YOUTUBE PLAYLIST

Wednesday, May 12, 2010

Nani hawa? Picha ilipigwa Dodoma 1961


Nimepigiwa simu leo na mzee mmoja akanambia amesikia kuhusu blog hii na ana kitu cha kuchangia. Kanipa picha hii ambayo pengine ni ya zamani kuliko nyingi humu ndani. Kanambia siku moja 1961 alitoroka shule ili aweze kumwona mwanamuziki ambaye alimpenda kuliko wote. Alikuwa anasoma Dodoma wakati huo, na aliweza kupata picha siku hiyo picha hii naiweka kwenu. Swali, nani anaweza kuwataja wanamuziki waliomo katika picha hii.? Wanaoimba hapo wote ni marehemu, anaepiga gitaa yu hai na picha yake ya sasa iko katika blog hii.

Tuesday, May 11, 2010

Zahir Ally Zorro


Muziki una mengi ya kushangaza, unaweza ukafika wakati ambapo mwanamuziki fulani kila akitoa nyimbo inatokea kupendwa. Hali hii inanikumbusha kipindi Zahir Ally Zorro alipokuwa JKT Kimulimuli Jazz , bendi iliyokuwa katika kambi ya Mafinga huko Iringa. Wakati huo ambapo JKT ilikuwa na makundi mawili ya askari kuna wale waliojitolea kwa ridhaa kujiunga na jeshi hilo na kulikuweko na wale waliolazimika kujiunga kwa mujibu wa sheria. JKT ilianzisha bendi mbili ambazo zote zilikuwa na muziki mkali. Dar es Salaam kulikuwa na JKT Kimbunga Stereo, jina lililotokana na staili yao ya Kimbunga, na Iringa kulikuwa na JKT Kimulimuli, hii ilitokana na kuwa na taa za steji zenye kuwakawaka. Bendi ya JKT Kimulimuli ilipata umaarufu sana baada ya mwanamuziki Zahir Ally Zorro kujiunga na bendi hii. Ilikuwa ni kama lazima usikie vibao vya bendi hii kila siku radioni. Kabwe..tungo kuhusu mtoto mtukutu alieanza uhuni toka mdogo na kulazimika kufungwa hata jela ya watoto. Kitu mapenzi kilianza zamani.....maneno ya kibao kingine kilichogusa sana hisia za watu, Tausi...wimbo unaohusu mwanamuziki aliyemtungia wimbo mpenzi wake. Ilikuwa kama vile kila kibao anachotunga Zahir kinakuwa hit.

Sunday, May 9, 2010

Mkongwe mwingine


Wengi tutakuwa tunamfahamu sana marehemu Ndala kasheba alieko kulia, je unamfahamu huyo anaesalimiana nae. Subiri usikie mchango wake katika muziki wa Tanzania

Abdalla Gama


Kwa wapenzi wa DDC Mlimani Park, jina la Abdallah Gama ni jina muhimu katika historia ya bendi hiyo. Mwanamuziki huyu mpigaji wa gitaa la rythm alipata umaarufu zaidi baada ya wimbo wa uliotungwa na Assossa -Gama, ambao mpaka leo bado unafurahisha sana. Gama na wenzie kama Joseph Mulenga, Abel Balthazar, Cosmas Chidumule chini ya King Michael Enoch waliweza kutunga na kutengeza nyimbo ambazo bado zinaleta burudani miaka thelathini baada ya kutungwa. Abdallah Gama tena atakumbukwa kwa kazi zake alipokuwa BimaLee wakiwa na watunzi kama Jerry Nashon, Shaaban Dede, solo la Mulenga , nba besi la Mwanyiro, hapo ilikuwa utamu kolea. Pichani Gama(mbele)akiwa na mpiga gitaa mwingine Huruka Uvuruge ambae sasa yuko Msondo, na mpiga drum Matei Joseph ambae kwa sasa anendesha bendi yake African Minofu

Friday, May 7, 2010

Wanamuziki ndugu 3


Kitendawili kingine. Picha hii ilipigwa Seaview 1974, kuna wanamuziki wa Afro70, na wanamuziki ndugu ambao nao wametoa mchango mkubwa katika fani ya muziki, unawatambua ni akina nani hapo?

Tuesday, May 4, 2010

Wanamuziki ndugu


Katika kila nyakati kunatokea ndugu ambao ni wanamuziki. Pengine hii inatokea kwa kuwa mtu anakulia katika mazingira ya nduguze kupiga muziki hivyo inakuwa rahisi kwake kuwa mwanamuziki, na nduguze wakiwa wanamuziki inamrahisishia njia, lakini hilo si jibu sahihi kwa kweli kuna mengi zaidi ya hilo. Katika picha hii ni wanamuziki ambao ukoo wao wako wanamuziki wengi na hii imekuwa inaendelea kwa vizazi vitatu sasa jina la ukoo huu kila mara likiwemo katika historia ya muziki. Ni akina nani hawa?

Monday, May 3, 2010

Mitindo ya Bendi

Nikisema tuanze kutaja mitindo ya bendi ni mingi sana maana kila bendi imekuwa inakuja na mtindo wake. Majina mengine ya mitindo yana historia na maana na mengine yana kuwa yakutunga na kwa kweli hata waliokuwa wanayatumia hawana maelezo ya maana ya maneno hayo. Mundo,Msondo, sokomoko, dondola, kiweke, segere matata,super mnyanyuo, vangavanga, chikwalachikwala, libeneke na kadhalika ilikuwa mitindo ya bendi mbalimbali, na muziki wa bendi ulikuwa ndiyo unaonyesha utofauti huo. Kwa mfano katika mji wa Tanga ulikuwa na bendi kubwa mbili, Jamuhuri Jazz na Atomic Jazz. Jamhuri ilikuwa na mtindo wa Toyota, na baadae Dondola, hata muziki katika awamu hizi mbili katika bendi hiyohiyo ulikuwa tofauti. Atomic walikuwa na mtindo wa Kiweke. Muziki wao ulikuwa tofauti na ule wa Jamhuri. Na wapenzi wa Jamhuri hata wakizeeka husifu mtindo wa upigaji wa Jamhuri na rythm la Harrison Siwale(Satchmo). Kadhalika wapenzi wa Atomic watakwambia hakuna kama Kiweke, upigaji solo wa John Kijiko, bass la Mwanyiro na kadhalika. Mtu ambae kisha sikia muziki katika mtindo wa Ambianse wa Cuban Marimba, hawezi kuchanganya na Likembe wa Moro Jazz. Nimeanza kwanza kwa kutaja bendi zilizokuwa katika mji mmoja tena huko mikoani ambapo watu walikuwa wachache na wanamuziki wanajuana na kuishi jirani. Hali hiyo ndio iliyokuwa Tabora, ambako pamoja na Tabora Jazz, kulikuweko na Nyanyembe Jazz, Kiko Kids, muziki wa kila bendi ulikuwa tofauti na mwingine. Dar es salaam kulikuwa na bendi nyingi na hivyo mitindo mingi. Hakuna aliyeweza kuchanganya Maquis na OSS, wala Sikinde na msondo, Sokomoko, afrosa, Katakata vumbi nyuma ya Kyauri voice havikuwa na mpka wa kulinganishwa. Kikubwa ninachotaka kueleza ni kuwa bendi kuwa na mtindo ilikuwa si jina tu bali kulikuweko na kazi ilifanyika ili kupata kulinda na kuendeleza mtindo ambao bendi iliamua kuwa nao. Nakumbuka wakati wa mazoezi enzi hizo unaweza ukatunga wimbo ukianza kuimba wenzio watakwambia mbona unafanana na bendi fulani na hapo utakarabatiwa mpaka uwe katika mtindo wa bendi husika.

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...