YOUTUBE PLAYLIST

Monday, February 1, 2010

Two generations

Huwa nafurahi kila nikipata chance ya kuona show ya Shaa u r great girl

Matangazo ya Bendi zamani yalikuwa yakipambwa na vituko mbalimbali. Wakati huo matangazo yalikuwa yakitoka katika magazeti tu. Na magazeti yalikuwa hayana teknolojia ya kutoa picha za rangi. Hili ni tangazo la bendi ya Maquis ambayo kwa wakati huo ilikuwa na wanamuziki karibu hamsini

Tulikuweko tupo tutakuweko


Enzi za ujana si mwingine ni Dr Remmy Ongala wakati huu akiwa na Orchestra Makassy

Tulikuweko tupo tutakuweko


Miaka hiyooo staili hii iliitwa bumping. ilianza hasa baada ya wimbo ulioitwa Kung Fu fighting. Hapa ni Marehemu Mbaraka Mwinyshehe akiwa Songea wakati huo na Morogoro Jazz Band

Album Throw down your heart ambayo ndani yake kuna nyimbo kadhaa ambazo amepiga mwanamuziki Anania Ngoliga imeshinda grammy awards

Wasanii ni kioo cha jamii, huu ni usemi ambao umezoeleka sana siku hizi katika vyombo vya habari na hata baina ya wasanii wenyewe. Usemi huu niliusikia kwa mara ya kwanza kutoka katika kinywa cha moja ya wasanii mahili nchini marehemu Mzee Godfrey Kaduma, ambaye pamoja na kuwa msanii mahiri ambaye kumbukumbu za usanii wake zinapatikana katika maandishi mengi na filamu kama vile Harusi ya Mariamu. Mzee Kaduma alieleza wazi kuwa usemi huo ni tafsiri ya usemi wa kiingereza ,”Artists are the mirror of the society”. Mirror ni kile kioo ambacho unajitizama ujione ukoje. Hivyo basi jamii ya Kitanzania ikitaka ijijue ikoje iwaangalie wasanii na kazi zao na ijue inajiangalia yenyewe. Msanii asie itafsiri jamii yake hujikuta yuko peke yake hana wapenzi.

Katika miezi miwili iliyopita kumejirudia jambo ambalo kila mara mimi huliona la ajabu sana. Na hii ni tabia ya viongozi kupiga marufuku shughuli fulani za kisanii. Nimesoma katika mikoa miwili wakuu wa mikoa wamepiga marufuku shughuli za kisanii. Kupiga marufuku ni jambo rahisi sana, tena rahisi zaidi katika sanaa kwani wasanii hawajawa na tabia ya kudai haki zao kisheria zinapopigwa marufuku, hivyo viongozi hutoa matamko ya namna hiyo bila woga wa kupata athari za matokeo ya matamko yao.

Tasisi moja imetangaza iko katika mchakato wa kutunga sheria ya kuwabana watunzi wa filamu kuhakikisha wanapeleka tungo zao kuhakikiwa kabla ya kuzitoa hadharani kwani nyingine zinakiuka maadili yetu.

Ningependa kuwakumbusha viongozi wanaopiga marufuku na hawa wanaotunga sheria za kubana watunzi kuwa wakumbuke, wasanii ni kioo cha jamii kwa hiyo yote yanayoendelea katika sanaa yanaonyesha jamii ilivyo. Hivyo basi kuvunja kioo, au kukataa kutumia kioo si njia ya kubadili ubaya wa sura yako.

Tatizo si wasanii, kwani wao ni sehemu tu ya jamii, tatizo ni mmomonyoko wa maadili katika jamii. Wakati unaruhusu vyombo vingine vionyeshe filamu zenye maadili ya kimagharibi masaa ishirini na nne na hivyo kutengeneza jamii inayokubali hayo, halafu kumkataza msanii wa Kitanzania asitunge hadithi ikiwa na maadili hayo mapya, atapata wapi wateja wa kazi zake? Atakachotengeza ataambiwa kazi zako zimepitwa na wakati.

Hata katika nchi ambazo zimeendelea kuna mfumo ambao hutengenezwa kulinda na kuendeleza maadili ya nchi hivyo wananchi kuishi wakiwa wana aina ya maadili ya nchi husika. Vyombo vya kurusha matangazo katika nchi nyingi huwa na asilimia iliyopangwa ya matangazo ambayo huitwa local content. Mfano kama mtu anataka kuendesha Radio au TV anajua kuwa asilimia sitini ya matangazo yake lazima yawe ni kutoka nchini, filamu, muziki na kadhalika, muziki hapa si bongo fleva na muziki wa dansi tu bali hata ngoma za kiasili. Jambo hili ni muhimu sana katika kujenga uzalendo lakini linajenga upenzi wa soko la kazi za sanaa za nchini, na hii inatengeneza ubunifu zaidi katika kazi za sanaa za nchi.

Wakati Balozi wa Japan anaweza akatoa DVD za bure zirushwe katika vituo vya TV nchini ambazo zinaonyesha utamaduni na maadili asili ya Japan, nabaki nawaza Balozi wetu yoyote yule atatoa nini kwenye nchi aliyoko akiambiwa nae atoe filamu toka kwao.

Serikali imeachia utamaduni unaendeshwa na wafanya biashara, matamasha mashindano , kutafuta vipaji na kadhalika kwa misingi ya biashara unafanya kitu kinacholipa. Serikali iwekeze tena kama zamani katika sekata hii ili kuweza kufufua na kukuza utamaduni wa Mtanzania ambao sasa unakokwenda ndio tunaonyeshwa na wasanii ambao kwa kuwazuia haisaidii kubadili mwelekeo wa maadili ya watu.

Thursday, January 21, 2010


Hebu jaribu kupata picha, umelima shamba lamba lako na kupanda mahindi ambayo umeyatunza vizuri na yako tayari kuvuna….. unaamka siku moja na kukuta kuna mtu kayavuna na ameanzisha biashara anapata fedha nzuri wewe huna hata fedha ya kula.

Au umenunua suti nzuri akaja mtu akaivaa harusini, kesho yake anakuja kukutaarifu jinsi walivyomsifia harusini.

Hiyo ndio picha ilivyo katika shughuli za sanaa Tanzania. Na haswa katika mambo ya muziki na filamu.

Wasanii hufanya kazi ngumu ya kutunga na kufanya mazoezi kisha kurekodi kazi zao, kabala hawajafaidi kazi zao hukuta shamba lao likiwa linavunwa kwa njia mbalimbali. Wengine hurudufu kazi zao, wengine huzitumia kutangaza biashara zao. Wengine huzitumia kuhamasisha mikutano yao, wengine huziuza kwa kuwarekodia watu katika simu, katika yote haya mwenye shamba haoni mafao yoyote.

Kutokana na matumizi mengi ambayo yanaweza kutokana na kazi zilizotungwa, na kutokana na ugumu wa kudhibiti kazi hizi sheria zinazitwa za Hakimiliki hutumika katika kulinda maslahi ya mtunzi kwa upande mmoja na mtumiaji kwa upande mwingine.

Ulinzi wa hakimiliki umekuwa mgumu sana hapa nchini kwetu hasa kutokana na kuweko kwa utamaduni wa kutokuheshimu ubunifu wala sheria zinazolinda haki za ubunifu. Labda nitoe mfano, leo ukianzisha kibanda cha chips chenye mapambo tofauti na vingine, muda mfupi baadae mtaa mzima utajaa vibanda vinavyofanana na chako. Watu hawaoni shida kunakili ubunifu. Fundi seremala akibuni staili fulani ya makochi baada ya muda mfupi maseremala kila mahali wataiga staili hiyo ya makochi bila hata kuwaza kuwa wanaiba ubunifu.

Katika maeneo yote ya karibu ya vyuo na sehemu za elimu ya juu utakuta biashara kubwa ya mashine za fotokopi, kazi ya mashine hizi ni kurudufu maandiko na vitabu mbalimbali vya watu bila kujali kuwa waliotunga vitabu hivyo wanahitaji viuzwe ili wapate mafao yao.

Kwa masaa ishirini na nne kila siku redio na baadhi ya Tv hurusha hewani nyimbo za watu, tena kwa vipindi ambavyo hutangazwa wazi kuwa vimedhaminiwa na kampuni kubwa mbalimbali zenye kuheshimika. Vituo hivi vinamilikiwa na kuendeshwa na watu wanaoheshimika katika jamii kwa kuhamasisha vijana wajiajiri, lakini ikishafika kwenye eneo la kulipia matumizi ya kazi za wasanii kigugumizi kikubwa kinatokea.

Watetezi wa haki mbalimbali za wananchi wa Tanzania, watatetea kila haki lakini wakati wa kampeni zao watatumia kazi za wasanii na kuwa wagumu kulipia matumizi hayo. Wanasiasa wakiwa katika kampeni za kuwaeleza wananchi ni jinsi gani wakipata madaraka watatetea haki zao hutumia kazi nyingi za sanaa bila kuzilipia na wala hawaoni kuwa tayari kuna wananchi wanawanyanyasa kwa kutumia kazi zao bila kulipia.

Sheria za hakimiliki humpa mtunzi haki zifuatazo katika tungo zake;

(a) Kurudufu kazi

(b) Kusambaza kazi

(c) Kukodisha kazi

(d) Kutafsiri kazi

(e) Kubadili matum izi ya kazi

(f) Kuonyesha kazi hadharani-exhibition

(g) Kuifanya kazi hadharani-public performance

(h) Kutangaza kazi katika vyombo vya habari-broadcasting

(i) Kuwasilisha kazi kwa umma kwa njia yoyote

(j) Kuingiza kazi nchini

Mtunzi anaweza akaingia katika makubalianao na mtu mwingine ili kutumia moja au zaidi ya haki hizo ili kupata mafao yake.

Nadhani ukiangalia haki hizo hapo juu utaweza kuona jinsi haki za watunzi zinavyovyunjwa masaa ishirini na nne.

Ununuapo CD au DVD elewa kuwa umeipata kwa ajili ya matumizi yako binafsi, ukianza kuitumia kwa shughuli yoyote ile nyingine unaanza kuingilia haki zilizotajwa hapo juu. Hivyo basi kununua CD hakukupi haki ya kuanza kutoa nakala za CD hiyo, wala kuanza kuirusha redioni au kuipiga hadharani kwenye baa au hoteli, hapana, utahitaji kupata ruksa kuanza kutumia kwa kazi hizo za ziada. Ruksa hizi hupatikana kwenye Chama kinachoshughulika na mambo ya Hakimiliki Tanzania yaani COSOTA.

COSOTA hutoa leseni ambazo watumiaji wa kazi za muziki huzilipia na fedha zinazopatikana hugawiwa watunzi. Katika nchi ambazo taratibu hizi zinafanya kazi wanamuziki na wadau wengine wa muziki hupata fedha nyingi kutokana na matumizi ya kazi zao. Bado kuna tatizo kubwa la hili kwani kama nilivyosema utamaduni wa kudharau haki za watunzi bado ni mkubwa katika jamii ya Tanzania.

Jambo la kufurahisha ni kuwa tayari kuna wafanya biashara kutoka sehemu mbalimbali nnchini ambao wamekuwa wanalipia kwa matumizi ya kazi za muziki na COSOTA wamekwisha gawa fedha kwa mara ya saba kwa watunzi wa kazi mbalimbali.

Ili kupata watunzi bora na kazi bora za muziki ni muhimu kuhakikisha watunzi wanalindiwa haki zao na kila mpenda sanaa.

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...