YOUTUBE PLAYLIST

Saturday, November 5, 2022

HISTORIA FUPI YA TAARAB YA TANGA

Marehemu Waziri Ally akiwa mdogo akiwa anapiga kinanda katika bendi ya Lucky star

Katika miaka ya 50 wanawake tisa wa Tanga walijikusanya na kuanzisha  kikundi cha kuimba walichokiita Raha til Fuad maana yake Raha ya Moyo. Akina mama hawa chini ya bibie aliyeitwa Mama Akida au aka Mama Lodi, waliendesha kikundi chao wakiwa wanaimba nyimbo za Siti Binti Sadi na tungo zao ambazo waliimba katika melody ya nyimbo za kihindi zilizotamba wakati huo. Kundi hili liliendelea na kuanza kuruhusu wanaume kujiunga hasa wakiwa wapiga vyombo. Hata mtoto wa Mama Akida, Akida Jumbe hatimaye alijiunga na kundi hili kama mpiga accordion kwenye mwaka 1962. Kundi hili ambalo baadae lilikuja kuitwa Young Noverty, liliendelea mpaka kukaweko na mgawanyiko uliozaa kundi la Shaabab Al Waatan ambalo lilitawaliwa zaidi na wanaume.
 Hapo ndipo kukaanza mtindo wa kuweko kundi pinzani katika muziki wa taarab wa Tanga. Jambo ambalo kwa njia ya ajabu sana kwa kipindi kirefu likawa  linadumu kiasi cha miaka kumi kumi. Miaka ya 60, Young Noverty na Shabaab al Waatan, Miaka ya 70 Lucky Star Musical Club na Black Star Musical Club, miaka ya 80 Golden Star Taarab na White Star Taarab, miaka ya 90, Babloom Modern Taarab na Freedom Modern Taarab. Taarab ya Tanga kwa kweli ndio  haswa inastahili kuitwa Modern Taarab, kwani wao hawakufuata Taarab ile iliyoletwa Zanzibar enzi ya Sultan Seyyid Barghash.
Taarab ya Tanga ilikuwa ni ya makundi  yenye wanamuziki wachache kuliko makundi ya Taarab ile ya Zanzibar.
Vyombo vya vikundi vya Taarab ya Tanga
vilikuwa ni pamoja na Gitaa la besi, gitaa la solo, drums bongos ,akodion au kinanda. Nyimbo zao zilikuwa fupi na si ndefu kama zaTaarab ya Zanzibar au ambayo huitwa Taarab asili. Nyimbo za Taarab ya Tanga zilitegemea mipigo ya ngoma za asili za kumbwaya na chakacha na hata baadaye mitindo kama rumba,bossa nova. Na Taarab ya Tanga ndio iliyoanzisha moto wa vikundi vya taarab Tanzania Bara. Moshi kulikuwa na New Alwatan, AzimioTaarab, na Blue Star Taarab , Arusha kulikuweko na Blue Star Taarab, Dodoma ilikuwepo Dodoma Stars, Kondoa  kulikuwa na Blue Stars, Mbeya kulikuweko na Magereza Kiwira, Mwanza kulikuwa na Ujamaa Taarab, Bukoba  walikuwa na Bukoba Stars, na muendelezo huu uliingia mpaka Burundi kutokana na mwana muziki mmoja alie julikana kama Athmani Mkongo, alitoka Burundi na bendi yake kufika Tanga akahama kutoka muziki wa dansi na kuwa mwanamuziki mahiri wa Taarab na baadae kuipeleka kwao Burundi kukazaliwa kundi maarufu la Jasmine Taarab.


Thursday, November 3, 2022

MKOANI PIA KUNA WANAMUZIKI WAKALI, KWANINI WANATENGWA?

 

Kila jamii ina muziki, kuna aina mbalimbali za muziki na zenye matumizi mbalimbali, kadri ya utamaduni wa jamii husika.
Katika zama hizi hasa mijini, muziki huonekana hasa kazi yake ni kwa kuleta burudani. Lakini kwa asili katika jamii zetu mbalimbali muziki ulikuwa na matumizi ya aina nyingi na hata kupewa majina kutokana na shughuli husika.
Kati ya shughuli ambazo muziki ulitumika na sehemu  nyingine bado unatumika ni kwenye  matambiko, tiba,  misiba, sherehe mbalimbali kama mavuno, harusi na kadhalika.
Leo niongelee muziki na siasa za nchi yetu.
Kabla ya Uhuru, katika maeneo mbalimbali nchini, wanamuziki kama marehemu Mzee Moses Nnauye walianzisha vikundi vya muziki kuhamasisha kudai Uhuru, vikundi vya kwaya, ngoma za asili, na muziki wa taarab na muziki wa dansi, vilitunga nyimbo zenye ujumbe  ambao uliwafikia vizuri wananchi wengi na hivyo  kuwahamasisha kuwa wana haki ya kujitawala na kuanza kudai Uhuru.
Mara baada ya kupata Uhuru,Disemba 9 1961, vikundi vya muziki  vilitunga nyimbo zilizoongelea furaha ya kupata Uhuru na pia kuanza kuelezea ndoto za  wananchi baada ya uhuru. Mahusiano ya muziki na siasa yaliongezeka sana, na baada ya Tanzania kuamua kuwa nchi ya Kijamaa, serikali iliwekeza sana katika sanaa, kwani ilitambua kuwa hiyo ilikuwa njia muhimu ya kufikisha taarifa ya malengo ya serikali. Pamoja na kuweko majengo yalikuwa maalumu kwa ajili ya maonyesho ya muziki, pia yalihamasishwa mashindano, matamasha na maonyesho ya aina mbalimbali ya muziki kila kona ya nchi.

Watu waliokuwa vijana na watoto katika miaka ya 60, 70, na 80 wanaweza kukueleza hadithi ndefu jinsi walivyokuwa wakishiriki kwa namna moja au nyingine katika nyimbo mbalimbali zilizohusu mambo ya nchi yao. Kulikuwa na shughuli za muziki kuanzia ngazi ya vijiji, mada mbalimbali zilitungiwa muziki kwa kutumia muziki wa asili, kwaya na muziki wa kisasa. Kwa njia hiyo taarifa za mambo mbalimbali zilieneka kila kona ya nchi japokuwa mawasiliano ya umma  yalikuwa hafifu mno kulinganisha na zama hizi.
 Kulikuweko na Maafisa Utamaduni wa Wilaya na Mkoa nchi nzima, na maafisa hawa wakahamasisha kuanzishwa vikundi vya muziki wa aina mbalimbali kwenye sehemu za kazi, shuleni, vijijini na kadhalika.  Taasisi za serikali na mashirika ya umma vilihamasishwa kuanzisha vikundi vya sanaa, na ndipo kukawepo kundi la sanaa la Taifa, vikundi vya sanaa majeshini ambapo huko pia kukawa na vikundi vya taarab na dansi, mashirika kama Bima, DDC, URAFIKI, TANCUT na mengine mengi yakawa na vikundi vya sanaa vizuri sana, Kurugenzi za mikoa Dodoma na Arusha nazo zikaanzisha vikundi, Umoja wa Vijana wa TANU nao ukawa na vikundi ikiwemo bendi yake maarufu Vijana Jazz band. Vikundi vyote hivyo vilishiriki sana katika kuimba nyimbo mbalimbali za maisha katika jamii na pia siasa, na maendeleo na nchi. Katika mfumo huo walikuja kupatikana akina Mzee makongoro , Mzee Mwinamila, John Komba na kadhalika.  
Viongozi wa ngazi mbalimbali walivitembelea vikundi vilivyo chini ya himaya yao kuvikagua navyo viljitayarisha kuonyesha umahiri wao, hivyo nchi nzima ilichangamka kwa ubunifu katika muziki wake.

Katika ziara ambazo zilichukuliwa kwa uzito mkubwa na  vikundi vyote, zilikuwa ziara za viongozi wakuu wa  nchi. Mazoezi yalikuwa makubwa, kwaya zilitunga nyimbo mpya, ngoma zilitunga nyimbo mpya, bendi na vikundi vya taarab vilitunga nyimbo mpya, kila moja ilijitahidi kwa umahiri ili tu kupata nafasi kuonyesha kazi mbele ya umma na viongozi hao wakuu. Na hakika kabla ya kiongozi kuanza shughuli au  hotuba, wanamuziki waliburudisha umma kwa kazi zao. Ni katika mfumo huo ambapo wanamuziki kama Bi Shakila walipogunduliwa. Ilikuwa ni siku Mwalimu Nyerere alipotembelea Pangani na Shakila akawa mmoja wa wanamuziki wa pale Pangani walioweza kutumbuiza mbele ya Mwalimu Nyerere, na umahiri wake kugunduliwa. Na hali kadhalika wasanii wengi waliokuja kuwa maarufu walionekana kwanza katika maonyesho mbele ya viongozi wakuu.
Machifu wengi wa zamani walitumia wasanii kupata taarifa za hali ya utawala wao. Wasanii wachekeshaji na wanamuziki waliweza kutunga vichekesho au nyimbo zilizokuwa zikielezea ukweli wa jinsi wananchi walivyokuwa wakijihisi wakiwa chini ya Chifu wao, nae alichukua ujumbe huo uliokuwa ukionekana kama utani au wimbo mzuri na kuufanyia kazi.
Zama hizi za dot com mambo ni tofauti sana, ni jambo la kawaida kabisa viongozi wa juu wakiwa katika ziara zao nchini,  kusindikizana na wanamuziki ‘maarufu’ Kitaifa.  Hali hii ya kuletewa msanii ‘maarufu’ kutumbuiza ‘nyumbani kwao’  na kuwadharau wasanii wenyeji ina waacha wasanii wenyeji wakijiuliza maswali kuhusu thamani yao mbele ya kiongozi huyo mkuu. Taratibu hii mpya pia inamyima kiongozi mkuu fursa ya kuona sura nyingine ya sanaa za wananchi anaowaongoza,  na muhimu zaidi anakosa kusikia ujumbe mpya kutoka kwa wananchi wa sehemu anayozuru.
Nina imani kabisa kabisa kuwa wasanii wote wana haki sawa mbele ya viongozi wakuu, hivyo si haki kudharauliwa kwa kipimo cha umaarufu wa kibiashara.

 

 

 

 

 

Monday, October 3, 2022

USHIRIKINA KATIKA MUZIKI HISTORIA NI NDEFUUUU


Imani ya uchawi ni utamaduni ambao umekuweko katika historia ya jamii zote za binadamu. Maandiko ya dini mbalimbali yanatuhakikishia kuwa jambo hilo lipo na hulilaani. Mara nyingi hudhaniwa kuwa kadri maendeleo na elimu yanavyoongezeka ndio imani ya ushirikina inavyopungua na kupotea, lakini ni wazi dhana hiyo si ya kweli, safari ya kuachana na uchawi bado ni ndefu sana, kwani ukipita katika mitaa mingi utaona vibao vikiashiria waganga wanaoweza kutibu matatizo  mbalimbali kama ‘kusafisha nyota’, ‘kuondoa majini’, ‘kurudisha mpenzi aliyekimbia’ na kadhalika, wasomi wenye milolongo ya shahada na stashahada si ajabu kabisa nao kuwakuta kwenye vibanda vya waganga wakitafuta kusaidiwa kwenye mambo ambayo  mtu mwingine ungetegemea yanawezekana kwa juhudi tu za kibinadamu.

Muziki haujakwepa kuguswa na dhana ya ushirikina. Muziki unatumika unatumika katika kufanikisha dhana ya uchawi na wanamuziki wengi wanaamini na kushiriki katika shughuli mbalimbali za uchawi.

Tuanze na dhana ya muziki iliyopewa jina la Kiingereza ‘ healing music’. Duniani kote waganga na wachawi hutumia muziki wa aina yake kupandisha mashetani au kuita mizimu na kadhalika, muziki huu ndio huitwa healing music, huku kwetu mara nyingine huitwa muziki wa kupandisha mashetani. 

Katika maisha yangu ya muziki niliona na kusikia vituko vingi vilivyohusishwa na imani ya uchawi. Mara ya kwanza kuanza kuona vitimbi hivi ‘live’ ni nilipojiunga bado mdogo na kuwa mwanamuziki katika bendi yetu ndogo huko Iringa. Tualianza kupiga muziki wenyewe wachache bila kuwa na wazo lolote la kuhusisha muziki wetu na imani yoyote ya kishirikina. Siku moja akaja mzee mmoja akatukaribisha kufanya mazoezi kwenye sehemu yake ya biashara, na kwa vile tulikuwa hatuna sehemu maalumu tuliona huu ni ufadhili mkubwa.  Tulihamishia vyombo vyetu vichache kwake, na haikuchukua muda mrefu tukagundua kuwa biashara yake ni uganga wa kienyeji. 
Siku moja akatueleza kuwa hatutaweza weza kuwa bendui kubwa bila ‘kusafishwa nyota’. Tulipewa dawa za kuoga na tukaendelea na mazoezi makali tukijua muda wetu wa kuwa bendi kubwa umewadia. Tulikubaliana kuwa tungepunguza deni la kazi yake ya kutusafisha nyota kwa kumlipa kidogo kidogo kila tulipofanya onyesho, kweli tukaanza kumlipa kila tulipopiga. Sikumbuki ni muda gani tuliendelea kumlipa yule mganga, japo kuwa hakuna chochote kilichobadilika katika hadhi ya bendi yetu.
Siku moja mganga yule alienda disco na akamtishia msichana mmoja kwa nyoka aliyekuwa nae mfukoni, hapo ndipo alipokamatwa na polisi na hatukumuona tena deni likayeyuka.
 Miaka mingi baadae nilikuja kujiunga na bendi moja kubwa jijini Dar es Salaam, hapo ndipo nilipoona tena shughuli za ushirikina. Ilikuwa ni siku chache baada ya kurekodi nyimbo mpya za bendi yetu katika studio za Radio Tanzania. Kulikuwa na kipindi kilichoitwa Misakato , kipindi ambacho kilitambulisha nyimbo mpya zilizorekodiwa na studio za redio hiyo, tulikuwa tumekubaliana kuwa wanamuziki wote tukusanyike nyumbani kwa kiongozi wetu ili wote tuzisikilize nyimbo zetu zikirushwa kwa mara ya kwanza hewani.  Zilipoanza kupigwa nyimbo zetu nikashuhudia mmoja wa viongozi wetu akiwa anaifukiza redio kwa moshi kutoka dawa zilizokuwa zimechomwa kwenye kifuu cha nazi,  hii ilikuwa kwa imani kuwa kwa kufanya hivyo, vibaovyetu vipya vikisikika vitatikisa roho za wasikilizaji wake. Katika kundi hili vituko vingi viliendelea hatimae tulizoea kuwa uongozi wa bendi yetu unaamini sana uchawi. Kuna wakati aliletwa mganga ambaye alidaiwa aliwahi kuifanya timu moja maarufu ya soka, ishinde kombe  na kuwa bingwa wa Taifa, hata jina lake aliitwa Bingwa, kutokana na sifa hizo bendi ilimchukua kwa mkataba na kazi yake ikawa ni kukaa mlangoni akijifanya ni muuza machungwa, hapo alitakiwa afanye vimbwanga vyake ili wateja wengi waingie kwenye muziki. Yeye alidai kila anapomenya chungwa kwa kuunganisha maganda kama mkanda, basi na wateja nao wataingia katika ukumbi kwa kuunganika kwa foleni ndefu, huyu alikaa nasi kiasi cha kuweza kuwa  katika misafara mbalimbali ya bendi tulipoenda ziara za mikoani. Harakati za bendi kutafuta umaarufu kwa uchawi ilifikia mpaka bendi ikasafiri hadi kwenda Mpanda, ambako viongozi wa bendi walikwenda kwa mganga na kufanya mambo yao ambayo yalihusisha na hata kumchinja mbuzi. Baadae walirudi na nyama ya mbuzi huyu mpaka tulipokuwa tumefikia, nadhani masharti yalikuwa ni sisi wanamuziki wote tule kipande cha mbuzi yule wa kafala. Sijajua mpaka leo viongozi walifanya nini na nyama ya mbuzi yule maana wanamuziki walifanya mgomo wa kumla yule mbuzi.
 Ushirikina una matatizo ya kufanya watu wasiaminiane hata kwenye bendi yenyewe, haikuchukua muda mrefu bendi ilipoanza kupoteza umaarufu, Kiongozi wa bendi akaaitisha mkutano na kutuambia kuwa kuanguka kwa bendi kunatokana na mmoja wetu kuiloga bendi, hapo ikatolewa tishio kuwa mtuhumiwa asipojitaja mwenyewe na kuomba msamaha mganga aliyeagua hilo aliahidi atamfanya awe kichaa. Jambo ambalo liliungwa mkono na wote kuwa kama ni kweli kuna mtu namna hiyo basi apate uchizi. Hakuna aliyekumbwa na tatizo hilo mpaka leo.
Miezi michache baadae, wanamuziki wawili walioamua kuacha bendi walirudisha sare za bendi kama ilivyokuwa kawaida zama zile. Shati zilikuwa zimechanywa kwenye kwapa na suruali kuchanywa kwenye maungio ya miguu kwa imani kuwa hizo ndizo sehemu zenye jasho kwa hiyo kama wangerudisha sare zao bila kuondoa sehemu hizo wangeweza kurogwa kirahisi na kuharibiwa maisha.

Mpiga tumba mmoja tuliyekuwa nae bendi moja alinichekesha aliponihadithia kuwa kiongozi wa bendi yao moja aliyopitia, aliwahi kuwapeleka kwa mganga aliyewataka waende na vyombo vyao vya muziki. Kisha akawa ana chanja chombo na kukipaka dawa,na baada ya hapo kumchanja mwenye chombo matakoni na kumpaka dawa!!!!
Katika mizunguko kwenye bendi mbalimbali, siku moja bendi yetu ilikuwa na mpambano wa kupiga bendi zaidi ya moja katika ukumbi mmoja. Hili lilichukuliwa kuwa ni jambo kubwa na la hatari linalohitaji matayarisho,  mganga maalumu lazima atafutwe ili kuilinda bendi isimalizwe na wapinzani. Ilikuwa inaaminika kuwa katika mpambano wa bendi, uchawi hutumika kuimaliza bendi ambayo itakuwa haina kinga, siku moja kabla ya pambano, maboksi ya spika yalifunguliwa na ndani yake  kuliwekwa tunguli na hirizi mbalimbali tayari kwa mpambano. Nakumbuka siku hiyo bendi pinzani nayo iligoma kupanga vyombo kwenye jukwaa kuu kwa madai kuwa kuna mbuzi alifukiwa katika jukwaa lile.

Kwa ukweli kabisa hata wanamuziki kutembeleana mara nyingine ilikuwa ni vigumu, kwani ukionekana mwanamuziki wa bendi nyingine katika ukumbi, basi bendi iliyo jukwaani haina raha, anaweza hata akatumwa mtu kufuatilia kila utakachofanya. Na ilikuwa vigumu kuruhusiwa kugusa vyombo vya bendi nyingine kwa wasiwasi wa kuwa unaweza ukaloga kile chombo. Niliwahi kuona bendi ikisimamisha muziki katikati ya onyesho na kudai shabiki mmoja wa bendi pinzani, tena alikuwa mwanamke, atolewe ukumbini kwani alikuwa ametumwa kufanya ushirikina, na hakika alitolewa nje.

Kulikuwa na hadithi nyingi zilizoonyesha ni kiasi gani cha ushirikina bendi ziliweza kufanya ili kupata wateja. Kuna bendi ambayo ilisifika kuwa kila wakimaliza kupiga muziki walipita katika kumbi mzima  na kuokota vizibo vya chupa za bia na soda, mifupa na mabaki ya nyama zilizotupwa na wateja, na hata kupata maji toka vyoo vya ukumbi na kwenda kuloga ili wale walioingia wasiingie bendi nyingine yoyote kasoro yao. Bendi nyingine zilidaiwa kuwa ziliweka mkataba ambapo zililazimika kutoa kafala ya mtu mmoja kila mwaka, hivyo viongozi wa bendi kufiwa na watoto, ndugu na hata wanamuziki wageni waliojiunga katika bendi hizo kukutwa na mauti ambayo habari za chini chini zilidai ni katika kutoa kafala.

 

Bendi mbili ambazo zilikuwa na upinzani mkubwa katika jiji la Dar es Salaam zilidaiwa hata kutaka kuweka uchawi katika chanzo cha maji Dar es Salaam , na kujikuta wakitaka kuumbuana hadharani kuhusu hilo.
Kuna wanamuziki wapiga magitaa wa zamani waliowahi kupatwa na matatizo ya akili na wazee wengi mpaka leo hudai matatizo yao yalitokana na ushindani wa uchawi katika bendi zao. Kama nilivyosema imani ya uchawi huleta kutokuaminiana na hata madhara makubwa ya kutuhumiana mambo ambayo mara nyingi hayana ukweli wowote. Kuna mwanamuziki niliyejaribu kumshawishi aingie katika bendi niliyokuwa nikipigia , alikataa katakata kwa kuwa alidai mmoja wa wanamuziki katika bendi hiyo ni mchawi.
Mwanamuziki mmoja mpiga gitaa mahiri aliwahi kunihadithia jinsi alivyopita uchochoro wa nyumba ya mwanamuziki mwenzake akashangaa kusikia jina lake likitajwa na mwenzie aliyekuwa chumbani kwake na kusema,’ Nyota ya …….(jina la mwanamuziki huyo) izimike kama kaa hili’, akadai alichungulia katika ufa na akakuta mwenzie anatumbukiza kaa la moto kwenye maji.
Ugonjwa wa ukimwi ulipoanza kuuwa wanamuziki kwa mara ya kwanza mara nyingi ulihusishwa na uchawi. Rafiki yangu mmoja nilipomtembelea wakati akiwa hoi kitandani akanambia,’Nikupe siri? Mi ntakufa lakini nauawa na wanamuziki wenzangu kwenye bendi. Nimepata mganga kanitajia na majina kabisa’. Miezi michache baadae mwanamuziki huyu kabla hajafariki alinambia,’Mjomba sijalogwa wala nini, udude huu, unaniua udude’. Alifariki siku chache baada ya kunambia haya.
Kama nilivyosema awali, elimu na teknolojia hazijaondoa kabisa dhana ya uchawi. Siku moja nilimsikia producer maarufu akiwakanya wasanii wa muziki wa Bongofleva wanaoingia studioni mwake, wasifanye mambo ya ushirikina kwenye studio yake.

Na siku chache baada ya hapo tena mwanamuziki mwingine wa muziki huo kawataja ambao aliwaita wabaya wake wanaomloga.!!!!!!! Nikaona loh kumbe shughuli bado inaendelea, wanamuziki hawa wenye umri mdogo tayari wamekwisha jenga imani ya kulogana katika enzi hizi za dijitali, safari bado ndefu sana, USHIRIKAINA BADO UKO HAI KATIKA SANAA YA MUZIKI

Monday, September 12, 2022

MITINDO ILITAMBULISHA BENDI NA MUZIKI WAKE

 



Katika miaka ya karibuni, utamaduni wa kila bendi kuwa na mtindo wake umefifia sana. Lakini ulikuwa utamaduni uliokuwa maarufu sana kuanzia miaka ya sitini. Kila bendi ilipoanza, ilijinasibu kwa kuja na mtindo wake, ingekuwa siku hizi ingetambulika kama kuji ‘brand’.
Ni vigumu kutaja mitindo yote iliyowahi kugunduliwa kwani kuna mingi ambayo haikuwahi kupata nafasi kutambuliwa katika vyombo vya utangazaji au kuwekwa  katika kumbukumbu za aina yoyote. Majina ya mitindo mingine ilikuwa na sababu au historia na maana maalumu, lakini majina mengine yalikuwa ya kutunga tu na kwa kweli hata waliokuwa waliokuwa wakiyatumia hawakuwa na maelezo ya maana ya maneno hayo. Nakumbuka nikiwa bado mwanamuziki mdogo huko Iringa tulikuwa na bendi ambayo mtindo wake ulikuwa ni Chikwala chikwala, namkumbuka aliyetunga jina hili, alikuwa mpiga gitaa la rhythm ambaye pia alikuwa fundi saa. Hata yeye hakuwa na maelezo ya maana kuhusu jina lile, ila kwa wakati ule, ilikuwa ni staili kwa majina ya mitindo  ya bendi kuwa na jina linalojirudia rudia, hii ilitokana na bendi kadhaa Kongo kuwa na majina yaliyojirudia rudia mfano Orchestra Lipua Lipua, Orchestra Bella Bella na Orchestra Shama Shama.
Baadhi ya majina ya mitindo ya bendi yalikuwa Mundo, Saboso,  Msondo, Sokomoko, Dondola, Toyota, Kiweke, Segere matata, Super mnyanyuo, Vangavanga, Libeneke, Chakachua, Sululu, Ambianse, Takatuka, Afrosa na majina mengineyo mengi. Bendi nyingi zilibuni hata aina ya uchezaji wa mitindo yao, na uchezaji mwingine ulibuniwa hata na wapenzi wa bendi hizi. Kila bendi ilikuwa ikijitahidi kuwa tofauti na bendi nyingine. Kwa mfano katika mji wa Tanga ulikuwa na bendi kubwa mbili, Jamhuri Jazz Band na Atomic Jazz Band, kuna wakati bendi ya Jamhuri ilikuwa na mtindo wa Toyota, na baadae Dondola, wakati  Atomic walikuwa na mtindo wa Kiweke, muziki wao ulikuwa tofauti, hivyo Jamhuri ikawa na wapenzi wake na Atomic ikawa na wapenzi wake, na mpaka leo, wazee waliokuwa wapenzi wa bendi hizi mbili hubaki kusifia ubora wa bendi zao, wazee wa Jamhuri husifu mtindo wa upigaji wa gitaa la rythm la Harrison Siwale(Satchmo), huku wapenzi wa Atomic watakwambia hakuna kama Kiweke, kwani upigaji wa gitaa la solo wa John Kijiko, au bass la Mwanyiro haukuwa na mpinzani. Kule Morogoro kulikuwa na Morogoro Jazz Band na Cuban Marimba, bendi hizi zilikuwa na mitindo mbalimbali kwa nyakati mbalimbali, na wapenzi wao walikuwa tayari kutetea ubora wa mitindo ya bendi zao. Cuban Marimba wakisifia mtindo wa Ambianse, Morogoro wakisifia Likembe, au sululu. Na hakika kulikuwa na tofauti kubwa ya mitindo hii miwili japo ilipigwa na bendi zilizotoka mji mmoja.
Nimeanza kwanza kwa kutaja bendi zilizokuwa katika mji mmoja, tena huko mikoani ambako kwanza miji ilikuwa bado na watu wachache kulinganisha na sasa, wanamuziki walikuwa wanajuana na kuishi jirani, hali hiyo ndio iliyokuwa Tabora, ambako pamoja na Tabora Jazz, kulikuweko na Nyanyembe Jazz, Kiko Kids, lakini muziki wa kila bendi ulikuwa tofauti na mwingine. Dar es salaam kulikuwa na bendi nyingi na hivyo mitindo mingi, na pia kulikuwa na bendi za watu wa mataifa kutoka nje ya Tanzania. Kulikuwa na bendi za Magoa, kulikuwa na bendi za Wakongo, nao pia wakawa na mitindo yao.  Hakuna aliyeweza kuchanganya mtindo wa Ogelea piga mbizi ya  Maquis na mtindo wa Chunusi wa  Orchestra Safari Sound, hata pale ambapo wanamuziki wa kutoka bendi moja walipohamia bendi pinzani kila bendi ilibaki na staili yake na kuilinda kwa kuongeza ubora kila mara. Hivyo haikuwezekana ukasema  Sikinde na Msondo zilipiga muziki uliofanana au mitindo ya Sokomoko na Afrosa ilikuwa na ukaribu. Kikubwa ninachotaka kueleza ni kuwa bendi kuwa na mtindo ilikuwa si jina tu bali kulikuweko na kazi ilifanyika ili kupata, kulinda na kuendeleza mtindo ambao bendi iliamua kuwa nao. Nakumbuka wakati wa mazoezi enzi hizo unaweza ukatunga wimbo ukianza kuimba wenzio watakwambia mbona unafanana na bendi fulani na hapo utakarabatiwa mpaka uwe katika mtindo wa bendi husika.

Wiki chache zilizopita nilipata bahati ya kuhudhuria onyesho moja la bendi iliyoko Mbeya, baridi ndio ilinilazimisha kukumbuka kuwa niko Mbeya, upigaji, uchezaji, uimbaji wa bendi hii ulikuwa kama bendi nyingi zilizopo Dar es Salaam. Bendi zimekuwa kama vile zimepewa amri kuwa lazima zipige muziki unaofanana. Toka umeingia mtindo wa ‘sebene’ mwanzoni mwaka 2000, basi ni kama kila ubunifu umesimamishwa. Hata zile bendi ambazo hupiga nyimbo za bendi ya zamani, hulazimisha kuingiza sebene, kwenye nyimbo hizo. Juzijuzi kwenye onyesho moja kubwa la muziki, bendi moja ilikuwa ikipiga wimbo wa Super Volcano unaoitwa Shida, ghafla ukabadilika kwa kuongezewa sebene.  Kipindi aina ya muziki wa sebene ulipokuwa ukiingia nchini, kulikuwa na aina ya muziki wa hapa nyumbani uliokuwa unaitwa Mchiriku. Sasa toka wakati huo,Mchiriku umeweza kujiongeza na kubadilika mpaka sasa unaitwa singeli, tena hata hiyo singeli imeanza kuota matawi, lakini wanamuziki wa dansi wamekwama palepale kwenye sebene. Hili linanikumbusha enzi za teknolojia ya santuri, santuri zilikuwa zinaweza kupata mchubuko na hivyo sindano ikakwama sehemu moja, ikawa inarudia kupiga muziki sehemu ileile haiendi mbele wala hairudi nyuma mpaka betri itakapoisha.

Wednesday, August 31, 2022

USUPA STAA NI DHANA YA ZAMANI INAYOBORESHWA NA TEKNOLOJIA

 




Ma ‘superstar’ ni watu ambao wametokea kujizolea umaarufu mkubwa katika jamii. Superstar anaweza kuwa ametokea katika nafasi mbalimbali katika jamii, anaweza akawa mwanasiasa, mwalimu, mkulima au mtu yeyote katika jamii, hapa kwetu sifa hii zaidi huhusiana na wasanii. Sifa ya ‘usupastaa’ imejitokeza zaidi baada ya tasnia ya filamu kukua, jambo ambalo limeenda sambamba na kuongezeka kwa vyombo vya utangazaji.  Na kwa kweli katika zama hizi tunao watu wengi ambao wanapewa sifa  ya ‘u superstar’ katika jamii. Hakuna chuo maalumu cha kufundisha usupastaa kwani umaarufu wa mtu huweza kutokana na sababu mbalimbali. 

Wasanii huingia katika sanaa kwa njia na sababu mbalimbali, wengine huzaliwa na kipaji, wengine huingia katika fani hiyo kama njia ya kutafuta maisha, wengine huingia kwa kuiga wenzao waliomo katika sanaa, kuna hata waliolazimishwa na ndugu na jamaa kuingia katika fani ya sanaa, na kadhalika. Kutokana na sababu hizi mbalimbali za kujiingiza kwenye sanaa, waliomo humu nao wanakuwa na mategemeo mbalimbali yatakayopatikana katika fani hiyo. Wengine nia yao ni kutengeneza sanaa nzuri, bila kujali sifa wala malipo, wengine wanafanya sanaa ili wapate kipato kizuri na wengine wakitegemea sifa tu kutokana na ubora wa kazi yao. Na wengine kutumia sanaa kama jukwaa la kufanyia shughuli nyingine kabisa ambazo hazihusiani na sanaa. Wasanii waliomo katika sanaa kutafuta kipato, hulazimika kutafuta mbinu mbalimbali ili sanaa yao iuzike, na moja ya njia kubwa ya kuhakikisha sanaa inauzika ni kwa wao kuwa maarufu. Watu wengi wanatabia ya kufuatilia maisha na kununua kazi za sanaa za watu maarufu. Kutokana na sababu hii, msanii huanza mbinu mbalimbali za kupata umaarufu. Msanii atajitokeza kwenye vyombo vya habari kutangaza kazi zake na hata kuelezea maisha yake, picha zake nzuri kusambazwa,na hata kazi hizo kusambazwa ili watu wengi wazifahamu.

Katika nchi ambazo tasnia imejengeneka vizuri, kuna makampuni maalumu ambayo hutumia mamilioni ya fedha kujenga sifa za msanii husika na kazi zake, kwa kutegemea faida kubwa baadae. Msanii huingia katika mikataba ya muda mrefu na kampuni huwekeza katika kujenga sifa ya msanii ili kupata wateja wengi wa kazi za msanii huyo.

Je unapataje ‘u super star’ hapa Tanzania? Kama ilivyo duniani kote kuna wasanii ambao kazi zao zimepokelewa vizuri na jamii na kuwafanya wasanii mbalimbali kuwa maarufu kwa urahisi sana. Lakini kuna mambo mengi ambayo yanapita nyuma ya pazia katika kupata ‘u superstar’ hapa kwetu. Rushwa ni moja ya jambo kubwa katika kujenga ‘ma superstar’ wa hapa kwetu. Na hili halikuanza karibuni, kwa wanamuziki wa zamani wanaelewa hali ilivyokuwa enzi kulipokuwa na redio moja tu, ilivyolazimika kutoa rushwa ili mashahiri ya nyimbo walizotaka kurekodi yakubalike na nyimbo zirekodiwe, kisha kutoa rushwa ili nyimbo zilizorekodiwa zipigwe kwenye vipindi mbalimbali huku sifa za kujenga usupastar wa wasanii hao zikimiminika, hali hii haiko tofauti sana na sasa japo kwa sasa kuna utititiri wa redio na luninga. Watangazaji wengi wamefaidika na rushwa kutoka kwa wasanii waliokuwa na hamu ya ‘kutoka’. Kuna wakati watangazi wa redio mbalimbali walitengeneza umoja, ambapo mwanamuziki alikuwa akilipia ili kazi zake zirushwe hewani. Watangazaji wa vipindi vya redio wengi waligeuka kuwa mameneja wa wasanii na hivyo kuhakikisha wanawatangaza wasanii wao ili wawezekuwa ‘ma supersta’. Rushwa ya ngono sio siri katika tasnia ya sanaa katika kutafuta ‘u superstar’ . Wasanii wa kike wengi wana hadithi ya kupitia katika mtihani huu katika kutafuta ‘kutoka’. Kuna wakati wasanii  wawili wakubwa wa kike, walitangaza mpango wa kuanza kuwajenga wenzao ili wasipitie adha ya kudaiwa rushwa hii. Jambo ambalo linaonyesha wazi kuwa rushwa hii bado iko hai.

Katika kutafuta ‘U superstar’, kuna wasanii ambao wamefanya mambo mengi ya ajabu ikiwemo kutunga visa ambavyo vingewaweka katika vichwa vya habari. Habari za msanii kufumaniwa, kupigwa, kulewa, kulazwa hospitali, kupendana, kuachana na kadhalika vimekuwa vikitungwa na wasanii mbalimbali ili kujiweka katika nafasi ya kutengeneza hadithi kwenye vyombo vya habari kujiongezea umaarufu. Ujio wa mitandao ya kijamii umekuwa tena nafasi nzuri za kutengeneza ‘U superstar’ wasichana ambao wamekuwa wanatumia sanaa kama daraja la kupata ‘U superstar’, wamekuwa wakitumia kurasa zao kwa kutundika picha wakiwa nusu utupu ili mradi kutafuta kujulikana na kupata wateja wa shughuli isiyohusiana na sanaa.

Matokeo ya vurugu hizo zote ni kuwa msanii kuwa ‘superstar’ si lazima awe msanii bora. Wako wasanii wa aina hiyo wengi na ukiulizia kazi zao za sanaa, hazionekani au hazijulikani. Na kwa kazi zao za kisanii ambazo hutolewa hadharani, huishia kupotea baada ya muda mfupi, lakini sifa za ‘u supersta’ zinaendelea kujengwa kwa namna moja au nyingine. Jambo ambalo ni bahati mbaya kwa tasnia nzima ya sanaa, nikuwa masupastaa hawa wajanja wajanja huaminiwa sana hata na viongozi wa ngazi za juu nchini,  na hutumika kama vigezo vya kukua kwa tasnia. Na mara nyingine huombwa hata kutoa ushauri wa namna ya kuboresha tasnia ya sanaa. Mungu isaidie tasnia ya sanaa Tanzania.

Monday, August 29, 2022

UZURI NA UBAYA WA TEKNOLOJIA ZA KISASA ZA KUREKODI MUZIKI

 

Tape recorder ya studio miaka ya 90 kurudi nyuma


Kwa manamuziki ambaye uliewahi kurekodi miaka ya 90 na kurudi nyuma, hakika studio za siku hizi ni tofauti sana. Teknolojia inayotumika kurekodi siku hizi  inarahisisha sana kurekodi. Mwanamuziki mmoja mmoja anarekodi kipande chake, akikosea kuna uwezekano wa kurudia peke yake na wala si kazi ngumu. Waimbaji pia wanaimba mmoja mmoja na kuna uwezekanao hata muimbaji mmoja akaimba mara nyingi kipande kimoja na hatimae ikasikika kama ni kwaya nzima ilikuwa inaimba. Teknolojia inawezesha hata mtu asiyejua kuimba vizuri akarekebishwa na kusikika akiimba kwa sauti tamu ya kuvutia, pia kwa utaratibu huu wimbo mmoja unaweza hata ukachukua mwezi mzima kukamilisha kuurekodi. Kwa kweli kuna tofauti kubwa sana.
Teknolojia imebadili taratibu zote za utengenezaji wa muziki.  Ngoja nirudi nyuma miaka ya 80, nielezea taratibu za kurekodi nyimbo ambazo siku hizi zinaitwa zilipendwa. Kurekodi haikuwa kazi rahisi, hakukuwa na kompyuta ya kutengeneza mapigo na kutoa sauti mbalimbali za muziki na hata kuelekeza mwendo wa wimbo, ililazimika waweko watu halisi wapige muziki na kurekodiwa kwenye kanda zilizoitwa tape. Mashine za kurekodia zilizoitwa ‘tape recorders’ zilikuwa na uwezo wa kurekodi njia mbili  (two track), hebu linganisha hilo na zama hizi ambazo  hata kompyuta ya kawaida ikiwa na program sahihi inaweza kurekodi mamia ya ‘tracks’ bila tatizo lolote.  Hivyo basi teknolojia hii ya two track ililazimisha kundi linalotaka kurekodi liupige wimbo wao wote bila kukosea ‘live’ na akikosea mtu mmoja tu, lazima kufuta wimbo wote na kuanza upya. Hii ilikuwa na maana kuwa kila kundi lililotaka kwenda kurekodi, ilikuwa lazima kufanya mazoezi magumu ya muda mrefu ili kila mwanamuziki awe anauhakika na vipande vyake atakavyovipiga.

Studio kubwa za kurekodi muziki zilikuwa mbili, studio ya Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) na studio za Tanzania Film Company (TFC). Zote zilikuwa na masharti yaliyofanya kazi ya kurekodi kuwa ngumu zaidi. Studio ya RTD ilikuwa inaipa kila bendi siku mbili za kurekodi. Siku ya kwanza kurekodi nyimbo mpya za bendi na siku ya pili kurekodi kipindi cha Club Raha Leo. Kila bendi ilikuwa inahitajika kuja na vyombo vyake. Mapema siku ya kwanza ya ratiba, bendi iliingiza vyombo studio na kazi ya kuvifunga na kuvitayarisha kwa kurekodi ilichukua muda wote wa asubuhi ya siku ya kwanza. Mchana baada ya kula ndipo wanamuziki walipoingia kurekodi nyimbo zao. Kulikuwa na sheria kuwa watu wote ambao si wafanyakazi wa RTD walitakiwa kuwa wameondoka eneo la RTD kabla ya kushushwa bendera saa 12 jioni. Hivyo basi bendi kama ilikuwa na nyimbo 4 au 10 ililazimika kukamilisha kazi ya kuzirekodi zote hizo kati ya saa 8 mchana mpaka saa kumi na mbili jioni. Kama nilivyosema awali, nyimbo zilitakiwa kupigwa na kuimbwa  bila kukosea, kwa kweli kazi iliyokuwa ikifanywa na wanamuziki wa enzi ile ni ya kusifika. Ukisikiliza kwa makini kuna nyimbo nyingi maarufu zilizopendwa huwa zinakuwa na makosa madogo madogo, lakini mara nyingi ilikuwa ni  kutokana na hali niliyoitaja hapo juu. Kuna wimbo mmoja wa African Fiesta ambao alikuwa anaimba Tabu Ley unaitwa Ndaya, wakati wa chorus unamsikia Tabu Ley akijichanganya maneno , lakini nadhani ilionekana upite, hii ilikuwa ikitokea pale wimbo umesharudiwa mara nyingi na wanamuziki wamekwisha choka.
Fundi mitambo alikuwa akitupigia wimbo tusikie baada ya kurekodi na alikuwa akiuliza' Vipi huu?' wenyewe tukiwa tumeridhika tulijibu 'Upite'.

TFC hawakuwa na masharti ya muda wa kuondoka studio, TFC ilikuwa shirika la umma na hivyo  lilikuwa likiendeshwa kibiashara na malipo ya studio yalikuwa kwa  siku. Kwa kuwa bendi hazikuwa na fedha, mara nyingi zililipa malipo ya kutumia studio siku mbili zikizidi sana tatu. Hapo ilikuwa wanamuziki wenyewe wanakuwa makini ili kutumia vizuri muda wao, ili usije ukaisha na fedha za kuongeza muda zisiweko. Nikiwa Vijana Jazz tulitumia studio za TFC kurekodi album iliyokuwa na nyimbo maarufu kama Thereza, VIP na Mfitini. Tulikesha siku mbili kukamilisha album ile.

Teknolojia ya sasa inaruhusu mtu mmoja kama unauwezo wa kupiga vyombo mbalimbali na kuimba,ukaweza hata kutengeneza nyimbo ambazo zitasikika kama vile ni bendi nzima ilikuwa kazini. Kwa mfano kati ya album za kwanza za wanamuziki wa Tanzania ambazo zilitoka kwa kutumia teknolojia hii ya sasa  ya ‘multi track’ ni album ya Dhiki ya Patrick Balisidya. Katika album hii Patrick alipiga vyombo karibu vyote na pia kuimba sauti zote, ukisikia nyimbo hizo utadhani zilipigwa na bendi nzima.

Pamoja na ubora wote wa teknolojia hii, kurekodi kwa mtu mmoja mmoja kunaondoa sehemu kubwa ya utamu katika nyimbo zilizorekodiwa. Hebu fikiria ngoma yoyote ya kiasili, irekodiwe kwa mpigaji ngoma moja moja kuingia studio na kurekodi mapigo yake, utamu ule wa wapigaji kupeana hamasa wakati wa kupiga wote utaondoka. Pengine ndio sababu nyimbo za sasa zinarekodiwa na kusikika vizuri lakini zinakosa uhai fulani wa wapigaji kupiga kwa pamoja, na kuhamasishana, kupata ile 'feeling ya live'. Nyimbo za bendi zamani zilikuwa kwanza tayari zimeshapigwa mara nyingi katika kumbi mbalimbali hivyo kuwa na aina ya uhai ambao huwezi kuupata katika wimbo ambao ni mpya kabisa. Utaratibu huu uliwezesha bendi kuboresha wimbo hatimae siku ya kurekodi wimbo unakuwa umeiva.

Wednesday, August 24, 2022

NIMEPITWA NA WAKATI NGOJA NIKAPUMZIKE

 


Nilipokuwa mdogo nilikuwa naona vibabu vya mtaani kwetu viko vya aina mbili, aina ya kwanza ilikuwa vibabu ambavyo vilikuwa havicheki kila saa vimenuna na kwa ujumla, watoto wote tuliviogopa, na tulianza hata kutunga hadithi kuwa vitakuwa vichawi, au vilipata matatizo makubwa wakati wa ujana na kadhalika. Kundi la pili la vibabu ilikuwa vile vibabu ambavyo huvikuti vimenuna, ukiviamkia vinakujibu kwa furaha na kuanza kuulizia wazazi wako, mambo yako ya shule na kadhalika. Vibabu hivi hata kama una shida ilikuwa rahisi kukusikiliza na kukupa ushauri hata msaada. Na pia kulikuwa na vibibi vya aina hiyohiyo pia, tulikuwa na rafiki yetu bibi yake alikuwa anauza maji, kila baada ya siku chache tulikuwa tukimtembelea bibi kwa kuwa lazima atatugawia senti  kumi kumi kutokana na biashara yake ndogo ya maji, kwa hesabu za harakaharaka alikuwa akitugawia pato lake la siku nzima bila hata kusita, na wala hatukuwa wajukuu zake wa moja kwa moja. Sasa yamenikuta siku hizi mimi ndie sasa nimekuwa babu, na polepole naanza kupata picha kwanini wale babu na bibi zangu walikuwa vile.
Wahenga walikuwa na msemo, nyani mkongwe kakwepa mishale mingi, na ndio ilivyo katika maisha, wakongwe wamekwepa mengi, wameona mengi, kwa asili ya mila na tamaduni zetu, wazee walikuwa na nafasi muhimu katika kutoa ushauri wa mambo kadhaa, lakini hili linapotea taratibu, na hasa ukichukua dhana ya siku hizi isemayo ‘wazee wamepitwa na wakati’.
Wasanii ni sehemu ya jamii, hivyo hata kwenye tasnia hii dhana ya ‘wazee wamepitwa na wakati’ inatumika sana.
Ukongwe katika fani unakupa elimu ya mambo mengi, mengine unafundishwa na wakongwe uliowakuta, mengine unajifunza kazini, hatimae kichwa kinakuwa na majibu ya mambo mengi ambayo kwa utamaduni wa zamani unatakiwa kuyarithisha kwa wanaochipukia katika fani. Lakini hili linakuwa gumu pale inapokuja dhana kuwa ‘wazee wamepitwa na wakati’. Ukisha kutana na hali ya kuonekana umepitwa na wakati kuna mambo mawili unaweza ukaamua, moja unaweza ukawa mtu wa kukasirika kila wakati, kiasi cha kwamba mtaani ukaonekana ni babu moja mwenye hasira zisizo na sababu, watoto wakaanza kuhadithiana kuwa utakuwa mchawi au ulipata matatizo ya akili ulipokuwa kijana. Jambo la pili linaloweza kutokea ni kuamua kuwa mchangamfu na kubaki unacheka na kila mtu, ili usisumbue kichwa chako, na hatimae kuondoka duniani na elimu yako kwa furaha.
Kwa kicheko na furaha sana nakumbuka enzi kabla hakujawa na Baraza la Sanaa la Taifa. Enzi hizo  kulikuwa na taasisi inaitwa Baraza la Muziki la Taifa (BAMUTA), chombo kilichoanzishwa mwaka 1974. Kazi ya BAMUTA ilikuwa kuratibu shughuli za muziki na muziki wa aina zote. BAMUTA iliuangalia muziki kwa mapana yake yote, elimu, vifaa, masoko, maadili, BAMUTA pia ilikuwa na kazi ya kuandaa sera za Taifa za muziki. Katika kipindi cha BAMUTA bendi zilisaidiwa vyombo vya muziki na serikali, BAMUTA ilitungwa vitabu kadhaa vilivyohusu muziki, ukiwemo muziki wa asili. Mitaala ya muziki ilitayarishwa na muziki ukawa somo mojawapo linalofundishika mashuleni, waalimu wake walitayarishwa katika vyuo vya waalimu wa sanaa kama vile Chuo cha Butimba, na wakaenezwa katika vyuo na mashule nchini kote, wengine wakawa maafisa utamaduni na wengine kuwa katika ngazi mbalimbali za wizara ya Utamaduni na sanaa. Kila mkoa ulikuwa na japo bendi moja iliyokuwa na umaarufu, kulikuwa na kwaya nyingi, madisco mengi,  japo wakati huo uwekezaji katika muziki haukuwa mkubwa kama ulivyo sasa. Mazingira yakawekwa yaliyoruhusu wapenzi wa muziki waweze kusikiliza aina mbalimbali za muziki hata muziki ule ambao si wa kibiashara lakini ni mzuri kwa ubora wake au kwa ujumbe wake. Mazingira hayo yaliwapa wanamuziki maktaba pana ya kuweza kutohoa aina mpya za muziki. Wajumbe wa BAMUTA walitoka kila kona ya nchi na hivyo kuipa BAMUTA sura ya Kitaifa, angalia orodha ya wajumbe wa Baraza la Muziki Tanzania;

1.   Boniface Musiba (Mwenyekiti wa BAMUTA)
2. D. R. Mbilinyi (Mwenyekiti Msaidizi wa BAMUTA)
3. S. Chidumizi (Mjumbe wa BAMUTA-Dodoma)
4. J.Y. Sapali (Mjumbe wa BAMUTA-lringa)
5. Padre J.M. Buluma (Mjumbe wa BAMUTA-Mwanza)
6. A. Kosana (Mjumbe wa BAMUTA-Shinyanga)
7. R. Singano (Mjumbe wa BAMUTA-Tanga)
8. Mbaraka Mwishehe (Mjumbe wa BAMUTA-Morogoro)
9. Padre Kayatto (Mjumbe wa BAMUTA-Mbeya)
10. Gwabukoba (Mjumbe wa BAMUTA-Kigoma)
11. P. Balisidya (Mjumbe wa BAMUTA-Dar es Salaam)
12. R. Mselewa (Katibu Mtendaji wa BAMUTA)
13. E. Kavalambi (Mkufunzi wa Muziki-Marangu CE.T.)
14. K. J. Nsibu (Aflsa Utamaduni-Korogwe)
15. E. Lameck (Mwanakwaya-Mwatex)
16. G. Kanyabwoya (Mwalimu-Kigoma)
17. T. Busyanya (Mkufunzi wa Muziki-DSM CE.T.)
18. G. Daudi (Afisa Sanaa za Maonyesho-Rukwa)
19. John Mgandu (Mwalimu wa Muziki-Tabora Shule ya Seko-ndari ya Wavulana)
20. E. G. Makala (Wizara ya Utamaduni)
21. F.E. Nkwera (Mkufunzi wa Muziki-Songea CE.T.)
22. T. Nkera (Mkufunzi wa Muziki-Ndwika CE.T.)
Wakati ufanisi wa Baraza hili ukiendelea, akatokea mtu mmoja akaanzisha wazo la kuwa na Baraza moja kwa ajili ya Sanaa zote, na ndipo likazaliwa Baraza la Sanaa la Taifa. muziki ukashushwa na kuwa ni Idara tu katika katika Baraza hili, tena hata hiyuo idara ilisha uwawa .

Lakini nisijichoshe, ngoja nikacheze na watoto, si unajua wazee tumepitwa na wakati.

 

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...