YOUTUBE PLAYLIST

Monday, August 29, 2022

UZURI NA UBAYA WA TEKNOLOJIA ZA KISASA ZA KUREKODI MUZIKI

 

Tape recorder ya studio miaka ya 90 kurudi nyuma


Kwa manamuziki ambaye uliewahi kurekodi miaka ya 90 na kurudi nyuma, hakika studio za siku hizi ni tofauti sana. Teknolojia inayotumika kurekodi siku hizi  inarahisisha sana kurekodi. Mwanamuziki mmoja mmoja anarekodi kipande chake, akikosea kuna uwezekano wa kurudia peke yake na wala si kazi ngumu. Waimbaji pia wanaimba mmoja mmoja na kuna uwezekanao hata muimbaji mmoja akaimba mara nyingi kipande kimoja na hatimae ikasikika kama ni kwaya nzima ilikuwa inaimba. Teknolojia inawezesha hata mtu asiyejua kuimba vizuri akarekebishwa na kusikika akiimba kwa sauti tamu ya kuvutia, pia kwa utaratibu huu wimbo mmoja unaweza hata ukachukua mwezi mzima kukamilisha kuurekodi. Kwa kweli kuna tofauti kubwa sana.
Teknolojia imebadili taratibu zote za utengenezaji wa muziki.  Ngoja nirudi nyuma miaka ya 80, nielezea taratibu za kurekodi nyimbo ambazo siku hizi zinaitwa zilipendwa. Kurekodi haikuwa kazi rahisi, hakukuwa na kompyuta ya kutengeneza mapigo na kutoa sauti mbalimbali za muziki na hata kuelekeza mwendo wa wimbo, ililazimika waweko watu halisi wapige muziki na kurekodiwa kwenye kanda zilizoitwa tape. Mashine za kurekodia zilizoitwa ‘tape recorders’ zilikuwa na uwezo wa kurekodi njia mbili  (two track), hebu linganisha hilo na zama hizi ambazo  hata kompyuta ya kawaida ikiwa na program sahihi inaweza kurekodi mamia ya ‘tracks’ bila tatizo lolote.  Hivyo basi teknolojia hii ya two track ililazimisha kundi linalotaka kurekodi liupige wimbo wao wote bila kukosea ‘live’ na akikosea mtu mmoja tu, lazima kufuta wimbo wote na kuanza upya. Hii ilikuwa na maana kuwa kila kundi lililotaka kwenda kurekodi, ilikuwa lazima kufanya mazoezi magumu ya muda mrefu ili kila mwanamuziki awe anauhakika na vipande vyake atakavyovipiga.

Studio kubwa za kurekodi muziki zilikuwa mbili, studio ya Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) na studio za Tanzania Film Company (TFC). Zote zilikuwa na masharti yaliyofanya kazi ya kurekodi kuwa ngumu zaidi. Studio ya RTD ilikuwa inaipa kila bendi siku mbili za kurekodi. Siku ya kwanza kurekodi nyimbo mpya za bendi na siku ya pili kurekodi kipindi cha Club Raha Leo. Kila bendi ilikuwa inahitajika kuja na vyombo vyake. Mapema siku ya kwanza ya ratiba, bendi iliingiza vyombo studio na kazi ya kuvifunga na kuvitayarisha kwa kurekodi ilichukua muda wote wa asubuhi ya siku ya kwanza. Mchana baada ya kula ndipo wanamuziki walipoingia kurekodi nyimbo zao. Kulikuwa na sheria kuwa watu wote ambao si wafanyakazi wa RTD walitakiwa kuwa wameondoka eneo la RTD kabla ya kushushwa bendera saa 12 jioni. Hivyo basi bendi kama ilikuwa na nyimbo 4 au 10 ililazimika kukamilisha kazi ya kuzirekodi zote hizo kati ya saa 8 mchana mpaka saa kumi na mbili jioni. Kama nilivyosema awali, nyimbo zilitakiwa kupigwa na kuimbwa  bila kukosea, kwa kweli kazi iliyokuwa ikifanywa na wanamuziki wa enzi ile ni ya kusifika. Ukisikiliza kwa makini kuna nyimbo nyingi maarufu zilizopendwa huwa zinakuwa na makosa madogo madogo, lakini mara nyingi ilikuwa ni  kutokana na hali niliyoitaja hapo juu. Kuna wimbo mmoja wa African Fiesta ambao alikuwa anaimba Tabu Ley unaitwa Ndaya, wakati wa chorus unamsikia Tabu Ley akijichanganya maneno , lakini nadhani ilionekana upite, hii ilikuwa ikitokea pale wimbo umesharudiwa mara nyingi na wanamuziki wamekwisha choka.
Fundi mitambo alikuwa akitupigia wimbo tusikie baada ya kurekodi na alikuwa akiuliza' Vipi huu?' wenyewe tukiwa tumeridhika tulijibu 'Upite'.

TFC hawakuwa na masharti ya muda wa kuondoka studio, TFC ilikuwa shirika la umma na hivyo  lilikuwa likiendeshwa kibiashara na malipo ya studio yalikuwa kwa  siku. Kwa kuwa bendi hazikuwa na fedha, mara nyingi zililipa malipo ya kutumia studio siku mbili zikizidi sana tatu. Hapo ilikuwa wanamuziki wenyewe wanakuwa makini ili kutumia vizuri muda wao, ili usije ukaisha na fedha za kuongeza muda zisiweko. Nikiwa Vijana Jazz tulitumia studio za TFC kurekodi album iliyokuwa na nyimbo maarufu kama Thereza, VIP na Mfitini. Tulikesha siku mbili kukamilisha album ile.

Teknolojia ya sasa inaruhusu mtu mmoja kama unauwezo wa kupiga vyombo mbalimbali na kuimba,ukaweza hata kutengeneza nyimbo ambazo zitasikika kama vile ni bendi nzima ilikuwa kazini. Kwa mfano kati ya album za kwanza za wanamuziki wa Tanzania ambazo zilitoka kwa kutumia teknolojia hii ya sasa  ya ‘multi track’ ni album ya Dhiki ya Patrick Balisidya. Katika album hii Patrick alipiga vyombo karibu vyote na pia kuimba sauti zote, ukisikia nyimbo hizo utadhani zilipigwa na bendi nzima.

Pamoja na ubora wote wa teknolojia hii, kurekodi kwa mtu mmoja mmoja kunaondoa sehemu kubwa ya utamu katika nyimbo zilizorekodiwa. Hebu fikiria ngoma yoyote ya kiasili, irekodiwe kwa mpigaji ngoma moja moja kuingia studio na kurekodi mapigo yake, utamu ule wa wapigaji kupeana hamasa wakati wa kupiga wote utaondoka. Pengine ndio sababu nyimbo za sasa zinarekodiwa na kusikika vizuri lakini zinakosa uhai fulani wa wapigaji kupiga kwa pamoja, na kuhamasishana, kupata ile 'feeling ya live'. Nyimbo za bendi zamani zilikuwa kwanza tayari zimeshapigwa mara nyingi katika kumbi mbalimbali hivyo kuwa na aina ya uhai ambao huwezi kuupata katika wimbo ambao ni mpya kabisa. Utaratibu huu uliwezesha bendi kuboresha wimbo hatimae siku ya kurekodi wimbo unakuwa umeiva.

No comments:

Post a Comment

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...