YOUTUBE PLAYLIST

Saturday, April 17, 2010

Msondo Ngoma


Msondo ngoma wana kila haki ya kujiiita Baba ya muziki. Bendi hii ilianza mwaka 1964,kama NUTA Jazz na imekuwa na mtindo wa Msondo miaka yote na imekuwa juu miaka yote. Nani anaweza kujipima na Msondo. Pichani Mzee Abel Balthazal akiwa anapiga gitaa, Mzee Mnenge kwenye saxaphone, jamani majina ya wengine tafadhali.

1 comment:

  1. Anonymous01:34

    Mkuu,

    Hawa jamaa walikuwa kiboko tena kiboko haswa. Nasema walikuwa kiboko kwa kuwafananisha NUTA na Msondo ya sasa. NUTA walikuwa wanapiga local stuff inayofanana na local atmosphere.

    Miaka kadhaa iliyopita jamaa yangu mmoja alibahatika kununua CD ya NUTA Jazz kwenye maduka ya duty free Jomo Kenyatta International Airport, Nairobi, Kenya. Akanipasia hiyo CD. Siku hiyo niliisikiliza ile CD kwa kuirudia rudia haswa nyimbo za Msondo Namba 3 na Tunawapongeza Wakulima Wetu.

    Baadaye nikanunua CD ya The Best of Msondo iliyotoka miaka ya karibuni. Kuna fofauti kati ya NUTA na Msondo wa sasa. Kimuziki wanaweza kufanana kidogo lakini kimaudhui NUTA walikuwa na nyimbo zenye ujumbe mzuri sana. Halafu Msondo wa sasa ulivyokubali kumezwa na uchezaji show uliovuma siku hizi umechusha ladha ya Msondo kwa kiasi fulani.

    Nakumbuka kuna kituko kimoja kilifanywa na washabiki wa Msondo pale Kariakoo sokoni. Huwa nikikumbuka nacheka sana. Ilikuwa katika kupokea mbio za Mwenge. Kuna ofisa bila kujua akawaalika Msondo waje kuburudisha. Msondo wakaja na mashabiki wao na ukizungumzia maeneo ya Kariakoo huko ndipo walipo mashabiki wa Msondo haswa.

    Basi Mwenge ukaja ukatua salama kabisa. Msondo wakaanza kupiga. Mashabiki wakaanza kucheza. Muziki ukawa unazidi kukolea. Mashabiki nao wakawa wanakolea. Basi shabiki mmoja akauchomoa Mwenge kwenye stendi yake akaanza kucheza nao. Polisi wakamkimbilia kutaka kumnyang'anya. Yule jamaa akaupasia kwa shabiki mwingine. Mara mashabiki wakauzunguka Mwenge. Polisi wakaanza kuwapiga virungu. Mashabiki wakawa wanapigwa virungu lakini Mwenge hawauachii. Marehemu Mama Benadeta Kunambi kuona hali inazidi kuwa tata akaamuru Msondo wazime muziki. Msondo wakazima muziki. AArrgghhh!! Akawa amefanya kosa kubwa sana. Mashabiki wakaanza kufanya fujo zaidi na kuanza kuondoka na Mwenge toka eneo la tukio. Polisi wakazidisha ukali na kusaidiwa na wanausalama wengine wakafanikiwa kuuokoa Mwenge na kuurudisha kwenye stendi yake na kuuwekea guard maalumu. Msondo hawakupewa tena nafasi ya kupiga. Sherehe zikaisha salama baada ya hapo.

    Kati ya mwaka 1988 na 1991 ndiyo ilikuwa mara zangu za mwisho kuhudhuria maonesho ya Msondo.

    ReplyDelete

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...