YOUTUBE PLAYLIST

Sunday, March 28, 2010


Unamkumbuka msanii huyu?

Katika makala za hapo nyuma tulitaja kundi la Barlocks lililokuwa na makao yao pale juu ya Patel Stores , jengo linaloangaliana na Printpak, Barlocks lilikuja badilika na kuwa Mionzi. Kundi hili la Mionzi lilikuwa likipiga mara nyingi New Afica Hotel katika ukumbi wa Bandari Grill na Kilimanjaro Hotel pale Simba Grill. Habari zaidi kuhusu kundi hili zinafuata lakini hapa kuna picha ya kundi hili wakati huo akiwemo Innocent Galinoma, Martin Ubwe, na Frank

Wednesday, March 24, 2010

Dr Ufuta enzi hizo na sasa



John,

Mimi ni mmjoja kati wa fans wa blog yako. Nilikuwa Morogoro mjini na kwa bahati nzuri wakati napata chai ya jioni pale B1 restaurant akapita mwanamuziki mkongwe DOKTA UFUTA Nilifanya nae maongezi mafupi maana alikuwa na haraka kidogo akiwahi kazini, kwa sasa ni mlinzi wa usiku" babu mlinzi" katika moja ya makampuni ya ulinzi pale Morogoro. Tuliongea sana na nikakumbuka last article uliyotoa ya Cuban Marimba na jinsi alivyokuwa akionenaka kijana very hundsome. sasa kupitia taswira hizi chache hivi ndivyo alivyo.

Louie
(Dr Ufuta ndiye mwenye miwani katika hili ganda la santuri enzi hizo)

Sunday, March 21, 2010

Bendi za Wilayani nje ya Dar Es Salaam



Nimeona nirudie tena posting hii pengine iliwahii mno, miaka iliyopita karibu kila wilaya ilikuwa na bendi, naomba tusaidiane kukusanya kumbukumbu hizi muhimu kwa historia ya muziki wa Taifa letu. Kwa mfano pale Same niliwahi kukuta band ya Tanu Youth League siikumbuki jina lake, pia nimeshakuta bendi pale Igunga, Mwadui, Sumbawanga, Makambako, kule Mbeya, nakumbuka ilikuweko bendi ya Bwana Remmy, hebu tuchangie tuone tutafika wapi. Bendi hizi ziliwahi kutoa vibao vingi vilivyotingisha anga za muziki wakati huo. Kwa mfano Shinyanga Jazz na kibao chao Tenda wema uende zako kilichotungwa na kuimbwa pia na Mzee Zacharia Daniel, ambae mpaka kifo chake aliitwa Mzee Tenda wema, au vibao vya Mzee Zahir Ally Zorro akiwa na Kimulimuli, Kabwe,Tausi na vingi vingine , waliopitia JKT Mafinga wakati huo wanakumbuka raha ya bendi hii. Unajua kwanini Bendi iliitwa Kimulimuli? Bendi ilipata taa za stage zinazowakawaka zilizokuwepo pamoja na bendi kwa hiyo taa hizo kumulikamulika ndo kukatoa jina la Kimulimuli kuna kitu kingine muhimu, kwa kuwa bendi zilitoka sehemu mbalimbali kila moja ilikuwa na staili yake na hivyo kuleta utamu katika anga za muziki. Kila mtu atakubali hakuna kitu kinakosesha raha kama kusikiliza muziki unaofanana kila kukicha,

(Pichani ni John Kitime na Kasaloo Kyanga wakiimba wimbo wa Masafa Marefu na kukumbuka walipokuwa wanaitwa Bush Stars)

Iringa-
Highland Stars
Tancut Almasi Orchestra
Chikwala chikwala
Ruaha International
Vico Stars
Mkwawa Orchestra

Kimulimuli JKT

TX Seleleka

Bose Ngoma
******
Morogoro
La Paloma Jazz
Cuban Marimba
Morogoro Jazz
Les Cubano
Vina vina Orchestra
Sukari JazzKilombelo Jazz
Malinyi Jazz
Kwiro Jazz
Mahenge Jazz

Kilosa Jazz

Les Cuban
******

Tanga

Atomic Jazz

Jamuhuri Jazz
Tanga International
Amboni Jazz

Bandari Jazz

Watangatanga

Lucky Star

Black Star
******
Tabora
Tabora Jazz
Nyanyembe Jazz
Kiko Kids

Usoke Jazz

******

Kigoma

Super Kibisa Orchestra

Mwanza
Orchestra Super Veya

******
Moshi
Orchestra Zaire Success
Bana Africa Kituli
********
Dodoma
Dodoma Jazz
Dodoma International
Materu Stars
Saki Band
Super Melody

Mpwapwa Jazz

(Pichani Kibonge, mwanamuziki mkongwe wa Super Melody ya Dodoma)

Mara

Mara Jazz

Musoma Jazz


Ruvuma
Tembo Jazz
Orchestra Sere sere

Super Matimila

******

Lindi
Mitonga Jazz
******
Masasi
Kochoko Jazz


Mtwara

Bandari Jazz


Shinyanga

Shinyanga Jazz

Friday, March 19, 2010

Cuban Marimba


Kuanzia miaka ya 1920 mpaka 1940 Tanzania, hususani Tanzania bara, wanamuziki na wapenzi wa muziki walifuatilia sana muziki kutoka Cuba kupitia sahani za santuri za wakati huo. Kulikuwa na vikundi kama Trio Matamoros and Sexteto Habanero, ambao walitoa santuri zikiwa na namba zinazoanzia GV1, GV2 na kuendelea na kupata upenzi mkubwa katika ukanda huu wa Afrika. Ni vikundi hivi ambavyo viliingiza mitindo kama rhumba, Bolelo, Chacha na kadhalika. Kwa kweli bendi za muziki wa dansi zingepata mengi ya kimapinduzi kama zingeweza kusikiliza na kuelewa muziki wanaoupiga kiini chake ni nini.

Kutokana na hamu hiyo ya kuujua na kuupiga muziki wa kicuba kisawasawa Marehemu Salum Abdallah aliwahi kutoroka kwao Morogoro akakimbilia Mombasa ili apande meli aende Cuba, bahati mbaya safari yake iliishia Mombasa kwa kuishiwa fedha, ambako alianza kupata shida lakini kwa kuwa baba yake alikuwa mwarabu, Ushirika wa waarabu wa Mombasa walimtaarifu mzee huyo kuhusu alipo mwanae na alimfuata na kumrudisha Morogoro. Salum Abdallah Yazidu aliyefahamika sana kama SAY, mwaka 1948 alianzisha bendi yake akaiita La Paloma, ambalo ni jina la wimbo maarufu ambao uliotoka Cuba ukiwa na maana Njiwa, wimbo huu unaendelea kupigwa hadi leo ukiimbwa na kurekodiwa kwa lugha mbalimbali, hata hapa Tanzania bendi nyingi huzisikia zikipiga wimbo huu na kuweka maneno yake ya papo kwa papo hasa kabla dansi rasmi halijaanza. Bendi ya La Paloma ndio ilikuja kuwa Cuban Marimba Band, Salum Abdallah aliiongoza bendi hiyo mpaka kifo chake 1965. Aliyeichukua na kuiendeleza alikuwa Juma Kilaza. Kilaza aliiendeleza vizuri kwa kutunga mamia ya nyimbo yaliyofurahisha sana watu miaka ya 60 na 70. Morogoro ulikuwa mji uliosifika kwa muziki, huku kukiwa na Mbaraka Mwinshehe na Morogoro Jazz, na huku Juma Kilaza na Cuban Marimba. Kuna watu walikuwa wakihamia Morogoro wikiendi na kurudi Dar siku ya Jumatatu asubuhi. Kati ya nyimbo maarufu za Cuban Marimba zinazodumu kwenye kumbukumbu ni wimbo Ee Mola Wangu, ambao Salum Abdallah awali aliutunga kwa mashahiri marefu lakini akachukua beti chache kutengenezea muziki akilalamika kuwa kuna walimwengu wanamtakia mabaya, lakini siku ya kufa atawashitakia maiti wenzake kuhusu ubaya huo.

Pichani ni Cuban Marimba baada ya Salum Abdallah, wa kwanza kulia Juma Kilaza, mwenye mawani Ufuta mpiga solo. Wadau malizieni majina ya hawa wanamuziki wengine. Mheshmiwa Tsere uliishi sana Morogoro tusaidie

Mheshimiwa mchango wako ni muhimu

Nimekuwa najaribu kumshawishi Mheshimiwa mmoja ambaye alikuwa Waziri kwa muda mrefu na sasa ni Mbunge atoe mchango katika blog hii, Mheshimiwa huyo katika miaka ya sitini alirekodi nyimbo moja nzuri sana ya kumsifu Mwalimu Nyerere. Mheshimiwa huyo alirekodi kibao hicho wakati akisoma Uholanzi.
Pia Balozi mmoja maarufu aliyekuwa akiimba nyimbo za James Brown miaka hiyo najaribu kumwomba ruksa atusaidie experience zake.
Mzee moja marehemu sasa lakini ana watoto wengi wanamuziki, japo yeye alikuwa mwalimu Tabora school alinieleza kisa cha Mheshimiwa mmoja (Mbunge muhimu), ambaye nitamwomba ruksa yake nitaje jina lake baadae, ambaye alilazimika kuwa anamlimia kajibustani kake ili afundishwe gitaa. Nashukuru kuwa mheshmiwa huyo mpaka sasa ni msaada mkubwa sana katika fani ya muziki hasa wa dini

Thursday, March 18, 2010

LIBENEKE

Mheshimiwa mmoja kaniomba niweke mwanga kwenye hili neno ambalo limetajwa hapo juu. Katika kumbukumbu zangu, Libeneke ulikuwa mtindo wa Butiama Jazz Band, bendi iliyokuwa chini ya uongozi wa marehemu mzee Mkwega, ikiwa na mpiga solo mzee Makelo ambae yuko Shikamoo Jazz, baadhi ya waimbaji akiwemo Saidi Hamisi ambaye kwa miaka mingi mpaka kifo chake alikuwa Vijana Jazz. Kulikuweko na wimbo ambao ulikuwa maarufu ukiwataja wanamuziki wa bendi hiyo na kibwagizo chake kilikuwa ....waache waseme, watachoka wao mtindo libeneke utatia fora...... Mkuu wa libeneke upo? Karibu wapenzi wa Butiama Jazz

Wednesday, March 17, 2010

The Tanzanites


Kabla ya kuwa na jina hili waliitwa the Barkeys, moja ya bendi za zamani sana Tanzania picha hii ya siku ya mwaka mpya 1991 itawapa watu kumbukumbu za kutosha. Bibie hapo mbele ni Juliet Seganga

Saturday, March 13, 2010

Wanamuziki ndugu 1



Katika historia ya muziki kumekuweko na familia kadhaa ambazo zimekuwa zikitoa wanamuziki zaidi ya mmoja. Moja ya familia iliyokuwa maarufu ilikuwa ni familia ya akina Sabuni. Unawakumbuka? Niko katika mawasiliano na mwanamuziki mmoja aliyepiga na ndugu watatu kati ya hao na tutapata kumbukumbu nyingi karibuni

Kushoto Cuthbert Sabuni, chini ni Raphael Sabuni akiwa na mwimbaji wa kike ambaye bado natafuta jina lake lakini alijulikana kama 'Lady Soul'

The Comets


Hawa ni wanamuziki wa The Comets kabla hawajawa the Sparks. Haya wadau nani unamfahamu hapa? Una stories za wakati huo. Nilipata bahati ya kuwasikia 1969 pale ambapo iko shule ya Forodhani wakipiga bugy, na ilikuwa mara yangu ya kwanza kusikia wimbo Mammy Blue, haujanitoka kichwani mpaka leo. Nakumbuka pamoja na nyimbo kama Direct Me, Hard to Handle, walipiga nyimbo za Isaac Hayes (Black Moses) ambazo zilikuwa top kwa wakati huo, unaukumbuka Move on?

Thursday, March 11, 2010

Nawaachia wananchi waseme 2




Mitindo ya Bendi Zetu

Kuwa na mitindo au staili ya muziki limekuwa jambo la kawaida kwa bendi zetu hapa Tanzania. Zamani mtindo mpya ulikuwa ni mapigo mapya ya muziki au hata uchezaji mpya. Hata bendi ikiwa mpya ulitegemea iwe na mapigo mapya na hivyo kuwa na maana ya kuwa na mtindo mpya. Hii ilifanya upenzi au unazi wa bendi kama ilivyojulikana wakati huo kuwa mkali na unaweza kuelezeka. Ilikuwa hata mwanamuziki akiwa mzuri vipi akiingia kwenye bendi alilazimika kujifunza kwanza mapigo ya bendi yake mpya kabla hajaruhusiwa kutoa nyimbo mpya, hii ilikuwa ni kuratibu mtindo wa bendi.

Mitindo ilikuwa tofauti hata uchezaji wake. Wakati nikiwa Vijana Jazz tuliwahi kupiga pamoja na Msondo Ngoma, wakati huo OTTU. Wapenzi wa pande zote mbili walikuwa wanasema wanashindwa kucheza staili ya bendi pinzani. Utakubaliana na mimi kuwa wakati Vijana ikipiga mtindo wa Takatuka ni muziki tofauti na Pambamoto ya Mary Maria au Bujumbura, na ni tofauti na Saga Rhumba ya enzi ya VIP, kwa hiyo majina hayo hayakuja tu , kulikuwa na sababu ya kuyatafuta kuonyesha aina mpya ya mapigo. Majina ya mitindo hii, na uchezaji wake, ulitokana na mambo mbalimbali , mengine yalitungwa na wanamuziki au mengine wapenzi, na mengine vituko mbalimbali vilivyotokea wakati huo. Kwa mfano Bomoa Tutajenga Kesho ya Mambo Bado, ilitokana na sentensi ya tajiri mwenye baa ya Lango la Chuma kutamka sentensi hiyo, wakati wa matayarisho ya uzinduzi wa bendi ya Mambo Bado. hilo. Fimbo Lugoda ilitokana na mwanamuziki mmoja kutandikwa viboko na bibi yake baada ya kukutwa na picha ya mwanamke mzungu. Washawasha ya Maquis ni baada ya steji shoo mmoja aliyekaa chini ya mti kuangukiwa na mawashwasha na kuanza kujikuna. Wadau mna vyanzio vingine vya mitindo ya bendi zenu watu tujikumbushe?

Tuesday, March 9, 2010

Nawaachia wananchi waseme








Vijana Jazz Baada ya Maneti

Ushindani uliokuwepo kati ya Maquis Original na Vijana Jazz ulikuwa mkali sana mwanzoni mwa miaka ya tisini hasa kwa ajili ya siku ya Jumapili ambapo Vijana walikuwa Vijana Kinondoni, wakati Maquis wakiwa kwenye ukumbi wao wa Lang’ata Kinondoni. Muda wa maonyesho yote mawili ulikuwa uleule hivyo kila kundi lilikuwa linatafuta kila njia ya kumpiku mwenziwe.

Vijana Jazz iliamua kupata wanamuziki wengine wapya. Hapo akaingia Suleiman Mbwebwe toka Sikinde,Jerry Nashon toka BIMA, Benno Villa kutoka Sikinde lakini wakati huo akitokea Nairobi, Rahma Shally kutoka Sambulumaa, wote hao waimbaji. Shaaban Dogodogo akitokea Nairobi (solo gitaa), Mhando (keyboards), Ally Jamwaka toka Sikinde (tumba).

Hapo ndipo ilipoanza Pambamoto Saga Rhumba.

Ujio wa TP Ok jazz ulibadilisha sana mtizamo wa bendi kimziki. Ok Jazz , wakiwemo wakongwe wote kasoro Franco, maana hii ilikuwa baada ya kifo chake. Ingawaje walikuja na kijana mmoja ambae alikuwa anaimba kama Franco pia alikuwa anapiga gittaa kama Franco , walikuja na mtindo wa kuweko kwa magitaa mawili ya solo, tofauti na kawaida iliyokuweko ya kuweko second solo. Tofauti yake ni kuwa katika mfumo wa OK jazz, wapiga solo wote wawili walikuwa mahiri na magitaa yalipewa uzito sawa. Katika mfumo wa second solo, gitaa hili huwa linasindikiza tu solo gitaa. Kwa kutumia mfumo huu, recording maarufu ya VIP ilirekodiwa katika studio za TFC. Mzee John Ndumbalo fundi mitambo mwenye uwezo mkubwa ambao bahati mbaya kama yalivyo mambo mengi mazuri ya zamani ya Tanzania umetupwa na kusahaulika. Aliirekodi album hiyo. Iliyojaa nyimbo ambazo zina kumbukwa mpaka leo, Thereza (Jerry Nashon), VIP (Jerry Nashon), Bahari imechafuka (Benno Villa), Mfitini (John Kitime). Sauti za waimbaji humo akiwemo Jerry Nashon , Benno Villa Anthony, Said Hamisi, Freddy Benjamin,Abdallah Mgonahazelu, Mohammed Gotagota Suleiman Mbwebwe zilileta burudani kubwa wakati huo.

Wapiga magitaa wa Vijana Jazz chini ya Shaaban Yohana (Wanted), walikuwa Shaaban Dogodogo Solo,Agrey Ndumbalo Rhythm, Bakari Semhando na Manitu Musa Bass, hapo ilikuwa utamu kolea………………



Picha ya juu Madiluu System kushoto kwake Baker Semhando mpiga Bass wa Vijana Jazz. Chini kushoto Mohamed Gota gota, chini Agrey Ndumbalo

Sunday, March 7, 2010

Tancut Almasi awamu ya kwanza

Mwaka 1986 wafanyakazi wa Kiwanda cha kuchonga Almasi cha Iringa chini ya Jumuiya yao ya Wafanyakazi (JUWATA), waliamua kukubaliana na mzungu mmoja tajiri wa almasi kuwa wao wamchongee almasi katika kipindi kifupi hivyo kufanya overtime na ile pesa ya overtime awaletee vyombo vya muziki. Kwa msaada wa wanamuziki waliokuweko pale Iringa, akina Mamado Kanjanika, Juma Msosi, Saidi Kananji waliweza kuchagua kupitia catalogues walizopata vyombo aina ya Yamaha. Ninauhakika bendi ingekuwa Dar es Salaam ingechagua Ranger FBT, kwani kilikuwa kipindi cha ukichaa wa Ranger hasa baada ya Mzee Makassy kupata vyombo hivyo.

Vyombo vilifika na kuanza kutumiwa na wanamuziki waliokuwepo wakati ule. Uongozi wa Bendi ulimuita Ndala Kasheba kuja kuzindua vyombo hivyo na ikiwezekana kuiongoza bendi, Kasheba alifika Iringa lakini wakashindana masharti na uongozi wa kiwanda cha Tancut.

Pamoja na kuwa alikuwa mwenyeji wa Iringa John Kitime alikuwa anapiga muziki Dar es Salaam ndipo alipoitwa nyumbani kujiunga na bendi hiyo. Kundi la wanamuziki toka Dodoma lilioitwa Super Melody likiwa na mtindo wao wa Zunguluke,nalo lilikuja ili kuteka kabisa bendi, lakini uongozi wa Bendi uliokuwepo uliwachukua wanamuziki wanne tu wa Bendi hiyo. Waimbaji wawili akiwemo Saburi Athuman (kiongozi wa sasa Vijana Jazz), mpiga gitaa Mohamed Ikunji, na mpiga saxophone ambae hakukugusa saxophone hilo hata siku moja. Baada ya hapa kulianza wimbi la wanamuziki kujiunga na bendi hii wakiwemo Shaaban Wanted, Abdul Salvador, Mohamed Shaweji, Banza Tax na wengineo.

Pamoja na kutokukubaliana na Tancut, Ndala Kasheba aliwataarifu mapacha Kasaloo Kyanga na Kyanga Songa kuhusu bendi, wao nao walikuja Iringa na kujiunga wakifuatana na Mafumu Bilali Bombenga. Hapa ndipo awamu ya kwanza ya Tancut ilipoanza kuwika na vibao kama Kashasha, Nimemkaribisha Nyoka, Tutasele, Mtaulage, The Big Four. Wanamuziki wa wakati huu walikuwa , Shaaban Wanted Solo, John Kitime Mamado Kanjanika Rhythm, Mohammed Ikunji Second Solo, Amani Ngenzi Bass, Saidi Kananji Tumba, Ray Mlangwa na Buhero Bakari Trumpet, Mafumu Bilali na Abdul Mngatwa Saxophone, Abdul Salvador Keyboards. Kasaloo Kyanga, Kyanga Songa, Hashim Kasanga, Mohammed Shaweji, Banza Tax alikaa muda mfupi akatoka kabla ya kurekodi awamu ya kwanza lakini alirudi awamu ya pili na kuweza kurekodi .


Picha ya juu Kasaloo na Marehemu Kyanga Songa.Picha ya chini toka kushoto Buhero Bakari,Abdul Salvador,Kasaloo Kyanga, Asha Salvador(mke wa Abdul), na Kyanga Songa Miembeni Bar Ilala

Saturday, March 6, 2010

Mlimani Park Orchestra

Mlimani Park ilianzishwa mwaka 1978,ikiwa na wanamuziki kama Abel Balthazar (solo na second solo), Muhiddin Maalim Gurumo(muimbaji), Cosmas Thobias Chidumule (muimbaji), Joseph Mulenga(Bass), Abdallah Gama (rhythm), Michael Enoch (Saxophone), Hamisi Juma(mwimbaji), George Kessy(kinanda), Haruna Lwali(Tumba), ikiwa chini ya TTTS (Tanzania Transport and Taxi Services).

Mwaka 1983 shirika hilo lilipopiga mueleka kifedha kama mashirika mengi wakati huo bendi ikawekwa chini ya himaya ya Dar es Salaam Development Corporation (DDC). Chini ya uangalizi wa mwanamuziki mkongwe king Michael Enoch ambaye atakumbukwa kuwa alikuwa mpiga solo hatari sana wa Dar Jazz enzi za mtindo wao Mundo (mpaka akapewa sifa ya King), bendi ilinyanyuka ikiwa na sauti ya kipekee na mpangilio wa vyombo uliofanya bendi ilitikise jiji. Michael Enoch ambaye mpaka mauti yake alijulikana pia kwa sifa ya Ticha kutokana na kufundisha wanamuziki wengi na pia kuweza kupiga vyombo vingi, alikuwa ndie kiongozi wa Bendi kwa miaka mingi baadae. Umahiri wa King au Ticha (mwite upendavyo sifa zote anastahili), utaweza kuusikia katika nyimbo Tucheze Sikinde na Nalala kwa taabu alipiga alto saxophone (saksafon ndogo yenye sauti za juu), kwenye nyimbo nyingine alikuw anapiga tenor saxophone (saks kubwa yenye sauti za chini)

Mlimani Park Orchestra na mtindo wao wa Sikinde uliotokana na ngoma ya Kizaramo. Na ukaongezwa kibwagizo Ngoma ya Ukae, yaani Sikinde ngoma ya nyumbani, umekuwa ndo nembo ya bendi hii iliyojiwekea nafasi katika historia ya muziki wa Tanzania. Ni vigumu kutaja wanamuziki wote waliopitia DDC Mlimani Park lakini najua kwa msaada wa wadau tutapata majina mengi kadri itakavyowezekana. Lakini nianze na listi ifuatayo lakini pengine nigusie jambo ambalo watu wengi hawalijui, wimbo maarufu wa Gama ulitungwa na Tchimanga Assossa katika kipindi kifupi alichopitia bendi hii. Haya baadhi ya wanamuziki ni:

Hassani Rehani Bitchuka, Muhiddin Maalim Gurumo, Cosmas Tobias Chidumule, Hamisi Juma, Benno Villa, Francis Lubua, Max Bushoke ,Shaaban Dede ,Tino Masinge, Hussein Jumbe, Fresh Jumbe, Hussein Mwinyikondo vocals; Joseph Mulenga, Abel Balthazar, Henry Mkanyia, Michael Bilali, solo guitar; Abdallah Gama, Muharami Saidi, Mohamed Iddi, Huruka Uvuruge 2nd solo and rhythm guitars;

Suleiman Mwanyiro, Julius Mzeru bass guitar; Habibu Abbas, Chipembere Saidi, Juma Choka drums;Haruna Lwali, Ally Omari Jamwaka, Mashaka Shaban tumba; George Kessy Omojo organ; Boniface Kachale, Ibrahim Mwinchande, Machaku Salum, Hamisi Mirambo, Ally Yahya trumpets; "King" Michael Enoch, Juma Hassan, Joseph Bernard, Shaban Lendi saxophones karibuni wadau kuongeza utamu.


Friday, March 5, 2010

Patrick Pama Balisidya


Jina Patrick Balisdya halitakuwa geni kabisa kwa wadau wa blog hii,lazima roho zimeanza kuwadunda kama inavyokuwa kwangu kila nikimkumbuka Blai. Patrick Pama Balisidya alizaliwa Mvumi Dodoma tarehe 18 April 1946. Kabila lake alikuwa Mgogo , kabila ambalo lina wanamuziki wengi maarufu kutokana na muziki kuwa sehemu muhimu ya maisha ya kabila hilo. Mama yake alikuwa anapiga kinanda kanisani na hivyo basi kutokana na asili ya kabila lake na pia kutokana na mama yake, hakika huyu angeweza kujisifu kuwa muziki uko katika damu yake.

Mdau mmoja alitutaarifu kuwa Balisidya alikuwa kiongozi wa Bendi ya shuleni kwake Dodoma secondary School. Ambapo kutoka hapo alijiunga na Chuo cha Ufundi , na baada ya kumaliza mafunzo alifanya kazi hiyo kwa muda na 1967 akawa tayari anapiga muziki Dar Es Salaam Jazz B. Kufikia mwaka 1970 Patrick alikuwa ameanzisha kikosi chake mwenyewe Afro70, kikiwa na mtindo wake Afrosa. Alikuwa mbunifu katika muziki wake, na kwa muda mrefu alikwepa sana kuingia katika wimbi la kufuata mapigo ya Kikongo kitu ambacho hata wakati huo bendi nyingi zilikifanya, japokuwa kukutana na Franco wakati alipofanya moja ya ziara zake nchini humu kulimfanya abadili mtindo kwa kipindi kifupi na katika nyimbo moja wapo aliiga kabisa solo la Franco alilolipiga kwenye wimbo wake Georgette.

Afro70 iliwakilisha wanamuziki wa Tanzania katika maonyesho ya mtu mweusi Lagos,Nigeria. (FESTAC festival 1977). Vyombo alivyotumia katika maonyesho haya vilimsumbua akili mpaka alipofariki, kwani muda mchache kabla ya Festac, wakati huo serikali ikiwa imeshamtaarifu kuwa ndie atakuwa mwakilishi wa Tanzania, vyombo vyake vyote vilihalibika katika ajali ya gari. Serikali ilinunua vyombo vipya ambavyo siku zote Balisdya alisema aliambiwa ni vyake baada ya maonyesho. Aliporudi kutoka Nigeria Kiongozi mwingine wa serikali aliamuru vyombo virudishwe serikalini na kwa kitendo kile kutangaza kifo cha Afro70. Vyombo hivyo vilitumika kuanzisha bendi ya Asilia Jazz ambayo ilikuwa Bendi ya Wizara ya Utamaduni na Vijana. Balisdya alitumia muda mwingi kujaribu kudai haki yake hiyo ambayo ilimkwepa mpaka mwisho wa maisha.

Mwaka 1979, Balisidya alikwenda Sweden na kushirikiana na kikundi cha Archimedes akatoa album nzuri sana iliyoitwa Bado Kidogo. Kuna wakati Patrick alijiunga na Orchestre Safari Sound, (masantula) na kupiga piano katika ule wimbo maarufu, ‘Unambie siri’, Patrick pia alikuwa mpigaji mahiri wa keyboards. Kwa kweli nyimbo za Patrick zilizokuwa juu katika chati ni nyingi. Harusi, Dirishani, Weekend, Tausi, Pesa, Nakupenda kama Lulu, Ni masahaka na mahangaiko, Afrika.

Patrick alifariki tarehe 7, Agosti 2004.

Daima tutakukumbuka Patrick Pama Balisidya,

Mungu akulaze pema peponi

Jiving


Katika aina ya muziki ambao ulisababisha bendi kuanza katika mashule, ilikuwa ni aina ya muziki na kucheza ulioitwa 'jiving'. Shule nyingi zilikuwa na vikundi hivi, sekondari za kike na kiume zilishindana katika jiving. Muziki huu ulikuwa umetoka haswa Afrika ya Kusini. Siasa zikaingilia kati katika miaka ya mwishoni ya sabini na kuuwa jiving katika mashule mengi. Jiving ilikuwa inaambatana mara nyingine na filimbi kama alivyokuwa anapiga Spokes Mashiyane. Mbaraka Mwinyshehe ni matokeo ya muziki huu alikuwa bingwa wa kupiga filimbi. Pichani ni kikundi cha jiving cha Mkwawa High School The Skylarks Jiving Group, akiwemo mwandishi maarufu Danford Mpumilwa (watano toka kushoto) ambaye pamoja na kuwa mwimbaji wa Bendi ya shule hiyo Mkwawa Orchestra, aliendelea mpaka kufikia kuwa na bendi yake mwenyewe pale Arusha.

Wednesday, March 3, 2010

Bendi za wanafunzi mashuleni


Katika miaka ya sitini na sabini shule nyingi za sekondari zilikuwa na Bendi (bendi ya magitaa), hata pale Chuo Kikuu Mlimani palikuwa na Bendi nzuri tu katika kipindi hicho, Kuna Bendi za shule nyingine zilipata umaarufu wa Kitaifa kama vile Bendi ya Shule ya Sekondari Kwiro ambayo iliweza kurekodi nyimbo zake Radio Tanzania. Niongelee shule moja nadhani itatoa changamoto ya kupata habari za bendi za namna hiyo katika shule nyingine. Pale Mkwawa high School Iringa ,kulikuwa na bendi mbili. Moja ilikuwa ikipiga muziki wa kiswahili ambayo ilikuwa na wanamuziki kama Sewando kwenye solo, Masanja kwenye rythm, John Mkama Bass,Manji,Danford Mpumilwa mwimbaji, mpiga tumba kwa sasa ni Askofu moja mashuhuri, wakati huo huo bendi ya pili ilikuwa na mwimbaji machachari Deo Ishengoma akiimba nyimbo za James Brown. Bendi hii ilikweza kurekodi RTD pia vibao kama Wikiendi Iringa na Ulijifanya lulu na kadhalika.

Dar Es Salaam pia palijaa bendi nyingi za shule na mitaani. Azania, Tambaza ni kati ya shule zilizokuwa na bendi za vijana katika enzi hizo, wakipiga muziki Jumapili mchana ukiitwa bugi. Bahati mbaya bugi lilipigwa marufuku na kuharibu mfumo mzima wa muziki wa vijana katika historia ya muziki Tanzania. (Pichani ni shule ya Mkwawa wakati huo.)


Tuesday, March 2, 2010

Swali la Leo

Bendi gani iliimba wimbo- Mali ya mwenzio sio mali yako? Na dongo lilikuwa likielekezwa kwa nani?

Chinyama Chiyaza

Tangazo jingine la dansi la miaka hiyo ambalo nina uhakika litaleta kumbukumbu kwa wapenzi wa Maquis wa enzi hizo za Mtindo wa Telemka Chekecha Scania LBT III, wakati huo gari za Scania ndizo zilikuwa maarufu nchini na Scania LBT III ilikuwa gari yenye saiz kubwa kuliko zote, na ndio yenye kusifika zaidi, karibuni tena wapenzi wa White House mchangie, mambo yalikuwa mazito chini ya uongozi wa Chinyama Chiyaza ambae alikuwa mpiga Saxophone katika bendi. Wakati huu Maquis ilikuwa na maendeleo makubwa sana ya kuwa na mashamba, magari, matrekta na hata kuwa na Kota zake pale Sinza Palestina. Hebu angalia majina yaliyopo katika bendi.

Monday, March 1, 2010

Swali la Leo

Swali la leo......... Bendi gani ilipiga wimbo wa Banchikicha? Kwa msaada tu bendi hiyo ilishinda mashindano ya Bendi Bora Tanzania 1973

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...