YOUTUBE PLAYLIST

Sunday, August 1, 2010

Harison Siwale-Satchmo


Kwa mara ya kwanza niliwaona 'Live', Jamhuri Jazz Band wakipiga katika ukumbi wa Community Centre Iringa, ukumbi maarufu kwa wenyeji wakati huo kwa jina la Olofea senta (Welfare Centre). Ni vigumu kuelezea jinsi nilivyokuwa najisikia kwani nilikuwa sidhani kama kutakuja kuweko na wanamuziki wanapiga vizuri namna ile. Lakini katika wote mpiga rythm guitar Harison Siwale, aliyejulikana kwa jina la Satchmo, alikuwa na anabakia kuwa mpiga gitaa aliyenifurahisha kuliko wote. Kwanza alikuwa na staili ya peke yake, na mpaka leo nikisikiliza nyimbo zake kama vile Blandina, Mganga no 1, Maria bembeleza mwana au Ewe ndege, nabaki kusifia kuwa huyu bwana alikuwa na kipaji cha pekee. Kuna rafiki yangu aliwahi kumuuliza wakati ule huwa anapataje mawazo ya kupiga gitaa lake kwa staili ile? alijibu kuwa huwa anajaribu kupiga sauti za viumbe mbalimbali wa porini katika gitaa lake.
Wanamuziki waliokuwa katika bendi ya Mkwawa High School, watakumbuka jinsi walivyoweza kupata nafasi ya kupiga pamoja na bendi hii kila ilipokuja Iringa mjini, maana hizo ndiyo zilikuwa taratibu wakati huo. Bendi ikifika katika mji, kama mji ule una bendi basi nao watapata nafasi ya kushirikiana na wageni. Wakati huo Mkwawa ilikuwa na wanamuziki kama vile Sewando, Manji, Mpumilwa,Kakobe waliweza pia kubadili hata muziki wao kutokana na kupiga na bendi hizi zilizokuwa kubwa wakati huo. (Pichani toka kushoto- Harison Siwale, Mbaraka Mwinyshehe na Abdul Mketema)

Kuzaliwa kwa Bana OK


Baada ya kifo cha Franco, Lutumba Simaro ndie alie liongoza kundi zima la TPOK Jazz kwa miaka minne. Ilionekana kuwa ili warithi wa Franco waendelee kufaidi matunda ya kundi hilo, wazo lilitolewa kuwa Simaro abakie na wanamuziki wote na familia iendeshe utawala mwingine wote, na warithi wawe wanapata asilimia 40 ya mapato yote, ambapo dada yake Franco ambaye ndiye alikuwa kiongozi wa familia angeyasimamia shughuli hizo. Dada wa Franco, baada ya kushauriana na nduguze aliamua kuwa familia ipewe asilimia 30,na isijihusishe kabisa na mambo ya bendi. Baada ya makubaliano haya bendi ilianza kazi na safari yake ya nje ya kwanza ilikuwa Tanzania na Kenya. Hali ilikuwa ngumu baada ya kifo cha Franco, lakini mambo polepole yalianza kuwa mazuri. Ghafla magazeti yakaanza kuwa na barua za wasomaji zikimlaani Simaro kuwa anaendesha bendi kama mali yake peke yake na kutokutoa msaada wa maana kwa watoto wa Franco. Hatimae akaandikiwa barua rasmi kuwa arudishe vyombo vyote vya muziki nyumbani kwa Franco.Hiyo ilikuwa mwishoni mwa mwaka 1993. Wakati huo huo mwanasheria wa familia ya Luambo alienda kwenye TV na kutangaza kuwa Simaro si kiongozi tena wa bendi.

Ilikuwa ni pigo kwa Simaro ambaye alijiunga na OK Jazz tangu 1961, na kupitia kwake wanamuziki kama Femi Joss, Kwammy, Isaac Musekiwa, Defao, Albino Colombo waliweza kuwika katika OK Jazz, na wote walikuwa wameondoka akabaki mwenyewe na sasa alikuwa akifukuzwa kupitia TV.

Katika onyesho lake la mwisho aliwaomba watu wa TV ya RTNC kuhudhuria,na kwa kutumia nafasi hiyo nae akatangaza kuwa yeye si mwanamuziki wa TP OK Jazz tena, ilikuwa ni tangazo la kusikitisha lililoleta simanzi kwa wengi. Na ndio ukawa mwanzo wa Bana OK, wanamuziki walikutana walikutana katika ukumbi wa Bar ya Zenith na kuamua kuanzisha bendi chini ya Rais wa Lutumba Simaro. Ilikuwa tarehe 4 January 1994. (Habari na picha kutoka www.afropop.org kwa ruksa ya Banning Eyre)

Upinzani...........

Leo hii kuna neno maarufu limetokana kwa wasanii wa Kimarikani-BIF. Si kwamba ni utamaduni mgeni, ila utekelezaji wake ndo umekuwa tofauti siku hizi, na kwetu hapa kumekuweko na utamaduni wa ushindani ambao kwa kuchochewa mara nyingine na vyombo vya habari ukageuka upinzani. Katika kipindi fulani cha miaka ya sitini muziki wa jiji la Dar katika nyanja ya Band za rumba ulitawaliwa na bendi mbili, Dar es Salaam Jazz- Majini wa Bahari na mtindo wao wa Mundo, na upande wa pili Kilwa Jazz. Ulikuwa mpambano mkali uliofikia hata wapenzi wa bendi hizi mbili kutandikana makonde. Bendi zilitungiana nyimbo za mafumbo moja maarufu ulikuwa ule wimbo wa Dar Es Salaam Jazz Mali ya mwenzio siyo mali yako, ukiwadhihaki kilwa Jazz kutokana na eneo la Klabu yao kuwa na utata wa kodi. Morogoro kulikuwa na miamba wawili, Morogoro Jazz na Cuban Marimba, ushindani wao uliweza kuwasha moto wa upenzi Afrika ya Mashariki nzima, watu walikuwa wanajitahidi kuwepo Morogoro siku za wikiendi, Morogoro Jazz wakiwa na mtindo wao wa Sululu, Cuban Marimba na mtindo wa Ambianse. Nao pia walitunga nyimbo zenye vijembe nyingi zilizowatia kiwewe wapenzi wao, Cuban walikuja na mtindo wao Subisubi, wakijisifu kuwa wao ni Jini Subiani linanyonya. Tanga kulikuwepo na vijana wa Barabara ya 4 Atomic Jazz wana Kiweke , wakipambana na Jamhuri Jazz Band na mitindo yao mingi kama vile Dondola na Toyota. Ushindani huu uliendelea katika bendi mbalimbali, kama vile Juwata na Sikinde. Kuna ushindani mwingine ulikuwa zaidi wa kufikirika kama ilivyokuwa inadhaniwa na wengi kati ya Vijana Jazz na Washirika Stars, kiasi cha kwamba kuna wakati ule wimbo wa Nimekusamehe lakini sintokusahau ulitafsiriwa kuwa ulikuwa umetungwa na Hamza Kalala kwa ajili ya kumtaarifu Hemed Maneti, japokuwa si Maneti wala Hamza ambae niliongea nae kuhusu wimbo huo karibuni aliyesema kuwa aliutunga kwa ajili hiyo. Kwa wapenzi wa muziki enzi za uhai wa Maquis Du Zaire, na Orchestra Safari Sound wanakumbuka ushindani mkubwa ulio kuwepo kati ya hizi bendi mbili ambazo kuna wakati huo zote zilikuwa zikiwa na makao makuu jirani, Maquis wakiwa Ubungo na OSS Kimara. Maquis walipoasisi mtindo wao wa Ogelea piga mbizi, OSS wakaja na Chunusi, wakiwa na maana ukiogelea kiboko yako Chunusi. Katika mtiririko wote huu wa ushindani mara chache sana ulifikia wanamuziki binafsi wakashikana mashati kwa sababu za ushindani. Na ushindani ulikuwa wa maana kwa kuwa kweli bendi zilipiga muziki tofauti, Jamhuri na Atomic zote za Tanga lakini kila moja ilikuwa na muziki tofauti, na vivyo hivyo Moro Jazz na Cubano, au Tabora Jazz na Nyanyembe Jazz. Kila Jumanne asubuhi, Radio Tanzania ilikuwa na kipindi kilichorusha nyimbo zilizorekodiwa katika studio yake, Misakato. Ilikuwa si ajabu kukuta wanamuziki wa bendi yenye ushindani ukisikiliza nyimbo mpya za washindani wao. Na hata kutoa sifa pale ambapo zinastahili, na kutokea hapo watu wanajipanga kutengeza kazi bora kuliko hiyo. Nakumbuka Tancut Almasi ilikuwa Morogoro wakati Vijana Jazz wakirushwa nyimbo zao za Ngapulila, Adza kwa mara ya kwanza katika kipindi cha misakato, ilikuwa uhimu kusikiliza kazi yao kwani wakati huo Shaaban Wanted ndio alikuwa kahama Tancut na kujiunga na Vijana, na mfumo wa vyombo wa Vijana ulikuwa sawa na Tancut na Washirika pia yaani Solo gitaa, Rythm Gitaa, Second solo, Keyboards, bass, na vyombo vya upulizaji. Hii haikuleta upinzani bali iliongeza ushindani, hapo tulikaa chini na hata kurekibisha baadhi ya nyimbo tulizoziona ziko chini ya kiwango cha vijana, matokeo yake ndio ile album, yenye nyimbo kama Helena Mtoto wa Arusha, Masikitiko na kadhalika

Saturday, July 31, 2010

Mbaraka Mwinyshehe Mwaluka 1



Ukikaa na kusikiliza muziki wa Mbaraka kwa makini unajifunza mengi sana, kwa mashahiri ya nyimbo hizo unapata picha ya maisha yalikuwaje enzi hizo. Furaha, machungu, vicheko, vilio na kadhalika. Upigaji wake wa gitaa, ni somo zuri sana kwa mpigaji anaetaka kujiendeleza katika upigaji wa solo. Katika vipindi vyake vya kuanzia Morogoro Jazz hadi Super Volcano alipitia staili nyingi za muziki, baadhi kama Sululu, Likembe, Masika Zolezole na kadhalika. Tofauti na bendi nyingi ambazo hubadili majina ya mitindo bila kubadili muziki wenyewe, staili za Mbaraka zilionyesha mabadiliko. Nyimbo katika staili ya Likembe zilikuwa tofauti na zile za Masika Zolezole. Kipindi hicho wapenzi wa muziki waliweza kuondoka Dar es Salaam na kwenda Morogoro kufaidi wiki endi ya muziki aidha wa Cuban Marimba, au Morogoro Jazz. Picha ya juu Mbaraka Mwinyshehe, ya chini toka kushoto Sulpis Bonzo, Mlinzi Mustafa(huyu baadae alipigia Urafiki Jazz), Shaaban Nyamwela, Abdul Mketema (mwenye Saxaphone),Samson Gumbo,Mbaraka Mwinyshehe.Hapa wakiwa Morogoro Jazz Band

Friday, July 30, 2010

Mwanamuziki Mheshimiwa Paul Kimiti


Kwa muda mrefu nilikuwa na nia ya kuweka taarifa kuhusu wimbo wa kumsifu Nyerere ambao uliimbwa na Mheshmiwa Paul Kimiti. Nilijitahidi kutaka kupata taarifa kutoka kwake ikawa haikuwezekana lakini karibuni nilisoma maelezo ya Mheshmiwa mwenyewe kuhusu kazi hiyo, ambayo alisema walifanya akiwa Mwenyekiti wa wanafunzi kutoka Tanganyika katika chuo kikuu cha Netherlands kati ya mwaka 1962 na 1965. Akiwa na wanamuziki wenzake wakiwa na kundi waliloliita Safari Brothers walirekodi nyimbo hii nzuri sana kuhusu Mwalimu Nyerere. Mheshimiwa alisema walitoa dola 20,000 walizozipata kutoka Philips records kwa Mwalimu alipotembelea Netherlands April 1965, pesa hizo walitoa ili kuchangia maendeleo ya nchi yetu, na huo ndio ulikuwa mwanzao wa uhusiano wake na Mwalimu.

Wednesday, July 28, 2010

Kida Waziri arudi ulingoni

Kida waziri miaka ya 90.

Kida Waziri au kama alivyokuwa akiitwa enzi zake Vijana Jazz Stone Lady amerudi na album yake yenye nyimbo 6 ikiwa na nyimbo kama Wifi zangu, Shingo Feni, Penzi haligawanyiki na nyinginezo, pia ameimba wimbo wa Mary Maria akishirikiana na mwanae Waziri, ambae kajitahidi kuimba zile sehemu za uimbaji wa marehemu babake.

Kida Waziri alivyo sasa.

Sunday, July 18, 2010

Drums

Ukisema drums katika anga za muziki utakuwa umeeleweka kuwa unaongelea zile ngoma za kizungu ambazo hupigwa kwa kutumia miguu na mikono. Uwingi wa drums huanzia ngoma kubwa moja na ndogo moja (snare), na tasa moja (Hi hat), na kuendelea kwa uwingi kadri ya utajiri na uwezo wa mpiga drum. Katika nyimbo za Dar es Salaam Jazz ambazo zilirekodiwa kwenye miaka ya 30, drums zilitumika hivyo si chombo kigeni katika muziki wa Tanzania. Katika miaka ya sitin chombo hiki kilitoweka katika bendi nyingi za muziki wa rumba, lakini kikarudi tena kwa nguvu baada ya kuingia kwa staili ya kavacha kutoka Kongo. Bendi ambazo zilikuwa zikipiga muziki wenye mahadhi ya kimagharibi ziliendelea na drums katika kipindi chote na kuweza kuunganisha na tungo za zao za rumba kwa ufanisi mkubwa kama ilivyotokea kwa bendi kama Afro70. Drum huwa chombo kinacholinda spidi ya wimbo, na staili ya wimbo, kama ni chacha, tango, waltz au ngoma ya Kimakonde au Kipogoro. Drums huweza kuleta utamu sana kama zikimpata mpigaji.
Siku hizi kuna drums za umeme, hizi huwa na uwezo wa kuongeza au kupunguza sauti, na kuzibadili zikalia milio mbalimbali, kwa mfano kulia kama ngoma za kihindi au kulia kama tumba au hata nyingine zinaweza zikipigwa zikawa zinatoa milio ya ndege!!!.Bendi ya kwanza kuwa na electronic drums ilikuwa Chezimba, wakati huo drums zikipigwa na Charles Mhuto, Tanzanite nao wakanunua zao, na kwa upande wa bendi za rumba MK Group, ikifuatiwa na Vijana Jazz na Bima Lee walikuwa wa mwanzo kuwa na drums hizi

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...