YOUTUBE PLAYLIST

Monday, July 25, 2022

MWAKA MMOJA BILA MPIGA KINANDA WAZIRI ALLY SEIF

 
















Ni mwaka mmoja toka mwanamuziki Waziri Ally Seif alipotutoka ghafla., naikumbuka vyema siku ili, ilikuwa siku ya Ijumaa tarehe 23 July 2021 , kama saa nne usiku hivi nilipoamshwa na mlio wa simu yangu, nilikuwa tayari usingizini kwani mchana ule nilikuwa nimefanya mizunguko mingi sana katika eneo la Ngome Kongwe Zanzibar, nikiwa katika harakati za Tamasha la filamu la ZIFF, kwani kulikuwa na filamu ambayo niliiweka muziki nayo ilikuwa ikishindana katika matuzo mbalimbali ya tamasha lile. Nilishangaa kona namba iliyokuwa ikiita, ilikuwa ya Lulu, binti wa marehemu mwanamuziki mwenzangu Mabruk Omari  maarufu kwa jina la Babu Njenje, binti huyu  makazi yake ni Uingereza. Nikapokea simu ile, cha kushangaza alikuwa analia, nikamuuliza vipi? Akanijibu ‘ Anko kwani we hujui? Kuna mtu kanipigia simu kuwa Anko Waziri  amefariki, hebu nihakikishie maana siamini’. Nikamwambia subiri kwani habari za uzushi wa vifo vya watu katika siku hizi za teknolojia rahisi za mawasiliano ni jambo la kawaida sana. Niliwapigia wanamuziki wawili wa bendi ya Kilimanjaro nao wakanambia hawana taarifa ya kifo, ila walikuwa na taarifa kuwa Waziri alikuwa kapelekwa hospitali nikapewa namba ya mmoja wa waliompeleka Waziri hospitali namba hiyo ikawa haipatikani. Hatimae ukaja ujumbe wa Whatsapp ukionyesha kuwa rafiki na ndugu mkubwa wa Waziri Ally, bwana Aboubakary Liongo alikuwa katoa taarifa kwenye ukurasa wake wa Instagram kuwa Waziri Ally hatunae tena. Nikampigia Aboubakary akanihakikishia kuwa Waziri Ally hatunae tena. Hatimae nilimtumia Lulu ujumbe  wa maandishi kuwa kweli Anko wake hatunae tena. Na ghafla simu nyingi zikaanza kupigwa nyingine za pole na nyingine za waandishi wakitaka taarifa na nyingine za wapenzi na mashabiki wa bendi ya Kilimanjaro wakitaka kujua kama walichokisikia ni kweli. Na hilo liliendelea usiku mzima.

Nilianza kukumbuka historia yangu na Waziri Ally, nilimuona kwa mara ya kwanza mwaka kati ya mwaka 1984 na 1985 wakati huo, bendi ya Kilimanjaro ilipokuwa ikiitwa The Revolutions na ikiwa na makazi yake Kilimanjaro Hotel Dar es Salaam. Bendi hiyo ilikuwa imetoa tangazo gazetini  ikataka watu wanaotaka kushindana kuimba wimbo wa ABBA wa I have a dream wafike katika ukumbi wa Simba Grill wa hoteli ya Kilimanjaro, kwa kuwa nilikuwa najua kuimba wimbo huo nikawa mmoja ya washiriki.  Baadae nikaja sasa kuongea nae binafsi baada ya bendi hiyo kuhamia hoteli iliyokuwa inaitwa Bushtrekker, na alikuwa akiuuza kinanda chake wakati huo nilikuwa katika bendi iliyokuwa ikihitaji kinanda, hapo tukaongea na kujadili kile kinanda, japo tulishindwa kukinunua. Tuliendelea kukutana hapa na pale katika shughuli mbalimbali za kimuziki kama vile semina na mikutano mbalimbali au hata matamasha kama vile mashindano ya bendi ya Top Ten Show.  Mwaka 1999 nikiwa Mwenyekiti wa CHAMUDATA, Waziri Ally alikuwa mmoja ya wajumbe wa Halmashauri Kuu ya chama hicho, katika mwaka huu juhudi za CHAMUDATA kupata studio yake ya kisasa ya kurekodi, gazeti lake na kituo chake cha redio zikafikia kileleni, tukaweza kuanzisha taasisi ya habari ya CHAMUDATA iliyoitwa Asilia News Agency, ambamo Waziri Ally alikuwa mmoja ya wajumbe wa bodi wa taasisi hiyo ambayo ingeendesha redio na gazeti la CHAMUDATA kwa msaada wa taasisi ya Norway iliyoitwa Stromme Foundation. Bahati mbaya sana sana  viongozi wa Halmshauri Kuu na Kamati kuu ya CHAMUDATA walikuja kuukataa mradi huo wote kwa kuwa walielezwa kuwa Katiba ya CHAMUDATA ilikuwa na mapungufu na ilitakiwa irekibishwe kabla ya kuendelea na mradi. Jambo ambalo viongozi hao waliliita kuiingiliwa kwa chama chao na kuukata mradi, jambo lililotulazimu baadhi ya viongozi  kuamua kujiuzuru uongozi wa CHAMUDATA, akiwemo Waziri Ally na Abdul Salvador na mimi ambaye nilikuwa mwenyekiti wakati huo.

 Kwa kuwa vifaa vya studio vilikuwa tayari vimeshaingia nchini, Abdul Salvador, Waziri Ally, mimi na bendi nzima ya Kilimanjaro, tulishirikiana kuhakikisha studio inatengenezwa na kuanza kufanya kazi kama ilivyopangwa katika maombi ya mradi, studio iliwekwa chini ya Bodi ya muda ikitegemewa kuwa viongozi wa CHAMUDATA wangeona kosa lao na kurudi kuja kuchukua na  kuendesha mradi wao,  jambo hilo hakilikutokea, Ubalozi wa Norway hatimae baada ya kutangaza gazetini ukaikabidhi studio hiyo kwa KIlimanjaro Band. Na ilikuwa katika kipindi hiki nilipojiunga na Kilimanjaro Band kama mwanamuziki na kuanza kufanya kazi kwa karibu na Waziri. Kwanza alikuwa makini sana kila kitu  alichokuwa akikifuatilia. Tulikuwa na ratiba nzuri sana ya mazoezi makali yaliyobebwa na upigaji wake mahiri wa kinandana upangaji wa sauti za waimbaji. Mwaka 2000 tukaweza kurekodi katika studio yetu album ya Kinyaunyau, na Waziri Ally alienda na ‘tracks’ Uingereza kufanya ‘mastering’ ya album  hiyo ambayo inatamba mpaka sasa na hata wanamuziki wa Bongofleva wameweza kurekodi tena na tena wimbo wa tupendane na vibwagizo vingi kutoka album hiyo bado vinaendelea kutumika katika nyimbo mpya zinazorekodiwa na wanamuziki wapya. Tuliweza kuchapisha CD, kanda za video na kanda za kaseti za album ya Kinyaunyau hukohuko UIngereza na hatimae kuziingiza nchini. Tulihakikisha tunalipa kodi zote vizuri na kuweka mahesabu yetu sawa, nia ilikuwa kuionyesha TRA makusanyo ambayo ingeweza kuyapata kutokana na biashara ya muziki, lakini pamoja na jitihada hizi TRA hawakuonyesha kujali au kuelewa nia yetu mara zote tulizojaribu kuwaona. Waziri Ally aliingiza Kilimanjaro Band LTD kuwa mmoja wa wanachama wa Chamber of Commerce ili kuonyesha kuwa muziki nayo ni biashara na alikuwa muwakilishi kwa muda mrefu wa bendi na wasanii kwa ujumla katika taasisi hiyo.  Busara za Waziri Ally zilimfanya kuchaguliwa kuwa mjumbe wa Bodi wa Tamasha la muziki la Sauti za Busara linalofanyika kila mwaka Zanzibar, na akawa mjumbe aliyetegemewa kwa muda mrefu.  Historia yake kimuziki ya Waziri  ilianzia Tanga ambako ndiko alikozaliwa. Akajiunga na kundi maarufu la Lucky Star kama mpiga kinanda wakati akiwa bado mtoto mdogo. Mzee Moses Nnauye alipokuwa Mkuu wa Mkoa wa Singida akaanzisha bendi iliyoitwa Ujamaa Jazz Band  na kuwakusanya wanamuziki mahiri akiwemo Waziri Ally na marehemu  Suleiman Mwanyiro, bendi hiyo ilikuwa ikipiga muziki kwa mtindo waliouita King’ita.  Waziri alirudi tena Tanga na kujiunga na kundi lililokuwa limeanzishwa na vijana wa Kigoa waliokuwa hapo Tanga, na kukutana huko na Marehemu Mabruki Omary maarufu kwa jina la Babu Njenje na Mohamed Mrisho  maarufu kwa jina la Moddy. Kundi hilo lilikuwa likiitwa Love Bugs. Baadae jina lilibadilika na kundi kuitwa The Revolutions. Kundi hili lilitoka Tanga na kuanza kuwa maarufu katika hoteli kubwa za Dar es Salaam na Arusha. Na ni wakati huu Waziri Ally aliondoka Revolutions na kujiunga na kundi la JUWATA. Katika kundi hili Waziri aliweza kushiriki katika nyimbo ambazo zilikuja kuleta mapinduzi katika umuhimu wa kinanda kwenye bendi za ‘rhumba’. Wimbo wa Beresa Kakere unaojulikana kama Sogea Karibu ulimpa nafasi Waziri kupiga kinanda ambacho kimeufanywa wimbo huo upendwe mpaka leo, na pia kukipa heshima kinanda katika muziki wa rhumba la Tanzania, katika zama hizo kinanda kilidharauliwa sana katika muziki wa rhumba na kuitwa chombo cha muziki wa Taarab au muziki wa hotelini. Waziri hakukaa sana JUWATA na baada ya miezi michache akarudi Revolutions, kuhama huku kukampatia jina la utani la Kissinger. Henry Kissinger alikuwa Waziri wa mambo ya nje wa Marekani kati ya mwaka 1973 hadi 1977 na alijukana sana kwa kusafiri kwake nchi mbalimbali, na kuhama kwa Waziri kutoka Revolutions na kwenda JUWATA kukafananishwa na Kissinger na akapewa jina hilo la utani mpaka umauti wake. Waziri hakuwahi kuhama tena Revolutions, mwaka 1997 bendi hii ikabadili jina na kujiita Kilimanjaro Band baada ya kuweka maskani ya muda katika jiji la London na kurekodi album ya kwanza iliyoitwa Katakata,  hivyo kuona bendi ingetambulika ya Kiafrika zaidi kwa jina la Kiafrika.  Waziri Ally ambaye amezaliwa mwezi Novemba mwaka 1954, aliwahi kunambia alipokuwa mdogo alikuwa akitaka kuwa hakimu, akawa anatoroka hata shule kwenda mahakamani na kusikiliza kesi zinavyoendelea. Mama yake alikuwa askari magereza, na baba yake Mzee Ally Seif yu hai. Kwa miaka kadhaa ya karibuni,  Waziri alikuwa na tatizo kubwa la moyo, na amewahi kwenda India mara mbili kwa ajili ya matibabu, alikuwa akitumia dawa kila siku ili kuwa katika hali ya unafuu. Ucheshi wake na utani wake ulificha maumivu aliyokuwa nayo moyoni mpaka kifo kilipomkuta. Nimalizie kusema Mungu amlaze pema peponi ndugu yetu na rafiki yetu Waziri Ally Seif.      


Saturday, June 3, 2017

TATIZO LA NIDHAMU KATIKA BENDI ZETU ZA MUZIKI....


Miezi chache zilizopita rafiki yangu mmoja alinambia ameamua kuunda bendi mpya kabisa, alikuwa na lengo la kuleta muziki mpya kabisa katika anga ya muziki Tanzania. Aliongea kwa furaha na ni wazi alikuwa ana nia ya kufanya kitu kikubwa, maana alikuwa amegharamia fedha nyingi kununua vifaa vipya kabisa vya kuanzisha bendi. Mwezi mmoja baada ya mazoezi kuanza alinitafuta na kunambia ameamua kuvunja bendi na vyombo anauza. Nilipomuuliza kwanini kabadili mawazo katika kipindi kifupi vile, hata onyesho moja halijafanyika? Akanijibu. ’Wanamuziki wamenishinda, wana matatizo makubwa ya ndhamu’. Kiukweli sikushangaa sana kwani jambo hili si geni kabisa kwenye tasnia ya muziki kwa siku hizi. Mfumo wa uendeshaji bendi siku hizi ni tofauti sana na miaka ya nyuma.

Nichukue mfano wa bendi Vijana jazz Band, bendi ambayo nilijiunga mwaka 1989. Kujiunga na bendi hii kulitokana na mwaliko niliyoupata kupitia kwa muimbaji rafiki yangu Marehemu Mohamed Shaweji. Shaweji tulikuwa wote Tancut Almasi Orchestra kisha yeye akaniacha kule na na kujiunga na Vijana Jazz Band, yeye na muimbaji mwingine Marehemu Gota gota wakiwa wamemfuata mpiga gitaa Shaaban ‘Wanted’ Yohana, aliyetoka Tancut pia na kuhamia Vijana Jazz Band miezi michache kabla. Hivyo siku moja nikiwa na bendi ya Tancut Almasi kwenye onyesho kwenye ukumbi wa CCM kata ya 14 Temeke, Shaweji alikuja na kunambia kuwa Hemed Maneti, kiongozi wa Vijana Jazz Band alikuwa anataka nijiunge na bendi yake. Nilikubali na mwezi Oktoba 1989 nilijiunga na Vijana Jazz. Kufikia mwezi wa Desemba mwaka huohuo nikawa nimepewa wadhifa wa kuwa Band Master, kazi za Band Master ni kuangalia nidhamu ya jumla ya wanamuziki, ikiwemo mahudhurio mazoezini na kazini, uchelewaji, ulevi, usafi binafsi wa mwanamuziki na pia kupanga ratiba ya nyimbo ambazo zinatakiwa kupigwa katika onyesho.  Kwa mfumo uliokuweko, Band Master aliweza kumsimamisha mwanamuziki yoyote aliyekiuka sheria za bendi, au kutoa adhabu ya kukatwa fedha kutoka kwenye mafao yake ya kila wiki ikiwa ni adhabu kwa makosa mbalimbali. Nguvu hizi zilifanya wanamuziki kuwa na nidhamu wakati wote wawapo kwenye shughuli za bendi. Ikumbukwe kuwa katika bendi kulikuweko na kiongozi mkuu Band Leader. Huyu alikuwa na mamlaka ya kufukuza mtu kazi na pia kuajiri na ndie anaepanga hata ukubwa wa mshahara, lakini alikuwa haingilii madaraka ya Stage Master. Kwa kawaida wanamuziki waliona ni heri matatizo yao yaishie kwa Band Master kwani yakifika kwa Band Leader yanakuwa ndio yamefika hatua ya mwisho isiyo na rufaa na inaweza kuwa hasara kubwa. Ili kuonyesha Band Master alivyokuwa na nafasi ya pekee, siku moja wakati niko Vijana jazz band, ilikuwa twende kwenye moja ya maonesho na kuna gari ilikuwa inatupitia wote majumbani kwetu, tulipofika nyumbani kwa Band Leader Hemed Maneti, alitoka nje akiwa na karatasi kutoka hospitali akaja kunitaarifu kama Band Master, kuwa hataweza kuja kazini kwani anaumwa, Maneti alikuwa Band Leader lakini alikuwa akiheshimu nafasi ya Band Master, tena nilikuwa bado mgeni katika bendi. Hii ilikuwa ni ishara wazi kwa wanamuziki wengine kuwa Band Master lazima aheshimiwe na wote.

Hali si hivi katika bendi nyingi siku hizi. Ngumu kujua nani mwenye madaraka gani kwani bendi zinakuwa na mwenye bendi, mkurugenzi wa bendi, meneja, maseneta, kiongozi wa bendi, wadau wa bendi. Wote hawa wana mamlaka zisizo na mipaka, wanaweza kuamua wimbo gani upigwe, wanaweza kuamua nani atimuliwe au nani aingizwe kwenye bendi, mmoja akimsimamisha mwanamuziki kwa utovu wa nidhamu mwingine anaweza akamrudisha, hakuna mtu mwenye amri ya mwisho kuhusu lolote lile, hivyo nidhamu imeshuka sana, na pasipo na nidhamu si rahisi kuweko na maendeleo yoyote yenye tija.

Sasa nizungumzie kosa la rafiki yangu aliyetaka kuanzisha bendi na ikamshinda, kwanza baada ya kununua vyombo, aliaanza kutafuta wanamuziki akisaidiana na watu wake wa karibu, kisha akamteua kiongozi wa bendi, ambae kimsingi kilikuwa kilemba cha ukoka kwani rafiki yangu ndie aliyekuwa na amri ya mwisho kuhusu lolote katika bendi. Na kwa kuwa hakuwa na muda wa kushinda kila mahala na bendi, kundi likawa halina kiongozi mwenye mamalaka  na mwisho kila mtu akawa anafanya lake, walevi wakalewa sana, wachelewaji wakendelea na uchelewaji wao, hakukuwa na mtu aliyekuwa na uwezo wa kutoa mwelekeo wa bendi kinidhamu wala kimuziki. Muziki wa bendi kwa ujumla umekumbwa na tatizo hili la kukosa uongozi, maamuzi mengi yanafanyika kwa vikao, hata maamuzi yale ambayo ni ya kitaaluma yanangoja makubaliano ya wengi, na kwa mtindo huu bendi zitachelewa sana kujikwamua kwenye tope ambalo zimenasa.  Ushauri kwa wanaotaka kufungua bendi, ni bora kumtafuta mwanamuziki mmoja ambaye unaamini anaweza kutengeneza muziki unaoutaka au unaodhani utakuletea biashara kisha umwachie aijege hiyo bendi na wanamuziki anaoona yeye wanafaa, hapa tayari utakuwa umejenga utawala unaoeleweka. Mwenye vyombo usiingilie moja kwa moja mambo ya bendi, wanamuziki wakishajua kuwa kiongozi wa bendi hana mamlaka kamili, nidhamu inavunjika.

Friday, June 2, 2017

MWANAMUZIKI HALILA TONGOLANGA ANAUMWA ANAHITAJI MSAADA WA HARAKA WA KUSAFIRISHWA KUTOKA NDANDA HOSPITAL KUJA MUHIMBILI


MWANAMUZIKI HALILA TONGOLANGA MTUNZI WA WIMBO MAARUFU WA KILA MUNU AVE NA KWAO, AMEUGUA GHAFLA AKIWA KATIKA ZIARA YA MUZIKI MIKOA YA KUSINI. ANATAKIWA KURUDISHWA DAR ES SALAAM MAPEMA APATE MATIBABU YA HARAKA MUHIMBILI. KWA SASA AMELAZWA KATIKA HOSPITALI YA NDANDA. ANAE ONA AMEGUSWA NA ANAWEZA KUTOA USAFIRI AU MSAADA WOWOTE  APIGE SIMU 0713644439 ILI KUWASILIANA NA KATIBU MTENDAJI WA BARAZA LA SANAA LA TAIFA.

NI MIAKA 27 TOKA KIFO CHA HEMEDI MANETI ULAYA

Picha niliyoipiga tukiwa chumba cha maiti Muhimbili, mbele yetu ulikuwa mwili wa Hemedi Maneti. Kati ya waliopo kwenye picha ni marehemu Mzee jacob John, mwenye shati jeusi na marehemu Salum Faya mwenye jaketi jekundu
Mara ya kwanza kukutana uso kwa uso na Hemedi Maneti ilikuwa ni wakati Vijana Jazz band ilipita Iringa  ikielekea Songea mwaka 1989. Wakti huo nilikuwa mwanamuziki wa Tancut Almasi Orchestra, na kama ilivyokuwa ada miaka ile, bendi ikipita katika mji ambao kuna bendi wanamuziki walikuwa wakipiga muziki pamoja. Tuliongea nae machache lakini aliongea kuhusu kufurahishwa na setting ya vyombo vyetu, alisema inafanya vyombo vyote visikike. Wakati huo hatukujua lakini kumbe alikuwa kishaongea na Shaaban Wanted, Mohamed Gotagota na Mohamed Shaweji ili wajiunge na Vijana Jazz band, na hakika walihamia bendi hiyo wiki chache zilizofuata.
Katika mlolongo huohuo nilijikuta nikiitwa kujiunga na Vijana Jazz Band mwezi wa September mwaka huohuo na kufikia Oktober 1989 niliwasili Dar es Salaam kujiunga na Vijana Jazz Band. Siku ya kwanza nilipofika Vijana maneti alinipa shilingi 300 za kuanza maisha. Nitafute guest house ya kuishi na chakula kwa wiki moja. Hiyo ndiyo kumbukumbu yangu ya kwanza ya Maneti ambaye miezi michache baadae, tarehe 31 May 1990 siku ya Alhamisi majira ya saa kumi na moja jioni, Hemed Maneti alifariki katika hospitali ya Mwananyamala.  Alikuwa ameanza kuwa na matatizo ya afya miezi kadhaa kabla ya hapo na  hatimae kupelekwa Tanga kwa ajili ya matibabu. Hali yake ilipozidi kuwa mbaya alirudishwa kwa ndege  kuwasili Dar Jumatano 30 May na kupelekwa moja kwa moja hospitali ya Mwananyamala ambapo alilala na kufariki kesho yake. Marehemu alisafirishwa kwenda kuzikwa Tanga siku moja baadae.
Wimbo wa mwisho kurekodi ulikuwa wimbo Nelson Mandela uliotungwa nami, ukiwa wimbo uliokuwa matayarisho ya ziara ya Nelson Mandela.

Sunday, April 2, 2017

TUMETIMIZA MIAKA 11 TOKA KUONDOKEWA NA TX MOSHI WILLIAM


Mazoezini katika ukumbi wa Amana katika uhai wake
Moshi William alizaliwa mwaka 1958 hale Mwakinyumbi Korogwe. Pale palikuwa na Mzee mwanamuziki maarufu aliyekuwa akiitwa Mzee Masongi na bendi yake ilikuwa chnzo cha wanamuziki wengi maarufu akiwemo Moshi William. Jina halisi la Moshi William lilikuwa Shaaban Ally Mhoja lakini alikuja kubadili na kuitwa Moshi William kutokana na kuja kulelewa na baba mwingine. Alipewa kisifa cha TX, na Julius Nyaisanga.

Moshi alifariki siku ya tarehe 29 March 2006 katika wodi ya Sewa Haji baada ya operesheni ya kuondoa chuma katika mguu wake uliovunjika kwenye ajali. Alifariki saa tatu kasoro robo asubuhi na kuzikwa siku hiyohiyo katika makaburi ya Keko Machungwa. Moshi lipitia bendi kadhaa baada ya kutoka Hale zikiwemo UDA Jazz, Safari Trippers, Polisi Jazz na hatimae kutua JUWATA 1982. Ambapo aliweza kutuacha na album 13. Na pia alishinda tuzo la mtunzi bora kuanzia mwaka 2003 hadi 2005.
Kaburi la Moshi William

Mungu amlaze pema Shaaban Ally Manongi, TX Moshi William

Sunday, February 23, 2014

MAPENDEKEZO YA WASANII KATIKA RASIMU YA KATIBA MPYA.



 Utangulizi
Baada ya maagizo kutoka Tume ya Katiba ya kuwa kila kundi kutayarisha mapendekezo ya rasimu ya Katiba, wasanii nao chini ya mashirikisho yao manne Shirikisho la Filamu, Shirikisho la Muziki, Shirikisho la Sanaa za maonyesho na Shirikisho la Sanaa za ufundi  waliweza kuja na mapendekezo kadhaa ambayo waliyawasilisha katika Tume, kwa bahati mbaya hakuna kipengele chochote cha mapendekezo hayo kilicho ingizwa katika Rasimu ya Katiba. Kwa ushirikiano, Mashirikisho haya ya sanaa yameamua kufikisha mapendekezo yao moja kwa moja kwa Wabunge wa Bunge la Katiba ili kuwezesha vipengele hivyo kuweko katika Katiba yetu mpya.
 Mapendekezo
1.    Kutambuliwa kwa wasanii kama kundi maalumu katika Katiba.
Katika Rasimu ya Katika kuna makundi maalumu kadhaa ambayo yametajwa, kama vile wakulima, wavuvi, wafugaji, na kadhalika  na hivyo kutambuliwa kikatiba. Wasanii ni kundi kubwa katika jamii ya Kitanzania. Wasanii wapo karibu katika kila kaya Tanzania. Wafinyanzi, wasusi, wapambaji, wanamuziki waigizaji, mafundi mbalimbali wa ushonaji ujenzi na kadhalika, wako wengi wala hata wao hawajitambui kama ni wasnii kutokana na mazingira waliyomo. Katika ripoti mojawapo ya BASATA ya mwaka 2006, idadi ya wasanii nchini wakati huo ilikuwa ni milioni 6, ni wazi kuwa idadi hiyo kwa sasa itakuwa imepanda.  Katika miaka ya karibuni vijana wengi wamekuwa wanaongezeka kujiunga na kundi hili kwani katika sanaa kumekuwa na uwezekano wa kujipatia ajira, tena isiyokuwa na ukomo. Na hivyo sanaa kwa sasa si utamaduni peke yake bali ni sehemu muhimu ya uchumi wa Tanzania. Wasanii ni sehemu muhimu katika sekta ya Hakimiliki, takwimu za ripoti ya WIPO(World Intellectual Property Organisation) ya mwaka 2010, kuhusu mchango wa sekta ya hakimiliki katika uchumi wa Tanzania, inaonaonyesha  kuwa sekta hii, kati ya 2007-2010 ilichangia kati ya asilimia 3-4.6% ya gross domestic product(GDP). Na kiasi cha kati ya TSH 38.930 bilioni na 86.686 billion kilipatikana kama kipato cha walioajiriwa katika sekta hiyo. Kati ya watu 28, 202 na 44, 331 waliajiriwa rasmi, na hiyo ilikuwa kati ya asilimia 4.5 na 5.2% ya kundi zima la waajiriwa wa Taifa hili. Kwa kipimo cha GDP, sekta hii ilikuwa zaidi ya sekta ya madini, ambayo wote ni mashahidi imekuwa katika mazungumzo kila kona ya nchi. Na katika ajira sekta hii ilikuwa juu zaidi ya sekta nyingi zikiwemo madini, usafirishaji, mawasiliano, afya na ustawi wa jamii, maji, gesi, na hata ujenzi. Kwa mchango wa sekta hii wa 3.2% katika GDP kwa mwaka 2009 , umeweka sekta hii kuwa bora kuliko sekta za aina yake katika nchi  kama Croatia 3%, Singapore 2.9%, Latvia 2.9%, Lebanon 2.5%, Kenya 2.3%. Na katika mchango wa ajira sekta hii ilikuwa juu ya Romania, Bulgaria, Lebanon, Jamaica, Colombia, Kenya na Ukraine. Takwimu hizi hazijionyeshi katika takwimu za serikali kwa kuwa sanaa bado inaonekana ni utamaduni tu, na thamani yake katika uchumi haitiliwi uzito. Kutambuliwa kwa kundi hili kutawezesha kutungwa sheria na taratibu za kuwezesha Wasanii kuongeza ajira na mapato, na Taifa kufaidika na uchumi wa  raslimali hii.
2.     Kutajwa kwa  MilikiBunifu Intellectual Property ) katika Katiba.
Mali ziko za aina 3. Kuna mali zinazohamishika, mali zisizohamishika na mali zitokanazo na ubunifu. Aina mbili za kwanza zimetajwa katika katiba na ulinzi wake hujulikana na ni wa jadi. Lakini hii aina ya tatu ya mali huwa ni ngumu kuilinda kutokana na mfumo wake kuwa haushikiki hivyo sheria maalumu hutungwa kulinda aina hii ya mali (IP Laws). Mali zitokanazo na ubunifu kwa sasa ndio mali zenye kipa umbele duniani. Uvumbuzi wa teknolojia mbalimbali, ugunduzi wa njia mbalimbali za kuboresha maisha, sanaa na mengi yanayolindwa na milikibunifu, vimeweza kutoa ajira kubwa na kutoa mchango mkubwa wa kipato kwa wagunduzi na nchi ambazo wagunduzi hao wamekuwa wakiishi au kuzisajili kazi zao. Kama wasanii, haki zetu katika milikibunifu zinajulikana kama Hakimiliki, lakini kama Watanzania tunaona ni muhimu kulinda haki zote za Milikibunifu kwa maendeleo ya nchi yetu.
Nchi zote ambazo zimeweka taratibu imara za kulinda Milikibunifu duniani, zimewezesha wabunifu wake kubuni mambo ambayo yameweza kubadilisha maisha ya binadamu wengine duniani kote. Marikani iliweka kipengele cha Ulinzi wa hakimiliki katika katiba yake tangu mwaka  Agosti 1787, na kazi za wagunduzi wa Marekani tunaziona kila wakati katika kazi za sanaa na teknolojia. Korea kusini ilinakiri sehemu ya katiba ya Marekani kuhusu ulinzi wa Milikibunifu kuanzia mwaka 1948, kwa wakati huu wote ni mashahidi wa bidhaa kama Samsung, Ld Daewoo, Hyundai na kadhalika.
Milikibunifu pamoja na kulinda haki katika kazi za sanaa ambazo picha ndogo ya mapato yake zimetajwa hapo juu, Milikibunifu italinda haki za wabunifu wetu, tafiti za wasomi wetu, ugunduzi mbalimbali, taratibu mbalimbali za mambo yetu ya kiasili, dawa za asili za miti yetu, na taratibu za matumizi ya dawa hizo, na mali asili zetu nyingine nyingi tunazozifahamu na ambazo bado hatujazifahamu .
Kuna hasara nyingi ambazo hupatikana kama nchi haina ulinzi wa Milikibunifu, mifano michache hapa Tanzania, ni kupoteza kwa Milikibunifu ya jina Tanzanite, ambayo licha ya kuwa inachimbwa Tanzania tu lakini jina linamilikiwa na kampuni ya Afrika ya Kusini. Vazi la kikoi, pamoja kuwa ni la asili ya Tanzania, milikibunifu imesajiliwa Kenya, staili ya michoro maarufu ya Tingatinga milikibunifu yake iko Japan. Na haya ni machache ambayo yameshitukiwa Milikibunifu ikifuatiwa vizuri ndipo haswa ukubwa wa tatizo utakapojulikana. Kuna ulazima mkubwa wa kutaja Milikibunifu katika katiba na kuanisha ulazima wa kulinda kuendeleza na kwezesha wabunifu wan chi kwa manufaa ya kizazi hiki na vizazi vijavyo








Wednesday, March 6, 2013

KABEYA BADU HATUNAE TENA

MWANAMUZIKI WA SIKU NYINGI AMBAYE ALIKUWA ANAIMBA KATIKA BENDI YA WAZEE SUGU- KABEYA BADU -AMEFARIKI LEO ASUBUHI KATIKA HOSPITALI YA MUHIMBILI BAADA YAKUPATA MATATIZO YA FIGO KUSHINDWA KUFANYA KAZI. KABEYA ALIPITIA BENDI NYINGI IKIWEMO, ORCHESTRA FAUVETTE, ORCHESTRA SAFARI SOUND, MAQUIS, INTIMATE RHUMBA, TANCUT ALMASI, NA WAZEE SUGU
MSIBA UTAKUWA KWAKE TANDIKA MUNGU AMLAZE PEMA PEPONI

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...