimbali za muziki hata muziki ule ambao si wa kibiashara lakini ni mzuri kwa ubora wake au kwa ujumbe wake. Mazingira hayo yaliwapa wanamuziki maktaba pana ya kuweza kutohoa aina mpya za muziki. Wajumbe wa BAMUTA walitoka kila kona ya nchi na hivyo kuipa BAMUTA sura ya Kitaifa, angalia orodha ya wajumbe wa Baraza la Muziki Tanzania;

1.   Boniface Musiba (Mwenyekiti wa BAMUTA)
2. D. R. Mbilinyi (Mwenyekiti Msaidizi wa BAMUTA)
3. S. Chidumizi (Mjumbe wa BAMUTA-Dodoma)
4. J.Y. Sapali (Mjumbe wa BAMUTA-lringa)
5. Padre J.M. Buluma (Mjumbe wa BAMUTA-Mwanza)
6. A. Kosana (Mjumbe wa BAMUTA-Shinyanga)
7. R. Singano (Mjumbe wa BAMUTA-Tanga)
8. Mbaraka Mwishehe (Mjumbe wa BAMUTA-Morogoro)
9. Padre Kayatto (Mjumbe wa BAMUTA-Mbeya)
10. Gwabukoba (Mjumbe wa BAMUTA-Kigoma)
11. P. Balisidya (Mjumbe wa BAMUTA-Dar es Salaam)
12. R. Mselewa (Katibu Mtendaji wa BAMUTA)
13. E. Kavalambi (Mkufunzi wa Muziki-Marangu CE.T.)
14. K. J. Nsibu (Aflsa Utamaduni-Korogwe)
15. E. Lameck (Mwanakwaya-Mwatex)
16. G. Kanyabwoya (Mwalimu-Kigoma)
17. T. Busyanya (Mkufunzi wa Muziki-DSM CE.T.)
18. G. Daudi (Afisa Sanaa za Maonyesho-Rukwa)
19. John Mgandu (Mwalimu wa Muziki-Tabora Shule ya Seko-ndari ya Wavulana)
20. E. G. Makala (Wizara ya Utamaduni)
21. F.E. Nkwera (Mkufunzi wa Muziki-Songea CE.T.)
22. T. Nkera (Mkufunzi wa Muziki-Ndwika CE.T.)
Wakati ufanisi wa Baraza hili ukiendelea, akatokea mtu mmoja akaanzisha wazo la kuwa na Baraza moja kwa ajili ya Sanaa zote, na ndipo likazaliwa Baraza la Sanaa la Taifa. muziki ukashushwa na kuwa ni Idara tu katika katika Baraza hili, tena hata hiyuo idara ilisha uwawa .

Lakini nisijichoshe, ngoja nikacheze na watoto, si unajua wazee tumepitwa na wakati.

 

Tuesday, August 23, 2022

SEHEMU YA RIPOTI YA TAMASHA LA BENDI LA TANZANIA LIVE MUSIC FESTIVAL 2012



Baada ya matayarisho mbalimbali yaliyochukua miezi mitatu hatimae tarehe 28 September 2012, bendi ziliweza kuanza kupanda jukwaani kufanya maonyesho katika viwanja vya Leaders Club.  Bendi zilizopanda jukwaani karibu zote zilikuwa na makubaliano ya kulipwa na zililipwa fedha ya awali wiki 2 kabla ya onyesho na fedha iliyobaki ilikamilishwa siku ambapo bendi zilipanda jukwaani. Hakuna bendi yoyote iliyokuwa ikiwadai watayarishaji.

Watayarishaji walijipanga kwa kuhakikisha kuna jukwaa la Kimataifa lililopambwa na taa za rangi za kiwango cha juu, na vifaa vya muziki ambavyo vilihakikisha kila bendi inapopiga muziki, muziki wake ulisikika kwa kiwango cha hali ya juu. Hakukusikika mpaka leo malalamiko kuhusu upande huo wa matayarisho.


MC BEN KINYAIA

Tamasha lilianza tarehe 28 September 2012, saa kumi na mbili jioni,  kwa bendi kuanza kufanya maonyesho, bendi ya kwanza kupanda jukwaani ilikuwa ni Msondo Ngoma Music Band na kufuatiwa na bendi ya Fm Academia, na baadae bendi za Akudo Impact, Mashujaa Band, kundi la Taarab la Mashauzi Classic na baadae vijana wa Orynx Band. Bendi zote zilifanya vizuri sana, bendi zilipanda  kwa zamu kama ratiba ilivyokuwa imewaelekeza na mshereheshaji  alikuwa ni Ben Kinyaiya alifanya kazi kwa umakini wa hali ya juu .

 

Tamasha liliendelea siku ya pili  kama ratiba ilivyokuwa imepangwa kwa bendi za Mlimani Park, Skylight band, B Band, Oryx Band, Bi. Khadija Kopa  kupanda jukwaani, na kama ilivyokuwa jana yake wakiongozwa na mshereheshaji  Ben Kinyaiya.





MAFANIKIO

Mafanikio yaliyopatikana ni uzoefu mkubwa wa namna ya kutayarisha tamasha la muziki wa bendi. Mawasiliano yaliweza kufunguliwa kati ya watayarishaji na wanamuziki wa bendi mbalimbali. Kumekuweko na mafanikio ya kujua namna ya kupata vyombo na mafundi bora wa sauti, upambaji wa jukwaa na matayarisho yote ya awali ya kuwezesha tamasha kufanyika. Kumepatikana uzoefu wa kuitisha press conference na kufanya mikutano na wadau mbalimbali wa matamasha, serikalini, katika kampuni binafsi na watu binafsi.



WADAU TAMASHA.

Tamasha hili liliandaliwa kwa ushirikiano kati ya Edge Entertaiment na Chama Cha Muziki  wa Dansi Tanzania(CHAMUDATA) baada ya makubaliano, ambayo yalifikiwa kukiweko na malengo ya kupata fedha kwa ajili ya kusaidia miradi ya CHAMUDATA na kutoa mchango kwa BASATA. Kampuni ya Edge Entertaiment iliingia  mkataba na Times Fm Radio ambao uliwezesha  Times Fm kulitangaza Tamasha  pia kutoa gharama za matumizi yote ya maandalizi ya tamasha  kwa makubaliano ya fedha zitakazotumika kurudishwa kutokana na mapato ya tamasha.



KAMATI.

Kamati ya pamoja ya Edge Entertaiment  na Times Fm Radio iliundwa na ikapewa majukumu ya kuhakikisha  tamasha linafanikiwa, kamati ilifanya kazi chini ya uangalizi wa upande zote mbili zilizokubaliana na kamati  iliomba kampuni ya Edge Entertaiment iajiri mtu wa PR atakayehakikisha mpangilio  mzuri wa Tamasha na Edge Entertainment ilifanya hivyo.



VYOMBO VYA HABARI.

Katika kuhakikisha tamasha linafanikiwa kamati ilitumia vyombo vya habari vifuatavyo Magazeti, Tv, Blogs, Radio

Magazeti yaliyotumika;

  (a)Mwananchi

  (b)Jambo leo

  (c)Mtanzania

  (d) Magazeti ya Global Publishers

Tv zilizotumika;

 (a) TBC - Mahojiano

 (b) Chanel Ten- Mahojiano

Blogs zilizotumika;

(a) Michuzi

(b) Full shangwe

(c) Dar blog

(d) www.musiciansintanzania.blogspot

Radio;

Radio iliyotumika ni Times Fm Radio hii ilitokana na udhamini ambao redio hii ilikuwa imetoa

 


MATATIZO.

Kulikuweko na matatizo kadha wa kadha, mengine ni kutokana na maamuzi yaliyofanyika, mengine ni kutokana na wadau mbalimbali wa Tamasha, na machache ambayo yalikuwa njee ya uwezo wa  Kamati ya tamasha

* Tamasha lilifanyika siku ya Ijumaa na Jumamosi, huu ulikuwa uamuzi ambao ulionekana kuwa ni mzuri, lakini kwa mawazo ya wadau waliohudhuria wengi waliona ingekuwa bora tamasha lingeanza Jumamosi na hatimae kufikia kilele Jumapili kwa maonyesho ambayo yangeanza Jumapili kuanzia saa nne asubuhi hadi kati ya saa4 na saa 6 usiku siku hiyo

* Pamoja na bendi kulipwa si chini ya shilingi laki saba kila bendi bendi ziliendelea kupanga ratiba zao na hata kutangaza kuwa wako katika sehemu nyingine kwa siku na wakati uleule ambapo bendi zilitegemewa kuwa jukwaani katika tamasha. Msondo Ngoma walipiga wimbo mmoja tu kwa malipo ya shilingi milioni 1.

* CHAMUDATA  kilikuwa mdau muhimu katika tamasha hili, kwanza kwa kuwa sehemu ya mapato yalikuwa yaiingie katika mfuko wa chama hicho, na pili hili lilikuwa tamasha la muziki wa bendi, hivyo kuwa linafanya kile ambacho chama hiki kinasimamia, lakini hakukuweko hata afisa mmoja wa  CHAMUDATA katika kipindi chote cha tamasha, ambapo ingetegemewa chama kiwe chombo kimojawapo cha kupigia debe mafanikio ya tamasha hili.

* Kulikuweko na matatizo ya matangazo ambapo palikuweko na matukio ya kubandua mabango, na wakati fulani kuchanganya taarifa katika matangazo ya magazeti.

* Pamoja na kuwa eneo la Leaders lilikuwa limelipiwa, bado uongozi wa bar ya Leaders ulikaidi na kuendelea kukiuka masharti kwa kuendelea kufanya mauzo ya vinywaji kinyume na utaratibu na makubaliano na wadhamini wakuu wa tamasha. Hili limepelekea wadhamini kugoma kulipa baki ya ada ya udhamini ambayo ni shilingi 10,000,000.

* Mgeni rasmi aliwasili kwa muda aliopangiwa ambao ulikuwa ni saa moja, hili lilikuwa kosa kwani muda huo ndio ratiba inaanza na si muda mzuri kwa mgeni rasmi kuwa ndio anawasili, pia hakukuweko na protokali za kumpokea mgeni rasmi jambo ambalo lilitia doa ujio wake. Na hivyo alishindwa hata kufanya shughuli ya kufungua rasmi tamasha

 


HITIMISHO.

Kwa ujumla Tamasha lilikuwa na mengi sana mazuri kiutendaji, vyombo vizuri na vya kisasa, stage kubwa ya kisasa, na  liliweza kufanyika  kwa bendi zaidi ya kumi kushiriki. Ni wazi ni muhimu utamaduni huu wa kuwa natamasha kila mwaka kuendelea japo matayarisho yanatakiwa kuanza sasa.
Wanamuziki wa mabendi walikatisha tamaa kwani wamekuwa wakilalamikia kukosekana kwa Tamasha lao,  lakini ni wazi walithamini zaidi kazi zao za kawaid kuliko Tamasha lililokuja kukidhi kiu yao.
 Kwa upande wa mapato hayakuwa mazuri waandaji  waliingia hasara  kubwa na  hivyo kushindwa kutimiza malengo yake likiwemo la kukisaidia Chama cha Muziki wa Dansi Tanzania (CHAMUDATA). Waandaji wataendelea na elimu na mafunzo mbalimbali kwa wanamuziki wa muziki wa dansi wakishirikiana na BASATA na CHAMUDATA ili kuweza kuleta mafanikio katika muziki wa dansi Tanzania.

Katibu

 


Monday, August 22, 2022

KUWA MWANAMUZIKI ZAMANI HAIKUWA LELEMAMA

 

Vijana Jazz Band tukielekea Ifakara

Kuwa mwanamuziki katika miaka ya tisini na kurudi nyuma haikuwa lelemama, ilikuwa kazi ngumu, iliyokuwa yakujitolea haswa. Kati mambo magumu miaka hiyo ilikuwa kusafiri kwenda kufanya maonyesho. Katika zama hizi mwanamuziki anapata mualiko, anatajiwa na fungu atakalolipwa, anachagua aina ya hoteli ya kulala na hata usafiri kama ni wa ndege au gari la abiria  au hata gari binafsi, fursa hizo hazikuweko miaka hiyo.
Kwanza kabisa kulikuwa na taratibu za kiserikali, ili bendi au kikundi cha muziki kitoke katika mkoa ambako ni masikani taratibu zilikuwa ngumu. Kikundi kilianza kwa kuandika barua kwa Afisa Utamaduni wa mkoa kuomba ruksa ya kutoka nje ya mkoa. Afisa Utamaduni akisha kutoa kibali kile, muwakilishi wa bendi hutangulia kwenda kuwakilisha kibali kwa Afisa Utamaduni wa mkoa ambao kundi linaenda ili kupata kibali cha kufanya kazi katika mkoa husika, Afisa Utamaduni Mkoa akisha toa kibali kuingia mkoa wake, ndipo nakala ya kibali hupelekwa kwa Afisa Utamaduni wa Wilaya ili nae atoe kibali cha kuruhusu kundi kufanya maonyesho katika wilaya yake. Kutokana na uchache wa magazeti, vikundi vingi vilianza safari bila matangazo yoyote, kwani kuna wilaya nyingine, magazeti hayakuwa yanafika kabisa au magazeti yalifika machache na hata hayo yaliweza kuchelewa hata siku nne.  Mwakilishi wa kikundi akishafika kwenye mji ambao bendi au kundi lingefanya maonyesho, alishirikiana na Afisa Utamaduni kupata kumbi na kufanya booking ya mahala pa kulala. Matangazo ilikuwa ni karatasi za kuandika kwa mkono na kisha kubandika katika kuta na nguzo mbalimbali. Baada ya hapo alitafutwa mwenyeji ambaye ni mtangazaji naye alipita katika mitaa mbalimbali akitangaza kupitia kipaza sauti cha mkononi. Nakumbuka mwaka mmoja mapema miaka ya 80, nikiwa na Orchestra Mambo Bado, tulifika Mpanda na kuelekezwa kuwa mtu maalumu ambaye hutangaza mambo yote pale, alikuwa bwana mmoja aliyepewa jina la utani la Mshindo Mkeyenge. Huyu alikuwa akipita mitaa mbalimbali na ngoma yake na hiyo hugonga  ili watu wamsikilize na ndipo hapo hutangaza kuwa kuna dansi linakuja na litakuwa wapi na kiingilio chake.

Usafiri wa bendi ulikuwa wa basi za abiria na mara nyingi malori ambamo wanamuziki walijazana humo wakiwa na vyombo vyao. Kati ya safari za aina hii nilizowahi kusafiri kwa roli ni toka Mbeya hadi Chunya na kurudi, kutoka Mtwara na kuzunguka miji ya kusini mingi kama Masasi , Nachingwea, Lindi kutumia lori la aina ya Isuzu Long base. Na nikiwa na bendi ya Tancut kwa ujumla usafiri wetu ulikuwa ni loti aina ya ‘canter’, humo tulizunguka miji kuanzia Makambako, Njombe, Songea, Mbeya, Tunduma na miji mingine mingi, tuliwahi pia kuzunguka miji mingi kanda ya ziwa kutumia  lori aina ya Leylan Albion. Huo ndio ulikuwa usafiri wa masupastaa wa mika hiyo.

 Malazi kwa kawaida hayakuwa ya kifahari, kwa kawaida vyumba vilivyokodishwa vilikuwa ni dabo ili kupunguza gharama, na gesti zenyewe zilikuwa ni zile ambazo gharama zake zikuwa chini. Kulala njaa halikuwa jambo la ajabu, hasa mkipiga dansi na kukosa wateja, hapo ndipo mnaweza kujikuta mmelala ukumbini ili pesa itoshe gharama za kuwasafirisha kwenda mji unaofuata. Miji mingi haikuwa na umeme hivyo bendi nyingine zilikuwa zikizunguka na jenereta, au kukodi kwa ajili ya kila onyesho.

Kama ilivyo katika biashara nyingine uongo nao ulikuwa mwingi sana, utasikia , ‘Bwana bendi ikienda Nyarugusu kule fedha nje nje, wachimba migodi wana pesa sana lazima mtarudi na pesa za kutosha kununua vyombo vipya’ . Hapo harakati za kwenda Nyarugusu zitaanza. Miaka hiyo Nyarugusu ilikuwa mji mmoja maarufu kwa wachimba dhahabu wadogowadogo, lakini sijawahi kuona bendi ikipata fedha za ajabu baada ya kwenda Nyarugusu. Kuna wakati  Bendi tatu tulikutana Mwanza kila moja ikiwa ina mpango wa kwenda Nyarugusu. Vijana Jazz Band,  Maquis  na Ngorongoro Heroes wote tukawa Mwanza. Hali ilikuwa mbaya sana kwa Maquis ambayo ilikuwa safarini huku  kwa zaidi ya miezi mitatu, ilifikia kiasi cha wanamuziki kuanza kurudi Dar es Salam mmoja mmoja.
Lakini ilikuwa ni baada ya safari hii walipojipanga upya na kurekodi vile vibao vyao vikali, Makumbele, Tipwa tipwa na Ngalula na kurudisha heshima yao mjini.

Kifupi hayo ndiyo yalikuwa maisha ya mwanamuziki wakati huo, ujana ulisababisha watu wafurahie kuzunguka huko na huku nchi nzima, wakipata mikasa na kuitungia nyimbo ambazo nyingine bado zinapendwa mpaka leo. Hakika sitaweza kukumbuka sehemu zote ambazo binafsi nimewahi kupiga muziki, kwani pamoja na miji mikubwa tulikuwa pia tunapiga katika vijiji ili mradi tupate pesa za kuendelea na safari.  Najaribu kupata picha vijana wa zama hizi kukubali kusafiri kwa lori kwenye barabara zilizokuwa duni na za vumbi. Nina uhakika madansi mengi yasingelia kwa supastaa kugom kupiga.

Sunday, August 21, 2022

KUJIBRAND SIO DHANA MPYA

 


Katika zama hizi ni kawaida kabisa kusikia wanamuziki wa kizazi kipya wakisema wanaji‘brand’. Kujibrand ni kujitengeneza kwa aina fulani ili uwe tofauti na watu wengine na huo kuwa utambulisho wako kibiashara. Katika mazungumzo ya wasanii wengi wa kiazi kipya, huwa wanaamini wao ndio wamegundua dhana ya kujibrand, niliwahi hata kumsikia msanii mmoja akisema tatizo la wana muziki wa dansi ni kuwa hawajibrand, kuna ukweli kiasi katika sentensi hiyo lakini msanii huyu alisema hivi kwa kudhani wasanii wa bendi hawajawahi kuelewa dhana ya kujibrand.

Kujibrand kumekuwa sehemu ya muziki wa dansi kwa muda mwingi wa historia ya muziki huo. Hebu turudi nyuma kuanzia miaka ya sitini. Bendi zilijitambulisha kwa majina mbalimbali, jina ni kipengele kimoja cha kujibrand. Kulikuwa na majina yaliyotokana na matukio mbalimbali ya kihistoria na bendi nyingine zilikuwa na majina yaliyotokana na masikani ya bendi na mara nyingine jina ambalo lilikuwa ni la ubunifu tu wasanii wahusika.

Baadhi ya bendi ambazo zilikuwa na majina kutokana na masikani ya bendi hizo ni  Morogoro Jazz, Tabora Jazz, Mbeya Jazz, Dodoma Jazz, Dar es Salaam Jazz Band, Super Matimila Orchestra, Mara Jazz na kadhalika. Butiama Jazz Band ilipata jina hilo kwa historia tofauti kidogo, bendi hiyo haikuwa na maskani Butiama, lakini ilijipatia hilo jina kama heshima kwa kijiji alikozaliwa Mwalimu  Nyerere,  ambaye ndie aliyewanunulia vyombo vyao vya muziki. Western Jazz Band ilijipa jina hilo kutokana na waanzilishi kuwa wanatoka jimbo la Magharibi la Tanganyika. Wakati wa ukoloni nchi iligawanywa katika majimbo yakiwemo Northern Province, southern Highlands Province, Western Province, Lake Province na majimbo mengine. Kilwa Jazz Band ilijibrand hivyo kutokana na muanzilishi wa bendi hiyo, Ahmed Kipande kutokea Kilwa.
 Kulikuwa na bendi zenye majina ya matukio kama Jamhuri Jazz, Ujamaa Jazz, Kilimo Jazz na kadhalika. Halafu kulikuweko na majina ya ubunifu kama Highland Stars, Mitonga Jazz, Kochoko Jazz, Makondeko Six, Cobash Brothers, jina lililotokana na muunganiko wa majina ya mwanamuziki waliokuwemo kwenye bendi hii, Orchestra Safari Sound, Kyauri Voice, Orchestra Toma Toma jina lililotokana na mwenye bendi aliyeitwa Timmy Thomas, kulikuweko na Super Rainbow, Rainbow Connection, Afro 70, Safari Trippers, Atomic Jazz Band, Super Volcano Orchestra, Orchestra Zela Zela,  Orchestra Super Veya, Zaire Success, orchestra Ban Africa Kituli na kadhalika.
Halafu kulikuweko na bendi ambazo zilijipa majina kutokana na kuwa chini ya kampuni au jumuiya ya kijamii. Kulikuweko na Vijana Jazz iliyokuwa chini ya Jumuiya ya Vijana wa CCM, Bima Lee iliyokuwa mali ya kampuni ya Taifa ya Bima, Tancut Almasi Orchestra iliyokuwa mali ya wafanyakazi wa kiwanda cha kuchonga almasi cha Iringa, Mwenge Jazz mali ya brigedi ya Mwenge na kadhalika. Kule Kilombelo kulikuwa na  Sukari Jazz Band, iliyokuwa ni mali ya kiwanda cha sukari cha Kilombelo, UDA Jazz Band iliyokuwa mali ya kampuni ya mabasi ya usafiri Dar es Salaam, kulikuweko na BAT Jazz iliyokuwa mali ya kiwanda cha sigara cha BAT,  na kadhalika.  Majina haya hakika yalikuwa njia mojawapo ya kujibrand.
Bendi hizi zilianzisha mitindo yao ya kupiga na kucheza na kuipa majina kama njia nyingine ya kujibrand. Katika kumbukumbu hizi lazima tuanze na ‘brand’ kongwe kuliko zote nayo ni mtindo wa  Msondo uliyoanzishwa na NUTA Jazz Band kati ya mwaka 1964 na 1965 na mpaka leo bado uko hai na una nguvu. Kumepita mitindo mingine kama Sikinde, Ndekule, Bayankata, Kiweke, Sensera, Dondola, Afrosa, Koka Koka, Ambianse, Sululu, Saboso, Paselepa, Segere Matata, Vangavanga, Sokomoko, Fimbo Lugoda, King’ita Ngoma, Disco Agwaya, Super Mnayanyuo, Washawasha,  Super Bomboka na mitindo mingine mingi sana,  itachukua kurasa kadhaa kuitaja yote.   
Bendi pia zilikuwa na mavazi mbalimbali, mashati na suruali zishonwa kwa rangi mbalimbali na mitindo ya kupendeza ilyofanya  wanamuziki wapendeze wanapokuwa jukwaani, tena wakicheza kwa utaratibu maalum wa mtindo wao. Kati ya mafundi maarufu na wabunifu wa nguo hizo walikuwa ni mtuma salam maarufu Loboko Lobi Papaa na Mzee Kitenge ambaye kwa sasa yupo soko la Machinga Ilala.
 Kulikuwa na kujibrand kwa mtu mmoja mmoja ambapo wasanii walijipa majina mbali mbali ya kuvutia. Kulikuwa na majina kama Sauti ya Zege, Stereo Voice, Electronic voice, Computer, Golden Fingers, Dudumizi, King Michael na  King Kiki, akina mama hawakuwa nyuma kulikuwa na Stone Lady, Super Mama na wengineo. Kuna wanamuziki waliojikuta wanapata majina kutokana na nyimbo zao, Mzee Zacharia Daniel alijulikana zaidi kama Zacharia Tendawema kutokana na wimbo aliouimba akiwa Shinyanga Jazz Band ulioitwa Tenda Wema Uende zako, Mabrouk Khamis alijulikana zaidi kwa jina la Babu Njenje kutokana na wimbo aliokuwa akiuimba ulioitwa Njenje. Eddy Sheggy nae alianza kuitwa Chaurembo kutokana wimbo alioutunga uliokuwa na jina hilo.

Kwa mifano michache hii, kujibrand si dhana ngeni, bali kutokana na teknolojia imechukua sura mpya na pana zaidi.  Ikihusisha kusambaza picha mnato na video kwenye mitandao, siku hizi hata kutumia mikasa ya uongo kama vile kujitangaza kufa, au kujitangaza kukutwa na jambo la aibu kama kufumaniwa kunatajwa kama kujibrand, hata kuimba nyimbo zisizo kubalika na wengi ili tu zilete mtafaruku  inachukuliwa kama njia ya kuji brand.

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...