YOUTUBE PLAYLIST

Saturday, June 3, 2017

TATIZO LA NIDHAMU KATIKA BENDI ZETU ZA MUZIKI....


Miezi chache zilizopita rafiki yangu mmoja alinambia ameamua kuunda bendi mpya kabisa, alikuwa na lengo la kuleta muziki mpya kabisa katika anga ya muziki Tanzania. Aliongea kwa furaha na ni wazi alikuwa ana nia ya kufanya kitu kikubwa, maana alikuwa amegharamia fedha nyingi kununua vifaa vipya kabisa vya kuanzisha bendi. Mwezi mmoja baada ya mazoezi kuanza alinitafuta na kunambia ameamua kuvunja bendi na vyombo anauza. Nilipomuuliza kwanini kabadili mawazo katika kipindi kifupi vile, hata onyesho moja halijafanyika? Akanijibu. ’Wanamuziki wamenishinda, wana matatizo makubwa ya ndhamu’. Kiukweli sikushangaa sana kwani jambo hili si geni kabisa kwenye tasnia ya muziki kwa siku hizi. Mfumo wa uendeshaji bendi siku hizi ni tofauti sana na miaka ya nyuma.

Nichukue mfano wa bendi Vijana jazz Band, bendi ambayo nilijiunga mwaka 1989. Kujiunga na bendi hii kulitokana na mwaliko niliyoupata kupitia kwa muimbaji rafiki yangu Marehemu Mohamed Shaweji. Shaweji tulikuwa wote Tancut Almasi Orchestra kisha yeye akaniacha kule na na kujiunga na Vijana Jazz Band, yeye na muimbaji mwingine Marehemu Gota gota wakiwa wamemfuata mpiga gitaa Shaaban ‘Wanted’ Yohana, aliyetoka Tancut pia na kuhamia Vijana Jazz Band miezi michache kabla. Hivyo siku moja nikiwa na bendi ya Tancut Almasi kwenye onyesho kwenye ukumbi wa CCM kata ya 14 Temeke, Shaweji alikuja na kunambia kuwa Hemed Maneti, kiongozi wa Vijana Jazz Band alikuwa anataka nijiunge na bendi yake. Nilikubali na mwezi Oktoba 1989 nilijiunga na Vijana Jazz. Kufikia mwezi wa Desemba mwaka huohuo nikawa nimepewa wadhifa wa kuwa Band Master, kazi za Band Master ni kuangalia nidhamu ya jumla ya wanamuziki, ikiwemo mahudhurio mazoezini na kazini, uchelewaji, ulevi, usafi binafsi wa mwanamuziki na pia kupanga ratiba ya nyimbo ambazo zinatakiwa kupigwa katika onyesho.  Kwa mfumo uliokuweko, Band Master aliweza kumsimamisha mwanamuziki yoyote aliyekiuka sheria za bendi, au kutoa adhabu ya kukatwa fedha kutoka kwenye mafao yake ya kila wiki ikiwa ni adhabu kwa makosa mbalimbali. Nguvu hizi zilifanya wanamuziki kuwa na nidhamu wakati wote wawapo kwenye shughuli za bendi. Ikumbukwe kuwa katika bendi kulikuweko na kiongozi mkuu Band Leader. Huyu alikuwa na mamlaka ya kufukuza mtu kazi na pia kuajiri na ndie anaepanga hata ukubwa wa mshahara, lakini alikuwa haingilii madaraka ya Stage Master. Kwa kawaida wanamuziki waliona ni heri matatizo yao yaishie kwa Band Master kwani yakifika kwa Band Leader yanakuwa ndio yamefika hatua ya mwisho isiyo na rufaa na inaweza kuwa hasara kubwa. Ili kuonyesha Band Master alivyokuwa na nafasi ya pekee, siku moja wakati niko Vijana jazz band, ilikuwa twende kwenye moja ya maonesho na kuna gari ilikuwa inatupitia wote majumbani kwetu, tulipofika nyumbani kwa Band Leader Hemed Maneti, alitoka nje akiwa na karatasi kutoka hospitali akaja kunitaarifu kama Band Master, kuwa hataweza kuja kazini kwani anaumwa, Maneti alikuwa Band Leader lakini alikuwa akiheshimu nafasi ya Band Master, tena nilikuwa bado mgeni katika bendi. Hii ilikuwa ni ishara wazi kwa wanamuziki wengine kuwa Band Master lazima aheshimiwe na wote.

Hali si hivi katika bendi nyingi siku hizi. Ngumu kujua nani mwenye madaraka gani kwani bendi zinakuwa na mwenye bendi, mkurugenzi wa bendi, meneja, maseneta, kiongozi wa bendi, wadau wa bendi. Wote hawa wana mamlaka zisizo na mipaka, wanaweza kuamua wimbo gani upigwe, wanaweza kuamua nani atimuliwe au nani aingizwe kwenye bendi, mmoja akimsimamisha mwanamuziki kwa utovu wa nidhamu mwingine anaweza akamrudisha, hakuna mtu mwenye amri ya mwisho kuhusu lolote lile, hivyo nidhamu imeshuka sana, na pasipo na nidhamu si rahisi kuweko na maendeleo yoyote yenye tija.

Sasa nizungumzie kosa la rafiki yangu aliyetaka kuanzisha bendi na ikamshinda, kwanza baada ya kununua vyombo, aliaanza kutafuta wanamuziki akisaidiana na watu wake wa karibu, kisha akamteua kiongozi wa bendi, ambae kimsingi kilikuwa kilemba cha ukoka kwani rafiki yangu ndie aliyekuwa na amri ya mwisho kuhusu lolote katika bendi. Na kwa kuwa hakuwa na muda wa kushinda kila mahala na bendi, kundi likawa halina kiongozi mwenye mamalaka  na mwisho kila mtu akawa anafanya lake, walevi wakalewa sana, wachelewaji wakendelea na uchelewaji wao, hakukuwa na mtu aliyekuwa na uwezo wa kutoa mwelekeo wa bendi kinidhamu wala kimuziki. Muziki wa bendi kwa ujumla umekumbwa na tatizo hili la kukosa uongozi, maamuzi mengi yanafanyika kwa vikao, hata maamuzi yale ambayo ni ya kitaaluma yanangoja makubaliano ya wengi, na kwa mtindo huu bendi zitachelewa sana kujikwamua kwenye tope ambalo zimenasa.  Ushauri kwa wanaotaka kufungua bendi, ni bora kumtafuta mwanamuziki mmoja ambaye unaamini anaweza kutengeneza muziki unaoutaka au unaodhani utakuletea biashara kisha umwachie aijege hiyo bendi na wanamuziki anaoona yeye wanafaa, hapa tayari utakuwa umejenga utawala unaoeleweka. Mwenye vyombo usiingilie moja kwa moja mambo ya bendi, wanamuziki wakishajua kuwa kiongozi wa bendi hana mamlaka kamili, nidhamu inavunjika.

No comments:

Post a Comment

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...