YOUTUBE PLAYLIST

Tuesday, August 31, 2010

The Upanga Story


Upanga ni eneo muhimu sana katika historia ya muziki Tanzania. Hata katika miaka ya karibuni kulizuka kilichoitwa East Coast, muungano fulani wa wasanii wa Bongoflava toka maeneo ya Upanga, hii haikuwa mara ya kwanza kwa Upanga kuwa na wanamuziki waliotingisha mji. Enzi hizo za muziki wa soul, vijana wa Upanga walilipa eneo hili la mji jina la Soulville.Kwenye kona ya barabara ya Mindu na United Nations, nyumbani kwa familia ya Jengo, hapo ndipo palikuwa mahala pa mazoezi pa kundi lile la Groove Makers. Baadhi ya wanamuziki wa kundi hili walikuwa Mohamed Maharage, Joseph Jengo, Emmanuel Jengo, Herbert Lukindo, Willy Makame, na mpiga Drums ambae mpaka leo yupo katika anga za muziki Jeff. Kipindi hiki kilikuwa ni wakati wa muziki wa soul na kundi hili lilikuwa kundi la ubora wa juu wakati huo. Upanga ilikuwa na kundi jingine The Strokers, hili lilikuwa na awamu mbili, awamu ya kwanza ilikuwa na wanamuziki akina Donald Max, David Max, Harry Chopeta, Vincet Chopeta, Pino Makame na Ochiwa na Freddy Lukindo. Awamu ya pili ya kundi hili lilkuwa na Sajula Lukindo,Onesmo Kibira,Innocent Galinoma,Ben Galinoma, Denis Pad,Francis Kasambala,Vicent na Harry Chopeta, Ally Mwarabu, Sabri Mmanga na wengineo. Barlocks ni Bendi nyingine iliyochipukia Upanga, jina la Barlocks lilitokana na kuweko kwa kundi la Barkeys ambalo leo linaitwa Tanzanites. Barlocks walikuwa wakitumia vyombo vya Barkeys kwani kwa wakati huo bendi hizi zilikuwa kama mkubwa na mdogo. Barlocks hiyo ya awamu ya kwanza ilikuwa na wanamuziki akina Jimmy Jumba,Pimbi Sokoine, huyu alipewa jina la utani Pimbi kutokana na kuwa mrefu sana, Said Mbonde kaka yake Amina Mbonde mwanamuziki mwingine muimbaji,Sajula Lukindo, Abraham. Kulikuweko na makundi mengine mengi hapo Upanga, kama White Horse, Aquarius hapa walikuweko producer maarufu Hendrico Figueredo, Joe Ball,Joel De Souza, Mark De Souza,Roy Figueredo, Yustus Pereira,Mike De Souza. Baadhi ya wanamuziki wake walienda na kuungana na wengine Arusha na kuvuma sana na kundi la Crimson Rage, baadae wakarudi Dar na kujiita Strange. Baadhi ya kumbi walizokuwa wakipiga zilikuwa DI, Marine,Gymkhana,Maggot, St Joseph na kwenye shule mbalimbali.
(Picha ya juu-Emmanuel 'Emmy' Jengo, Joseph 'Joe' Jengo, Herbert 'Herby' Lukindo. Kati-Jeff 'Funky' nyuma yake ni Willy Makame. Picha ya chini Willy Makame)

19 comments:

  1. Sam Mnkande06:49

    John, Shukrani nyingi once again kwa kazi unayoifanya. I knew all these guys and grew up with them.I still remember nyumbani kwa kina Jengo(practice ilikuwa servant quarters), nyumba ya akina Lukindo, Balozi Maharage, na akina Chopeta. I know the whereabouts of most of them except for akina Chopeta ambao walikuwa ni good family friend. Hivi unajua wapo wapi ? I would luv to reconnect with them

    ReplyDelete
  2. Anonymous19:11

    Sasa bro unaibuka alafu unapotea, sasa tukueleweje? manake unatuonjesha alafu unazama,vitu vyako hamna mtu anatoa! style yako ya habari ni special! nakupa shukrani ya shingo upande kama unavyotupa mavitu nusunusu!

    ReplyDelete
  3. Anonymous22:01

    Ndg yangu! ninaamini mimi pamoja na wewe Anony wa pili tuna hamu sana ya kujua mambo ya muziki makini. Lakini amini usiamini maandalizi ya makala hizi yanakula muda mwingi sana wa kutafuta nyaraka muhimu na makini. Ninaamini John anafanya kazi ya ziada . Asante John tutakuvumilia pale unapo chelewa. Huvi unaweza kujua alipo Amani mpiga bass wa Tancut almasi wa siku hizoo! tumepotezana muda sana

    ReplyDelete
  4. Ndugu yangu Anon 12:01, aksante, ni wazi kweli hujaonana na Amani Ngenzi miaka mingi sana, maana mara ya mwisho nilikutana nae May 1995 akiwa hoi kitandani na hata yeye alinambia haoni kama atapona na kweli alifariki muda mfupi baada ya hapo

    ReplyDelete
  5. Anonymous09:10

    Kaka shukrani sanaa!!!! kwa yote unayotuletea.
    Mimi napenda kujua ule mwimbo tuliokuwa tukicheza mitaa(watoto) "BANICHIKICHA" uliwahi kupigwa na mojawapo ya bendi zetu za zamani,-ni kina nani hao ambao waliopiga mwimbo huo?

    ReplyDelete
  6. Banchikicha uliwahi kupigwa, na hata kutolewa katika santuri ya label ya TFC na kundi la Sunburst, kundi machachari lililokuwa likipiga mtindo uliokuwa ukijulikana wakati huo kama Afrorock, wakifuatia njia za Osibisa. Sunburst pia waliwahi kushinda tuzo ya Bendi Bora 1973

    ReplyDelete
  7. Anonymous09:50

    Asante sana John kwa taarifa ya Kifo cha Amani Ngezi. mwenyezi mungu amrehemu. Nimepata taarifa kwamba mpiga drums Tengeneza yuko mwanza na bendi ya jambo stars. Nitafanya bidii nitume mtu afanye nae mahojiano na kisha nitakutumia baada ya kumaliza mfungo

    ReplyDelete
  8. Nitashukuru sana msalimie Tengeneza, pia natafuta funding nije mwanza kwa wiki mbili ili nikusanye dat za muziki upande huo. Bendi kama Super Veya, Mara Jazz, Musoma Jazz na kadhalika ni muhimu kuwekwa katika kumbukumbu

    ReplyDelete
  9. Anonymous17:44

    Mkuu/Wakuu,

    1: Ni kweli Upanga ina mchango mkubwa katika muziki wa dansi:

    Mitaa hiyo ya Soulville ndipo pia alipotokea yule Bassist maarufu Andy Swebe na mdogo wake Mpeli na Guitarist Martin Cox Ubwe pia ndiyo mitaa aliyotokea in 1980s a seasonal bassist Jerome Kiango.

    Ni hiyo hiyo mitaa ya Soulville ndipo alipoibukia mwanamuziki maarufu wa Reggae Marehemu Justin Kalikawe.

    Safu yao ni ndefu.
    ---------------------------------------
    Mkuu/Wakuu,

    2: Banchikicha ilishinda tuzo ya Bendi Bora mwaka 1973. Je unaweza kutupa safu ya washindi wa tuzo hizo na nyimbo zilizoshindanishwa?

    Wewe binafsi, Mh Balozi Tsere, Mh Balozi Maharage,Salim Willis, James Mpungu, Freddy Macha na wadau wengine wa blog hii wanaweza kukumbuka na kusaidia kuiweka hiyo safu ya washindi wa Tuzo ya Bendi Bora ya mwaka 1973.

    Ninachokokotoa na kuchokonoa hapa ni kuona jinsi gani sisi wenyewe wanamuziki tulianza kufanyiana mizengwe ya kukatishana tamaa hata kabla bado hazijaja hizi tuzo za muziki za siku hizi.

    Asante.

    ReplyDelete
  10. Anonymous00:17

    Mkuu/Wakuu,

    Kwa kuongezea tu, kweli Soulville ni hazina ya muziki kwa sababu hata mwanamuziki wa kike aliye juu katika anga ya muziki Carola Kinasha alitokea mitaa hiyo.

    Mizoa ya wanamuzki tokea Soulville haikuishia miaka ya 60, 70, na 80. Mizao ya wanamuziki toka Soulville imeendelea hadi miaka ya 90 walipokuja East Coast na miaka ya 2000 ambapo mwanamuziki wa kizazi kipya Saganda aliyetoa hit kiboko ya Bongofleva ya Chuwa Naye Alikuwepo pia naye ametokea mitaa hiyo ya Soulville.

    Hata Babu Njenje ana kaasili au uhusiano fulani na mitaa ya Soulville.

    Hata Biribi Disco ambalo ni chimbuko la Clouds Media Group nao pia ni mzao wa Soulville. + Madj kadhaa akiwemo Emperor na Bon Luv nao pia ni mizao ya mitaa ya Soulville.

    ---------------------------------------

    Swali: Ni sababu zipi zilizochangia mitaa ya Soulville kutoa wanamuziki wengi tena mahiri?

    ReplyDelete
  11. Moja ya sababu kubwa ni ushiriki wa wazazi katika kuendeleza vipaji vya watoto wao. Wazazi walinunua vyombo, kama tulivyoona kwa Groove Makers mazoezi yalikuwa nyumbani, kwa akina Jengo, na Maharage, na ndivyo ilivyokuwa kwa familia nyingine kama akina Swebe, ambapo Mzee Brown Swebe pia alikuwa mpiga gitaa aliyewahi kunihadithia kuwa aliwahi kumfundisha Mh Samuel Sitta kupiga gitaa kwa malipo fulani enzi hizo Tabora School. Sura ya Upanga ilitokea pia Chang'ombe,na dhani kuna uhusiano pia wa hali ya maisha kati ya wakazi wa Upanga na Chang'ombe wakati huo. Wazazi walidiriki hata kuwatafutia kazi wanamuziki ambao watoto wao waliwahitaji kama ilivyokuwa kwa Jeff Funky.

    ReplyDelete
  12. Anonymous10:49

    Mkuu,

    Asante sana kwa majibu mazuri. Ni kweli kabisa kuna uhusiano wa hali ya maisha kati ya wakaziwa Upanga na Chang'ombe wakati huo. Kwa kuongezea kwenye majibu yako:

    Ni kweli kwamba wazazi wa watoto wa Upanga waliweza kuwanunulia watoto wao vyombo vya muziki na rekodi. Wazazi hao pia waliuona muziki kama shughuli nzuri kwa vijana wao ama kwa kujifurahisha, kupanua wigo wa ubunifu au kama ajira.

    Wazazi wa maeneo ya Upanga wengi walikuwa na vipato vizuri na waliopata kusoma, kuona na kusikia mengi mengine (exposure)hivyo kuwa na wigo mkubwa wa uelewa. Ambapo baadhi ya wazazi walipata kusoma muziki walipokuwa mashuleni au kuwahi kuwa wanamuziki. Hali hii iliwapelekea wazazi kuwaruhusu watoto wao kuwa wanamuziki au kujishughulisha na muziki kama hobby.

    Tatu, (a)ni mazingira waliyokuwa wanaishi hawa vijana wa Soulville. Wengi walijikuta katika mazingira yaliyokuwa yamezingirwa na muziki na hivyo kuwa rahisi kuambukizwa muziki. (b)Upanga ilikuwa ni makazi yao ya kudumu ambapo aidha wazazi wao walikuwa wamejenga au kupanga kwenye makazi yao. Kwa kuishi pamoja na kusoma pamoja kwenye mashule kulileta mshikamano mkubwa miongoni mwa vijana wa Soulville. Hapa linaweza kuja swali kwa nini Oyster Bay haikuwa kama Upanga? Jibu lake tunaweza kusaidiana kulijibu sote, ok!?

    ---------------------------------------
    Mkuu,

    Naomba tuendeleze series hii ya maeneo na wanamuziki tukiendelea kuelekea Chang'ombe, Kurasini, na Temeke. Halafu Magomeni hususani Mapipa na Mikumi. Pia Kariakoo hadi Jangwani. Na Baadaye Mji Kasoro Bahari, Morogoro hususani mitaa ya Nunge, Konga, Kingo, hadi Mlapakolo.

    ---------------------------------------
    Bado tunabaki na lile swali la Tuzo ya
    Bendi Bora ya Mwaka 1973 kuhusu orodha ya washindi na nyimbo zao. Wadau naomba tuilete hapa hiyo orodha ya washindi na nyimbo zao kwa mijadala zaidi.

    Asante sana na weekend njema.

    ReplyDelete
  13. Anonymous12:43

    Hizi picha zimenipa nostagia kali sana. Nilisikia mahali kuwa Herbert Lukindo alifariki, ni kweli au jamaa alim-cofuse na herbert mwingine? Mi nilikuwa Upanga 1970's.

    ReplyDelete
  14. Anonymous15:35

    Balozi JK,

    Sijui nimekosea huyu Jeff mbona anafanana yule mpiga drums was Mlimani Park?

    -Muarubaini

    ReplyDelete
  15. Anon 02;43 HERBERT ALIFARIKI MWAKA 2000, Anon 05:35 Huyo ndie Jeff wa Mlimani Park na ndie alikuwa Funky drummer wa Groovemakers

    ReplyDelete
  16. Anon 02;43 HERBERT ALIFARIKI MWAKA 2000, Anon 05:35 Huyo ndie Jeff wa Mlimani Park na ndie alikuwa Funky drummer wa Groovemakers

    ReplyDelete
  17. Sam Mnkande04:07

    JK,
    Tusisahau contribution ya sehemu ya Magomeni kwenye histiria ya vijana wa musiki enzi hinzo. Flaming Stars,Sparks & Comets,Black Beatles,Tonics wote walikuwa na maskini yao Magomeni. Pia vijana wengi was Mission Quarters( Misheni Kota)walikuwa ni members was Sparks,Rifters,Dynamites,Sunburst etc etc

    And keep it it coming brother JK, I luv this blog

    ReplyDelete
  18. Anonymous11:26

    Umenikumbusha mbali: just wondering Sajula na Ali Mwarabu wako wapi???? Sijawaona zaidi ya miaka takriban 20!!! Fredo.

    ReplyDelete
  19. Habari nzuri...je Joseph Jengo yuko wapi siku hizi? Wakati akisoma Ilboru-(Arusha) alikuwa kaka yetu mkubwa na tulimpa jina la "mfalme wa Mabitoz."
    Leo itakuwa kama mfalme wa "Masharobaro"
    Nikiwa kidato cha kwanza (yeye ndo anamaliza cha nne 1969) tulikuwa tunamwiga mpaka vile anavyotembea. Alikuwa na kitu "staili"...

    ReplyDelete

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...