YOUTUBE PLAYLIST

Friday, February 26, 2010

Vumbi





Kwa wapenzi wa Maquis Original jina la "Vumbi" ni la kutia kumbukumbu nyingi sana, na kwa wale ambao wamekuwa wakiusikia ule wimbo wa Chatanda Ngalula walisikia tena na tena Tchimanga Assossa akilitaja jina hilo wakati Vumbi anacharaza gitaa tamu la solo kwenye wimbo huo. Vumbi kwa sasa anaendelea na muziki huko Sweden na maelezo ya maisha yake kimuziki ni haya. Jina lake kamili ni Alain Kahanga Dekula , alizaliwa katika jimbo la Kivu katika Jamhuri ya Kongo. Baada ya kumaliza High School alianza kupiga gitaa katika bendi ya Bavy National iliyokuweko Uvira Kusini mwa Kivu. Baadae akiwa na kaka yake Rachid King wakajiunga katika bendi ya Grand's Mike Jazz Band wakati huo ikiwa na wanamuziki kama Remmy Ongala,Kasaloo Kyanga,na Kawele Mutimanwa. Akaja Tanzania na kujiunga na Orch.Maquis Original na kati ya nyimbo ambazo anajulikana nazo sana ni Ngalula and Makumbele.Wakiwa na mtindo wa Zembwela-Sendema,alikuwa jukwaa moja na miamba wa magitaa wakati huo akina Nguza Viking "Big Sound" na marehemu Ilunga Lubaba. Vumbi kwa sasa yuko Sweden akiwa na yule mwanamuziki maarufu toka Uganda Sammy Kasule wakiwa na bendi ya Ba makonde wamekwisha toa album CD mbili- Bamakonde na Asante. Akiwa na bendi ya kaka yake Rachid King Orch Grand’s Mike wametoa album ya CD Bolingo Ekeseni


Monday, February 22, 2010

Historia fupi ya muziki wa dansi

Ukitaka kuongea muziki wa dansi uliingiaje nchini ni muhimu kujua historia ya mji wa Tanga. Tanga ndipo muziki wa dansi ulipoingilia nchini. Wajerumani waliusambaratisha mji wa Tanga kwa mizinga kati mwaka 1888 na 89. Na baada ya hapo kuujenga upya kwa kufuata mpangilio uliosababisha Tanga kuwa na mitaa maarufu kama barabara ya kwanza ya pili na kuendelea. Wajerumani walianzisha shule ya kwanza ya serikali Tanga 1892 na hapohapo wakanzisha bendi ya shule ya kwanza, pamoja na kuwa Wajerumani hawakutawala muda mrefu baada ya hapo lakini Waingereza waliiendeleza sana bendi hiyo iliyokuwa ikipiga aina mbalimbali za muziki wa kigeni. Dansi ilianza kwanza kama klabu ambapo watu walialikana kuja kucheza aina mbalimbali za muziki wa kizungu mtindo maarufu unaojulikana kama ballroom dancing. Aina hizi za klabu zilianzia Mombasa na kuingia nchini kupitia Tanga na kisha kuletwa Dar Es Salaam na klab iliyokuwa maarufu Tanga iliyoitwa Tanga Young Comrades Club, klabu nyingine ilianzishwa ikaitwa New Generation Club ambayo ilianzisha matawi miji mbalimbali. Klabu hizi ndizo zilizozaa bendi za dansi. Inaonekana Dar Es Salaam ndio ilikuwa ya kwanza kuwa na bendi yake African Association Jazz Band, ambapo wanamuziki wengine waliihama na kuanzisha Dar Es Salaam Jazz Band, hiki kilikuwa kipindi kati ya miaka 1930 na 1940, kwenye 1950 kulikuwa na bendi maarufu Bagamoyo iliyoitwa Lucky Star jazz band ambayo ilikuwa na urafiki na Dar Jazz. Baada ya hapo kulianza bendi ambazo wanamuziki na wanachama wake walipatikana kutokana na wanakotoka, kulikuweko na Ulanga Jazz band ya Wapogolo, Rufiji Jazz Band iliyoanzishwa na Wandengeleko, Western Jazz iliyoanzishwa kwanza na Wanyamwezi. Bendi zote hizi baadae zilikuja kuwa na wanachama mchanganyiko bila kujali uzawa. Na kulikuweko na Skokian Jazz Band hii ilikuwa ni bendi na klabu ya watu mchanganyiko. Mwaka 1958 wanamuziki kutoka Kilwa walianzisha Kilwa Jazz Band wanamuziki hawa walitoka bendi iliyoitwa Tanganyika Jazz. Ilipofika 1966 bendi ilikuwa na wanamuziki takribani 26, 15 wakiwa Kilwa A na 11 Kilwa B. Zamani bendi zilikuwa na mtindo wa kuwa na bendi B ambayo ni ya Vijana. Patrick Balisdya aliwahi kuwa Dar Jazz B. Kilwa Jazz ilikuwa na wanachama kama 50 wengine wakiwa viongozi wa juu serikalini. Waliolipa ada ya uanachama na hivyo kuweza kuingia madansi ya bendi bila kulipa. Wakati huo makao makuu ya Kilwa Jazz yalikuwa katika ukumbi ambao kwa sasa unaitwa Kwa Madobi maeneo yaa Jangwani…itaendelea.

Friday, February 19, 2010

Jerry Nashon aka Dudumizi


Nimeweza kumpata mtu ambae ndiye aliyemlea Jerry Nashon kimuziki na haya ndo aliyoniambia kuhusu Jerry. Nae si mwingine bali ni Bwana Ruyembe ambae kwa sasa ni kiongozi pale Baraza la Sanaa la Taifa

Jerry alikulia Musoma Mjini kijiji kiitwacho Kigera kilichopo Halmashauri ya Manispaa ya Musoma jirani na shule ya Sekondari Mara. Nilikutana naye mara ya kwanza akiwa Musoma Catholic Mission club ambayo leo ni Mwembeni secondary School akiwa anajifunza kupiga gitaa. Alikuwa ana mazoea ya kwenda kwenye hiyo social club ya kanisa iliyowaunganisha vijana wanamichezo mbalimbali. Nilimchukua katika Bendi yangu niliyokuwa nimeiunda muda huo 1980s ikiitwa Special Baruti Band. Nilimuunganisha na Mpiga rhythm wangu akiitwa Charles Koya ambaye hivi sasa anapiga na Bendi ya Mwanza Hotel (solo guitar), ili amwendeleze na akiwa pia mwana Bendi wetu. Alikuwa mwanafunzi mzuri alikuwa na bidii na akaweza baada ya muda mfupi kupiga programu yetu kubwa! Mimi nilikuwa mtunzi na mwimbaji licha ya kumiliki Bendi hiyo. Tulirekodi naye mara ya kwanza TFC pia RTD na baadaye tulirekodi Kenya katika studios mbalimbali na producers mbalimbali na tumepiga muziki clubs mbalimbali Nairobi ikiwa kama vile Bombax Hotel, Kaka Night Club, Rwadhia Night Club na nje ya Jiji katika mikoa takribani yote ya Kenya kasoro Mombasa na Kisumu! Hapa tulishirikiana na mwanamuziki hodari Joseph Kamaru. Muda huo yeye akipiga gitaa la rythm na Bendi yetu wakisaidiana na Koya. Jerry alivutiwa na uimbaji pia utunzi baada ya kuona nafasi niliyokuwa nayo na umaarufu nilioupata enzi hizo Nairobi. Alijifunza nikampa mwanga na kipaji chake kikajitokeza katika kuimba na utunzi pia!.Hatimaye Jeshi la Magereza Musoma walimchukua kwa nia ya kumleta Dar ajiunge na Bendi yao ya Magereza. Alipitia mafunzo na aliondoka baada ya kuwa na Special Baruti kwa miaka miwili na nusu hivi au mitatu. Muda huo Musoma kulikuwa na Musoma Jazz Band(segese) ambayo mimi na wanamuziki wengi wa Special Baruti tulipigia baadaye tukahama na kuiacha hali mbaya! Ilikuwepo pia Mara Jazz Band(Sensera) hizi ndizo zilikuwa Band maarufu mjini hapo wakati huo. Aidha ilikuwapo bendi iliyomilikiwa na Parokia ya Catholic Mission Makoko Seminary ikiitwa Juja Jazz Band lakini ilikuwa ndogo sana na haikuwa kwa misingi ya kibiashara zaidi!. jerry Baadae alijiunga na Bima Orchestra na kisha Vijana Jazz mpaka mauti yake.


Thursday, February 18, 2010

Wednesday, February 17, 2010

Wanamuziki wanawake



Muziki wa dansi uliweza kupambwa na wanawake wengi waliopata sana umaarufu kutokana na umahiri wao enzi hizo. Wanamuziki wa dansi wanawake walichelewa sana kukubalika kwa wanamuziki wanaume tofauti na ilivyokuwa kwenye muziki wa aina nyingine kama taarab, na kwaya. Lakini wengi walijitokeza na kuzoa umaaruf mkubwa labda niwataje wachache na baadhi ya nyimbo zilizowapa umaarufu. Nianze na mama lao Tabia Mwanjelwa, huyu dada wa kinyakyusa alikuwa na sauti nzito ya kukwaruza lakini akiimba mwili utakusisimka. Pamoja na kuwa alikuwa akipanda katika majukwaa ya bendi mbalimbali ni bendi ya Maquis ndiyo iliyofanya hatua ya ziada na kumruhusu arekodi jambo ambalo lilikuwa gumu kwa wanawake katika bendi kabla ya hapo, wimbo uliompa umaaruf sana ni Jane..Jane mi nahangaika juu yako kwa maisha yako..... Pichani Tabia Mwanjelwa akiwa na gitaa, unaweza kupata mengineyo na kuwasiliana nae kupitia
Rahma Shally mwimbaji mwingine mahiri aliyepitia bendi nyingi na kurekodi kwanza na Mwenge Jazz nyimbo nyingi tu maarufu, akapitia MK Group Ngulupa tupa tupa akasikika katika kibao kile Jua asubuhi lapendeza, Sambulumaa akarekodi Sitaki sitaki visa vyako, akatua Vijana Jazz na kurekodi wimbo Sadi Badili mawazo. Alikuwa mwanamama shupavu jukwaani. Nana Njige binti mzuri aliyepitia Orchestra Mambo Bado ambapo alitamba na ule wimbo Lilikuwa jambo dogo tu, akapitia bendi kadhaa ikiwemo Vijana jazz , Tancut Almasi, Legho Stars. Bibie Emma Mkello ambaye hukumbukwa katika ule wimbo alioimba akiwa na Eddy Sheggy wakiwa Super Rainbow..Milima ya kwetu. Kida Waziri akionekana hapa katika picha aliopiga 1991 kwenye ukumbi wa Vijana Kinondoni, kwa sasa yuko Arusha atakumbukwa kwa nyimbo kama Shingo Feni,Penzi Haligawanyiki na Wifi Zangu ambazo zote alirekodi akiwa Vijana Jazz. Pia alipitia kundi la Roots and Culture lililoongozwa na Jah Kimbuteh.
Wapenzi wa Maquis watamkumbuka Rose Mwape ambae nae aliimbia Maquis kwa muda mrefu baada ya kuondoka Tabia Mwanjelwa.Jemsina Msuya pia alikuwa kati ya magwiji alikuwa Legho na akarekodi na Assossa nyimbo ya Mzazi mwenzangu. Wako wengine kama Karola Kinasha ambao bado wako katika muziki. Karola yuko Shada, Ana Mwaole yuko na Mzee King Kiki, Nuru Mhina baada ya kuondoka Police Jazz ametua Vijana Jazz mpaka leo. Nyota Waziri ambaye baada ya kuondoka Bicco Stars ametua Kilimanjaro Band akiwa bado na heshima yake katika wimbo Tupendane na Gere. Ni muhimu kumgusia Asia Darwesh ambay licha ya kuimba alikuwa pia mpiga Keyboards mahiri sana kama alivyoonyesha katika nyimbo alizorekodi MK Group na bendi yake Zanzibar Sounds. Nakaribisha kumbukumbu nyingine

Vijana Jazz Vs Maquis

Katika kipindi cha mwisho cha miaka ya 80, Kinondoni ilkuwa inawaka moto kwa Vijana siku ya Jumapili. Lang'ata ambayo baadae ilikuja kuwa Club ASET na sasa kanisa, palikuwa ndo ukumbi wa Dansi za kuanzia mchana kwa Bendi ya Maquis. Ukija hapa mbele Vijana Jazz Pambamoto awamu ya pili chini ya uongozi wa Hemed Maneti walikuwa nao kila Jumapili mchana wanaporomosha Dansi, na siku hiyo ilipewa jina Vijana Day. Kwa kweli Maquis walikuwa wanajaa watu na Vijana wanajaa watu. Kulikuweko na wapenzi wa kudumu wa Vijana kama ilivyokuwa Maquis. Wakati huo nyimbo kama Ngalula, Makumbele zilikuwa zinalia Lang'ata huku Vijana wanateremsha Shingo feni, Ngapulila, Azda. Ushindani huu ulilazimisha bendi kujitahidi kupiga vizuri na kwa displine au la wapenzi wanahamia bendi jirani. Kuna wakati Vijana Jazz walikuwa wanaanza muziki saa kumi na moja jioni na kupumzika saa tatu na nusu usiku kisha kumaliza dansi saa nne. Maquis wakawa wanaanza saa kumi na kumaliza saa tano usiku. Na wakaanza kuruhusu mtu yeyote atakayekuwa kapigwa muhuri wa kuruhusu kutoka nje ya ukumbi Vijana Jazz,aliruhusiwa kuingia Maquis bure. Vijana wakabadili ratiba na kuanza kupiga saa 9 mchana, kwa mtindo wa bandika bandua, yaani muziki nonstop. Na kufuta kupumzika hadi saa tano. Hiyo ndo ilikuwa raha kwa wapenzi. Vijana haikuwa na show wakati wa Maneti, Lakini show ilikuja baadae katika kukabili show ya Maquis ambayo ilikuwq nzuri sana chini ya mwalimu wao Wabangoi. Majina makubwa yalitawala madansi hayo Maquis kulikuwa na Dekula Vumbi kwenye solo,second solo Mbwana Cox (aliyetoka Vijana Jazz), banza Mchafu Bass, Nguza Viking, Adios, Tshimanga Assossa,Parashi Lukumbule Vijana Jazz kulikwa Shaaban Wanted, Hemed Maneti, Eddy Sheggy, Adam Bakari, Kida Waziri, Abou Semhando, Rashid Pembe na wengine wengi, basi raha kila jumapili ilikuwa kama tamasha

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...