YOUTUBE PLAYLIST

Thursday, February 4, 2010


John Mwenda Bosco,ni kati ya wanamuziki ambao w alileta mabadiliko mengi katika muziki wa Afrika ya Mashariki. Muziki wake unapendwa sana mpaka leo. Je unajua alikuwa nani?

Peter Colmore ambaye alifanya kazi kwa karibu sana na Mzee Ally Sykes ambaye kwa bahati mbaya hajatunukiwa nafasi anayostahili katika historia ya muziki wa Tanzania ndie aliye mleta John Mwenda Bosco Afrika ya Mashariki. Bosco alitambulishwa kwa Colmore kupitia Edward Masengo,mwanamuziki mwingine toka Kongo ambae alikuwa maarufu sana na hasa kutokana na matangazo ya biashara yaliyokuwa yanafanywa na kampuni ya Colmore na Mzee Sykes, Colmore akalazimika kumfuata Bosco hadi Congo ambapo serikali ya Kibergiji wakati huo ilimlazimisha alipe Faranga 30,000 kama pesa ya kuhakikisha atamrudisha Bosco kwao. Bosco alikuwa tayari anajulikana sana Afrika ya Mashariki kupitia santuri zake. Kati ya nyimbo maarufu za Bosco ni ule wimbo wa ala tupu ambao hutumika na Radio Tanzania kuashiria kuanza kwa kipindi cha zilipendwa.

8 comments:

  1. Patrick Tsere12:58

    John mbona umemsahau Omari Kungubaya? Mara ya mwisho nilikutana naye maeneo ya Luguruni na KIbaha akiwa na gita lake. HUpiga kwenye mabar halafu wanywaji humpa vijisenti ili angalau aishi.Very challenging I must say. Unaukumbuka ule wimbo wa kipindi cha wagonjwa.Ndiye alieutunga. Kungubaya zamani alipiga muziki marehemu Salum Abdallah na Cuban Marimba Band.

    ReplyDelete
  2. Sijamsahau Mzee Kungubaya nia ilikuwa kueleza tatizo la kutokuthaminiwa kwa Mzee Frank. Tanzania kulikuwa na wengi wenye muziki aina ya John Mwenda Bosco na bila kumsahau Mzee John Ondolo Chacha na wimbo wake maarufu Kilimanjaro. Ntauongelea muda ukifika

    ReplyDelete
  3. Patrick Tsere16:11

    Hongera kwa kuwa na blog kama hii. Unajua upo umuhimu wa kuweka kumbukumbu za wanamuziki wakongwe na nyimbo zao. Hasa kwa faida yao na kwa ajili ya maslahi ya copyrights. Bila ya hivyo kijana wa sasa anaweza akaja na nyimbo ambazo kumbe 'kaiba' beats halafu anajifanya yuko original.

    Siyo siri binafsi sifurahishwi hata kidogo na baadhi ya gospel singers ambao wanaiga beats za nyimbo za South Africa mithili ya jive tulizokuwa tukiimba shule, na wanajifanya ni zao na kutualika kuwa wageni rasmi ati kwenye uzinduzi wa album. No no no. Huu ni utamaduni wa kitapeli na plagiarism. Maana wanadandia beats za wenzao. That is plagiarism. Lazima ipigwe vita na COSOTA.

    ReplyDelete
  4. Anonymous17:23

    Wimbo ule maarufu unaitwa Masanga au Masanga Djiya! Umepata kuigizwa na wanamuziki na bendi kadhaa ulimwenguni akiwemo Sir William Walton na pia kundi la Rhumbanella Band. Niliwahi kumuomba Marehemu Freddy Ndalla Kasheba anipigie wimbo huu lakini aliniambia haujui au haelewi nazungumzia nini!..(!?).

    Mwaka 1988 Patrick Lee - Thorp alitoa rekodi ya Mwenda wa Bayeke Jean Bosco - The African Guitar Legend The Last Studio Album (The last Studio Recording Of This Master of The Dry Guitar) - ambayo ilirekodiwa na Jerry Barnard mjini Cape Town, Afrika ya Kusini. Kwenye album hii kuna dibaji ya historia ya Jean Bosco. Ni album ambayo ukiisikiliza huwezi kuchoka.

    Jean Bosca aliimba nyimbo zake kwa lugha ya Kiswahili.

    Jean Bosco anaungana katika kundi la wapiga magitaa baridi mabingwa wa Africa wa kariba ya wale palmwine guitarists kutoka Sierra Leone kama Marehemu S.E. Rogie, Abdul Tee-Jay na wengineo.

    PS/ Siku moja nilisafiri na wanamuziki wa Mwenge Jazz Band toka bagamoyo kwenda Dar es Salaam. Tukiwa njiani mwanamuziki mmoja wa Mwenge Jazz akawa anapiga gitaa ule wimbo wa signal tune wa kipindi cha Lala Salama/Usiku Mwema wa RTD wa miaka ya 70, 80 hadi 90. Sijui kama kipindi kile bado kipo? Lilikuwa gitaa zuri mno kulisikiliza tena ukizingatia kwamba alikuwa anapiga ala ile kwa gitaa la umeme lililozimwa sasa sijui kama angekuwa anapiga kwa gitaa baridi ingekuwaje? SWALI: nani anayefahamu jina na mtunzi wa nyimbo ile? Ningependa sana kupata nakala yake.

    ReplyDelete
  5. Hakuna ubishi kabisa Jean Mwenda Bosco ni kundi moja na S E Rodgie. Nyimbo ya Masanga ilipigwa na Edward Masengo ambae alikuwa binamu ya Mwenfa Bosco. Nitajitahidi kusikiliza maneno upya nijue anazungumzia nini, lakini ilikuwa kama anamwelekeza mtu jinsi ya kumpata Mwenda Bosco wa Bayeke.
    Wimbo uliokuwa unapigwa kuashiria kipindi cha lala salama enzi hizo unajulikana kama Yellow Bird,ni wimbo wenye asili ya Kihaiti uliyotungwa 1893 na Michel Mauleart Monton ambaye baba yake alikuwa Mmarekani na mama Mhaiti. Aliitunga kama muziki kwa ajili ya shahiri moja lililohusu binti wa Kihaiti. Maneno YA Kiingereza yalitungwa katika karne ya ishirini na kuitwa Yellow Bird. Umeshapigwa na wanamuziki wengi sana akiwemo Harry Belafonte na Chet Atkins

    ReplyDelete
  6. Anonymous01:25

    Asaante sana kwa maelezo ya Yellow Bird. Nitautafuta mpaka niupate. Kama yule mwanadada aliyetungiwa ilikuwa ni kwa minajiri ya kuomba penzi sijui kama alikataa!

    ReplyDelete
  7. Naomaba kujisahihisha, Masanga ulipigwa na John Mwenda Bosco, na nimebahatika kupata video yake karibu usikilize kwa makini

    ReplyDelete
  8. Dekula Kahanga Kitime hongera kwa Blog,kuna Jamaa kaulizia Nyimbo MASANGA ya John Bosco Mwenda wa Bayeke hii hapa:
    Masanga by John Bosco Mwenda wa Bayeke
    --------------------------------------
    Nani namwenda njia yetu Jadotville
    upitiye njia yetu ya Buluo.
    Umwambiye Baba Bosco wa Bayeke
    umwambiye ende akale kwabo.

    Kanamuke kasipo na Bwana,Tu...mba
    ni kama Kinga yasipo na Lampi,Tumba
    siwende umwambiye Baba Bosco wa Bayeke
    umwambiye ende akalale kwabo (Kiswahili cha Kongo).
    ------------------------------------
    Ni nani atakae kwenda njia yetu ya Jadotville(Kolwezi-DRCongo)
    upitie njia yetu ya Buluo
    umwambie baba Bosco wa Bayeke
    umwambie aende akalale kwao.

    Mwanamke asiekua na Mume,Tumba
    ni kama Baskeli isiokua na Taa,Tumba. Nenda umwelezee baba Bosco wa Bayeke,umwambie aende akalale kwao.(Kiswahili cha Afrika Mashariki)

    Mdau Vumbi Dekula Sweden

    ReplyDelete

SAFARI ZANGU NA BENDI sehemu ya kwanza.

  TANCUT ALMASI ORCHESTRA  wakiwa Jamhuri Stadium Dodoma   Sikumbuki ni safari ngapi za kimuziki nilizowahi kuzifanya hapa nchini katika m...