YOUTUBE PLAYLIST

Sunday, April 25, 2010

Akina mama nao- Asia Darwesh


Asia Darwesh ni miongoni mwa wanamuziki wanaoheshimika sana katika jamii ya wanamuziki na wapenzi wa muziki waliowahi kusikia au kufurahia kazi zake. Katika picha hapo juu Asia ambae alikuwa mpiga Keyboards wa kutumainiwa anaoneka picha ya juu akiwa na King Kiki enzi za Double O, na chini akiwa Mk Sound. Asia aliwahi pia kupigia Bicco Stars ambapo yeye pamoja na Andy Swebe na Mafumu Bilali na wenzao (waliihama MK sound), waliweza kuipandisha sana chati bendi hii. Hatimae Asia aliweza kumiliki bendi yake na alipatwa na umauti akiwa na bendi yake ambayo ilifanya vizuri sana huko Uarabuni.

Mzee Joseph Nyerere


Mzee Joseph Nyerere alikuwa mpenzi sana wa Vijana Jazz Band. Nakumbuka siku za Jumapili ambapo Bendi ilikuwa na onyesho lake lililoitwa Vijana Day mara nyingi ungemkuta pembeni akisikiliza muziki na pengine akiomba special request. Ilikuwa ni burudani pale ambapo aliamua siku hiyo kucheza maana alikuwa na staili ya peke yake iliyofanya mtu apende kumuangalia. Historia inasema alisoma Tabora Boys na alikuwa Band Master wa bendi ya shule na alipendwa sana kutokana na mbwembwe zake alipokuwa akiongoza na kifimbo cha Band Leader. Mzee Joseph aliwahi kuwa Katibu Mkuu wa TANU Youth League. Pichani akiwa jukwaani na Marehemu Hemedi Maneti katika Ukumbi wa Vijana Kinondoni, kwa mbali nyuma anaonekana Aggrey Ndumbalo akiwa ameshika gitaa na Said Hamisi muimbaji wa Vijana akiwa napiga makofi, wote wamekwisha tangulia mbele ya haki.

Libeneke 2

Katika blog hii tuliwahi kuzungumzia chanzo halisi cha neno LIBENEKE. Nilieleza kuwa neno hili na hasa linapounganishwa na kusema 'endeleza libeneke', lilitokana na wimbo wa Butiama Jazz Band uliokuwa ukitaja majina ya wanamuziki wa bendi hiyo na kila mmoja akiambiwa aendeleze libeneke. Nimepata bahati ya kuongea na aliyekuwa Kiongozi na mpiga solo wa Butiama Jazz Band. Alikuwa na haya ya kusema. Butiama Jazz Band ilianzishwa mwaka 1971, makao yake makuu yalikuwa mtaa wa Kongo maeneo ya Kariakoo, Dar es Salaam, jirani kabisa na DDC. Ilianzishwa na asilimia kubwa ya wanamuziki kutoka Ifakara na ndio maana waliamua kuchukua jina la ngoma ya kwao na kuuita mtindo wa bendi yao Libeneke. Kiongozi wa bendi alikuwa Mzee Makelo na Katibu wa Bendi Mzee Mustafa Mkwega. Mzee Mkwega aliwahi kufanya kazi kwa Hayati Mwalimu Julius K Nyerere na hivyo alikuwa anawasiliana nae kwa karibu. Alikwenda kwa niaba ya wenzie na kumuomba Mwalimu awasaidie vyombo vya muziki, na aliwatuma wakalete Profoma invoice ya vyombo, walipoleta Mwalimu aliitia saini na ilitosha kwenda kupewa vyombo vipya dukani. Kama shukrani kwa Mwalimu waliita bendi yao Butiama Jazz Band. Na kuanzia hapo kila mwalimu alipoenda likizo ya mwaka Butiama bendi ilikwenda huko kutumbuiza wageni mbalimbali waliokuwa wanamfuata Mwalimu huko.

Saturday, April 24, 2010

Maquis Original


Maquis Original wakiwa katika uwanja wa Jamhuri Dodoma. Mwenye nyeusi tupu akiwa na gitaa ni Dekula Kahanga Vumbi, wa pili toka kushoto na suruali nyeusi ni Issa Nundu haya tuwataje wengine hapa.

Baziano na Kasheba


Kwa wapenzi wa Fauvette na baadae Kasheba Group na Zaita Muzika, sauti ya Baziano si rahisi kusahaulika. Lakini kwa mapenzi yake Mungu, Baziano(wa kwanza kushoto) na mpiga gitaa wake Ndala Kasheba (wa pili kutoka kulia) hatunao tena duniani Mungu awalaze pema peponi. Pichani pia yupo Kasongo Mpinda (mwimbaji) wa pili kushoto, na Matei Joseph (mpiga drums).

Akina mama nao


Ni jambo lisilopingika kuwa akina mama wamekuwa sambamba na wanaume katika kuendeleza gurudumu la muziki wa nchi hii. Kumekuwa na tatizo la mtizamo na hivyo kufanya akina mama kutokuonekana sana katika fani hii kwa vile siyo siri imekua ikipigwa vita katika miaka yote. Pamoja na kuwa hakuna anaetamka hadharani kuwa wanamuziki ni wahuni, lakini taratibu na sheria zinaongea lugha ya kimya kuwa hivyo ndivyo. Nitoe mifano
1. Pamoja na kuwa kuna syllabus ya muziki kuanzia darasa la kwanza, kumekua hakuna jitihada kubwa ya kuhakikisha waalimu wanapatikana. Chuo cha Butimba ndio kimekua chanzo cha waalimu wa muziki lakini akishafika mashuleni hupangiwa vipindi vingine, na muziki huacha kama ulivyo.
2. Leo hii akiingia mwanamuziki kutoka nje ya nchi huhitajika kuwa na work permit, lakini kwa wanamuziki wa nyumbani hakuna taratibu zozote za ajira inayotambulika, hata wahudumu wa ndani wanatetewa bungeni lakini si wanamuziki. Angalia hata Waziri anaeshughulika na Vijana wa Tanzania na Kazi haoni soni kutoa ajira kwa vijana kutoka nje ya nchi yake katika fani ya muziki. Idadi ya wanawake katika muziki imekua kubwa sana kwa sasa ikilinganishwa na zamani lakini bado kuna wanawake wengi waliotikisa anga hizi zamani. Pichani ni muimbaji wa kike wa Afro 70 kutoka South Africa ambaye alisaidia sana kufanya muziki wa Afro kuwa na vionjo tofauti na bendi nyingine. Muimbaji huyu aliitwa Nini, na alirekodi nyimbo moja na Afro70, Mayele. Nini alikua na kaka yake aliyeitwa Vuli ambaye alipiga pia muziki hapa Tanzania na kutunga nyimbo ambayo bado inapiga na bendi kadhaa Tanzania'Lonely Child'. Vuli aliendelea na hatimaye kuwa manamuziki wa Lucky Dube.

Friday, April 23, 2010

Kilimanjaro Band 1




Kilimanjaro Band ni kati ya bendi kongwe hapa Tanzania. Ilianza mwanzoni mwa miaka ya sabini. Imewahi kutokea bendi ikapiga katika harusi ya mzazi na pia mtoto. Generation nzima ya familia. Maelfu ya watu wamekwisha hudhuria maonyesho ya Kilimanjaro Band hebu hapa tuone kati ya picha zao za zamani.

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...