Kila jamii
ina muziki, kuna aina mbalimbali za muziki na zenye matumizi mbalimbali, kadri
ya utamaduni wa jamii husika.
Katika zama hizi hasa mijini, muziki huonekana hasa kazi yake ni kwa kuleta
burudani. Lakini kwa asili katika jamii zetu mbalimbali muziki ulikuwa na
matumizi ya aina nyingi na hata kupewa majina kutokana na shughuli husika.
Kati ya shughuli ambazo muziki ulitumika na sehemu nyingine bado unatumika ni kwenye matambiko, tiba, misiba, sherehe mbalimbali kama mavuno, harusi
na kadhalika.
Leo niongelee muziki na siasa za nchi yetu.
Kabla ya Uhuru, katika maeneo mbalimbali nchini, wanamuziki kama marehemu Mzee
Moses Nnauye walianzisha vikundi vya muziki kuhamasisha kudai Uhuru, vikundi
vya kwaya, ngoma za asili, na muziki wa taarab na muziki wa dansi, vilitunga
nyimbo zenye ujumbe ambao uliwafikia
vizuri wananchi wengi na hivyo kuwahamasisha kuwa wana haki ya kujitawala na
kuanza kudai Uhuru.
Mara baada ya kupata Uhuru,Disemba 9 1961, vikundi vya muziki vilitunga nyimbo zilizoongelea furaha ya
kupata Uhuru na pia kuanza kuelezea ndoto za
wananchi baada ya uhuru. Mahusiano ya muziki na siasa yaliongezeka sana,
na baada ya Tanzania kuamua kuwa nchi ya Kijamaa, serikali iliwekeza sana
katika sanaa, kwani ilitambua kuwa hiyo ilikuwa njia muhimu ya kufikisha
taarifa ya malengo ya serikali. Pamoja na kuweko majengo yalikuwa maalumu kwa
ajili ya maonyesho ya muziki, pia yalihamasishwa mashindano, matamasha na
maonyesho ya aina mbalimbali ya muziki kila kona ya nchi.
Watu
waliokuwa vijana na watoto katika miaka ya 60, 70, na 80 wanaweza kukueleza
hadithi ndefu jinsi walivyokuwa wakishiriki kwa namna moja au nyingine katika
nyimbo mbalimbali zilizohusu mambo ya nchi yao. Kulikuwa na shughuli za muziki
kuanzia ngazi ya vijiji, mada mbalimbali zilitungiwa muziki kwa kutumia muziki
wa asili, kwaya na muziki wa kisasa. Kwa njia hiyo taarifa za mambo mbalimbali
zilieneka kila kona ya nchi japokuwa mawasiliano ya umma yalikuwa hafifu mno kulinganisha na zama hizi.
Kulikuweko na Maafisa Utamaduni wa Wilaya
na Mkoa nchi nzima, na maafisa hawa wakahamasisha kuanzishwa vikundi vya muziki
wa aina mbalimbali kwenye sehemu za kazi, shuleni, vijijini na kadhalika. Taasisi za serikali na mashirika ya umma vilihamasishwa
kuanzisha vikundi vya sanaa, na ndipo kukawepo kundi la sanaa la Taifa, vikundi
vya sanaa majeshini ambapo huko pia kukawa na vikundi vya taarab na dansi,
mashirika kama Bima, DDC, URAFIKI, TANCUT na mengine mengi yakawa na vikundi
vya sanaa vizuri sana, Kurugenzi za mikoa Dodoma na Arusha nazo zikaanzisha
vikundi, Umoja wa Vijana wa TANU nao ukawa na vikundi ikiwemo bendi yake
maarufu Vijana Jazz band. Vikundi vyote hivyo vilishiriki sana katika kuimba
nyimbo mbalimbali za maisha katika jamii na pia siasa, na maendeleo na nchi. Katika
mfumo huo walikuja kupatikana akina Mzee makongoro , Mzee Mwinamila, John Komba
na kadhalika.
Viongozi wa ngazi mbalimbali walivitembelea vikundi vilivyo chini ya himaya yao
kuvikagua navyo viljitayarisha kuonyesha umahiri wao, hivyo nchi nzima
ilichangamka kwa ubunifu katika muziki wake.
Katika ziara
ambazo zilichukuliwa kwa uzito mkubwa na vikundi vyote, zilikuwa ziara za viongozi
wakuu wa nchi. Mazoezi yalikuwa makubwa,
kwaya zilitunga nyimbo mpya, ngoma zilitunga nyimbo mpya, bendi na vikundi vya
taarab vilitunga nyimbo mpya, kila moja ilijitahidi kwa umahiri ili tu kupata
nafasi kuonyesha kazi mbele ya umma na viongozi hao wakuu. Na hakika kabla ya
kiongozi kuanza shughuli au hotuba,
wanamuziki waliburudisha umma kwa kazi zao. Ni katika mfumo huo ambapo wanamuziki
kama Bi Shakila walipogunduliwa. Ilikuwa ni siku Mwalimu Nyerere alipotembelea
Pangani na Shakila akawa mmoja wa wanamuziki wa pale Pangani walioweza
kutumbuiza mbele ya Mwalimu Nyerere, na umahiri wake kugunduliwa. Na hali
kadhalika wasanii wengi waliokuja kuwa maarufu walionekana kwanza katika
maonyesho mbele ya viongozi wakuu.
Machifu wengi wa zamani walitumia wasanii kupata taarifa za hali ya utawala
wao. Wasanii wachekeshaji na wanamuziki waliweza kutunga vichekesho au nyimbo
zilizokuwa zikielezea ukweli wa jinsi wananchi walivyokuwa wakijihisi wakiwa chini
ya Chifu wao, nae alichukua ujumbe huo uliokuwa ukionekana kama utani au wimbo
mzuri na kuufanyia kazi.
Zama hizi za dot com mambo ni tofauti sana, ni jambo la kawaida kabisa viongozi
wa juu wakiwa katika ziara zao nchini,
kusindikizana na wanamuziki ‘maarufu’ Kitaifa. Hali hii ya kuletewa msanii ‘maarufu’
kutumbuiza ‘nyumbani kwao’ na kuwadharau
wasanii wenyeji ina waacha wasanii wenyeji wakijiuliza maswali kuhusu thamani
yao mbele ya kiongozi huyo mkuu. Taratibu hii mpya pia inamyima kiongozi mkuu
fursa ya kuona sura nyingine ya sanaa za wananchi anaowaongoza, na muhimu zaidi anakosa kusikia ujumbe mpya
kutoka kwa wananchi wa sehemu anayozuru.
Nina imani kabisa kabisa kuwa wasanii wote wana haki sawa mbele ya viongozi
wakuu, hivyo si haki kudharauliwa kwa kipimo cha umaarufu wa kibiashara.
No comments:
Post a Comment