YOUTUBE PLAYLIST

Wednesday, August 31, 2022

USUPA STAA NI DHANA YA ZAMANI INAYOBORESHWA NA TEKNOLOJIA

 




Ma ‘superstar’ ni watu ambao wametokea kujizolea umaarufu mkubwa katika jamii. Superstar anaweza kuwa ametokea katika nafasi mbalimbali katika jamii, anaweza akawa mwanasiasa, mwalimu, mkulima au mtu yeyote katika jamii, hapa kwetu sifa hii zaidi huhusiana na wasanii. Sifa ya ‘usupastaa’ imejitokeza zaidi baada ya tasnia ya filamu kukua, jambo ambalo limeenda sambamba na kuongezeka kwa vyombo vya utangazaji.  Na kwa kweli katika zama hizi tunao watu wengi ambao wanapewa sifa  ya ‘u superstar’ katika jamii. Hakuna chuo maalumu cha kufundisha usupastaa kwani umaarufu wa mtu huweza kutokana na sababu mbalimbali. 

Wasanii huingia katika sanaa kwa njia na sababu mbalimbali, wengine huzaliwa na kipaji, wengine huingia katika fani hiyo kama njia ya kutafuta maisha, wengine huingia kwa kuiga wenzao waliomo katika sanaa, kuna hata waliolazimishwa na ndugu na jamaa kuingia katika fani ya sanaa, na kadhalika. Kutokana na sababu hizi mbalimbali za kujiingiza kwenye sanaa, waliomo humu nao wanakuwa na mategemeo mbalimbali yatakayopatikana katika fani hiyo. Wengine nia yao ni kutengeneza sanaa nzuri, bila kujali sifa wala malipo, wengine wanafanya sanaa ili wapate kipato kizuri na wengine wakitegemea sifa tu kutokana na ubora wa kazi yao. Na wengine kutumia sanaa kama jukwaa la kufanyia shughuli nyingine kabisa ambazo hazihusiani na sanaa. Wasanii waliomo katika sanaa kutafuta kipato, hulazimika kutafuta mbinu mbalimbali ili sanaa yao iuzike, na moja ya njia kubwa ya kuhakikisha sanaa inauzika ni kwa wao kuwa maarufu. Watu wengi wanatabia ya kufuatilia maisha na kununua kazi za sanaa za watu maarufu. Kutokana na sababu hii, msanii huanza mbinu mbalimbali za kupata umaarufu. Msanii atajitokeza kwenye vyombo vya habari kutangaza kazi zake na hata kuelezea maisha yake, picha zake nzuri kusambazwa,na hata kazi hizo kusambazwa ili watu wengi wazifahamu.

Katika nchi ambazo tasnia imejengeneka vizuri, kuna makampuni maalumu ambayo hutumia mamilioni ya fedha kujenga sifa za msanii husika na kazi zake, kwa kutegemea faida kubwa baadae. Msanii huingia katika mikataba ya muda mrefu na kampuni huwekeza katika kujenga sifa ya msanii ili kupata wateja wengi wa kazi za msanii huyo.

Je unapataje ‘u super star’ hapa Tanzania? Kama ilivyo duniani kote kuna wasanii ambao kazi zao zimepokelewa vizuri na jamii na kuwafanya wasanii mbalimbali kuwa maarufu kwa urahisi sana. Lakini kuna mambo mengi ambayo yanapita nyuma ya pazia katika kupata ‘u superstar’ hapa kwetu. Rushwa ni moja ya jambo kubwa katika kujenga ‘ma superstar’ wa hapa kwetu. Na hili halikuanza karibuni, kwa wanamuziki wa zamani wanaelewa hali ilivyokuwa enzi kulipokuwa na redio moja tu, ilivyolazimika kutoa rushwa ili mashahiri ya nyimbo walizotaka kurekodi yakubalike na nyimbo zirekodiwe, kisha kutoa rushwa ili nyimbo zilizorekodiwa zipigwe kwenye vipindi mbalimbali huku sifa za kujenga usupastar wa wasanii hao zikimiminika, hali hii haiko tofauti sana na sasa japo kwa sasa kuna utititiri wa redio na luninga. Watangazaji wengi wamefaidika na rushwa kutoka kwa wasanii waliokuwa na hamu ya ‘kutoka’. Kuna wakati watangazi wa redio mbalimbali walitengeneza umoja, ambapo mwanamuziki alikuwa akilipia ili kazi zake zirushwe hewani. Watangazaji wa vipindi vya redio wengi waligeuka kuwa mameneja wa wasanii na hivyo kuhakikisha wanawatangaza wasanii wao ili wawezekuwa ‘ma supersta’. Rushwa ya ngono sio siri katika tasnia ya sanaa katika kutafuta ‘u superstar’ . Wasanii wa kike wengi wana hadithi ya kupitia katika mtihani huu katika kutafuta ‘kutoka’. Kuna wakati wasanii  wawili wakubwa wa kike, walitangaza mpango wa kuanza kuwajenga wenzao ili wasipitie adha ya kudaiwa rushwa hii. Jambo ambalo linaonyesha wazi kuwa rushwa hii bado iko hai.

Katika kutafuta ‘U superstar’, kuna wasanii ambao wamefanya mambo mengi ya ajabu ikiwemo kutunga visa ambavyo vingewaweka katika vichwa vya habari. Habari za msanii kufumaniwa, kupigwa, kulewa, kulazwa hospitali, kupendana, kuachana na kadhalika vimekuwa vikitungwa na wasanii mbalimbali ili kujiweka katika nafasi ya kutengeneza hadithi kwenye vyombo vya habari kujiongezea umaarufu. Ujio wa mitandao ya kijamii umekuwa tena nafasi nzuri za kutengeneza ‘U superstar’ wasichana ambao wamekuwa wanatumia sanaa kama daraja la kupata ‘U superstar’, wamekuwa wakitumia kurasa zao kwa kutundika picha wakiwa nusu utupu ili mradi kutafuta kujulikana na kupata wateja wa shughuli isiyohusiana na sanaa.

Matokeo ya vurugu hizo zote ni kuwa msanii kuwa ‘superstar’ si lazima awe msanii bora. Wako wasanii wa aina hiyo wengi na ukiulizia kazi zao za sanaa, hazionekani au hazijulikani. Na kwa kazi zao za kisanii ambazo hutolewa hadharani, huishia kupotea baada ya muda mfupi, lakini sifa za ‘u supersta’ zinaendelea kujengwa kwa namna moja au nyingine. Jambo ambalo ni bahati mbaya kwa tasnia nzima ya sanaa, nikuwa masupastaa hawa wajanja wajanja huaminiwa sana hata na viongozi wa ngazi za juu nchini,  na hutumika kama vigezo vya kukua kwa tasnia. Na mara nyingine huombwa hata kutoa ushauri wa namna ya kuboresha tasnia ya sanaa. Mungu isaidie tasnia ya sanaa Tanzania.

No comments:

Post a Comment

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...