YOUTUBE PLAYLIST

Saturday, July 31, 2010

Mbaraka Mwinyshehe Mwaluka 1



Ukikaa na kusikiliza muziki wa Mbaraka kwa makini unajifunza mengi sana, kwa mashahiri ya nyimbo hizo unapata picha ya maisha yalikuwaje enzi hizo. Furaha, machungu, vicheko, vilio na kadhalika. Upigaji wake wa gitaa, ni somo zuri sana kwa mpigaji anaetaka kujiendeleza katika upigaji wa solo. Katika vipindi vyake vya kuanzia Morogoro Jazz hadi Super Volcano alipitia staili nyingi za muziki, baadhi kama Sululu, Likembe, Masika Zolezole na kadhalika. Tofauti na bendi nyingi ambazo hubadili majina ya mitindo bila kubadili muziki wenyewe, staili za Mbaraka zilionyesha mabadiliko. Nyimbo katika staili ya Likembe zilikuwa tofauti na zile za Masika Zolezole. Kipindi hicho wapenzi wa muziki waliweza kuondoka Dar es Salaam na kwenda Morogoro kufaidi wiki endi ya muziki aidha wa Cuban Marimba, au Morogoro Jazz. Picha ya juu Mbaraka Mwinyshehe, ya chini toka kushoto Sulpis Bonzo, Mlinzi Mustafa(huyu baadae alipigia Urafiki Jazz), Shaaban Nyamwela, Abdul Mketema (mwenye Saxaphone),Samson Gumbo,Mbaraka Mwinyshehe.Hapa wakiwa Morogoro Jazz Band

Friday, July 30, 2010

Mwanamuziki Mheshimiwa Paul Kimiti


Kwa muda mrefu nilikuwa na nia ya kuweka taarifa kuhusu wimbo wa kumsifu Nyerere ambao uliimbwa na Mheshmiwa Paul Kimiti. Nilijitahidi kutaka kupata taarifa kutoka kwake ikawa haikuwezekana lakini karibuni nilisoma maelezo ya Mheshmiwa mwenyewe kuhusu kazi hiyo, ambayo alisema walifanya akiwa Mwenyekiti wa wanafunzi kutoka Tanganyika katika chuo kikuu cha Netherlands kati ya mwaka 1962 na 1965. Akiwa na wanamuziki wenzake wakiwa na kundi waliloliita Safari Brothers walirekodi nyimbo hii nzuri sana kuhusu Mwalimu Nyerere. Mheshimiwa alisema walitoa dola 20,000 walizozipata kutoka Philips records kwa Mwalimu alipotembelea Netherlands April 1965, pesa hizo walitoa ili kuchangia maendeleo ya nchi yetu, na huo ndio ulikuwa mwanzao wa uhusiano wake na Mwalimu.

Wednesday, July 28, 2010

Kida Waziri arudi ulingoni

Kida waziri miaka ya 90.

Kida Waziri au kama alivyokuwa akiitwa enzi zake Vijana Jazz Stone Lady amerudi na album yake yenye nyimbo 6 ikiwa na nyimbo kama Wifi zangu, Shingo Feni, Penzi haligawanyiki na nyinginezo, pia ameimba wimbo wa Mary Maria akishirikiana na mwanae Waziri, ambae kajitahidi kuimba zile sehemu za uimbaji wa marehemu babake.

Kida Waziri alivyo sasa.

Sunday, July 18, 2010

Drums

Ukisema drums katika anga za muziki utakuwa umeeleweka kuwa unaongelea zile ngoma za kizungu ambazo hupigwa kwa kutumia miguu na mikono. Uwingi wa drums huanzia ngoma kubwa moja na ndogo moja (snare), na tasa moja (Hi hat), na kuendelea kwa uwingi kadri ya utajiri na uwezo wa mpiga drum. Katika nyimbo za Dar es Salaam Jazz ambazo zilirekodiwa kwenye miaka ya 30, drums zilitumika hivyo si chombo kigeni katika muziki wa Tanzania. Katika miaka ya sitin chombo hiki kilitoweka katika bendi nyingi za muziki wa rumba, lakini kikarudi tena kwa nguvu baada ya kuingia kwa staili ya kavacha kutoka Kongo. Bendi ambazo zilikuwa zikipiga muziki wenye mahadhi ya kimagharibi ziliendelea na drums katika kipindi chote na kuweza kuunganisha na tungo za zao za rumba kwa ufanisi mkubwa kama ilivyotokea kwa bendi kama Afro70. Drum huwa chombo kinacholinda spidi ya wimbo, na staili ya wimbo, kama ni chacha, tango, waltz au ngoma ya Kimakonde au Kipogoro. Drums huweza kuleta utamu sana kama zikimpata mpigaji.
Siku hizi kuna drums za umeme, hizi huwa na uwezo wa kuongeza au kupunguza sauti, na kuzibadili zikalia milio mbalimbali, kwa mfano kulia kama ngoma za kihindi au kulia kama tumba au hata nyingine zinaweza zikipigwa zikawa zinatoa milio ya ndege!!!.Bendi ya kwanza kuwa na electronic drums ilikuwa Chezimba, wakati huo drums zikipigwa na Charles Mhuto, Tanzanite nao wakanunua zao, na kwa upande wa bendi za rumba MK Group, ikifuatiwa na Vijana Jazz na Bima Lee walikuwa wa mwanzo kuwa na drums hizi

Friday, July 16, 2010

Gitaa la rythm




Katika mfumo wa awali bendi zilikuwa zikitumia magitaa matatu, Solo, rythm na Bass. Gitaa la solo lilikuwa na sauti ya juu huku rythm ikiwa na sauti nzito kidogo ya kati, na mwisho Bass likiwa na sauti nzito kuliko magitaa mengine. Kimuundo gitaa la rythm na la solo hakuna tofauti. Yote yana nyuzi 6,lakini katika kutyuni kwenye amplifier, gitaa la rythm hunyimwa treble kiasi na kuongeza bass zaidi kuliko gitaa la solo ambalo huwa na treble zaidi ya magitaa mengine. Inasemekana kaka yake Dr Nico, ndie aliyeanzisha mtindo wa kuongeza gitaa la nne lililoitwa second solo. Hili lilikuwa likipigwa kwa mifumo mbalimbali katika bendi mbali mbali. Bendi nyingine zilitumia second solo kama gitaa lililokuwa linajibizana na solo, na bendi nyingine lilikuwa linajibizana na rythm. Bendi ya Cuban Marimba chini ya Juma Kilaza liliongeza ubunifu na kuongeza gitaa la 5 na kuliita chord guitar. Lakini leo tuzungumzie gitaa la rythm. Chombo hiki bado kinapigwa katika bendi nyingi lakini umaaarufu wake umeshuka sana. Katika kipindi cha miaka ya 60 na 70, gitaa hili lilikuwa na umuhimu mkubwa na wapigaji wake waliweza kubuni staili zao wenyewe. Kati ya wapiga rythm maarufu namkumbuka Satchmo, hilo ndio lilikuwa jina la kisanii la Harrison Siwale mpiga rythm wa Jamhuri Jazz. Yeye alikuwa na staili peke yake ya kupiga rythm, sikumbuki kusikia mtu mwingine akipiga rythm ya aina yake kabla ya hapo. Rythm yake ilitawala nyimbo za Jamhuri wakati huo. Kumbuka wimbo kama Mganga no 1 na 2, au Blandina. Marehemu Mzee Kasim Kaluwona nae alikuwa na staili tofauti ya upigaji uliyoifanya Tabora Jazz kuwa na staili yake peke yake, kumbuka gitaa lake katika wimbo Asha, au Dada Lemmy. Charles Kazembe akiwa na Morogoro Jazz anakumbukwa katika upigaji wa rythm kwenye nyimbo kama Wajomba Wamechacha. Hao ni wachache tu kulikoweko na wengi marufu. Katika kipindi hiki huko Zaire kulikuwa na mipigo mbalimbali ya gitaa la rythm, ila kitu kipya kikaanzishwa ambapo katika ufungaji wa nyuzi ,wapiga rythm wakauondoa uzi namba nne na kuweka uzi namba moja, hivyo kukawa na nyuzi namba moja 2 katika gitaa, hapo ndipo akina Vata Mombasa wakaweza kuleta utamu mpya katika upigaji wa rythm. Wakati huo Orchestra Kiam wakawa wanajivunia kupiga rythm kwa spidi kali sana,vibao kama Kamiki, Bomoto ni ushahidi wa kazi hizo. Utamu wa ufungaji wa nyuzi kwa staili hii uliweza kusikika vizuri katika gitaa lililopigwa mwanzo kabisa wa wimbo Andoya. Leo vionjo vya upigaji huo vinarudi kwa njia ya ajabu sana. Vikundi vya taarab vimeanza 'kuachia rythm' gitaa moja kubaki linapiga peke yake, japo wao hupiga gitaa la solo lakini staili ni ile ya enzi. Siku hizi kelele huwa nyingi kiasi unaweza ukatembelea bendi 3 ukaona mtu anapiga gitaa la rythm lakini husikii anapiga nini.

Thursday, July 15, 2010

Uliwafahamu Hot 5 wa Magomeni Kota?

Kuna swali nimeulizwa sina jibu,na kila ninae muuliza hana kumbukumbu nalo. Nimeulizwa kama nilikuwa nalifahamu kundi lililoitwa Hot 5 ambalo masikani yake yalikuwa Magomeni Kota, kundi hili lilikuwepo kabla ya Flaming Stars kuhamia Mombasa.....kuna mwenye taarifa?

Atomic Jazz Band


Atomic ilikuwa moja kati ya bendi zilizowika sana nchi hii. Bendi iliyokuwa na makazi yake Tanga, Tanga wakati huo ikiwa na vikundi vingi maarufu vya muziki, kama vile Jamhuri, White Star, Amboni, Lucky Star, Black Star. Bass katika bendi hii kwa kweli lilikuwa likiingiza upigaji wa bezi katika kiwango kipya,wapigaji wake walileta changamoto hata walipokuja hamia katika bendi mpya. Pichani toka kushoto John Mbula -Saxophone,Rodgers- mwimbaji, John Kilua-Thumba(huyu alikuwa ni ndugu ya Julius Kiluwa ambaye ndiye alikuwa mwenye bendi),John Kijiko-Solo gitaa, Hemed Mganga-rythm gitaa (niliwahi kupiga bedni moja na mzee Mganga kwa wakati fulani. Tulikuwa wote Orchestra Makassy na ndie baba mzazi wa mwimbaji wa kizazi kipya Kassim Mganga),Mohamed Mzee-Bass.
Picha hii ilikuwa ni jarada la santuri iliyokuwa na wimbo maarufu Mado Mpenzi Wangu. Wimbo ulikuwa ni ujumbe wa kweli kutoka kwa mwanamuziki mmoja kwenda kwa mpenzi wake ambae jina kidogo linafanana na Mado ili kuficha ukweli. Mtunzi wa wimbo huu alikuwa mpenzi sana wa bendi hii na bado kwa rafiki zake anajulikana kwa jina la Mado. Siku hizi amekuwa mpenzi tu wa kawaida wa muziki.

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...