YOUTUBE PLAYLIST

Friday, August 19, 2022

KIINGILIO KINYWAJI NINI HATIMA?

 


Ni kawaida kabisa siku hizi kukuta bango likitangaza onyesho la kundi la muziki, na chini kukawa na maneno, kiingilio kinywaji au hata mara nyingine kiingilio bure.  Ni wazi wanamuziki magwiji marehemu kama wangeweza kurudi wangeshangaa na kuuliza hii inawezekana vipi?

Binafsi nimekulia katika utamaduni wa maonyesho kuwa na viingilio, tofauti ilikuwa ni kiwango cha viingilio, makundi maarufu yalikuwa na viingilio vikubwa na makundi machanga yalikuwa na viingilio vidogo. Wenye kumbi walikuwa wakizifuata bendi kubembeleza ziwe zinapiga katika kumbi zao na bendi zikawa na nguvu ya kutoa masharti, kwa mfano mwenye ukumbi angeambiwa atalipwa gharama ya umeme tu, fedha zote za kiingilio ni za bendi, au pengine kukubaliana kuwa baa itapata gawio la asilimia kumi ya mapato ya kiingilio baada ya kuondoa gharama, na makubaliano mengine ya namna hiyo. Hivyo bendi ziliuza muziki mlangoni na mwenye baa akawa anauza vinywaji na chakula chake. Kulikuwa hakuna muingiliano kiasi cha kwamba ilikuwa kawaida saa sita kasoro dakika chache usiku, kulikuwa kunatolewa tangazo kuwa, ‘Ikifika saa sita kaunta inafungwa’,  Hii ilitokana na sheria iliyohusu mauzo ya pombe, watu walinunua vinywaji vya ziada na saa sita biashara ya pombe ilifungwa biashara ya muziki iliendelea mpaka saa nane au tisa usiku.
Lakini kwa zama hizi ni jambo ambalo la kawaida kukuta kiongozi wa bendi anazunguka kutafuta ukumbi kwa kazi za ‘kiingilio bure’. Bendi inaahidiwa kiasi malipo, ambayo mara nyingi ni madogo sana, na kuanza kupiga muziki ili watu wapate burudani wakati wakinywa.
Utamaduni huu umeanza lini? Turudi nyuma miaka ya tisini mwishoni mwishoni. Kulikuwa na kampuni mbili kubwa za bia zilizokuwa na ushindani mkubwa. Kampuni moja ikabuni kitu kilichokuja kufahamika kama ‘promosheni’. Kampuni hii ikaanza kukusanya wasanii wa Sanaa za maigizo na kuwazungusha kwenye kumbi mbalimbali kunapouzwa pombe, huko wasanii walifanya maonyesho na kisha kulipwa na kampuni. Haukupita muda mrefu bendi ndogondogo zikaanza kugombea kujiunga katika katika biashara hiyo, na kwa kweli kulikuwa na bendi ambazo zingetangaza kuwa zinafanya maonyesho hakika hazingepata kiwango ambacho kilikuwa kikitolewa na kampuni ile ya bia, hivyo ilikuwa ni jambo la faida kwa bendi hizi. Pia wakati huohuo kukaanzisha kitu kilichopewa jina la bonanza, hasa ziku za mwisho wa wiki, huko nako bendi na wasanii wa Sanaa za maonyesho hasa wasanii wachekeshaji wakapata kazi na kulipwa  wakati wapenzi wa Sanaa wakifaidi bila kulipa. Miaka ikaenda bendi  za kupiga kwa kiingilio taratibu zikaanza kupungua. Wakati utaratibu huu unakolea, kukatokea tatizo moja kubwa, moja ya hizo kampuni za mbili za bia, ikapotea kwenye soko. Ushindani wa makampuni ukawa haupo, kwa hiyo umuhimu wa ‘promosheni’ ukapungua, kazi zikafifia, wasanii wengi wakapotea moja kwa moja, ikiwemo bendi kadhaa ambazo zilijua ingekuwa vigumu kuanza kutangaza kuwa sasa zimeanza kupiga kwa kiingilio, baya zaidi kukawa kumetengenezwa jamii ambayo imelelewa kutokulipia maonyesho ya Sanaa. Wasanii walikuwa wameshiriki wenyewe  kutengeneza wateja wa ‘maonyesho ya bure’.
Lakini pia kukawa kumezaliwa utamaduni wa wanywaji kuzoea kinywaji na maonyesho ya Sanaa, hili likwafanya wenye kumbi kulazimika kuanza kubeba jukumu la kutafuta wasanii wa kufanya maonyesho kwenye kumbi zao. Lakini uwezo wa wenye kumbi kulipia ‘promosheni’ ukawa mdogo, hivyo basi bendi zimekuwa zikipiga kwa ujira mdogo sana.
Malipo madogo yanafanya ishindikane kuendesha bendi kwa misingi inayotakiwa. Bendi zinashindwa kununua vyombo vizuri, zinashindwa kufanya mazoezi, au hata kurekodi nyimbo mpya. Na baya zaidi mtizamo wa wanamuziki katika utunzi unakuwa mfinyu sana, tungo zinalenga kufurahisha wanywaji tu, hivyo kiwango cha utunzi nacho kinashuka sana. Na si ajabu ukisikia siku hizi kuwa kiwango cha muziki wa bendi kimeshuka, mfumo wa muziki unafanya aina ya utunzi ufanye bendi zionekane zimeshuka kiwango.

Kuna haja ya wanamuziki hasa wa dansi kukaa na kutafakari namna ya kuondoka kwenye hili shimo ambalo ni baya sana. Bendi ikiwa inaamka na kulala kwa kujipanga kwenda kupigia wanywaji tuu, haitakuwa na mawazo ya kushindana katika ulimwengu wa muziki, ni wazi mtu mwenye safari ya kutoka mtaa mmoja hadi mwingine kamwe hawezi kuhangaika kutafuta passport kwani haimuhusu.  Bendi nyingi sasa hazina hata tungo zake binafsi, bendi zinategemea kurudia tungo za wanamuziki wengine. Karibuni tumeanza kusikia viongozi wa vikundi wakilalamika kuwa kuna vikundi vipya vinaundwa vikitegemea nyimbo za kuiga tu kwenye maonyesho yao, hiyo ni changamoto kubwa kwenye muziki wa ‘live’. Pia muda umefika kwa wenye kumbi kuelewa kuwa kama watahitaji muziki bora utakaoleta wateja wengi kwenye kumbi zao ni vizuri wachangie katika swala la kulipa vizuri zaidi. 

Japo swali la wahenga litakuja. Nini kilianza kuku au yai? Malipo mazuri au muziki mzuri?

3 comments:

  1. Dah umegusa maada muhimu sana.. Ni kweli hawa makampuni ama Corporates wamechangia kama sio kupandikiza desturi ya kutumia muziki kama chombo cha kutangaza bidhaa au huduma zao.
    ila angalau siku hizi naona taratibu watu wanakubali kulipa. nafikiri kwa kuwa muziki wa bure inakosa uhuru wa kupata kile anachohitaji mlaji.

    ReplyDelete
  2. Aliko16:41

    Ikipigwa ile Amapiano yenye chorus *sisi ni walevi*😃 kuna baadhi yetu humu tuna sing along kwa sautibya kwanza.. hehehe.Ijumaa karim.

    Kwa kuleta live music kwenye bar kwa wateja, you are giving them a significant source of entertainment, and adding vibrancy and excitement to the atmosphere of the venue.

    Hence Live music lifts the vibe and instantly draws a crowd. Whether it’s because the music wafts out to the street and attracts passersby, or it provides a fun and distracting reason for customers to prolong their stay past stopping for a pint of beer.
    Vile vile kuna pub food business ambayo kwa kweli ni ngumu.
    Pale wateja wanapo endelea kujichana makuku bila hatacya *kupay attention* msanii anaimba nini nakumbuka Case ya Nina Simon kuchoma mteja mwenye kelele kupita wote kisu cha mezani Huko Ufaransa wakati Nina ana perform, ambayo ilimpelekea Nina kupelekwa Rehabilitation... ila nilimuelewa.
    Kule Zanzibar kwenye mahotel ya kitalii wanamuziki hulazimishwa kupiga back ground yaani wawepo kama hawapo.
    La msingi ni kurejesha ustaarabu wa kumbi za starehe yaani Performance spaces maalum kwa Sanaa za maonyesho tuu.
    Mfano Makumbusho yataifa.. ambapo kazi ni moja tuu Art.
    Napenda kwapa tano Asedeva Ndugu Abeneko na wenzake kwa hilo
    Muda Dance na Nafasi Art space kwa kutilia maanani Sanaa zaidi ya biashara ya pombe.

    ReplyDelete
  3. Anonymous12:01

    Mwakitime ngweliwe sana tena sana...
    Nikukaribishe tarehe 27 agust 2022 F2 florida, morogoro tukupe hata dakika 3 za kutusalimia

    Naitwa kikoti mkurugenzi wa special one entertainment

    ReplyDelete

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...