YOUTUBE PLAYLIST

Thursday, February 18, 2010

Wednesday, February 17, 2010

Wanamuziki wanawake



Muziki wa dansi uliweza kupambwa na wanawake wengi waliopata sana umaarufu kutokana na umahiri wao enzi hizo. Wanamuziki wa dansi wanawake walichelewa sana kukubalika kwa wanamuziki wanaume tofauti na ilivyokuwa kwenye muziki wa aina nyingine kama taarab, na kwaya. Lakini wengi walijitokeza na kuzoa umaaruf mkubwa labda niwataje wachache na baadhi ya nyimbo zilizowapa umaarufu. Nianze na mama lao Tabia Mwanjelwa, huyu dada wa kinyakyusa alikuwa na sauti nzito ya kukwaruza lakini akiimba mwili utakusisimka. Pamoja na kuwa alikuwa akipanda katika majukwaa ya bendi mbalimbali ni bendi ya Maquis ndiyo iliyofanya hatua ya ziada na kumruhusu arekodi jambo ambalo lilikuwa gumu kwa wanawake katika bendi kabla ya hapo, wimbo uliompa umaaruf sana ni Jane..Jane mi nahangaika juu yako kwa maisha yako..... Pichani Tabia Mwanjelwa akiwa na gitaa, unaweza kupata mengineyo na kuwasiliana nae kupitia
Rahma Shally mwimbaji mwingine mahiri aliyepitia bendi nyingi na kurekodi kwanza na Mwenge Jazz nyimbo nyingi tu maarufu, akapitia MK Group Ngulupa tupa tupa akasikika katika kibao kile Jua asubuhi lapendeza, Sambulumaa akarekodi Sitaki sitaki visa vyako, akatua Vijana Jazz na kurekodi wimbo Sadi Badili mawazo. Alikuwa mwanamama shupavu jukwaani. Nana Njige binti mzuri aliyepitia Orchestra Mambo Bado ambapo alitamba na ule wimbo Lilikuwa jambo dogo tu, akapitia bendi kadhaa ikiwemo Vijana jazz , Tancut Almasi, Legho Stars. Bibie Emma Mkello ambaye hukumbukwa katika ule wimbo alioimba akiwa na Eddy Sheggy wakiwa Super Rainbow..Milima ya kwetu. Kida Waziri akionekana hapa katika picha aliopiga 1991 kwenye ukumbi wa Vijana Kinondoni, kwa sasa yuko Arusha atakumbukwa kwa nyimbo kama Shingo Feni,Penzi Haligawanyiki na Wifi Zangu ambazo zote alirekodi akiwa Vijana Jazz. Pia alipitia kundi la Roots and Culture lililoongozwa na Jah Kimbuteh.
Wapenzi wa Maquis watamkumbuka Rose Mwape ambae nae aliimbia Maquis kwa muda mrefu baada ya kuondoka Tabia Mwanjelwa.Jemsina Msuya pia alikuwa kati ya magwiji alikuwa Legho na akarekodi na Assossa nyimbo ya Mzazi mwenzangu. Wako wengine kama Karola Kinasha ambao bado wako katika muziki. Karola yuko Shada, Ana Mwaole yuko na Mzee King Kiki, Nuru Mhina baada ya kuondoka Police Jazz ametua Vijana Jazz mpaka leo. Nyota Waziri ambaye baada ya kuondoka Bicco Stars ametua Kilimanjaro Band akiwa bado na heshima yake katika wimbo Tupendane na Gere. Ni muhimu kumgusia Asia Darwesh ambay licha ya kuimba alikuwa pia mpiga Keyboards mahiri sana kama alivyoonyesha katika nyimbo alizorekodi MK Group na bendi yake Zanzibar Sounds. Nakaribisha kumbukumbu nyingine

Vijana Jazz Vs Maquis

Katika kipindi cha mwisho cha miaka ya 80, Kinondoni ilkuwa inawaka moto kwa Vijana siku ya Jumapili. Lang'ata ambayo baadae ilikuja kuwa Club ASET na sasa kanisa, palikuwa ndo ukumbi wa Dansi za kuanzia mchana kwa Bendi ya Maquis. Ukija hapa mbele Vijana Jazz Pambamoto awamu ya pili chini ya uongozi wa Hemed Maneti walikuwa nao kila Jumapili mchana wanaporomosha Dansi, na siku hiyo ilipewa jina Vijana Day. Kwa kweli Maquis walikuwa wanajaa watu na Vijana wanajaa watu. Kulikuweko na wapenzi wa kudumu wa Vijana kama ilivyokuwa Maquis. Wakati huo nyimbo kama Ngalula, Makumbele zilikuwa zinalia Lang'ata huku Vijana wanateremsha Shingo feni, Ngapulila, Azda. Ushindani huu ulilazimisha bendi kujitahidi kupiga vizuri na kwa displine au la wapenzi wanahamia bendi jirani. Kuna wakati Vijana Jazz walikuwa wanaanza muziki saa kumi na moja jioni na kupumzika saa tatu na nusu usiku kisha kumaliza dansi saa nne. Maquis wakawa wanaanza saa kumi na kumaliza saa tano usiku. Na wakaanza kuruhusu mtu yeyote atakayekuwa kapigwa muhuri wa kuruhusu kutoka nje ya ukumbi Vijana Jazz,aliruhusiwa kuingia Maquis bure. Vijana wakabadili ratiba na kuanza kupiga saa 9 mchana, kwa mtindo wa bandika bandua, yaani muziki nonstop. Na kufuta kupumzika hadi saa tano. Hiyo ndo ilikuwa raha kwa wapenzi. Vijana haikuwa na show wakati wa Maneti, Lakini show ilikuja baadae katika kukabili show ya Maquis ambayo ilikuwq nzuri sana chini ya mwalimu wao Wabangoi. Majina makubwa yalitawala madansi hayo Maquis kulikuwa na Dekula Vumbi kwenye solo,second solo Mbwana Cox (aliyetoka Vijana Jazz), banza Mchafu Bass, Nguza Viking, Adios, Tshimanga Assossa,Parashi Lukumbule Vijana Jazz kulikwa Shaaban Wanted, Hemed Maneti, Eddy Sheggy, Adam Bakari, Kida Waziri, Abou Semhando, Rashid Pembe na wengine wengi, basi raha kila jumapili ilikuwa kama tamasha

Kati ya Bendi ambazo Mzee J Mwendapole aliziendesha kwa muda mrefu ni Afriso ngoma. Hiyo ilikuwa bendi yake, ikawa na wanamuziki kama Maida na Belly Kankonde, iliweza kurekodi nyimbo kadhaa, lakini bendi hii iliongezeka umaarufu alipoingia marehemu Lovy Longomba, wakati huo akiwa na akina Kinguti system, Anania Ngoliga, Toffy Mvambe, Salim Shaaban Malik Nduka Masengo(Maliky Star) hao wakiwa waimbaji, Solo Gitaa- John Maida, Peter Kazadi, Robert Tumaini Mabrish, Rythm- Mjusi Shemboza, Bass-George na Kasongo, Drum -Ayub Karume, Abdul, Tumba- Magoma Sony, Trumpet-Juma Urungu, Ramadhani, Mbaraka Othman. wengi kati niliowataja wametangulia mbele ya haki. Baada ya hapo aliwahi pia kuwa na bendi ambayo ilikuwa na wanamuziki kadhaa kutoka sikinde ikawa inaitwa Sikinde Academia, ambayo haikudumu sana. Baada ya hapo amekuwa msaada mkubwa wa kuwasaidia wanamuziki wengi vyombo wakati wananzisha bendi zao.
Pichani ni Marehemu Lovy Longomba

Tuesday, February 16, 2010

Kwa heri Juma Mwendapole

Kwa masikitiko makubwa nimepata taarifa ya kifo cha mdau muhimu wa muziki wa dansi Juma Mwendapole. Amefariki Ijumaa tarehe 12 February 2010 na kuzikwa kesho yake. Mwendapole ndiye aliyekuwa mmiliki wa Bendi ya Afriso Ngoma iliyokuwa na wanamuziki maarufu kama Lovy Longomba. Kwa miaka ya karibuni wanamuziki wengi wamekuwa wakimtegemea kwa kukodi vyombo vya muziki toka kwake. Bendi nyingi zisingekuweko kama si msaada wa Juma Mwendapole.
Mungu Amlaze pema peponi Amin

Saturday, February 13, 2010

Historia za mfumo wa Bendi

Utaratibu wa bendi hapa nchini ulifuata sana utaratibu wa bendi za nje kutokana na muziki wa bendi kuwa ni wa mapokeo. Hapa naongelea aina ya vyombo vilivyotumika stejini. Katika rekodi za kwanza zaidi za bendi kama vile zile za Cuban Marimba bendi zilipiga bila chombo chochote kilichotumia umeme kwa kuiga staili ya Cuba, na pia teknolojiaa ya vifaa vya umeme ilikuwa bado kuingia. Hivyo kulikuwa na gitaa moja na ngoma za kizungu (drums), bongoz, na vyombo vya kupuliza, filimbi, trumpet, saxaphone. Nyimbo za zamani za Salum Abdallah na Dar es Salaam Jazz Band zinatoa picha za vyombo hivyo. Mwanzoni mwa miaka ya 60, vifaa vya umeme vilianza kutumika na bendi kwa kawaida zilikuwa na Gitaa la bezi, rithim na solo,tarumbeta na saksafon. Halafu kulikuwa na bongoz. Baadae tumba zilichukua nafasi ya bongoz. Baadae bendi ziliingiza gitaa jingine ambalo liliitwa second solo. Hili lilikuwa gitaa ambalo lilipigwa katikati ya rithm na solo. Cuban Marimba katika kipindi fulani cha Mzee Kilaza aliweza kuongeza gitaa jingine waliloliita chord gitaa.
Kuingia kwa vinanda kuliliondoa gitaa la second solo katika bendi, japo kwenye bendi kama Tancut almasi na Vijana Jazz gitaa hilo liliendelea sambamba na kinanda. Kinanda pia kikachukua nafasi ya tarumbeta na saxaphone katika bendi nyingi. Kwa bendi zile ambazo zilikuwa zikifuata muziki wa magharibi mpangilio wao haukuwa na mfumo maalumu kutokana nani aina gani ya muziki wanafuatia. Mpaka sasa bendi kama The Kilimanjaro kwa kawaida hupiga gitaa moja,vinanda vitatu, gitaa la bezi, drums na conga au maarufu tumba. Wakati bendi kama Shada ni wana kinanda magitaa mawili na ngoma ya kiasili. Tatizo kubwa sana sasa ni bendi zinaigana katika mfumo katika kila kitu ubunifu ziro. Franko Makiadi aliondoka kwenye mfumo wa second solo akawa na solo gitaa 2, yeye mwenyewe akipiga solo na akawa na mpiga solo mwingine katika wimbo uleule. Ni wakati sasa wanamuziki kuangalia nyuma na kuona ni nini wanaweza kujifunza kitakachofanya muziki wao uwe tofauti na wa wengine.

Friday, February 12, 2010


Mwaka 1982/83 Tchimanga Kalala Assossa alianzisha na kuongoza bendi iliyoweza kutia changa moto katika ulimwengu wa muziki wakati huo. Bendi hiyo iliitwa Orchestra Mambo Bado na mtindo wake wa Bomoa Tutajenga Kesho. Wanamuziki katika bendi hiyo walikuwa Tchimanga Assossa, Kiongozi na muimbaji, Kazembe wa Kazembe mpiga solo (pamoja na jina hilo alikuwa Msukuma), William Maselenge, rythm guitar, Huluka Uvuruge second solo guitar, Sadi Mnala drums, Mzee Albert Milonge second solo, Lucas Faustin muimbaji, John Kitime muimbaji na rythm guitar, George Mzee muimbaji, Athuman Cholilo muimbaji, Likisi Matola Bass na keyboards, Jenipher Ndesile muimbaji, selemani Nyanga Drums. Album ya kwanza ya bendi hii ilikuwa na nyimbo zilizotamba kama vile Kutokuelewana, Bomoa Tutajenga Kesho , hii ilipigwa marufuku. Picha ya Assossa iliyotoka kwenye tangazo la kwanza la bendi, hapa akiwa amevaa shati la ndege ambalo kwa siku hizo walikuwa wanavaa wajanja tu.

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...