Katika
miaka ya karibuni, utamaduni wa kila bendi kuwa na mtindo wake umefifia sana.
Lakini ulikuwa utamaduni uliokuwa maarufu sana kuanzia miaka ya sitini. Kila
bendi ilipoanza, ilijinasibu kwa kuja na mtindo wake, ingekuwa siku hizi
ingetambulika kama kuji ‘brand’.
Ni vigumu kutaja mitindo yote iliyowahi kugunduliwa kwani kuna mingi ambayo
haikuwahi kupata nafasi kutambuliwa katika vyombo vya utangazaji au
kuwekwa katika kumbukumbu za aina
yoyote. Majina ya mitindo mingine ilikuwa na sababu au historia na maana
maalumu, lakini majina mengine yalikuwa ya kutunga tu na kwa kweli hata
waliokuwa waliokuwa wakiyatumia hawakuwa na maelezo ya maana ya maneno hayo.
Nakumbuka nikiwa bado mwanamuziki mdogo huko Iringa tulikuwa na bendi ambayo
mtindo wake ulikuwa ni Chikwala chikwala, namkumbuka aliyetunga jina hili,
alikuwa mpiga gitaa la rhythm ambaye pia alikuwa fundi saa. Hata yeye hakuwa na
maelezo ya maana kuhusu jina lile, ila kwa wakati ule, ilikuwa ni staili kwa
majina ya mitindo ya bendi kuwa na jina
linalojirudia rudia, hii ilitokana na bendi kadhaa Kongo kuwa na majina
yaliyojirudia rudia mfano Orchestra Lipua Lipua, Orchestra Bella Bella na
Orchestra Shama Shama.
Baadhi ya majina ya mitindo ya bendi yalikuwa Mundo, Saboso, Msondo, Sokomoko, Dondola, Toyota, Kiweke,
Segere matata, Super mnyanyuo, Vangavanga, Libeneke, Chakachua, Sululu,
Ambianse, Takatuka, Afrosa na majina mengineyo mengi. Bendi nyingi zilibuni
hata aina ya uchezaji wa mitindo yao, na uchezaji mwingine ulibuniwa hata na
wapenzi wa bendi hizi. Kila bendi ilikuwa ikijitahidi kuwa tofauti na bendi
nyingine. Kwa mfano katika mji wa Tanga ulikuwa na bendi kubwa mbili, Jamhuri
Jazz Band na Atomic Jazz Band, kuna wakati bendi ya Jamhuri ilikuwa na mtindo
wa Toyota, na baadae Dondola, wakati Atomic walikuwa na mtindo wa Kiweke, muziki
wao ulikuwa tofauti, hivyo Jamhuri ikawa na wapenzi wake na Atomic ikawa na
wapenzi wake, na mpaka leo, wazee waliokuwa wapenzi wa bendi hizi mbili hubaki
kusifia ubora wa bendi zao, wazee wa Jamhuri husifu mtindo wa upigaji wa gitaa
la rythm la Harrison Siwale(Satchmo), huku wapenzi wa Atomic watakwambia hakuna
kama Kiweke, kwani upigaji wa gitaa la solo wa John Kijiko, au bass la Mwanyiro
haukuwa na mpinzani. Kule Morogoro kulikuwa na Morogoro Jazz Band na Cuban
Marimba, bendi hizi zilikuwa na mitindo mbalimbali kwa nyakati mbalimbali, na
wapenzi wao walikuwa tayari kutetea ubora wa mitindo ya bendi zao. Cuban
Marimba wakisifia mtindo wa Ambianse, Morogoro wakisifia Likembe, au sululu. Na
hakika kulikuwa na tofauti kubwa ya mitindo hii miwili japo ilipigwa na bendi
zilizotoka mji mmoja.
Nimeanza kwanza kwa kutaja bendi zilizokuwa katika mji mmoja, tena huko mikoani
ambako kwanza miji ilikuwa bado na watu wachache kulinganisha na sasa,
wanamuziki walikuwa wanajuana na kuishi jirani, hali hiyo ndio iliyokuwa
Tabora, ambako pamoja na Tabora Jazz, kulikuweko na Nyanyembe Jazz, Kiko Kids,
lakini muziki wa kila bendi ulikuwa tofauti na mwingine. Dar es salaam kulikuwa
na bendi nyingi na hivyo mitindo mingi, na pia kulikuwa na bendi za watu wa
mataifa kutoka nje ya Tanzania. Kulikuwa na bendi za Magoa, kulikuwa na bendi
za Wakongo, nao pia wakawa na mitindo yao. Hakuna aliyeweza kuchanganya mtindo wa Ogelea
piga mbizi ya Maquis na mtindo wa
Chunusi wa Orchestra Safari Sound, hata
pale ambapo wanamuziki wa kutoka bendi moja walipohamia bendi pinzani kila
bendi ilibaki na staili yake na kuilinda kwa kuongeza ubora kila mara. Hivyo
haikuwezekana ukasema Sikinde na Msondo
zilipiga muziki uliofanana au mitindo ya Sokomoko na Afrosa ilikuwa na ukaribu.
Kikubwa ninachotaka kueleza ni kuwa bendi kuwa na mtindo ilikuwa si jina tu
bali kulikuweko na kazi ilifanyika ili kupata, kulinda na kuendeleza mtindo
ambao bendi iliamua kuwa nao. Nakumbuka wakati wa mazoezi enzi hizo unaweza
ukatunga wimbo ukianza kuimba wenzio watakwambia mbona unafanana na bendi
fulani na hapo utakarabatiwa mpaka uwe katika mtindo wa bendi husika.
Wiki
chache zilizopita nilipata bahati ya kuhudhuria onyesho moja la bendi iliyoko
Mbeya, baridi ndio ilinilazimisha kukumbuka kuwa niko Mbeya, upigaji, uchezaji,
uimbaji wa bendi hii ulikuwa kama bendi nyingi zilizopo Dar es Salaam. Bendi
zimekuwa kama vile zimepewa amri kuwa lazima zipige muziki unaofanana. Toka umeingia
mtindo wa ‘sebene’ mwanzoni mwaka 2000, basi ni kama kila ubunifu
umesimamishwa. Hata zile bendi ambazo hupiga nyimbo za bendi ya zamani,
hulazimisha kuingiza sebene, kwenye nyimbo hizo. Juzijuzi kwenye onyesho moja
kubwa la muziki, bendi moja ilikuwa ikipiga wimbo wa Super Volcano unaoitwa
Shida, ghafla ukabadilika kwa kuongezewa sebene. Kipindi aina ya muziki wa sebene ulipokuwa
ukiingia nchini, kulikuwa na aina ya muziki wa hapa nyumbani uliokuwa unaitwa
Mchiriku. Sasa toka wakati huo,Mchiriku umeweza kujiongeza na kubadilika mpaka
sasa unaitwa singeli, tena hata hiyo singeli imeanza kuota matawi, lakini wanamuziki
wa dansi wamekwama palepale kwenye sebene. Hili linanikumbusha enzi za
teknolojia ya santuri, santuri zilikuwa zinaweza kupata mchubuko na hivyo
sindano ikakwama sehemu moja, ikawa inarudia kupiga muziki sehemu ileile
haiendi mbele wala hairudi nyuma mpaka betri itakapoisha.
No comments:
Post a Comment