YOUTUBE PLAYLIST

Sunday, May 9, 2010

Abdalla Gama


Kwa wapenzi wa DDC Mlimani Park, jina la Abdallah Gama ni jina muhimu katika historia ya bendi hiyo. Mwanamuziki huyu mpigaji wa gitaa la rythm alipata umaarufu zaidi baada ya wimbo wa uliotungwa na Assossa -Gama, ambao mpaka leo bado unafurahisha sana. Gama na wenzie kama Joseph Mulenga, Abel Balthazar, Cosmas Chidumule chini ya King Michael Enoch waliweza kutunga na kutengeza nyimbo ambazo bado zinaleta burudani miaka thelathini baada ya kutungwa. Abdallah Gama tena atakumbukwa kwa kazi zake alipokuwa BimaLee wakiwa na watunzi kama Jerry Nashon, Shaaban Dede, solo la Mulenga , nba besi la Mwanyiro, hapo ilikuwa utamu kolea. Pichani Gama(mbele)akiwa na mpiga gitaa mwingine Huruka Uvuruge ambae sasa yuko Msondo, na mpiga drum Matei Joseph ambae kwa sasa anendesha bendi yake African Minofu

Friday, May 7, 2010

Wanamuziki ndugu 3


Kitendawili kingine. Picha hii ilipigwa Seaview 1974, kuna wanamuziki wa Afro70, na wanamuziki ndugu ambao nao wametoa mchango mkubwa katika fani ya muziki, unawatambua ni akina nani hapo?

Tuesday, May 4, 2010

Wanamuziki ndugu


Katika kila nyakati kunatokea ndugu ambao ni wanamuziki. Pengine hii inatokea kwa kuwa mtu anakulia katika mazingira ya nduguze kupiga muziki hivyo inakuwa rahisi kwake kuwa mwanamuziki, na nduguze wakiwa wanamuziki inamrahisishia njia, lakini hilo si jibu sahihi kwa kweli kuna mengi zaidi ya hilo. Katika picha hii ni wanamuziki ambao ukoo wao wako wanamuziki wengi na hii imekuwa inaendelea kwa vizazi vitatu sasa jina la ukoo huu kila mara likiwemo katika historia ya muziki. Ni akina nani hawa?

Monday, May 3, 2010

Mitindo ya Bendi

Nikisema tuanze kutaja mitindo ya bendi ni mingi sana maana kila bendi imekuwa inakuja na mtindo wake. Majina mengine ya mitindo yana historia na maana na mengine yana kuwa yakutunga na kwa kweli hata waliokuwa wanayatumia hawana maelezo ya maana ya maneno hayo. Mundo,Msondo, sokomoko, dondola, kiweke, segere matata,super mnyanyuo, vangavanga, chikwalachikwala, libeneke na kadhalika ilikuwa mitindo ya bendi mbalimbali, na muziki wa bendi ulikuwa ndiyo unaonyesha utofauti huo. Kwa mfano katika mji wa Tanga ulikuwa na bendi kubwa mbili, Jamuhuri Jazz na Atomic Jazz. Jamhuri ilikuwa na mtindo wa Toyota, na baadae Dondola, hata muziki katika awamu hizi mbili katika bendi hiyohiyo ulikuwa tofauti. Atomic walikuwa na mtindo wa Kiweke. Muziki wao ulikuwa tofauti na ule wa Jamhuri. Na wapenzi wa Jamhuri hata wakizeeka husifu mtindo wa upigaji wa Jamhuri na rythm la Harrison Siwale(Satchmo). Kadhalika wapenzi wa Atomic watakwambia hakuna kama Kiweke, upigaji solo wa John Kijiko, bass la Mwanyiro na kadhalika. Mtu ambae kisha sikia muziki katika mtindo wa Ambianse wa Cuban Marimba, hawezi kuchanganya na Likembe wa Moro Jazz. Nimeanza kwanza kwa kutaja bendi zilizokuwa katika mji mmoja tena huko mikoani ambapo watu walikuwa wachache na wanamuziki wanajuana na kuishi jirani. Hali hiyo ndio iliyokuwa Tabora, ambako pamoja na Tabora Jazz, kulikuweko na Nyanyembe Jazz, Kiko Kids, muziki wa kila bendi ulikuwa tofauti na mwingine. Dar es salaam kulikuwa na bendi nyingi na hivyo mitindo mingi. Hakuna aliyeweza kuchanganya Maquis na OSS, wala Sikinde na msondo, Sokomoko, afrosa, Katakata vumbi nyuma ya Kyauri voice havikuwa na mpka wa kulinganishwa. Kikubwa ninachotaka kueleza ni kuwa bendi kuwa na mtindo ilikuwa si jina tu bali kulikuweko na kazi ilifanyika ili kupata kulinda na kuendeleza mtindo ambao bendi iliamua kuwa nao. Nakumbuka wakati wa mazoezi enzi hizo unaweza ukatunga wimbo ukianza kuimba wenzio watakwambia mbona unafanana na bendi fulani na hapo utakarabatiwa mpaka uwe katika mtindo wa bendi husika.

Wednesday, April 28, 2010

DJ wa kwanza

Katika kuzungumza na watu kupata mambo kwa ajili ya blog hii, nimepata hili ambalo naomba maoni. Kijana wa zamani mmoja kaniambia DJ wa kwanza anaemkumbuka alikuwa akikaa maeneo ya Keko Cocacola, alikuwa Mkongo fulani ambae jina kamsahau. Je, kuna mwenye kumbukumbu kuhusu hilo?

The Dynamites

Kikundi kingine toka enzi za miaka ya 69/70 hawa waliitwa The Dynamites. Hapa kwa kweli namtambua Salim Willis tu ambaye baadae alikuja kuwa mpiga second solo wa Afro70.

Midomo ya Bata

Upigaji wa vyombo vya kupuliza umepungua sana katika bendi zetu hapa Tanzania. Kumekuwa na maelezo kuwa tatizo hili limetokana na kuanza kutumika kwa Keyboards au vinanda aina ya synthesizer. Vinanda hivi vina uwezo wa kutoa milio mbalimbali ikiwemo ya vyombo vya kupuliza kama trumpet na saxophone. Lakini mi nadhani ni maendeleo ya mtiririko wa uigaji wa nini kinachotokea Kongo. Ni jambo lisilopingika kuwa kwa miaka mingi sana bendi nyingi zimekuwa zikiiga kile kinachotokea Kongo. Mara nyingine hata kufikia kuiga nyimbo nzima kutoka kwa bendi za Kongo. Na mara nyingine kuiga mfumo wa muziki kutoka huko. Kwa misingi hiyo, bendi zetu nyingi ziliamua kuacha kupiga vyombo vya kupuliza mara baada ya kuona bendi nyingi za Kongo zikiacha kutumia vyombo hivyo.
Lakini kwa ukweli kabisa vyombo vya upulizaji vina raha yake na utamu wake. Wapigaji wake hutengeneza step zao za kucheza na hupanga sauti za kupishana kati ya trumpet na saxaphone na huongeza raha sana katika muziki. Kwa sasa ni bendi chache kama vile DDC Mlimani Park, OTTU, Vijana Jazz, MAK Band, African Beat ndio wanaendeleza upigaji wa vyombo vya kupuliza.

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...