YOUTUBE PLAYLIST

Wednesday, April 7, 2010

Taarab inakwenda wapi?



Muziki wa Taarab umekuwa na historia ya kukua na kubadilika kama muziki wa aina nyingine. Lakini nimejitahidi kusikiliza muziki huu wa sasa ambao bado unatangazwa kama muziki wa Taarabu naanza kupata taabu kukubali kama kweli kinachoendelea sasa ni Taarab. Upigaji wake sasa unaanza kusisitiza sana uchezaji, ni ukweli usiopingika kuwa sasa sebene ya Kikongo imeanza kutawala katika tungo mpya za taarabu. Uchezaji wake ambao unaleta utata katika maadili ya Watanzania wengi. Naomba wapenzi wa Taarab na wanaoona wanaifahamu Taarab hii ya sasa ya Alamba alamba watumegee nini hasa kinachoendelea? Juzi nimepata barua pepe kutoka Mtanzania mwenzangu mmoja alioko USA, akilalamika kuwa walitangaziwa kuwa kuna onyesho la Taarab na alipofika huko akakuta mwimbaji mmoja maarufu wa Taarab akiwa na CD yake na kufanya play back ta Taarab, kwa kifupi hakustahimili maana aliona kapunjwa mno. Haya ndugu zangu ukumbi ni wenu

10 comments:

  1. Patrick Tsere21:17

    Nakubaliana na wewe kuwa muziki wa sasa wa taarab siyo ile ya akina Shakila, Juma Balo, Asmaha na wengineo. Hii ya sasa ni rhumba in disguise ambayo inaitwa taarab. Halafu sema inapendwa zaidi na imekaa kike zaidi. Kwa sababu ryhthim yake inaendana na mipasho na masimango ya kike. As a man siwezi kuchukua patna nikacheza nao kwa vile unakuwa umeshabiana na wanawake. In short muziki wa taarab ni wa kijinsia zaidi ya chochote kile.

    Zamani miaka ya nyuma actually ya sitini hadi sabini yale maeneo ya Kariakoo na mitaa ya Jangwani karibu na Yanga kila Jumamosi usiku ilikuwa kawaida kuanzia saa tatu usiku mitaa hufungwa halafu muziki wa chakacha ulikuwa unachezwa. Wachezaji hawakuwa wengine zaidi ya mashoga. Watazamaji wakubwa walikuwa ni watu wa aina zote. Wanaume zaidi na wanawake wachache. Some of us we went there out of sheer curiosity. Siyo siri nilikuwa napata kichefuchefu.

    ReplyDelete
  2. Mkereketwa09:34

    Ni kweli muelekeo wa Taarab unatia mashaka.-Muziki wa Taarab ilikuwa inautambulisho wa aina nyingi sana,-kuanzia vyombo vyake pamoja na mavazi,-na pia watu waliokuwa wanaudhuria honyesho lenyewe.
    Chakushangaza siku hizi kunamwibaji wa Kiume anasuka nywele,-sasa mimi naona uhalisia wa Taraab unapotea kabisa japokuwa wenyewe wanasema eti ni Modern Taarab.
    mimi sioni kama kutoa uhalisia wa kitu ndio kunafanya iwe ni kisasa.-Tulikuwa tunaenda kwenye taarab kipindi hicho,tunasikia nyimbo za mapenzi na mafundisho zikiwa katika mashairi mazuri sanaa!!!.-Nyimbo za leo hii ni vijembe kwa kwenda mbele na maneno yasiojificha kwa hata watoto wanaelewa nini kusudio la mwimbaji.
    Najuwa watakataa kubadilika,-kama kunachombo kinaweza kuwashauri au kuwakemea basi ifanyike hivyo.Huko tuendako ni hatari zaidi.

    ReplyDelete
  3. Ukweli ni kuwa "modern Taarab" ilikuwa utambulisho wa muziki wa Taarab walipoanza kutumia kinanda kimoja chenye milio mingi(synthesizer),na hii ilitokea hsa baada ya vikundi kuanza kualikwa Uarabuni na jivyo ili kupunguza gharama wakaanza kutumia drum za kwenye kinanda na kinanda peke yake. Kama ilivyokuwa mwanzo kwa East African Melody. Hiki kinachofanyika sasa kinahitaji jina jipya si Taarab, maana hata mtaani kinaitwa Rusha Roho ......

    ReplyDelete
  4. nakunukuu "Muziki wa Taarab umekuwa na historia ya kukua na kubadilika kama muziki wa aina nyingine"

    nakunukuu tena "Hiki kinachofanyika sasa kinahitaji jina jipya si Taarab, maana hata mtaani kinaitwa Rusha Roho"

    Ni Rusha Roho ndio jina husika. hao wanaorushana roho keshawasema mheshimiwa Balozi. nadhani ni nature tu inachukua mkondo wake. Kinachokosewa ni kuiita 'taarab'. ukisikiliza vionjo vya mzee yusuph it's pure sebene.

    mathalani tutazame muziki wa kikongo ulivyopitia awamu kadhaa kuanzia akina dk niko mpaka sasa akina fali ipupa (naomba siku moja utupe somo la hizi phases za muziki wa kikongo. mambo ya kavasha,sokous, sijui nini, ndombolo nakadhalika )

    ReplyDelete
  5. Waheshimiwa, nakubaliana nanyi kabisa kuwa muziki huu sio taarabu. Hii ni aina mpya ya muziki iliyo kati ya taarabu na rumba. Kwa kuwa inaonekana ina wapenzi wengi, ambao wengi wao si wale wapenzi wa taarabu asilia, basi tuukubali na kuupa jina.
    Ijulikane kwamba hapa nchini kuna muziki wa bongo fleva, muziki wa dansi, muziki wa mipisho/rusha roho (au jina lolote), muziki wa taarabu, na muziki wa kwaya.

    Nakumbuka kundi moja kubwa la burudani hapa nchini lenye makundi ya taarabu, dansi, kwaya, nk. ndani yake, nililipoanza kufanya maonyesho ya makundi yake kwa pamoja na kuwatumia wanamuziki wa dansi ndani ya taarabu, ndio masebene yalipoingizwa kwenye taarabu. Muziki ukapata ladha, ukajipatia wapenzi, na sasa kila mtu ameiga.
    Kwa hiyo basi tuukubali kama sehemu ya muziki wetu lakini isiitwe taarabu. Wale wanamuziki wa taarabu asilia waendelee kutupigia taarabu la mwambao.
    Ila sasa suala la huo uchezaji ndani ya huu muziki mpya, ambao unakinzana na maadili, hapo lazima pakemewe.

    ReplyDelete
  6. Anonymous16:31

    Japo muziki unabadilika na wakati, taarabu ya siku hizi si taarabu, nimepeleleza video za youtube (kwani sipo nyumbani) inasikitisha.

    Wapi Malindi? (ikhwani) hapo ndio taarabu iliko - mfano ule wimbo wa Hidaya, kwanza ala dakika 5, shairi na mlengwa anapata ujumbe wake, ikesha wanachangamsha mwishoni. Hiyo ndiyo taarabu.

    ReplyDelete
  7. Anonymous13:38

    Mkuu,

    Mada hii tuliwahi kuijadili siku za nyuma na maoni yangu yalikuwa haya:

    Mkuu,

    Tunaweza kukubaliana mabadiliko katika kila kitu kwamba hata binadamu ana mabadiliko ya marika yaani utoto, ujana, umakamo, uzee hatimaye ukongwe. Mabadiliko haya ya kimaumbile hayamfanyi mtu/binadam abadilike kuwa ngedere. Lakini si vyema kumfananisha au kughafilisha wasifu wa mtu/mwanadamu na ngedere. Kwa sababu mtu/mwanadamu asilani atabaki kuwa mtu/mwanadamu hali kadhalika ngedere asilani atabaki kuwa ngedere.

    Taarab ni taarab na huu muziki mpya ambao bado haujapata jina kamili iwe ni mipasho au rusha roho utabakia kuwa rusha roho au mipasho na asilani huwezi kuwa taarab.

    Kuhusu maswali uliyouliza yanaweza kujibiwa na tafiti nyingi kuhusu muziki wa Taarab zilizoandikwa na kurekodiwa na taasisi na watafiti mahiri wa muziki(Outstanding Musicologists)kama vile kina Said A.M. Khamis, Werner Graebner, Mohamed El-Mohammady Rizk, K.M. Askew, Global Music Centre na vyuo vikuu mbali mbali hususani vya Ulaya na Marekani.

    ZAIDI: Said A.M. Khamis anapagawishwa na mabadiliko katika nidhamu ya muziki wa Taarab - Wondering About Change: The Taarab Lyric and Global Openness.Nordic journal of African Studies 11(2): 198-205 (2002). Said A.M. Khamis* University of Bayreuth, Germany.
    (http://www.njas.helsinki.fi/pdf-files/vol11num2/khamis2.pdf).
    Nadhani Bwana Said A.M. Khamis tupo kwenye upande mmoja wa mtazamo kwamba hii iliyokuja sasa ni mipasho au rusha roho ni aina nyingine ya muziki na siyo taarab.

    February 5, 2010 7:50 AM

    ReplyDelete
  8. Anonymous13:54

    Mkuu,

    Kipimo changu cha taarab halisi kinaanzia kwenye tungo (Ushairi wenye vina na maudhui au hata kama ni bashrafu ni bashrafu iliyopigika katika mtindo na ala za okestra ya taarab). Tofauti nyingine imelalia kwenye muziki wa Taarabu: kimuziki (ala zitumikazo, mtindo wa muziki unaopigwa kimapigo (Rhythm), ghani (melody), na mwafaka (harmony).

    Halafu linakuja suala la nidhamu ya muziki wa taarab: Mtindo wa utumbuizaji wa muziki wa taarab (presentation style) kuanzia wajihi wa wanamuziki (performers personalities), muundo ukaaji jukwaani (stage arrangement), mtindo wa jukwaani na majukwaa (stage setting and arrangement), mazingira ya utumbuizaji (performance aura), wahudhuriaji na aina wahudhuriaji onyesho (audience and audience target/ audience demography). vigezo hivyo nilivyovitaja na vinginevyo ndivyo vinavyoitofautisha taara na chakacha au na mipasho au rusha roho. Kabla ya mipasho na rusha roho palikuwepo chakacha lakini haikuwahi kutokea kuchanganya taarab na chakacha. Au siyo?

    ReplyDelete
  9. Anonymous13:54

    Mkuu,

    Baada ya kutuma yale maoni ya mwanzo kwenye ule mjadala ukanijibu, nanukuu:

    ..Ni Kweli Mkuu wengi wanapagaishwa na mabadiliko yanayoendelea ambayo yanatokana na sababu nying, lakini pia ni vizuri kujiuliza kama taarab "halisi" ni ipi ambayo ndicho kipimo cha taarabu..

    Nikakujibu

    ReplyDelete
  10. Anonymous15:26

    Mkuu,

    Kipimo cha kuwapima hawa wana "modern taarab" ni kuwatafutia nafasi kwenye Tamasha la Sauti za Busara au kumpata promota awapeleke Zanzibar wakatumbuize na mitindo yao hiyo hiyo. Nina hakika watafukuzwa kama nguruwe aliyeingia msikitini!

    ReplyDelete

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...