YOUTUBE PLAYLIST

Tuesday, August 23, 2022

SEHEMU YA RIPOTI YA TAMASHA LA BENDI LA TANZANIA LIVE MUSIC FESTIVAL 2012



Baada ya matayarisho mbalimbali yaliyochukua miezi mitatu hatimae tarehe 28 September 2012, bendi ziliweza kuanza kupanda jukwaani kufanya maonyesho katika viwanja vya Leaders Club.  Bendi zilizopanda jukwaani karibu zote zilikuwa na makubaliano ya kulipwa na zililipwa fedha ya awali wiki 2 kabla ya onyesho na fedha iliyobaki ilikamilishwa siku ambapo bendi zilipanda jukwaani. Hakuna bendi yoyote iliyokuwa ikiwadai watayarishaji.

Watayarishaji walijipanga kwa kuhakikisha kuna jukwaa la Kimataifa lililopambwa na taa za rangi za kiwango cha juu, na vifaa vya muziki ambavyo vilihakikisha kila bendi inapopiga muziki, muziki wake ulisikika kwa kiwango cha hali ya juu. Hakukusikika mpaka leo malalamiko kuhusu upande huo wa matayarisho.


MC BEN KINYAIA

Tamasha lilianza tarehe 28 September 2012, saa kumi na mbili jioni,  kwa bendi kuanza kufanya maonyesho, bendi ya kwanza kupanda jukwaani ilikuwa ni Msondo Ngoma Music Band na kufuatiwa na bendi ya Fm Academia, na baadae bendi za Akudo Impact, Mashujaa Band, kundi la Taarab la Mashauzi Classic na baadae vijana wa Orynx Band. Bendi zote zilifanya vizuri sana, bendi zilipanda  kwa zamu kama ratiba ilivyokuwa imewaelekeza na mshereheshaji  alikuwa ni Ben Kinyaiya alifanya kazi kwa umakini wa hali ya juu .

 

Tamasha liliendelea siku ya pili  kama ratiba ilivyokuwa imepangwa kwa bendi za Mlimani Park, Skylight band, B Band, Oryx Band, Bi. Khadija Kopa  kupanda jukwaani, na kama ilivyokuwa jana yake wakiongozwa na mshereheshaji  Ben Kinyaiya.





MAFANIKIO

Mafanikio yaliyopatikana ni uzoefu mkubwa wa namna ya kutayarisha tamasha la muziki wa bendi. Mawasiliano yaliweza kufunguliwa kati ya watayarishaji na wanamuziki wa bendi mbalimbali. Kumekuweko na mafanikio ya kujua namna ya kupata vyombo na mafundi bora wa sauti, upambaji wa jukwaa na matayarisho yote ya awali ya kuwezesha tamasha kufanyika. Kumepatikana uzoefu wa kuitisha press conference na kufanya mikutano na wadau mbalimbali wa matamasha, serikalini, katika kampuni binafsi na watu binafsi.



WADAU TAMASHA.

Tamasha hili liliandaliwa kwa ushirikiano kati ya Edge Entertaiment na Chama Cha Muziki  wa Dansi Tanzania(CHAMUDATA) baada ya makubaliano, ambayo yalifikiwa kukiweko na malengo ya kupata fedha kwa ajili ya kusaidia miradi ya CHAMUDATA na kutoa mchango kwa BASATA. Kampuni ya Edge Entertaiment iliingia  mkataba na Times Fm Radio ambao uliwezesha  Times Fm kulitangaza Tamasha  pia kutoa gharama za matumizi yote ya maandalizi ya tamasha  kwa makubaliano ya fedha zitakazotumika kurudishwa kutokana na mapato ya tamasha.



KAMATI.

Kamati ya pamoja ya Edge Entertaiment  na Times Fm Radio iliundwa na ikapewa majukumu ya kuhakikisha  tamasha linafanikiwa, kamati ilifanya kazi chini ya uangalizi wa upande zote mbili zilizokubaliana na kamati  iliomba kampuni ya Edge Entertaiment iajiri mtu wa PR atakayehakikisha mpangilio  mzuri wa Tamasha na Edge Entertainment ilifanya hivyo.



VYOMBO VYA HABARI.

Katika kuhakikisha tamasha linafanikiwa kamati ilitumia vyombo vya habari vifuatavyo Magazeti, Tv, Blogs, Radio

Magazeti yaliyotumika;

  (a)Mwananchi

  (b)Jambo leo

  (c)Mtanzania

  (d) Magazeti ya Global Publishers

Tv zilizotumika;

 (a) TBC - Mahojiano

 (b) Chanel Ten- Mahojiano

Blogs zilizotumika;

(a) Michuzi

(b) Full shangwe

(c) Dar blog

(d) www.musiciansintanzania.blogspot

Radio;

Radio iliyotumika ni Times Fm Radio hii ilitokana na udhamini ambao redio hii ilikuwa imetoa

 


MATATIZO.

Kulikuweko na matatizo kadha wa kadha, mengine ni kutokana na maamuzi yaliyofanyika, mengine ni kutokana na wadau mbalimbali wa Tamasha, na machache ambayo yalikuwa njee ya uwezo wa  Kamati ya tamasha

* Tamasha lilifanyika siku ya Ijumaa na Jumamosi, huu ulikuwa uamuzi ambao ulionekana kuwa ni mzuri, lakini kwa mawazo ya wadau waliohudhuria wengi waliona ingekuwa bora tamasha lingeanza Jumamosi na hatimae kufikia kilele Jumapili kwa maonyesho ambayo yangeanza Jumapili kuanzia saa nne asubuhi hadi kati ya saa4 na saa 6 usiku siku hiyo

* Pamoja na bendi kulipwa si chini ya shilingi laki saba kila bendi bendi ziliendelea kupanga ratiba zao na hata kutangaza kuwa wako katika sehemu nyingine kwa siku na wakati uleule ambapo bendi zilitegemewa kuwa jukwaani katika tamasha. Msondo Ngoma walipiga wimbo mmoja tu kwa malipo ya shilingi milioni 1.

* CHAMUDATA  kilikuwa mdau muhimu katika tamasha hili, kwanza kwa kuwa sehemu ya mapato yalikuwa yaiingie katika mfuko wa chama hicho, na pili hili lilikuwa tamasha la muziki wa bendi, hivyo kuwa linafanya kile ambacho chama hiki kinasimamia, lakini hakukuweko hata afisa mmoja wa  CHAMUDATA katika kipindi chote cha tamasha, ambapo ingetegemewa chama kiwe chombo kimojawapo cha kupigia debe mafanikio ya tamasha hili.

* Kulikuweko na matatizo ya matangazo ambapo palikuweko na matukio ya kubandua mabango, na wakati fulani kuchanganya taarifa katika matangazo ya magazeti.

* Pamoja na kuwa eneo la Leaders lilikuwa limelipiwa, bado uongozi wa bar ya Leaders ulikaidi na kuendelea kukiuka masharti kwa kuendelea kufanya mauzo ya vinywaji kinyume na utaratibu na makubaliano na wadhamini wakuu wa tamasha. Hili limepelekea wadhamini kugoma kulipa baki ya ada ya udhamini ambayo ni shilingi 10,000,000.

* Mgeni rasmi aliwasili kwa muda aliopangiwa ambao ulikuwa ni saa moja, hili lilikuwa kosa kwani muda huo ndio ratiba inaanza na si muda mzuri kwa mgeni rasmi kuwa ndio anawasili, pia hakukuweko na protokali za kumpokea mgeni rasmi jambo ambalo lilitia doa ujio wake. Na hivyo alishindwa hata kufanya shughuli ya kufungua rasmi tamasha

 


HITIMISHO.

Kwa ujumla Tamasha lilikuwa na mengi sana mazuri kiutendaji, vyombo vizuri na vya kisasa, stage kubwa ya kisasa, na  liliweza kufanyika  kwa bendi zaidi ya kumi kushiriki. Ni wazi ni muhimu utamaduni huu wa kuwa natamasha kila mwaka kuendelea japo matayarisho yanatakiwa kuanza sasa.
Wanamuziki wa mabendi walikatisha tamaa kwani wamekuwa wakilalamikia kukosekana kwa Tamasha lao,  lakini ni wazi walithamini zaidi kazi zao za kawaid kuliko Tamasha lililokuja kukidhi kiu yao.
 Kwa upande wa mapato hayakuwa mazuri waandaji  waliingia hasara  kubwa na  hivyo kushindwa kutimiza malengo yake likiwemo la kukisaidia Chama cha Muziki wa Dansi Tanzania (CHAMUDATA). Waandaji wataendelea na elimu na mafunzo mbalimbali kwa wanamuziki wa muziki wa dansi wakishirikiana na BASATA na CHAMUDATA ili kuweza kuleta mafanikio katika muziki wa dansi Tanzania.

Katibu

 


No comments:

Post a Comment

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...