YOUTUBE PLAYLIST

Wednesday, August 24, 2022

NIMEPITWA NA WAKATI NGOJA NIKAPUMZIKE

 


Nilipokuwa mdogo nilikuwa naona vibabu vya mtaani kwetu viko vya aina mbili, aina ya kwanza ilikuwa vibabu ambavyo vilikuwa havicheki kila saa vimenuna na kwa ujumla, watoto wote tuliviogopa, na tulianza hata kutunga hadithi kuwa vitakuwa vichawi, au vilipata matatizo makubwa wakati wa ujana na kadhalika. Kundi la pili la vibabu ilikuwa vile vibabu ambavyo huvikuti vimenuna, ukiviamkia vinakujibu kwa furaha na kuanza kuulizia wazazi wako, mambo yako ya shule na kadhalika. Vibabu hivi hata kama una shida ilikuwa rahisi kukusikiliza na kukupa ushauri hata msaada. Na pia kulikuwa na vibibi vya aina hiyohiyo pia, tulikuwa na rafiki yetu bibi yake alikuwa anauza maji, kila baada ya siku chache tulikuwa tukimtembelea bibi kwa kuwa lazima atatugawia senti  kumi kumi kutokana na biashara yake ndogo ya maji, kwa hesabu za harakaharaka alikuwa akitugawia pato lake la siku nzima bila hata kusita, na wala hatukuwa wajukuu zake wa moja kwa moja. Sasa yamenikuta siku hizi mimi ndie sasa nimekuwa babu, na polepole naanza kupata picha kwanini wale babu na bibi zangu walikuwa vile.
Wahenga walikuwa na msemo, nyani mkongwe kakwepa mishale mingi, na ndio ilivyo katika maisha, wakongwe wamekwepa mengi, wameona mengi, kwa asili ya mila na tamaduni zetu, wazee walikuwa na nafasi muhimu katika kutoa ushauri wa mambo kadhaa, lakini hili linapotea taratibu, na hasa ukichukua dhana ya siku hizi isemayo ‘wazee wamepitwa na wakati’.
Wasanii ni sehemu ya jamii, hivyo hata kwenye tasnia hii dhana ya ‘wazee wamepitwa na wakati’ inatumika sana.
Ukongwe katika fani unakupa elimu ya mambo mengi, mengine unafundishwa na wakongwe uliowakuta, mengine unajifunza kazini, hatimae kichwa kinakuwa na majibu ya mambo mengi ambayo kwa utamaduni wa zamani unatakiwa kuyarithisha kwa wanaochipukia katika fani. Lakini hili linakuwa gumu pale inapokuja dhana kuwa ‘wazee wamepitwa na wakati’. Ukisha kutana na hali ya kuonekana umepitwa na wakati kuna mambo mawili unaweza ukaamua, moja unaweza ukawa mtu wa kukasirika kila wakati, kiasi cha kwamba mtaani ukaonekana ni babu moja mwenye hasira zisizo na sababu, watoto wakaanza kuhadithiana kuwa utakuwa mchawi au ulipata matatizo ya akili ulipokuwa kijana. Jambo la pili linaloweza kutokea ni kuamua kuwa mchangamfu na kubaki unacheka na kila mtu, ili usisumbue kichwa chako, na hatimae kuondoka duniani na elimu yako kwa furaha.
Kwa kicheko na furaha sana nakumbuka enzi kabla hakujawa na Baraza la Sanaa la Taifa. Enzi hizo  kulikuwa na taasisi inaitwa Baraza la Muziki la Taifa (BAMUTA), chombo kilichoanzishwa mwaka 1974. Kazi ya BAMUTA ilikuwa kuratibu shughuli za muziki na muziki wa aina zote. BAMUTA iliuangalia muziki kwa mapana yake yote, elimu, vifaa, masoko, maadili, BAMUTA pia ilikuwa na kazi ya kuandaa sera za Taifa za muziki. Katika kipindi cha BAMUTA bendi zilisaidiwa vyombo vya muziki na serikali, BAMUTA ilitungwa vitabu kadhaa vilivyohusu muziki, ukiwemo muziki wa asili. Mitaala ya muziki ilitayarishwa na muziki ukawa somo mojawapo linalofundishika mashuleni, waalimu wake walitayarishwa katika vyuo vya waalimu wa sanaa kama vile Chuo cha Butimba, na wakaenezwa katika vyuo na mashule nchini kote, wengine wakawa maafisa utamaduni na wengine kuwa katika ngazi mbalimbali za wizara ya Utamaduni na sanaa. Kila mkoa ulikuwa na japo bendi moja iliyokuwa na umaarufu, kulikuwa na kwaya nyingi, madisco mengi,  japo wakati huo uwekezaji katika muziki haukuwa mkubwa kama ulivyo sasa. Mazingira yakawekwa yaliyoruhusu wapenzi wa muziki waweze kusikiliza aina mbalimbali za muziki hata muziki ule ambao si wa kibiashara lakini ni mzuri kwa ubora wake au kwa ujumbe wake. Mazingira hayo yaliwapa wanamuziki maktaba pana ya kuweza kutohoa aina mpya za muziki. Wajumbe wa BAMUTA walitoka kila kona ya nchi na hivyo kuipa BAMUTA sura ya Kitaifa, angalia orodha ya wajumbe wa Baraza la Muziki Tanzania;

1.   Boniface Musiba (Mwenyekiti wa BAMUTA)
2. D. R. Mbilinyi (Mwenyekiti Msaidizi wa BAMUTA)
3. S. Chidumizi (Mjumbe wa BAMUTA-Dodoma)
4. J.Y. Sapali (Mjumbe wa BAMUTA-lringa)
5. Padre J.M. Buluma (Mjumbe wa BAMUTA-Mwanza)
6. A. Kosana (Mjumbe wa BAMUTA-Shinyanga)
7. R. Singano (Mjumbe wa BAMUTA-Tanga)
8. Mbaraka Mwishehe (Mjumbe wa BAMUTA-Morogoro)
9. Padre Kayatto (Mjumbe wa BAMUTA-Mbeya)
10. Gwabukoba (Mjumbe wa BAMUTA-Kigoma)
11. P. Balisidya (Mjumbe wa BAMUTA-Dar es Salaam)
12. R. Mselewa (Katibu Mtendaji wa BAMUTA)
13. E. Kavalambi (Mkufunzi wa Muziki-Marangu CE.T.)
14. K. J. Nsibu (Aflsa Utamaduni-Korogwe)
15. E. Lameck (Mwanakwaya-Mwatex)
16. G. Kanyabwoya (Mwalimu-Kigoma)
17. T. Busyanya (Mkufunzi wa Muziki-DSM CE.T.)
18. G. Daudi (Afisa Sanaa za Maonyesho-Rukwa)
19. John Mgandu (Mwalimu wa Muziki-Tabora Shule ya Seko-ndari ya Wavulana)
20. E. G. Makala (Wizara ya Utamaduni)
21. F.E. Nkwera (Mkufunzi wa Muziki-Songea CE.T.)
22. T. Nkera (Mkufunzi wa Muziki-Ndwika CE.T.)
Wakati ufanisi wa Baraza hili ukiendelea, akatokea mtu mmoja akaanzisha wazo la kuwa na Baraza moja kwa ajili ya Sanaa zote, na ndipo likazaliwa Baraza la Sanaa la Taifa. muziki ukashushwa na kuwa ni Idara tu katika katika Baraza hili, tena hata hiyuo idara ilisha uwawa .

Lakini nisijichoshe, ngoja nikacheze na watoto, si unajua wazee tumepitwa na wakati.

 

1 comment:

  1. Anonymous19:07

    Ha ha ha hakika uendeshaji wa masuala ya muziki kwa hivi sasa nchini yamebadilika sana. Hoja yako nimeielewa ila wakati, tekinolojia na utandawazi vimebadilisha kabisa namna yetu ya kuendesha shughuli na biashara nzima ya muziki hapa nchini Tanzania.

    ReplyDelete

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...