YOUTUBE PLAYLIST

Monday, October 3, 2022

USHIRIKINA KATIKA MUZIKI HISTORIA NI NDEFUUUU


Imani ya uchawi ni utamaduni ambao umekuweko katika historia ya jamii zote za binadamu. Maandiko ya dini mbalimbali yanatuhakikishia kuwa jambo hilo lipo na hulilaani. Mara nyingi hudhaniwa kuwa kadri maendeleo na elimu yanavyoongezeka ndio imani ya ushirikina inavyopungua na kupotea, lakini ni wazi dhana hiyo si ya kweli, safari ya kuachana na uchawi bado ni ndefu sana, kwani ukipita katika mitaa mingi utaona vibao vikiashiria waganga wanaoweza kutibu matatizo  mbalimbali kama ‘kusafisha nyota’, ‘kuondoa majini’, ‘kurudisha mpenzi aliyekimbia’ na kadhalika, wasomi wenye milolongo ya shahada na stashahada si ajabu kabisa nao kuwakuta kwenye vibanda vya waganga wakitafuta kusaidiwa kwenye mambo ambayo  mtu mwingine ungetegemea yanawezekana kwa juhudi tu za kibinadamu.

Muziki haujakwepa kuguswa na dhana ya ushirikina. Muziki unatumika unatumika katika kufanikisha dhana ya uchawi na wanamuziki wengi wanaamini na kushiriki katika shughuli mbalimbali za uchawi.

Tuanze na dhana ya muziki iliyopewa jina la Kiingereza ‘ healing music’. Duniani kote waganga na wachawi hutumia muziki wa aina yake kupandisha mashetani au kuita mizimu na kadhalika, muziki huu ndio huitwa healing music, huku kwetu mara nyingine huitwa muziki wa kupandisha mashetani. 

Katika maisha yangu ya muziki niliona na kusikia vituko vingi vilivyohusishwa na imani ya uchawi. Mara ya kwanza kuanza kuona vitimbi hivi ‘live’ ni nilipojiunga bado mdogo na kuwa mwanamuziki katika bendi yetu ndogo huko Iringa. Tualianza kupiga muziki wenyewe wachache bila kuwa na wazo lolote la kuhusisha muziki wetu na imani yoyote ya kishirikina. Siku moja akaja mzee mmoja akatukaribisha kufanya mazoezi kwenye sehemu yake ya biashara, na kwa vile tulikuwa hatuna sehemu maalumu tuliona huu ni ufadhili mkubwa.  Tulihamishia vyombo vyetu vichache kwake, na haikuchukua muda mrefu tukagundua kuwa biashara yake ni uganga wa kienyeji. 
Siku moja akatueleza kuwa hatutaweza weza kuwa bendui kubwa bila ‘kusafishwa nyota’. Tulipewa dawa za kuoga na tukaendelea na mazoezi makali tukijua muda wetu wa kuwa bendi kubwa umewadia. Tulikubaliana kuwa tungepunguza deni la kazi yake ya kutusafisha nyota kwa kumlipa kidogo kidogo kila tulipofanya onyesho, kweli tukaanza kumlipa kila tulipopiga. Sikumbuki ni muda gani tuliendelea kumlipa yule mganga, japo kuwa hakuna chochote kilichobadilika katika hadhi ya bendi yetu.
Siku moja mganga yule alienda disco na akamtishia msichana mmoja kwa nyoka aliyekuwa nae mfukoni, hapo ndipo alipokamatwa na polisi na hatukumuona tena deni likayeyuka.
 Miaka mingi baadae nilikuja kujiunga na bendi moja kubwa jijini Dar es Salaam, hapo ndipo nilipoona tena shughuli za ushirikina. Ilikuwa ni siku chache baada ya kurekodi nyimbo mpya za bendi yetu katika studio za Radio Tanzania. Kulikuwa na kipindi kilichoitwa Misakato , kipindi ambacho kilitambulisha nyimbo mpya zilizorekodiwa na studio za redio hiyo, tulikuwa tumekubaliana kuwa wanamuziki wote tukusanyike nyumbani kwa kiongozi wetu ili wote tuzisikilize nyimbo zetu zikirushwa kwa mara ya kwanza hewani.  Zilipoanza kupigwa nyimbo zetu nikashuhudia mmoja wa viongozi wetu akiwa anaifukiza redio kwa moshi kutoka dawa zilizokuwa zimechomwa kwenye kifuu cha nazi,  hii ilikuwa kwa imani kuwa kwa kufanya hivyo, vibaovyetu vipya vikisikika vitatikisa roho za wasikilizaji wake. Katika kundi hili vituko vingi viliendelea hatimae tulizoea kuwa uongozi wa bendi yetu unaamini sana uchawi. Kuna wakati aliletwa mganga ambaye alidaiwa aliwahi kuifanya timu moja maarufu ya soka, ishinde kombe  na kuwa bingwa wa Taifa, hata jina lake aliitwa Bingwa, kutokana na sifa hizo bendi ilimchukua kwa mkataba na kazi yake ikawa ni kukaa mlangoni akijifanya ni muuza machungwa, hapo alitakiwa afanye vimbwanga vyake ili wateja wengi waingie kwenye muziki. Yeye alidai kila anapomenya chungwa kwa kuunganisha maganda kama mkanda, basi na wateja nao wataingia katika ukumbi kwa kuunganika kwa foleni ndefu, huyu alikaa nasi kiasi cha kuweza kuwa  katika misafara mbalimbali ya bendi tulipoenda ziara za mikoani. Harakati za bendi kutafuta umaarufu kwa uchawi ilifikia mpaka bendi ikasafiri hadi kwenda Mpanda, ambako viongozi wa bendi walikwenda kwa mganga na kufanya mambo yao ambayo yalihusisha na hata kumchinja mbuzi. Baadae walirudi na nyama ya mbuzi huyu mpaka tulipokuwa tumefikia, nadhani masharti yalikuwa ni sisi wanamuziki wote tule kipande cha mbuzi yule wa kafala. Sijajua mpaka leo viongozi walifanya nini na nyama ya mbuzi yule maana wanamuziki walifanya mgomo wa kumla yule mbuzi.
 Ushirikina una matatizo ya kufanya watu wasiaminiane hata kwenye bendi yenyewe, haikuchukua muda mrefu bendi ilipoanza kupoteza umaarufu, Kiongozi wa bendi akaaitisha mkutano na kutuambia kuwa kuanguka kwa bendi kunatokana na mmoja wetu kuiloga bendi, hapo ikatolewa tishio kuwa mtuhumiwa asipojitaja mwenyewe na kuomba msamaha mganga aliyeagua hilo aliahidi atamfanya awe kichaa. Jambo ambalo liliungwa mkono na wote kuwa kama ni kweli kuna mtu namna hiyo basi apate uchizi. Hakuna aliyekumbwa na tatizo hilo mpaka leo.
Miezi michache baadae, wanamuziki wawili walioamua kuacha bendi walirudisha sare za bendi kama ilivyokuwa kawaida zama zile. Shati zilikuwa zimechanywa kwenye kwapa na suruali kuchanywa kwenye maungio ya miguu kwa imani kuwa hizo ndizo sehemu zenye jasho kwa hiyo kama wangerudisha sare zao bila kuondoa sehemu hizo wangeweza kurogwa kirahisi na kuharibiwa maisha.

Mpiga tumba mmoja tuliyekuwa nae bendi moja alinichekesha aliponihadithia kuwa kiongozi wa bendi yao moja aliyopitia, aliwahi kuwapeleka kwa mganga aliyewataka waende na vyombo vyao vya muziki. Kisha akawa ana chanja chombo na kukipaka dawa,na baada ya hapo kumchanja mwenye chombo matakoni na kumpaka dawa!!!!
Katika mizunguko kwenye bendi mbalimbali, siku moja bendi yetu ilikuwa na mpambano wa kupiga bendi zaidi ya moja katika ukumbi mmoja. Hili lilichukuliwa kuwa ni jambo kubwa na la hatari linalohitaji matayarisho,  mganga maalumu lazima atafutwe ili kuilinda bendi isimalizwe na wapinzani. Ilikuwa inaaminika kuwa katika mpambano wa bendi, uchawi hutumika kuimaliza bendi ambayo itakuwa haina kinga, siku moja kabla ya pambano, maboksi ya spika yalifunguliwa na ndani yake  kuliwekwa tunguli na hirizi mbalimbali tayari kwa mpambano. Nakumbuka siku hiyo bendi pinzani nayo iligoma kupanga vyombo kwenye jukwaa kuu kwa madai kuwa kuna mbuzi alifukiwa katika jukwaa lile.

Kwa ukweli kabisa hata wanamuziki kutembeleana mara nyingine ilikuwa ni vigumu, kwani ukionekana mwanamuziki wa bendi nyingine katika ukumbi, basi bendi iliyo jukwaani haina raha, anaweza hata akatumwa mtu kufuatilia kila utakachofanya. Na ilikuwa vigumu kuruhusiwa kugusa vyombo vya bendi nyingine kwa wasiwasi wa kuwa unaweza ukaloga kile chombo. Niliwahi kuona bendi ikisimamisha muziki katikati ya onyesho na kudai shabiki mmoja wa bendi pinzani, tena alikuwa mwanamke, atolewe ukumbini kwani alikuwa ametumwa kufanya ushirikina, na hakika alitolewa nje.

Kulikuwa na hadithi nyingi zilizoonyesha ni kiasi gani cha ushirikina bendi ziliweza kufanya ili kupata wateja. Kuna bendi ambayo ilisifika kuwa kila wakimaliza kupiga muziki walipita katika kumbi mzima  na kuokota vizibo vya chupa za bia na soda, mifupa na mabaki ya nyama zilizotupwa na wateja, na hata kupata maji toka vyoo vya ukumbi na kwenda kuloga ili wale walioingia wasiingie bendi nyingine yoyote kasoro yao. Bendi nyingine zilidaiwa kuwa ziliweka mkataba ambapo zililazimika kutoa kafala ya mtu mmoja kila mwaka, hivyo viongozi wa bendi kufiwa na watoto, ndugu na hata wanamuziki wageni waliojiunga katika bendi hizo kukutwa na mauti ambayo habari za chini chini zilidai ni katika kutoa kafala.

 

Bendi mbili ambazo zilikuwa na upinzani mkubwa katika jiji la Dar es Salaam zilidaiwa hata kutaka kuweka uchawi katika chanzo cha maji Dar es Salaam , na kujikuta wakitaka kuumbuana hadharani kuhusu hilo.
Kuna wanamuziki wapiga magitaa wa zamani waliowahi kupatwa na matatizo ya akili na wazee wengi mpaka leo hudai matatizo yao yalitokana na ushindani wa uchawi katika bendi zao. Kama nilivyosema imani ya uchawi huleta kutokuaminiana na hata madhara makubwa ya kutuhumiana mambo ambayo mara nyingi hayana ukweli wowote. Kuna mwanamuziki niliyejaribu kumshawishi aingie katika bendi niliyokuwa nikipigia , alikataa katakata kwa kuwa alidai mmoja wa wanamuziki katika bendi hiyo ni mchawi.
Mwanamuziki mmoja mpiga gitaa mahiri aliwahi kunihadithia jinsi alivyopita uchochoro wa nyumba ya mwanamuziki mwenzake akashangaa kusikia jina lake likitajwa na mwenzie aliyekuwa chumbani kwake na kusema,’ Nyota ya …….(jina la mwanamuziki huyo) izimike kama kaa hili’, akadai alichungulia katika ufa na akakuta mwenzie anatumbukiza kaa la moto kwenye maji.
Ugonjwa wa ukimwi ulipoanza kuuwa wanamuziki kwa mara ya kwanza mara nyingi ulihusishwa na uchawi. Rafiki yangu mmoja nilipomtembelea wakati akiwa hoi kitandani akanambia,’Nikupe siri? Mi ntakufa lakini nauawa na wanamuziki wenzangu kwenye bendi. Nimepata mganga kanitajia na majina kabisa’. Miezi michache baadae mwanamuziki huyu kabla hajafariki alinambia,’Mjomba sijalogwa wala nini, udude huu, unaniua udude’. Alifariki siku chache baada ya kunambia haya.
Kama nilivyosema awali, elimu na teknolojia hazijaondoa kabisa dhana ya uchawi. Siku moja nilimsikia producer maarufu akiwakanya wasanii wa muziki wa Bongofleva wanaoingia studioni mwake, wasifanye mambo ya ushirikina kwenye studio yake.

Na siku chache baada ya hapo tena mwanamuziki mwingine wa muziki huo kawataja ambao aliwaita wabaya wake wanaomloga.!!!!!!! Nikaona loh kumbe shughuli bado inaendelea, wanamuziki hawa wenye umri mdogo tayari wamekwisha jenga imani ya kulogana katika enzi hizi za dijitali, safari bado ndefu sana, USHIRIKAINA BADO UKO HAI KATIKA SANAA YA MUZIKI

2 comments:

  1. Anonymous16:42

    Ushirikina ni sumu Kubwa sana

    ReplyDelete
  2. Anonymous17:16

    Aisee, Mimi ni mmoja wa watu wasioamini mambo hayo ya ushirikina, ninachoamini ni juhudi ya kazi, Kwa upande wa Muziki na Wanamuziki kikubwa ni ubunifu wa Kazi zao, ubunifu ndiyo hasa mlango wa mafanikio kwa kazi zao

    ReplyDelete

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...