YOUTUBE PLAYLIST

Saturday, November 5, 2022

HISTORIA FUPI YA TAARAB YA TANGA

Marehemu Waziri Ally akiwa mdogo akiwa anapiga kinanda katika bendi ya Lucky star

Katika miaka ya 50 wanawake tisa wa Tanga walijikusanya na kuanzisha  kikundi cha kuimba walichokiita Raha til Fuad maana yake Raha ya Moyo. Akina mama hawa chini ya bibie aliyeitwa Mama Akida au aka Mama Lodi, waliendesha kikundi chao wakiwa wanaimba nyimbo za Siti Binti Sadi na tungo zao ambazo waliimba katika melody ya nyimbo za kihindi zilizotamba wakati huo. Kundi hili liliendelea na kuanza kuruhusu wanaume kujiunga hasa wakiwa wapiga vyombo. Hata mtoto wa Mama Akida, Akida Jumbe hatimaye alijiunga na kundi hili kama mpiga accordion kwenye mwaka 1962. Kundi hili ambalo baadae lilikuja kuitwa Young Noverty, liliendelea mpaka kukaweko na mgawanyiko uliozaa kundi la Shaabab Al Waatan ambalo lilitawaliwa zaidi na wanaume.
 Hapo ndipo kukaanza mtindo wa kuweko kundi pinzani katika muziki wa taarab wa Tanga. Jambo ambalo kwa njia ya ajabu sana kwa kipindi kirefu likawa  linadumu kiasi cha miaka kumi kumi. Miaka ya 60, Young Noverty na Shabaab al Waatan, Miaka ya 70 Lucky Star Musical Club na Black Star Musical Club, miaka ya 80 Golden Star Taarab na White Star Taarab, miaka ya 90, Babloom Modern Taarab na Freedom Modern Taarab. Taarab ya Tanga kwa kweli ndio  haswa inastahili kuitwa Modern Taarab, kwani wao hawakufuata Taarab ile iliyoletwa Zanzibar enzi ya Sultan Seyyid Barghash.
Taarab ya Tanga ilikuwa ni ya makundi  yenye wanamuziki wachache kuliko makundi ya Taarab ile ya Zanzibar.
Vyombo vya vikundi vya Taarab ya Tanga
vilikuwa ni pamoja na Gitaa la besi, gitaa la solo, drums bongos ,akodion au kinanda. Nyimbo zao zilikuwa fupi na si ndefu kama zaTaarab ya Zanzibar au ambayo huitwa Taarab asili. Nyimbo za Taarab ya Tanga zilitegemea mipigo ya ngoma za asili za kumbwaya na chakacha na hata baadaye mitindo kama rumba,bossa nova. Na Taarab ya Tanga ndio iliyoanzisha moto wa vikundi vya taarab Tanzania Bara. Moshi kulikuwa na New Alwatan, AzimioTaarab, na Blue Star Taarab , Arusha kulikuweko na Blue Star Taarab, Dodoma ilikuwepo Dodoma Stars, Kondoa  kulikuwa na Blue Stars, Mbeya kulikuweko na Magereza Kiwira, Mwanza kulikuwa na Ujamaa Taarab, Bukoba  walikuwa na Bukoba Stars, na muendelezo huu uliingia mpaka Burundi kutokana na mwana muziki mmoja alie julikana kama Athmani Mkongo, alitoka Burundi na bendi yake kufika Tanga akahama kutoka muziki wa dansi na kuwa mwanamuziki mahiri wa Taarab na baadae kuipeleka kwao Burundi kukazaliwa kundi maarufu la Jasmine Taarab.


No comments:

Post a Comment

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...