YOUTUBE PLAYLIST

Wednesday, April 28, 2010

Midomo ya Bata

Upigaji wa vyombo vya kupuliza umepungua sana katika bendi zetu hapa Tanzania. Kumekuwa na maelezo kuwa tatizo hili limetokana na kuanza kutumika kwa Keyboards au vinanda aina ya synthesizer. Vinanda hivi vina uwezo wa kutoa milio mbalimbali ikiwemo ya vyombo vya kupuliza kama trumpet na saxophone. Lakini mi nadhani ni maendeleo ya mtiririko wa uigaji wa nini kinachotokea Kongo. Ni jambo lisilopingika kuwa kwa miaka mingi sana bendi nyingi zimekuwa zikiiga kile kinachotokea Kongo. Mara nyingine hata kufikia kuiga nyimbo nzima kutoka kwa bendi za Kongo. Na mara nyingine kuiga mfumo wa muziki kutoka huko. Kwa misingi hiyo, bendi zetu nyingi ziliamua kuacha kupiga vyombo vya kupuliza mara baada ya kuona bendi nyingi za Kongo zikiacha kutumia vyombo hivyo.
Lakini kwa ukweli kabisa vyombo vya upulizaji vina raha yake na utamu wake. Wapigaji wake hutengeneza step zao za kucheza na hupanga sauti za kupishana kati ya trumpet na saxaphone na huongeza raha sana katika muziki. Kwa sasa ni bendi chache kama vile DDC Mlimani Park, OTTU, Vijana Jazz, MAK Band, African Beat ndio wanaendeleza upigaji wa vyombo vya kupuliza.

11 comments:

  1. Anonymous10:55

    John!
    Kwa hili ulilo sema ni kweli. Kwangu mimi naona katika zama hizi za muziki wa kileo vijana wetu wamekosa ujasiri wa kuzitumia akili zao kufanya maamuzi mazito ya kuuboresha muziki wetu. Band nyingi za vijana walio zaliwa miaka ya 70 na kuendelea wamekuwa wakipenda mambo rahisi rahisi. Upulizaji wa sax ama trumpet unataka nidhamu na ujasiri wa kujifunza muziki wa kusoma na kuandika. Nimepata kumuona rashid pembe akimpa mpiga gita wake wa solo TUNE toka kwenye sax. Ni jambo linalotaka ujasiri na uhakika na uwe feet maana unatakiwa upulize note kwenye kiwango chake.
    Band kama msondo, DDC Mlimani, na mabendiya jeshi yamekuwa yakifanikiwa sana kwa kuwa na upekee katika miziki yao.
    Utashi wa kuamua ni aina gani ya muziki unaotakiwa kufanyika ninaamini bado ni haki ya wanaomiliki bend kwa mfano bendi ya kilimanjaro wana njenje. Sehemu kubwa ya muziki wao unatawaliwa na vinanda na hasa pale inapotakiwa kufanyika blowing ama ya sax ama trumpet Waziri Ally huwa ni mjanja sana na ana utundu mkubwa wa kujua ama kukifanya kinanda chake kitoe ladha halisi ya chombo husika. Kwa hilo wamefanikiwa ila kwa wanaopenda kusikiliza kwa umakini muziki wao watagundua kuna upungufu fulani. Nimepata bahati ya kuona kupitia DVD show ya wana njenje waliofanya arusha wakati wa mkutano wa sulivan. Aina ya muziki wa classic waliotumbuiza pale ilikuwa sii rahisi kubaini kwamba sax ilikuwa inapigwa kwa synthesizer ama violin utadhani mpigaji alikuwa back stage.
    sasa changa moto kwenu je mnampango wa kuwa na mpiga sax halisi katika jukwaa la kilimanjaro band?

    ReplyDelete
  2. Anonymous17:19

    MIDOMO YA BATA ILITUPA MSISIMKO
    Kweli kabisa kulikuwa hakuna mziki wenye raha kuusikiliza kama uliopigwa na vyombo vya kupulizwa,nikiwa mdogo saana mwishoni 69 mama yangu alikuwa na gramafoni ya kuzungurusha kwa mkono ili ipambe moto kutupa mziki wa santuri za wapigaji maarufu wakati ule kina mbaraka Mwinshehe na wengineo kulikuwepo na vyombo vya kupulizwa kabla hata wakongo hawajaivamia Tanzania na walipoivamia mwanzoni 70`s wengi hawakutaka kuondoka tena Mlimani Park ilikuwa masikani kwa wakongo wengi,nimebahatika marafiki zangu wakongo wa miaka ile sasa tupo pamoja huku scandinavien kama mtamkumbuka Nguza na Kalonga vyombo vya kupuliza vilikuwa na msisimko wa kipekee na ulirahisisha uchezaji au usakataji wa rumba kwa vijana naa wazee hata Simba wa vita mzee Kawawa alikuwa mgeni wa heshima kila week end.

    EDDY KWELI UNA KUMBUKUMBU:
    ukumbi wa New Palace sasa mbowe,tuliwasiri pamoja mimi na Rafael Sabuni wa Rifters tukitokea magomeni mikumi,Flamming Stars walipiga nyimbo nne tuu, Rifters waliendelea pamoja na Disco mpaka usiku wa manane.
    Flamming Stars walikuwa na ratiba ya kupiga usiku pale zamani tulipaita "Ettiens Hotel" karibu na "Sew view hotel" wakatoweka mapema.
    Mickey Jones
    Denmark

    EDDY said:
    Nakumbuka 1969, nilipokuwa form iv nilikwenda kwenye boogie moja ya Rifters either Splendid (sasa kuna jengo la extelecoms) au New Palace (baadaye Mbowe hotel). Wakati wa mapumziko Flaming Stars walipewa "lift" wakapiga nyimbo chache including ya Beatles. Nalini wimbo ambao naukumbuka mpaka leo (baada ya miaka 40) ni "amen" wa otis reding uliowafany watu wawe mesmesized!!!Eddy.

    ReplyDelete
  3. Anonymous19:06

    BW.KITIME, NAFURAHI UMELILETA HILI SUALA LA KUPOTEA KWA SAFU YA VYOMBO VYA KUPULIZA(WIND INSTRUMENTS)KATIKA BENDI ZETU. MBALI NA SABABU ULIZOTOA, MI NADHANI SABABU NYINGINE NI KUBANA MATUMIZI! KAMA MLIO WA VYOMBO HIVYO UMEWEZA KUIGIZWA NA SYNTHESIZER NA WATU WAKAFURAHI, THEN NAFUU YA MCHUKUZI! SABABU NYINGINE NI HII GENERATION YA SASA YA WAENDAO MADANSINI AU WAPENZI WA MUZIKI, WENGI WAMEKUTA VYOMBO HIVI VIMEKWISHA POTEAPOTEA, NA UKWELI NI KWAMBA KIZAZI HIKI WALA HAKIJALI UBORA WA MUZIKI NA UPIGAJI WA VYOMBO, KINAJALI KELELE ZOZOTE ZINAZOITWA MUZIKI! HATA ATHMANI HALFANI ANGEGHANI YALE MASHAIRI YAKE MAARUFU(ENZI ZA RTD) WANGECHEZA TU! SABABU NYINGINE NADHANI NI WANAMUZIKI WENYEWE KUKATA TAMAA! SIDHANI KAMA KUNA WAPIGAJI WENGI WA VYOMBO HIVYO HATA KAMA BENDI ZILIZOKO ZINGEWAHITAJI! NASEMA WAPIGAJI NA SIYO WABABAISHAJI. UPIGAJI WA VYOMBO VYA UPEPO UNAHITAJI UFUNDI WA HALI YA JUU NA SIYO LIPUA LIPUA!NADIRIKI KUSEMA KUWA HATA ENZI ZILE AMBAZO ALMOST KILA BENDI ILIKUWA NA SAFU YA SAX NA TRUMPETS, NI WAPULIZAJI WACHACHE SANA AMBAO WALIMILIKI IPASAVYO UPIGAJI WA VYOMBO HIVYO, WENGI WALIKUWA WABABAISHAJI! UKITAKA MAJINA NITAKWAMBIA...WATAALAM NA WABABAISHAJI..

    ReplyDelete
  4. Anonymous20:44

    mimi nawakumbuka Twahir Mohammed wa Masantula Ngoma Ya Mpwita na Hatibu Iteitei, hawa jamaa pamoja miaka hiyo ya mwishoni ya sabini nilikuwa sijafikishs umri wa miaka 15, lakini ndio nawafagilia kwa sana.
    mdau
    mtaa wa lincoln.

    ReplyDelete
  5. Anonymous13:25

    Ni kweli kabisa Bwana Kitime. Hili la kuiga muziki wa Congo linafifisha muziki wetu. Nilikuwa shabiki mkubwa wa muziki wa Congo hapo nyuma lakini sasa sioni cha kushabikia kwa kuwa muziki wa nchi hiyo umepoteza kabisa mwelekeo. Hakuna anaeweza kupinga ukweli kuwa muziki wa sasa wa DRC hauna mvuto hasa kwetu sisi Watanzania ambao tunafuatilia upangaji wa vyombo na sauti za waimbaji kwa kuwa wengi wengu hatuelewi Kilingala. Kuna siku nilisikiliza albamu ya Fally Ipupa na nikashindwa kuelewa kwa nini mwanamuziki huyu ana sifa kemkem hadi Tanzania. Kwanza inaelekea ameamua kumuiga Kofi Olomide kwa asilimia mia moja. Halafu muziki wake hauna mpangilio mzuri. Nina hakika hata mtu ukisilikiza wimbo wa Fally Ipupa mara ngapi hutaweza kuuimba au kukumbuka vyombo vilipigwaje kama ilivyokuwa enzi za soukous na cavacha (kavasha). Kwa bahati mbaya sana hii ndio aina ya muziki inayopigwa na wanamuziki wengi wa Congo hivi sasa. Hawa jamaa wamepotoka na hakuna haja ya wanamuziki wetu kuwaiga.

    ReplyDelete
  6. Anonymous19:31

    jumapili ya leo, saa kumi na mbili za Tanzania nasikiliza voa music mix, ebwanaeee kuna midomo ya bata huko balaaa, mulizeni sunday shomari lazima hatakuwa anakijua hicho kipindi, dah wenzetu USA bado wanaitumia kwenye jazz maana ni live jamaa wanashangilia sana, wamenikumbiusha club raha leo show, tembelea j2 maana natumia laptop yangu kipindi kama sikosei mountain stage on Mpo,filimbi zirudishwe primary school na ikiwezekana hadi secondary, hizi ni salamu pia kwa wajomba, maana huku kuna magitaa na matrampet na kuimba hadi raha, uondo na ubunifu wa ajabu

    ReplyDelete
  7. Perez00:27

    Eee Bwana Kitime umenikumbusha mbali sana.
    Hebu sikiliza Saxaphone na trumpets zinavyojibizana katika wimbo wa Kimulimuli - HAIFAI SI VIZURI
    Yaani we acha tu.
    Nani aliyepiga saxaphone kwenye wimbo huo?

    "...Leo tasema sana, na majirani wasikie, unanifanya niwe, mzembe kwa nini, kama maendeleo na mi ninayapenda..."
    ZAKARIA TENDAWEMA huyo mwanangu!
    Hivi bado yuko hai? Yuko wapi?

    Pia nani alipiga Rythm kwenye wimbo huo?

    ReplyDelete
  8. ZAKARIA TENDAWENA Jina lake halisi alikuwa Zakaria Daniel, Tendawema alipewa kutokana nawimbo aliotunga wajkati yuko Shinyanga Jazz ulioitwa Tenda wema nenda zako.Mzee Zacharia aamekwisha fariki siku nyingi sana.

    ReplyDelete
  9. Perez19:46

    Ok. Daah! Mungu amuweke pema peponi.

    Nani alipiga saxaphone na rythm kwenye wimbo huo?

    Solo nadhani alikuwa mwenye Muungwana Zahir Ali wa Zoro

    ReplyDelete
  10. Anonymous20:03

    Midomo ya bata katika Orch. Safari Sound - Masantula ya kina King Kiki na kibao 'Kata Tamaa (Mama Kachiki usikate tamaa tuchunge watoto) tembelee webusaiti ya http://music.ntwiga.net/?p=515 ufungue Orchestre Safari Sound with King Kiki

    Hapo ndipo unapotambua safu ya michango ya yapulizaji midomo ya bata ktk muziki wa Tanzania wakiwamo kina Twahir.

    Mdau
    BabaJunior

    ReplyDelete
  11. Anonymous23:14

    Haya wadau sikilizeni midomo ya bata ndani ya wimbo "Rufaa Ya Kifo' na Marijani Rajabu midomo ya bata ikienda sambamba na sauti tamu za Marijani na vyombo kwa ujumla, ingia ktk kiungo hiki http://cowbell.fm/artist/Marijani+Rajabu+%2526+Orchestra+Dar+International

    Mdau
    BabaJunior

    ReplyDelete

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...